Habari za Punde

Dk Shein: Suala la mafuta lisipotoshwe kwa manufaa ya kisiasa

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
    Zanzibar                                            29 Septemba, 2015
---
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Mgombea Urais wa Zanzibar kupitia Chama Cha Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema suala la mafuta kutolewa katika mambo ya muungano ni matokeo ya jitihada za pamoja kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na viongozi wake hivyo asitokee mtu au chama kikalitumia suala hilo kama lake binafsi.

“Hakuna haja ya mbwembwe wala kujisifu wote katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano tulishirikiana na kushauriana pamoja kwa muda mrefu hadi kufikia hatua ya kupitisha sheria ya mafuta katika kikao cha Bunge cha mwezi Julai 2015” Dk. Shein alisema.

Akizungumza katika mkutano wa kampeni huko Paje leo katika jimbo la uchaguzi la Paje, Mkoa wa Kusini Unguja, Dk. Shein amesema wako baadhi ya wanasiasa Zanzibar wanalitumia suala hilo kama mtaji wa kisiasa kwa kuwaeleza wananchi kuwa hatua iliyofikia sasa ni jitihada zao binafsi.

Katika mkutano huo ambao ulivunja rekodi za mahudhurio tangu kufanyika mkutano wa uzinduzi wa kamepeni, Dk. Shein amesema suala hilo limekuwa likipotoshwa kwa makusudi kwa manufaa ya kisiasa hasa wakati huu wa kampeni.

“ningewaelewa wenzangu hawa kama wangewaeleza wananchi kuwa hatua iliyofikiwa ni jitihada za serikali yetu ambao wao ni washirika katika serikali lakini kusema wao ndio waliofanikisha jambo hili inasikitisha na si jambo la kiungwana” Dk. Shein alieleza na kuongeza kuwa kama ni sifa angeweza kujisifu yeye kwani ndie aliyekuwa msimamizi mkuu pamoja na Rais Kikwete.


Alisema yeye amefanya ziara katika nchi za Uholanzi na Ras El Khaima ambako alifanya mazungumzo na kutia saini makubaliano ya awali ya ushirikiano katika kuendeleza sekta hiyo pamoja na kufanya mazungumzo na makampuni mengi yenye azma ya kuja kushiriki katika kuendeleza sekta ya mafuta na gesi.

Dk. Shein alibainisha kuwa baada ya kuwepo makampuni ya kutafuta mafuta Tanzania mwaka 2002 wakati huo akiwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alimtuma aliyekuwa Waziri wa Nishati wakati huo Edgar Maokola Majogo kuzungumza na Waziri mwenzake wa Zanzibar wakati huo Burhan Saadat kuhusu suala hilo uchimbaji wa mafuta.

“Majibu ya mashauriano hayo yalikuwa ni kuwa suala hilo lisiharakishwe kwa kuwa linahitaji mashauriano zaidi” Dk. Shein alisimulia na ndipo mazungumzo yalipoanza.

Mgombea huyo wa CCM aliwaeleza wananchi kuwa 
jitihada za kuliondoa suala la mafuta katika mambo ya muungano lilijadiliwa katika Bunge la Katiba lakini baada ya kuwa mchakato huo haukukamilika yeye na Rais wa Jamhuri ya Muungano walilipeleka suala hilo kwa wanasheria wakuu ili kutumia bunge kulikamilisha na ndivyo lilivyofanyika.

“Ilikuwa ni busara yetu viongozi kulipelekea suala hili kwa wanasheria wetu wakuu baadae tukalijadili katika vikao vyetu hadi sheria kupitishwa bungeni” Dk. Shein alisisitiza.

Hata hivyo aliongeza kuwa ni jambo la kushangaza watu hao wanaojinasibu kuwa wamefanikisha suala hilo ndio hao hao waliopinga suala hilo na kukimbia bungeni wakati sheria ya mafuta ilipokuwa ikipitishwa. 

Akibainisha zaidi Dk. Shein kuwa wakati hayo yakiendelea huku Serikali ya Zanzibar ilikuwa ikitayarisha sera yake na kudokeza kuwa imekamilika pamoja na kwamba rasimu ya sheria iko tayari ikisubiri kupitishwa katika Baraza la Wawakilishi ili kazi ya kuendeleza sekta ya mafuta na gesi ianze kwa kasi.

Aliwataka wananchi wasihadaike na maneno ya viongozi hao kuwa uchimbaji huo utaanza mara moja na kuwatahadharisha kuwa hadi kuyachimba mafuta itachukua sio chini ya miaka mitano.



Postal Address: 2422 Tel.+255 776 613 015, Fax: 024 2231822 
                                               

  


     

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.