Habari za Punde

Dk Shein Asema Ujenzi wa Bandari Mpya ya Mpiga Duri Zanzibar.Kuongeza Kasi ya Kukua kwa Uchumi wa Zanzibar.

STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar                                                                2.12.2015
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema ujenzi wa bandari mpya ya Mpigaduri unaotarajiwa kuanza mwanzoni mwa mwaka 2016 ni hatua muhimu ya kuongeza kasi ya kukua kwa uchumi sambamba na kuharakisha maendeleo ya kiuchumi na kijamii Zanzibar.

Akijibu maswali ya waandishi wa habari wakati wa ziara yake fupi ya kutembelea eneo litakalojengwa bandari hiyo leo, Dk. Shein alieleza kuwa mradi huo pamoja na ule wa upanuzi wa kiwanja cha ndege cha Abeid Amani Karume itafungua milango zaidi ya kiuchumi kwa Zanzibar.

“Huu ni mradi mkubwa kwa uchumi wetu hivyo wananchi watarajie maendeleo makubwa na yenye kasi zaidi ya uchumi wetu” Dk. Shein alieleza.

Aliwaambia waandishi wa habari na viongozi waliokuwepo kuwa mradi wa ujenzi wa bandari ya Mpigaduri si mradi mpya ulianza tangu Awamu ya Tano iliyoongozwa na Dk. Salmin na kuendelea kushughulikiwa katika Awamu ya Sita hadi ndani ya miaka mitano ya Awamu ya Saba ndio ilipofanikiwa kufikia hatua hii ya utekelezaji.

“Sisi awamu hii tumekwenda mbele zaidi,tumetafuta fedha na tumefanikiwa kutokana na urafiki wetu na serikali ya Jamhuri ya Watu wa China tutapata mkopo wa kujenga bandari hii” Dk. Shein alidokeza.

Alifafanua kuwa mazungumzo yake na Rais Xi Jinping wa China wakati wa ziara yake nchini Tanzania na baadae alipofanya ziara nchini China suala hilo lilizungumzwa kwa kirefu na matokeo yake ndio utekelezaji wa mradi huo.

Kuhusu wananchi wanaofanya shughuli zao katika eneo hilo litakalojengwa bandari Dk Shein aliwaeleza wizara na mamlaka husika kuhakikisha kuwa kunakuwepo na mpango maalum wa kuwapatia eneo ambalo litakuwa na miundombinu ya kisasa kufanya shughuli zao na kusisitiza kuwa ni vyema suala hilo likashughulikiwa haraka iwezekanavyo kuepusha migogoro na wananchi hao.

Akijibu swali kuhusu hatua za serikali kuendana na kasi ya kupambana na maovu katika jamii hasa ufisadi, Dk. Shein alisema katika miaka mitano iliyopita Serikali imepitisha sheria nyingi na kali kama vile za uhujumu uchumi na sheria ya maadili ya viongozi hivyo  ipo haja ya kutekelezwa ipasavyo na si suala la kuelezwa kila mara”.

Awali akitoa maelezo kwa Mheshimiwa Rais, Katibu Mkuu wa Wizara ya Miundombinu na Mawasiliano Dk. Juma Malik Akil alieleza kuwa ujenzi utakuwa wa awamu tatu tofauti ambapo awamu ya kwanza itakayogharimu Dola za kimarekani milioni 231.4 itaanza mwezi Januari, 2016.

Alifafanua kuwa awamu ya kwanza ambayo inatarajiwa kukamilika ndani ya miaka mitatu itakuwa bandari kamili yenye kila huduma zitakiwazo kwa bandari za kisasa na awamu nyingine zitatekelezwa kulingana na kuongezeka kwa mahitaji ya miaka ijayo.

Kuhusu suala la wananchi wanaofanya shughuli zao katika eneo hilo Dk. Akil alieleza kuwa wao wamejulishwa hivi majuzi tu na mkandarasi kuwa ujenzi utaanza mapema mwezi Januri 2016 lakini alieleza “watakutana na wizara ya Ardhi kulijadili suala hilo na kuchukua hatua zifaazo mara moja”

Kwa maelezo ya Muhandisi Mkuu wa Shirika la Bandari, Bwana Mbarouk Hamad Mbarouk alisema kuwa, Kampuni ya CHEC kutoka nchini China ndio inayotarajiwa kufanya ujenzi  wa bandari hiyo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.