Habari za Punde

Watoto Wanaoishi katika Mazingira Magumu Wilayani Ilemela Wanufaika na Kituo cha Shaloom Care House.

Na:Binagi Media Group
Zaidi wa Wanafunzi 400 wanaoishi katika mazingira magumu na hatarishi katika Manispaa ya Ilemela Mkoani Mwanza, wamenufaika na msaada wa vifaa vya elimu vyenye thamani ya zaidi ya shilingi Milioni Kumi ili kuwawezesha hao kupata elimu.

Msaada huo umetolewa na Kituo cha kulelea watoto wanaoishi katika Mazingira Magumu na hatarishi cha Shaloom Care House kilichopo katika Manispaa hiyo.

Mratibu wa Kituo hicho Msafiri Wana amebainisha kwamba wanafunzi 221 wa shule za Msingi na wanafunzi 187 wa shule za Sekondari, wamenufaika na msaada huo ambao ni pamoja na madaftari, kalamu na sare za shule ambapo thamani yake ni shilingi Milioni Kumi na Laki Tano.

Baadhi ya wanafunzi waliopokea msaada huo wametoa shukrani zao kwa Kituo hicho ambapo pia wamewasihi wanafunzi wengine ambao wazazi ama walezi wao hawana uwezo wa kuwahudumia mahitaji ya kielimu, kufika katika kituo hicho ili wapate usaidizi huo.

Wakati huo huo Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Magesa Mulongo amewataka Wakuu wa Shule za Msingi, Sekondari pamoja na Maafisa Elimu kusimamia vema matumizi ya fedha kiasi cha shilingi Milioni Mia Tisa Tisini na Tisa, Laki Tatu na Elfu sabini na Sita zilizotolewa na serikali katika Mkoa wa Mwanza kwa mwezi huu ikiwa ni katika kutimiza ahadi yake ya kutoa elimu bure nchini.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.