Habari za Punde

Wandishi wa Habari Zanzibar Watakiwa Kuelimisha Jamii juu ya Maradhi ya Kipindupindu.

Na.Mwashungi Tahir - Maelezo Zanzibar.
Daktari dhamana kanda ya Unguja Dkt. Fadhil Mohammed  Abdallah amewataka wananchi kuchukua tahadhari kuhusu maradhi ya kipindupindu ambayo kwa sasa ni tishio kubwa  Zanzibar.

Hayo ameyasema  katika Ukumbi wa Gereji ya Wizara ya Afya  Mombasa kwenye mafunzo ya waandishi wa habari  juu ya kujikinga na ugonjwa huo  ambao bado unaendelea katika sehemu mbali mbali  Zanzibar.

Amesisitiza kuchukuliwa tahadhari  zaidi  kupambana na maradhi ya kipindu pindu ikiwemo kuweka  mazingira  safi, kufuata  masharti ya afya,  kuchemsha maji ya kunywa  ama kutumia maji yaliyotiwa dawa ya kuulia bektiria wanaosababisha maradhi hayo..

Dkt. Fadhil amewataka  wananchi   kuacha tabia ya kula ovyo  njiani, kukosha matunda na mboga mboga kabla ya kula na kuchukua tahadhari kubwa wakati wa kumshughulikia maiti ya maradhi ya kipindu pindu kwani  ni miongoni mwa njia za maambukizi ya maradhi hayo.

Amewataka waandishi wa habari kutekeleza majuku yao  ya kutoa elimu kwa wananchi ili  wapate uelewa mkubwa zaidi kukabiliana na maradhi hayo.


Amesema maradhi ya kipindu pindu ingawa ni tishio kwa maisha ya wananchi lakini ni rahisi zaidi kuyadhibiti kuliko maradhi mengine iwapo wananchi watafuata masharti ya afya.

“Waandishi wa habari  mnao mchango mkubwa wa kutoa elimu  kwa jamii  katika kukabiliana na maradhi ya kipindupindu  hivyo  tunategemea mashirikiano makubwa kutoka kwenu,” alisisitiza  Dkt. Fadhili

Akifungua mafunzo hayo Mkurugenzi  Mtendaji Kamisheni ya Maafa Zanzibar ndugu  Ali Juma  Hamad amesema juhudi za pamoja zinahitajika  katika kukabiliana na kipindupindu  na  mchango wa kila mtu na taasisi unahitajika.

Amesema kumekuwa na changamoto kubwa katika kukabiliana na maradhi hayo tokea yalipogundulika mwezi  Septemba mwaka jana ikiwa ni kipindi cha jua kali, kuchukua muda mrefu na kusambaa sehemu mbali mbali za Unguja na Pemba kinyume na watu walivyozoea vipindi vya  nyuma.

Akiwasilisha mada ya majukumu ya vyombo vya Habari katika kudhibiti miripuko ya maradhi ya kuambukiza, Mkurugenzi wa Idara y Habari Maelezo  Zanzibar Rafii Haji Makame  amesema vyombo hiyo vinajukumu la lazima katika kusaidia umma kudhibiti vifo na athari nyengine za kiuchumi na kijamii zinazosababishwa na miripuko ya maradhi .

Katika kufanikisha majukumu hayo Mkurugenzi Rafii ametaka kuongezwa ushirikiano kati ya vyombo vya habari na sekta ya afya ili kupata taarifa sahihi kwa wakati katika kufikisha ujumbe kwa umma.

Aidha  amesema utoaji wa elimu ya kudhibiti magonjwa ya kuambukiza kupitia vyombo vya habari liwe suala endelevu ili jamii iweze kupata uwelewa na kubadilika kitabia.

Jumla ya kambi 18 zilifunguliwa na kuhudumia  wagonjwa 1066 Unguja na Pemba na kati yao wagonjwa 22 walifariki. Hivi sasa kuna kambi nne tu zinazoendelea kupokea wagonjwa katika kisiwa cha Unguja.

Wakati huo huo Katibu wa Jumuiya  ya maafisa wa afya Zanzibar Ahmed Suleiman Saidi amewashauri wananchi wa shehia ya Shaurimoyo kubadili tabia na kuweka mazingira wanayoishi katika hali ya  usafi ili kujikinga na kipindupindu.

Alitoa ushauri huo alipokuwa akizungumza na wananchi wa shehia hiyo katika skuli ya Shaurimoyo walipowatembelea kutoa taaluma  juu yamaradhi hayo kwa vile shehia hiyo ni miongozi kati ya shehia zilizoathirika na kipindupindu.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.