STATE HOUSE
ZANZIBAR
OFFICE OF THE
PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar 12.4.2016
WAZIRI wa Nchi Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Issa
Haji Ussi Gavu ameeleza haja kwa viongozi na wafanyakazi wa Wizara hiyo kuendeleza
mashirikiano ya pamoja katika utendaji wao wa kazi ili kufikia lengo la
Serikali la kuwatumikia na kuwahudumia wananchi wote.
Hayo aliyasema mara baada ya makabidhiano
ya Ofisi hiyo yaliofanyika kati yake na aliyekuwa Waziri wa Ofisi hiyo Mhe. Dk.
Mwinyihaji Makame Mwadini, hafla iliofanyika katika ukumbi wa Ofisi ya Waziri wa Nchi Ofisi ya
Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi iliopo Ikulu mjini Zanzibar na kuhudhuriwa
na baadhi ya viongozi na wafanyakazi wa Wizara hiyo.
Aidha Mhe. Gavu alieleza kuwa mashirikiano ya pamoja yatafikia lengo katika
kumsaidia Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed
Shein la kuwaletea maendeleo wananchi wote.
Waziri huyo alitoa shukurani kwa Rais
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein kwa kumteua kushika wadhifa huo na kuahidi
kwa mashirikiano ya pamoja na viongozi pamoja na wafanyakazi wa Wizara hiyo
lengo la Rais la kuiletea maendeleo Zanzibar litafikiwa.
Mhe. Gavu alieleza kuwa hakuna kubwa
litakaloshinda iwapo kutakuwa na mashirikiano ya pamoja katika kutekeleza
majukumu na wajibu sambamba na kufuata taratibu na sherika kwa kila mfanyakazi.
“Nimekuja hapa kwa ajili ya kufanya kazi
hivyo sote tujiandae kwa kufanya kazi na kuendeleza mashirikiano yetu ili tumsaidia
Mhe. Rais...” alisema Waziri Gavu.
Katika maelezo yake, Waziri Gavu
alisisitiza haja wka wafanyakizi na viongozi wa Wizara hiyo kuwepo kwa
mashirikiano na kuahidi kwa upande wake atatoa mashirikiano makubwa na kufanya
kazi kwa kuelekezana na kushirikiana huku akiahidi kufanya kazi kwa taratibu na
sheria za nchi zilizopo.
Waziri Gavu alitumia fursa hiyo kutoa
shukurani kwa Dk. Mwinyihaji Makame kwa kuendelea kuwa na mashirikiano nae na
kuahidi kuendelea kuchota mawazo na busara sambamba na hekima kutoka kwake.
Mapewa Mhe. Dk. Mwinyihaji Makame alitoa
pongezi kwa Waziri Gavu kwa kuteuliwa kuwa Waziri katika Wizara hiyo na kueleza
kuwa hatua hiyo imekuja kutokana na utendaji wake wa kazi mzuri alioufanya
katika Wizara yake ya zamani na imani yake ni kuwa katika wadhifa wake huo mpya
atazidisha juhudi.
Dk. Mwinyihaji ambaye pia, ni Mwakilishi
wa Jimbo la Dimani aliwataka wafanyakazi na viongozi wa Wizara hiyo kumpa
mashirikiano makubwa Waziri huyo mpya kama walivyompa yeye wakati akiwa Waziri
katika Wizara hiyo ambapo katika uongozi wake ilikuwa ni Wizara ya Nchi Ofisi
ya Rais, Ikulu na Utawala Bora.
Aidha, Dk. Mwinyi alisisitiza haja kwa
wafanyakazi wa Wizara hiyo kufanya kazi kwa juhudi kubwa kama wanavyosisitiza
viongozi wakuu hapa nchini akiwemo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk.
Johm Pombe Magufuli pamoja na Dk. Shein ili kuendelea kuiletea maendeleo Zanzibar.
Dk. Mwinyi alitoa shukurani kwa Dk. Shein
kwa kupata ushindi wa kishindo katika uchaguzi mkuu uliopita na kutoa pongezi
za pekee kwa Ofisi ya Faragha ya Mhe. Rais kwa mashirikiano waliyompa huku
akimuomba Waziri huyo mpya kuwatumia wafanyakazi wa Ofisi hiyo katika utendaji
wake wa kazi.
Akitoa neno la shukurani kwa niaba ya
wafanyakazi wa Wizara hiyo, Katibu wa Rais Haroub Shaib Mussa alitoa pongezi
kwa viongozi hao wote katika utendaji wao wa kazi sambamba na kuwa karibu na
wafanyakazi pamoja na wananchi wa Majimbo yao.
Katibu Shaibu alimuahidi Waziri Gavu kuwa
wafanyakazi wa Wizara hiyo wataendelea kumpa mashirikiano makubwa na kuendelea
kumuunga mkono katika utendaji wake wa kazi kwa lengo moja la kuwaletea
wananchi wa Zanzibar maendneleo endelevu.
Rajab Mkasaba,
Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment