STATE HOUSE
ZANZIBAR
OFFICE OF THE
PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Pemba 31.5.2016
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed
Shein amewaeleza wananchi kisiwani Pemba kuwa Zanzibar hapatakuwa tena na uchaguzi
hadi mwaka 2020 na kwa hivi sasa yeye ndie Rais aliyechaguliwa kihalali na
wananchi.
Dk. Shein aliyasema hayo huko Tibirinzi
Chake Chake Pemba, alipokwenda kukagua Tawi la CCM lililochomwa moto katika
ziara yake ya kukagua athari zilizofanywa dhidi ya WanaCCM kwa kuendelea
kukiunga mkono chama hicho kiswani humo.
Katika maelezo yake, Dk. Shein aliwataka
wananchi kutambua kuwa hapatakuwa na uchaguzi tena hapa Zanzibar hadi mwaka
2020 na kuwasisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa
Chama Cha Mapinduzi (CCM) ipo na itaendelea kuwepo.
Dk. Shein aliwataka wananchi kuyapuuza
maneno hayo ya wapinzani kwani ni utani na dhihaka wanayoambiwa wananchi kuwa
uchaguzi mkuu hapa Zanzibar utarejewa na kusema kuwa hilo halipo na hakuna hata
taifa ama nchi inayoweza kuishurutisha Zanzibar kufanya uchaguzi.
Alisema kuwa Zanzibar inaongozwa kwa
Katiba na Sheria za nchi, hivyo hakuna wa kuiongoza na kuleta matakwa yake ili
yafuatwe na Zanzibar ili uchaguzi
urejewe.
Dk. Shein alisema kuwa yeye amewekwa na
wananchi kwa mujibu wa Sheria na Katiba ya nchi, hivyo maneno ya dhihaka na
utani yanayopitwa yakisemwa na wapinzani kuwa uchaguzi utarejewa ni kasumba za
kisiasa.
Aidha, Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar ipo na yeye ndie Rais na kamwe hujuma wanazofanyiwa
wanaCCM kisiwani humo hazitoiondoa ama kuifanya isifanye kazi zake.”wataumwa
hadi kuvimba matumbo lakini mimi ndie Rais halali wa Zanzibar na nitaendelea
kuiongoza Zanzibar hadi mwaka 2020 utakapoitishwa uchaguzi mwengine”,alisema
Dk. Shein.
Sambamba na hayo, Dk. Shein alisisitiza
kuwa Serikali haipatikani kwa hujuma, vitimbi ama kufukiza udi, uvumba na ubani
bali serikali hupatikana kwa kufuata misingi ya demokrasia na sheria za nchi kama
ilivyofanya CCM na hatimae kushika dola.
Dk. Shein aliwataka wananchi hao kutokuwa
na hasira kwani chama chao cha CCM kimeshinda na ndicho kinachoongoza Serikali
na yeyote mwenye nia ya kuvuruga amani na utulivu uliopo hapa nchini basi nguvu
za dola zipo na zitapambana nao.
“Mimi nimewekwa kwa ridhaa za wananchi
kwa mujibu wa sheria na Katiba na hata Mwenyezi Mungu anajua kuwa mimi ndie
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwani yeye ndie alieniwetaka
na asingelitaka yeye nisiwe rais basi nisingelikuwa rais”,alisisitiza Dk.
Shein.
Pamoja na hayo, Dk. Shein aliwataka
wananchi na wanaCCM kuendelea na kazi zao kama kawaida na kushirkiana na serikali
kutekeleza mipango mbalimbali ya maendeleo kwa kuamini kuwa Serikali yao ipo na
itaendelea kushirikiana nao.
Nao WanaCCM wa Tawi hilo walieleza
masikitiko yao juu ya hujuma walizofanyiwa za kutiliwa moto Tawi lao kwa
makusudi jambo lililopelekea hasara ya zaidi ya Shilingi milioni 9 za
Kitanzania.
WanaCCM hao walieleza kuwa usiku wa
kuamkia Machi 10 mwaka huu watu wasiojulikana waliliunguza kwa makusudi Tawi
lao hilo moto na kuweka matairi sehemu ya mlangoni na kuliunga paa pamoja na
vifaa vyote vilivyomo ndani jambo waliloliita kuwa ni hujuma kwa ushahidi wa
kimazingira.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment