Habari za Punde

Viongozi wa CCM Pemba Watowa Pongezi kwa Dk Shein kwa Ushindi wake wa Kishindo.

Na Mwandishi Wetu Pemba.

WANACHAMA wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) kisiwani Pemba wameeleza kuwa ushindi wa chama hicho katika uchaguzi mkuu uliopita umetokana na umoja na ushirikiano kati yao na viongozi wa chama hicho sambamba na ukomavu wa kisiasa alionao Makamo Mwenyekiti wa CCM Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein.

Maelezo hayo waliyatoa Viongozi wa chama hicho walipokuwa wakisalimiana na  Makamo Mwenyekiti wa CCM, Zanzibar na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein kwa nyakati tofauti kisiwani humo.

Viongozi hao walitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Dk. Shein kwa ushindi mkubwa alioupata katika uchaguzi mkuu uliopita na kusisitiza kuwa ushindi huo utaendelezwa mpaka katika uchaguzi ujao wa mwaka 2020 kwani wanaamini kuwa hakuna tena uchaguzi katika kipindi hichi.

Katika maelezo yao viongozi hao walieleza kuwa ukomavu wa kisiasa alianao Makamo Mwenyekiti wao Dk. Shein ndio chachu ya mafanikio ndani ya chama chao pamoja na ushindi wake katika chaguzi zote.


Aidha, viongozi hao walimueleza Dk. Shein kuwa yeye ndio Rais halali wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi aliechaguliwa na wananchi kwa kura nyingi hivyo wataendelea kumuunga mkono katika kuhakikisha Zanzibar inaendelea kupata maendeleo endelevu.

Pamoja na hayo, viongozi hao walitoa pongezi kwa Dk. Shein kwa kuunda Serikali makini na kueleza imani zao kwa viongozi aliowateua kushirikiana nao ndani ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar huku wakieleza imani zao kuwa viongozi hao wanaweza kwenda na kasi ya Dk. Shein.

Pia, viongozi hao walitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli kwa ushindi wake mkubwa pamoja na Makamu wake Mama Samia Suluhu Hassan.

Viongozi hao walisisitiza kuwa ushindi wa CCM na viongozi wake umewapa mwanga mkubwa wa mafanikio na utekelezaji katika kukiimarisha chama chao kwa kuamini kuwa chama hicho ndicho kinachoweza kusimamia maendeleo ya wananchi sambamba na amani na utulivu hapa nchini.

Viongozi hao walisisitiza kuwa Ibara ya 5 ya Katiba ya CCM, inasisitiza haja ya  chama hicho kushinda uchagazi mkuu kwa upande wa Zanzibar na Tanzania Bara na kueleza kuwa hilo limefanyika kwa kuwepo umoja wao na mshikamano na ndio unaowafanya waendelee kutembea kifua mbele hadi hivi leo.
Walieleza kuwa busara na hekima za Dk. Shein ndio zinazoipelekea Zanzibar kuendelea kuwa ni nchi yenye amani, utulivu na maendeleo huku wakiahidi kuendelea kumuunga mkono Dk. Shein pamoja na chama chao cha CCM.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.