HOTUBA YA MAONI
YA KAMATI YA FEDHA, BIASHARA NA KILIMO KUHUSU MAKADIRIO YA MAPATO NA MATUMIZI
YA WIZARA YA KILIMO, MALIASILI, MIFUGO NA UVUVI KWA MWAKA WA FEDHA 2016/2017
Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa,
naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mtukufu , Mwingi wa Rehema, ambaye
ametujaalia neema ya uzima na afya njema na kutuwezesha kukutana hapa leo
tukiwa ndani ya Baraza lako tukufu, tukitekeleza majukumu yetu mbali mbali ya
kuwatumikia wananchi wetu.
Mheshimiwa Spika, kwa dhati kabisa, napenda pia kukushukuru wewe binafsi
Mheshimiwa Spika kwa kunipa nafasi hii ya kuwasilisha Maoni ya Kamati ya Fedha,
Biashara na Kilimo kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Maliasili,
Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
Mheshimiwa Spika, baada
ya maelezo hayo, napenda kuchukua nafasi hii kuishukuru na kuipongeza Wizara ya
Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi kwa kuweza kuwasilisha mbele ya Baraza lako
tukufu Bajeti ya Wizara hiyo kwa mwaka wa fedha 2016/2017 kwa ufanisi mkubwa
katika mfumo mpya wa bajeti unaozingatia programu “Program Based Budget” (PBB).
Mheshimiwa Spika, aidha
nitakuwa mkosefu wa fadhila kama sitatoa shukrani zangu za dhati kwa Wajumbe na
Makatibu Kamati ya Fedha, Biashara na Kilimo kwa mashirikiano tuliyokuwa nayo
kwa pamoja katika kutekeleza jukumu hilo kwa pamoja, pamoja na mashirikiano
tuliyoyapata kwa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi. Naomba
niwatambue kwa kuwataja kwa majina Waheshimiwa Wajumbe hao pamoja na Makatibu wake kama ifuatavyo:-
1. Mhe. Yussuf Hassan Iddi - Mwenyekiti
2. Mhe. Hamida Abdalla Issa - Makamo
Mwenyekiti
3. Mhe. Ussi Yahya Haji - Mjumbe
4. Mhe. Hamad Abdalla Rashid - Mjumbe
5. Mhe. Shadya Mohammed Suleiman - Mjumbe
6. Mhe. Ali Salum Haji - Mjumbe
7. Mhe. Bihindi Hamad Khamis
- Mjumbe
8. Mhe. Moh’d Mgaza Jecha - Mjumbe
9. Ndg. Abuubakar Mahmoud Iddi - Katibu
10. Ndg. Salum Khamis Rashid - Katibu
Mheshimiwa
Spika, ni ukweli usiopingika kuwa, Wizara hii
ndio uti wa mgongo kwa wananchi wa Zanzibar kwani imebeba sekta muhimu sana
ambazo ni sekta ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi ambapo wananchi wengi huzitegemea
kwa ajili ya kuongeza kipato chao na kwa ajili ya mahitaji yao ya kila siku.
Bado ipo haja kubwa sana kwa Serikali kupitia Wizara hii kuelekeza nguvu zake zaidi
ili kuimarisha sekta hizi nchini. Hii inatokana na ukweli kwamba, tathmini
inaonesha kuwa mchango wa sekta hizi katika pato la Taifa kwa mwaka 2015
umeshuka kutoka asilimia 27.9 ya mwaka 2014 hadi kufikia asilimia 19.2 mwaka
2015.
Mheshimiwa
Spika, pamoja na umuhimu mkubwa wa sekta hizi
nchini, bado uingizwaji wa fedha katika sekta hizi ni wa wastani jambo ambalo
linazorotesha utekelezaji wa mipango iliyojipangia Wizara. Kwa mwaka wa fedha
2015/2016 iliyokuwa Wizara ya Kilimo na Maliasili imeidhinishiwa jumla ya
Shilingi Bilioni Arobaini na Nane, Milioni Mia Moja Sabiini na Nne na Laki Tatu
(48,174,300,000) hadi kufikia mwezi wa Aprili, 2016 Wizara imepata jumla ya
Shilingi Bilioni Tisa, Milioni Mia Moja Themanini na Tano na Laki Tano Elfu
Arubaini na Moja, Mia Saba na Hamsini (9,185,541,750) sawa na asilimia 69.6. na
kwa upande wa fedha za maendeleo Wizara ilikadiriwa kutumia jumla ya TZS
Bilioni Thelathini na Nne, Milioni Mia Tisa themanini na tatu na laki mbili
(34,983,200,000/-) hadi kufikia aprili, 2016 fedha zilizopatikana ni TZS
11,641,070,476.
Mheshimiwa
Spika, kwa iliyokuwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi
imeidhinishiwa jumla ya TZS Bilioni Nne,Milioni Mia Mbili na Elfu Kumi na Saba
na Laki Nne (4,217,400,000) ambapo hadi kufikia mwezi wa aprili, 2016 Wizara
imepata jumla ya TZS Bilioni Mbili, Milioni Mia Nne Tisiini na Nane, Laki Sita
na Elfu Ishirini na tano, Mia Nne na thelathini na Sita (2,498,625,436) sawa na
asilimia 59. Na kwa upande wa fedha za maendeleo Wizara ilikadiriwa kutumia
jumla ya TZS 12,910,100,000 hadi kufikia Aprili fedha zilizopatikana ni TZS Bilioni
Mbili, Milioni Mia Tatu Tisiini na Moja, Laki Mbili Arubaini Mbili Elfu, Mia
Saba Sitini na Nne (2,391,242,764) sawa na asilimia 19.
Mheshimiwa
Spika, pamoja na nia njema ya Serikali
kuimarisha sekta hizi juhudu za ziada zinahitajika khasa kuipatia Wizara hii
fedha kwa wakati, ili wazisimamie sekta hizi kwa lengo la kuziimarisha kwa
maslahi ya wananchi na kupunguza malalamiko kwa wadau wa sekta hizi nchini.
Mheshimiwa Spika,
Wizara hii ni moja kati ya Wizara ambazo zinategemewa kukusanya mapato kupitia
sekta zake inazozisimamia, katika mwaka mwaka wa fedha 2015/2016 Wizara ilikadiriwa
kukusanya mapato ya TZS Bilioni Moja, Milioni Mia Tisa na Ishirini na Mbili, Laki
Saba na Hamsini na Tano (922,755,000)hadi kufikia Aprili,2016 Wizara kwa ujumla
imekusanya mapato ya TZS Bilioni Moja,Milioni Mia Nane na Thamanini, Laki Saba
na Tisini, Mia Nane Thelasini na Sita(1,680,790,836) sawa na asilimia 87.4 ya
malengo ya Wizara.
Mheshimiwa
Spika, pamoja na jitihada kubwa inayofanywa na
Wizara katika ukusanyaji wa mapato, Kamati yangu haijaridhishwa na asilimia ya
ukusanyaji iliyofikiwa na Wizara. Kwahivyo, Kamati inaitaka Wizara kuangalia
upya vianzio vyake vya mapato na kufanya tathmini katika suala zima la uvujaji
wa mapato ili kuhakikisha miyanya yote inayopelekea kuvuja kwa mapato ya Wizara
hii inazibwa na hatua kali za kisheria zichukuliwe kwa yeyote atakayehusika na
eidha kukwepa kodi au kusababisha kuvuja kwa mapato ya Wizara.
Mheshimiwa
Spika, Wizara imetoa takwimu kadhaa katika
sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi ili kutoa mwelekeo wa sekta hizi kujifahamu
wapi tulipotoka, wapi tulipo na wapi tunaelekea katika sekta hizi. Ni dhahiri
kuwa takwimu za mifugo na uvuvi zinazotolewa na Wizara bado zinatolewa kienyeji
sana kwani maeneo mengi yanayohusika na mifugo na uvuvi hayafikiwi na hivyo
kupelekea takwimu zinatolewa ni za kubahatisha na sio sahihi. Kamati yangu
inaitaka Wizara kuangalia upya vyanzo vya takwimu zinazotolewa na Wizara ili
takwimu zinazotolewa zionekane kuwa vipo vianzio vya upatikanaji wa takwimu
sahihi katika sehemu zinazohusika.
Mheshimiwa
Spika, Kamati yangu inaipongeza sana Wizara
kwa kuliangalia suala la bei ya mwani kwa jinsi wakulima wa zao hili wanavyopata
tabu juu ya kilimo hiki ukilinganisha na bei ya zao lenyewe. Jitahada za Wizara
kutaka kuandaa utaratibu maalum wa ununuzi wa zao la mwani kupitia Shirika la
Biashara la taifa la Zanzibar (ZSTC) kwa lengo la kuwahakikishia soko la
uhakika la zao hili linaungwa mkono na Kamati yangu kwani litaondoa kabisa
tatizo la bei ya mwani kwa wakulima na kuwapatia soko la uhakika. Kamati
inaiomba sana serikali iharakishe suala hili ili kupunguza kilio kwa wakulima
wa zao la mwani.
Mheshimiwa
Spika, Kamati pia imeridhika kwa jitihada za
uanzishaji wa vikundi 144 vya wafugaji wa samaki, lakini Kamati inaishauri
Wizara isiishie kwenye uanzishaji tu lakini pia iwe na ufuatiliaji juu ya
maendeleo ya vikundi hivyo ili kujuwa mafanikio yao na changamoto zao. Kwani
katika utendaji wetu jitihada zinaonekana sana kwenye uanzishaji wa mambo mbali
mbali ya kimaendeleo katika jamii lakini hakuna ufuatiliaji, jambo ambalo
hupelekea kutokuendelea kwa yale yanayoanzishwa. Na hivyo kurudisha nyuma
jitihada za Serikali na jitihada za wananchi.
Mheshimiwa
Spika, katika kuimarisha sekta ya kilimo
nchini, Kamati yangu pia inaipongeza sana Wizara kwa ununuzi wa mbolea na dawa
za kuulia magugu, lakini bado Kamati inasikitishwa sana na utaratibu wa ugawaji
wa mbolea na dawa pamoja na zinavyotumiwa. Aidha, Wizara ni vyema kufanya
utafiti zaidi ili kuelewa mahitaji ya mbolea kwa wakulima wetu kwani ni dhahiri
kuwa mbolea inayotolewa haitoshi na hivyo kusababisha malalamiko kwa wakulima
wetu na kurudisha nyuma sekta hii ya kilimo.
Mheshimiwa
Spika, Kamati yangu ililijadili kwa kina suala
la ununuzi wa matrekta na matumizi yake kwa wakulima, kwa mujibu wa tathmini ya
Wizara ili kukidhi mahitaji ya wakulima yanahitajika matrekta 80, lakini sasa
hivi yapo matrekta 48 (Unguja 29 na Pemba 19). Lakini kati ya matrekta hayo si
chini ya matrekta 10 hayafanyi kazi na yanahitaji matengenezo. Kamati
inaendelea kuishauri Wizara iwe makini sana na iwatumie wataalamu wake kabla ya
ununuzi wa matrekta ili yatumike kwa muda mrefu na kuipunguzia gharama
Serikali.
Mheshimiwa
Spika, Kamati yangu pia ilijadili sana suala
la uendelezwaji wa mashamba ya mipira, ni dhahiri kuwa mashamba haya
yanaingizia mapato makubwa katika Serikali na kwa sasa hivi mashamba haya
yamekodishwa kwa watu binafsi, lakini hayashughulikiwi ipasavyo jambo ambalo
linapelekea miti mingi inakufa, mashamba yanavamiwa lakini pia hayaendelezwi
kwa kupandwa miti mipya. Kamati inaitakwa Wizara kuliangalia vizuri suala hili
na kama aliyekodishwa hayaendelezi basi mashamba haya yarudi kwenye mikono ya
Serikali.
Mheshimiwa
Spika, Kamati imefurahishwa kwa kupewa taarifa
ya kukamilika kwa ujenzi wa kituo cha usarifu wa mazao, lakini Kamati
imesikitishwa sana na udanganyifu uliofanywa wa kutokukamilika kwa kufungwa kwa
mashine na vifaa vya ujenzi huo na hatimae kushindwa kukamilika kama
ilivyokusudiwa. Tunaomba sana hatua za kisheria zichukuliwe kwa yeyote
aliyehusika na udanganyifu huo.
Mheshimiwa
Spika, Kamati yangu inaipongeza sana Wizara
kwa ujenzi wa Barabara za mashamba kilomita 148.5 kwa Unguja na Pemba chini ya
mradi wa MIVARF kwa kiwango cha fusi, hata hivyo, Kamati inaishauri Serikali
kupitia Wizara ya Mawasiliano kuzikamilisha barabara hizi kwa kiwango cha lami
kwani kubakia kama zilivyo zitaharibika na hivyo kushindwa kufikia malengo
yaliyokusudiwa na kuitia gharama kubwa Serikali ya kuzijenga tena upya barabara
hizo au kuzifanyia ukarabati.
Mheshimiwa
Spika, Kamati ilifurahishwa sana baada ya
kupata taarifa kuwa yapo mabonde mengi ya mpunga hapa Zanzibar ambapo kama
yatalimwa mpunga yote basi yatakidhi mahitaji ya chakula kwa asilimia 80% kwa
wananchi wa Zanzibar, Kamati yangu inaendelea kuitaka Serikali kuongeza juhudi
katika kilimo ili tupunguze kununua vyakula kutoka nje ya nchi.
Mheshimiwa
Spika, Kamati yangu inaipongeza Wizara kwa
kuotesha miche ya mikarafuu 347,650 kwa Unguja na Pemba kwa lengo la kuimarisha
kilimo na zao la karafuu nchini. Lakini Kamati inaiomba sana Wizara baada ya
kugawa miche kuwe na ufuatiliaji ili kufahamu ni miche mingapi ilipandwa na
mingapi imeshika na mingapi imekufa ili isijekuwa tathmini yetu inakuwa kubwa
katika kuotesha miche lakini karafuu zinazovunwa hazionekanwi kuongezeka, hapo
itakuwa hatujafanya kitu.
Mheshimiwa
Spika, tuna tatizo la bandari bubu ambazo kwa
kiasi kikubwa sana linaathiri kupungua kwa mapato ya nchi lakini pia linaathiri
katika sekta mbali mbali zikiwemo kilimo na mifugo kwasabubu wanyama na mbegu
za mimea huingizwa kiholela na hatimae kupelekea kutokea kwa maradhi ya mimea
na mifugo. Kamati yangu inaitaka Serikali kwa kushirikiana na vikosi vyake vya
SMZ kukomesha moja kwa moja tatizo hili ili kuokoa mapato ya nchi na madhara
yote yanayotokana na tatizo hili. Lakini pia mashirikiano baina ya wananchi na
Serikali yanahitajika ili kukomesha tatizo hili.
Mheshimiwa
Spika, tatizo la matumizi ya msumeno wa moto
bado lipo Zanzibar na linaendelea kuathiri sana miti katika maeneo tofauti ya
Zanzibar, pamoja na jitihada zinazochukuliwa na Wizara kukomesha matumizi ya
msumeno wa moto lakini bado jitihada za ziada zinahitajika kwa wananchi kutoa
mashirikiano kwa vyombo na taasisi husika ili kuinusuru miti yetu na hatimaye
nchi yetu isijekuwa jangwa.
Mheshimiwa
Spika, uvuvi haramu ni tatizo jengine lipo
katika visiwa vyetu ambalo kwanza hupoteza mapato ya nchi na kuharibu mazalia
ya samaki na hivyo kusababisha madhara makubwa katika sekta ya uvuvi nchini.
Tunaiomba Serikali na tunaamini kuwa inaweza kukomesha moja kwa moja jambo hili
ili tuokoe mapato yetu na kuweka matumizi mazuri ya rasilimali yetu ya bahari.
Mheshimiwa
Spika, Kamati yangu inaipongeza sana Serikali
pamoja na Wizara hii kwa kufikia pahala pazuri katika ujenzi wa soko la Malindi
ambapo mwanzo lilishindwa kuanza kujengwa kwasababu michoro ya awali kutoendana
na majengo ya Mji Mkongwe ambao upo kwenye urithi wa dunia.Tunaimani kuwa
kwakuwa hatua zote zimeshakamilika ujenzi huu utaanza muda wowote kuanzia
sahivi ili kuimarisha sekta ya uvuvi nchini.
Mheshimiwa
Spika, hotuba ya Mheshimiwa Waziri
imezungumzia mambo mengi sana na hayo ni machache tu kati ya mambo yaliyojadiliwa
na Kamati yangu naamini yapo mengi Waheshimiwa Wajumbe watayazungumza, kwahivyo
sasa baada ya mchango huo wa jumla naomba kwa ruhusa yako niende kwenye
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa mwaka wa fedha 2016/2017 kwa Wazara hii ya
Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi.
Mheshimiwa
Spika, kwa ujumla Kamati yangu ilipitishia
Bajeti ya Wizara hii pamoja na marekebisho ambapo marekebisho haya
yalipendekezwa na Wizara kwa kuongeza fedha katika baadhi ya vifungu ambavyo
vilisahaulika.
Marekebisho haya yamebadilisha jumla ya fedha katika matumizi ambapo kabla
ya marekebisho ilikuwa ni TZS Bilioni Arobani Nane, Milioni Mia Tisa Arobani na
Mbili, Laki Tatu (48,942,300,000) na baada ya marekebisho ni TZS Bilioni Arobani
Nane, Milioni Mia Tisa Sabini na Saba, Laki Tatu (48,977,300,000). Vifungu
ambavyo vimefanyiwa marekebisho ni hivi vifuatavyo:-
Kifungu L0105
|
Kabla ya Marekebisho
|
Baada ya Marekebisho
|
Program Kuu ya
Mipango na usimamizi wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi
|
19,481,687,000
|
19,516,647,000
|
Kifungu L010502
|
||
Program Kuu ya Mipango, Sera na Utafiti wa Kilimo, Maliasili, Mifugo na
Uvuvi
|
14,765,449,000
|
14,800,449,000
|
Kifungu L01050205
|
||
Miundombinu ya masoko
ya mazao ya Kilimo
|
1,908,964,000
|
Mheshimiwa
Spika, katika mwaka huu wa fedha 2016/2017
Wizara inakadiria kukusanya TZS 2,817,599,000/. Ni imani yetu kuwa makusanyo
haya yatakusanywa zaidi endapo kutakuwa na mikakati mizuri katika kukusanya wa mapato na udhibiti wa uvujaji wa mapato.
Tunaiomba sana Wizara katika kuhakikisha kuwa tufanikisha malengo
tuliyojipangia kwanza tusiwe na muhali katika suala la ukusanyaji wa mapato
nahatua kali zichukuliwe kwa yeyote atakaye kwepa kulipa kodi au atakae
sababisha kuvuja kwa mapato, na hilo tunaomba sana lizingatiwe katika maeneo
yote ya ukusanyaji kodi. Lakini pia Kamati inaendelea kuishauri Wizara
isiridhike na vianzio tulivyonavyo itumie wataalamu wake kubuni vyanzo vipya
vya mapato na jambo hili tunaamini linawezekana.
Mheshimiwa
Spika, katika Kifungu L0105 jumla ya TZS 28,641,000 zimetengwa kwa ajili ya Kusimamia
mapato na matumizi ya Wizara. Kwakuwa zipo fedha maalumu ambazo zimetengwa kwa
ajili ya kusimamia mapato, tunaamini kuwa suala la uvujaji wa mapato katika
Wizara hii halitakuwepo.
Mheshimiwa
Spika, Kamati yangu inaitaka Wizara
kuyasimamia mapato ya Wizara hii kwa nguvu zake zote lakini maeneo yafuatayo
yanahitaji usimamizi zaidi kwani ni maeneo ambayo yanafanyiwa udanganyifu sana
na kusababisha kuvuja kwa mapato, maeneo yenyewe ni haya yafuatayo:
Ø Ada za uuzaji wa mawe,mchanga na kokoto
Ø Leseni za uvuvi
Ø Mapato ya mashamba
Ø Ada ya uingizaji wa wageni
Ø Mapato ya mifugo
Ø Mapato ya uvuvi wa bahari kuu
Mheshimiwa
Spika, kama ilivyoelezwa na Mheshimiwa Waziri
kuwa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi ambayo Fungu lake ni L01 inazo Programu Kuu 5 na Programu
ndogo 13. Katika utekelezaji wa Programu hizo tano Wizara imepanga kutumia
jumla ya TZS 48,977,300,000 kwa mwaka 2016/2017 kati ya fedha hizo TZS
15,743,300,000/ kwa ajili ya kazi za kawaida na 33,234,000,000/ kwa ajili ya
kazi za Maendeleo ambapo katika fedha hizi za maendeleo TZS 1,068,000,000/
kutoka kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na 32,168,000,000/ kutoka kwa
washirika wa maendeleo.
Programu Kuu ya Maendeleo ya Kilimo
Mheshimiwa Spika, katika kifungu L0101
Programu Kuu ya Maendeleo ya Kilimo ambayo imetengewa jumla ya TZS
6,615,744,000, ndani yake zimetengwa TZS 3,382,472 kwa ajili ya Maendeleo ya Huduma za Kilimo na Karakana
ya Matrekta. Naomba sana fedha hizi ziingizwe kwa wakati ili kuboresha na
kuimarisha kilimo na kuindeleza karakana yetu ya matrekta na kuacha kutengeza
vyombo vya Seriklai kwa watu binafsi. Suala hili la kutengeneza vyombo vya
Serikali kwa watu binafsi siku hizi limekuwa ni la kawaida sana wakati Serikali
inayo maeneo yake maalum ya kutengeneza vyombo vyake, tunaomba sana karakana ya
Serikali iwezeshwe kwa kupewa vifaa vya kutosha ili tuzilinde fedha
zinazotumika kwa ajili ya kutengeneza vyombo nje ya karakani zetu.
Mheshimiwa Spika, aidha katika Programu hii jumla ya TZS 1,068,660,000
zimetengwa kwa ajili ya umwagiliaji maji. Wakati Kamati ikijadili suali hili ilielezwa
kuwa, Wizara inadaiwa takriban TZS 600,000,000/- na Shirika la Umeme la
Zanzibar (ZECO) kwa gharama za umeme, na umeme mwingi unatumika kwa ajili ya
umwagiliaji maji. Kamati yangu inaishauri Wizara iangalie njia mbadala ya
matumizi ya umeme wa jua (solar power) ili kupunguza gharama za matumizi ya
umeme katika shughuli hii ya umwagiliaji maji na kuwapunguzia gharama wakulima
wetu.
Mheshimiwa Spika, vile vile katika Programu hii jumla ya TZS 344,454,000
zimetengwa kwa ajili ya Uhakika wa
Chakula na Lishe. Kamati yangu inaiomba sana Serikali kuhakikisha fedha
hizo zinapatika kwa wakati ili ghala yetu tuliyonayo iweze kutumika kwa
kuhifadhia chakula hicho na kupunguza usumbufu kwa wananchi ikitokea kuadimika
kwa chakula nchini.
Mheshimiwa Spika, katika Programu hii vile vile jumla ya TZS 1,425,000,000
zimetengwa kwa ajili ya Kuimarisha
Upatikanaji wa Pembejeo za Kilimo. Kamati yangu inaiomba sana Serikali
kuingiza fedha hizi mara tu baada ya kupitisha bajeti hii, kwani kuna wakulima
ambao wanaidai fedha kwa Wizara hii ambazo
walikopeshwa mbegu na wakulima. Deni hili ni la muda mrefu na kutokuwalipa
wakulima fedha zao tutakuwa tuna wavunja moyo sana wakulima wetu na hivyo
kurudisha nyuma sekta ya Kilimo. Kamati yangu haitaridhia endapo madeni haya
itafika bajeti ya mwakani hayajalipwa kwa wakulima wanaoidai Wizara. Wanaodai
fedha hizo wameshalalamika mpaka kwenye vyombo vya habari kuonesha hisia zao.
Programu Kuu ya Maendeleo ya Rasilimali za misitu na
Maliasili zisizorejesheka
Mheshimiwa Spika, katika kifungu L0102
Programu Kuu ya Maendeleo ya Rasilimali
za Misitu na Maliasili Zisizorejesheka jumla ya TZS 1,667,436,000
zimetengwa. Dhumuni la Programu ni kuhifadhi na kuendeleza misitu, kupitia
Programu hii tunaiomba sana Wizara ihakikishe kuwa misitu inahifadhiwa na
kuendelezwa ili iwe ni kivutio kikubwa cha watalii wanaotembelea katika misitu
hiyo, na iweze kuingiza mapato zaidi katika nchi. Lakini pia pamoja
nakuihafadhi na kuilinda misitu yetu, Kamati inaitaka Wizara pia iitangaze
misitu yetu ndani na nje ya nchi ili tupate wageni wengi wanaotembelea katika
misitu yetu. Kwa maana kwamba isiishie kwenye kuhifadhi na kuendeleza lakini
iitangaze pia ili ijulikane ndani na nje ya nchi.
Mheshimiwa Spika, katika programu hii kiasi cha TZS 1,570,725,000
zimetengwa kwa ajili ya Uhifadhi na
Kusimamia Misitu na Mashamba ya Serikali.
Kamati yangu wakati inajadili Programu hii
ilitaka kujua kuhusu uwepo wa hati miliki kwa mashamba ya Seriklai kama
ni njia moja ya kuhifadhi na kusimamia mashamba hayo, Kamati ilielezwa kuwa
Serikali inayo jumla ya mashamba 52, kati ya hayo mashamba 12 yameshapatiwa
hati miliki na mashamba 40 bado hayajapatiwa. Kamati inaitaka Serikali kwa
kushirikiana na Wizara ilifuatilie suala hili la upatikanaji wa hati miliki ya
mashamba ya Serikali yaliyobaki kwani uvamizi wa mashamba haya unaendelea siku
hadi siku.
Programu Kuu ya Maendeleo ya Mifugo
Mheshimiwa Spika, katika kifungu L0103
Programu Kuu ya Maendeleo ya Mifugo jumla ya TZS 1,760,746,000 zimetengwa.
Fedha hizi zimetengwa kwa ajili uzalisahji wa mifugo na huduma za utabibu wa
mifugo.
Mheshimiwa Spika, naomba nieleze kuwa Wizara hii kupitia Idara ya Mifugo
ina mifugo 95 kati ya hiyo 75 ni ng’ombe ambao kati ya hao shamba la Pangeni
lina ng’ombe 44 na Chamanangwe 31 na Kitumba mbuzi 20. Kwakuwa, Wizara kupitia Idara
hii ambayo ndio tegemeo kwa wafugaji tulitarajia tuone idadi kubwa ya mifugo
ili iweze kuwasaidia wafugaji wengine, lakini Kamati yangu inasikitishwa sana
kuona kuwa katika mashamba haya wapo wafanyakazi wa Serikali ambao wanalipwa mishahara
na Serikali kushughulikia mashamba hayo lakini idadi ya mifugo iliyopo
hairidhishi. Tunaomba Serikali kupitia Wizara ya fedha iipatie idara hii fedha ili
idadi ya mifugo iongezeke na izalishe
mifugo kwa wingi na hatimae kuweza kuwasaidia wafugaji.
Mheshimiwa
Spika, Katika Programu hii jumla ya TZS 106,540,000 zimetengwa kwa ajili ya
Kudhibiti Maradhi ya Mifugo. Maradhi
ya mifugo yapo na yanaathiri sana sekta hii ya mifugo kwa wafugaji wote walioko
Unguja na Pemba. Tunaamini fedha hizi zitapatikana ili kudhibiti moja kwa moja
maradhi ya mifugo. Lakini Kamati yangu imesikitishwa sana baada ya kuona kuwa
katika Idara hii ya mifugo kwa upande wa Unguja wapo madaktari 10 na kwa Pemba
yupo (1) mmoja tu. Tunaomba sana Wizara iliangalie sana suala hili kwani wataalamu
wanahitajika kwa wingi kwa pande zote mbili ili kuinusuru mifugo yetu na
maradhi.
Programu
Kuu ya Maendeleo ya Uvuvi
Mheshimiwa
Spika, katika L0104 Programu Kuu ya Maendeleo
ya Uvuvi jumla ya TZS 19,416,727,000 zimetengwa. Fedha hizi zimetengwa kwa
ajili ya kuimarisha ufugaji wa mazao ya baharini na Maendeleo ya uvuvi na
hifadhi za baharini, katika fedha hizo jumla ya TZS 15,045,000 kwa ajili ya Kuimarisha Kilimo cha Mwani lakini pia
TZS 2,297,000 zimetengwa kwa ajili ya kuimarisha Usarifu na Uongezaji Thamani wa Zao la Mwani. Tunaimani kuwa fedha
hizi zitaingizwa kwa wakati ili kupunguza kilio kwa wakulima wa mwani na ni
matarajio yetu kuwa uzalisaji wa mwani utaongezeka zaidi endapo fedha hizi
zitapatikana.
Mheshimiwa
Spika, vile vile katika Program hii jumla ya TZS 9,000,000 zimetengwa kwa ajili ya Kusimamia Mali za Wizara na Manunuzi kwa Mujibu
wa Sheria. Mheshimiwa Spika, kwa
ujumla Wizara hii ni Wizara pekee ambayo inazo mali nyingi sana za Serikali
hasa vyombo vya moto kama vile magari, pikipiki, matrekta nakadhalika ambavyo
vinahitaji kusimamiwa vizuri ili vitumike kwa madhumuni yaliyokusudiwa na
Serikali. Kamati yangu inapata mashaka sana juu ya fedha hizi zilizotengwa kwa
ajili ya usimamizi wa mali za Wizara ukilinganisha na idadi ya vyombo vilivyomo
ndani ya Wizara hii. Pamoja na ufinyu wa fedha hizo Kamati yangu inaitaka
Wizara kuhakikisha kuwa mali za Wizara zinatumika kwa madhumuni yaliyokusudiwa
na sio vyenginevyo.
Mheshimiwa
Spika, Aidha, katika Programu hii jumla ya TZS
14,970,993,000 zimetengwa kwa ajili ya Kuimarisha
Uvuvi wa Bahari Kuu. Mheshimiwa Spika suala hili la uvuvi wa bahari kuu
limekuwa likizungumzwa sana katika Baraza lako tukufu, tunaomba sana Serikali
iharakishe kuanzishwa kwa uvuvi wa bahari kuu kwani rasilimali yetu kubwa
visiwani ni bahari. Kamati yangu pamoja na Wajumbe wa Baraza lako tukufu
tunaamini kuwa kuanzishwa uvuvi huu kutaimarisha uchumi wa Zanzibar kwani kutaingiza
mapato mengi katika nchi na kutaongeza ajira kwa vijana.
Mheshimiwa
Spika, matumizi ya rasilimali ya bahari katika
kisiwa chetu bado ni madogo sana hususan katika suala la uvuvi, kwani bado
tunatumia uvuvi wa kienyeji, jambo hili limepelekea sasa hivi katika visiwa
vyetu tunaagiza samaki kutoka nje jambo ambalo ni la kusikitisha sana, takwimu
za upatikanaji wa samaki kwa Zanzibar kwa mwaka 2015 ni tani 34,104 wakati nchi
kama China inavua samaki tani 49,467,463; Peru inavua samaki tani 9,416,285 na
India 6,318,639 na zipo nchi nyigi ambazo zinavua samaki wengi sana na
zimeendelea kupitia sekta hii ya uvuvi.
Tunaiomba sana Serikali
suala hili sasa sio la kuzungumzwa tena bali ni la kuanza kufanyiwa kazi kwani
tumeshuhudia kuwa zipo nchi nyingi ambazo zimeendelea kwa matumizi mazuri ya
rasilimali ya bahari na sisi tuwe ni miongoni mwa nchi hizo.
Tunaishauri Serikali
itafute wawekezaji wa ndani au nje katika suala hili la uvuvi wa bahari kuu ili
rasilimali yetu ya bahari itumike kwa maslahi ya wananchi wa Zanzibar na kuinua
uchumi wetu. Tunaomba sana katika Wizara hii kipaombele cha Wizara katika
bajeti ya mwaka huu iwe ni kuanzishwa kwa uvuvi wa bahari kuu.
Programu
Kuu ya Mipango na Usimamizi wa Kilimo,Maliasili,Mifugo na Uvuvi
Mheshimiwa
Spika, katika kifungu L0105 Programu Kuu ya Mipango na Usimamizi wa Kilimo, Maliasili,
Mifugo na Uvuvi jumla ya TZS 19,481,647,000 zimetengwa, ambapo ndani yake zipo
programu ndogo za utawala na uendeshaji wa kazi za kilimo, maliasili, mifugo na
uvuvi. Katika Programu hii jumla ya TZS 352,830,000 zimetengwa kwa ajili ya kuwajengea uwezo wa kitaaluma wafanyakazi.
Mheshimiwa Spika, katika kifungu hiki Kamati yangu ilichukuwa muda mrefu
kujadiliana na Wizara ili kupatiwa maelezo ya fedha hizo kuzielekeza kwenye
kusomesha wafanyakazi badala ya kuimarisha kwenye kilimo chenyewe. Tatizo
lilipo ni kuwa, Zanzibar tunayo Bodi yetu ya Mikopo kwanini wafanyakazi hawa
wasisomeshwe na Bodi ya Mikopo ili kuokoa fedha hizo kwenda kwenye kilimo, na
kwakuwa wanaosomeshwa ni wafanyakazi ingekuwa rahisi fedha hizo kurudishwa ili
wasomeshwe watu wengine.
Mheshimiwa
Spika, Kamati imeelezwa kuwa wafanyakazi wengi
ambao wanasomeshwa na Wizara wana umri zaidi ya miaka 35 ambapo moja ya vigezo
vya kupata mkopo mtu awe na umri usiopungua miaka 35. Kwa msingi huo, Kamati
yangu inashauri kuwa Wizara ya Elimu kupitia Bodi ya Mikopo sasa iangalie
uwezekano wa kusomesha wafanyakazi ambapo
faida mbili zitapatikana; kwanza fedha zitakazotumika kwa ajili kuwafundisha
zitakuwa na uhakika wa kuwarudishwa na la pili tutaokoa fedha nyingi katika
mawizara ambazo zinatumika kuwasomesha wafanyakazi, jambo ambalo baadhi yao
wakishakusomeshwa huwa wanahama kwenye zile taasisi na hivyo malengo
yaliyokusudiwa kutokufikiwa.
Mheshimiwa
Spika, katika Programu hii jumla ya TZS
8,044,968,000 zimetengwa kwa ajili ya Kuimarisha
uzalishaji wa mpunga. Kamati yangu inaipongeza sana Wizara kwa kutenga
fedha maalum kwa ajili ya kuzalishaji mpunga, na kama tunavyofahamu kuwa
chakula kikuu kwa wananchi wa Zanzibar ni wali ambao unatokana na mpunga.
Kamati yangu inaiomba sana Serikali iipatie Wizara fedha hizo huku ikizingatia
kuwa mabonde yetu tuliyonayo yatumike ipasavyo na kwa utaalamu ili tuzalishe
mpunga kwa wingi na tupunguze kuagiza mchele kutoka nje ya nchi.
Mheshimiwa
Spika, naomba nitoe angalizo kwa Serikali kuwa
katika miradi ya maendeleo iliyomo ndani ya Wizara hii ambapo jumla ya TZS 33,234,000,000/ zimetengwa kwa ajili ya kazi za
Maendeleo, katika fedha hizi za maendeleo TZS 1,068,000,000/ kutoka kwa
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na 32,168,000,000/ kutoka kwa washirika wa
maendeleo. Katika sekta hii muhimu fedha nyingi tumeziweka kwa washirika wa
maendeleo ambazo upatikanaji wake sio wa uhakika, kwa maana kuwa zikikosekana
hizo fedha miradi hii haitafanyika na kutokufanyika kwa miradi hii tutakuwa
tunazirudisha nyuma sana sekta hizi. Kwahiyo, kuna haja kwa Serikali kuingalia
miradi hii kwa jicho jengine ili tuhakikishe kuwa miradi inatekelezwa hata kama
fedha hizi hazikupatikana kutoka kwa washirika wa maendeleo.
HITIMISHO
Mheshimiwa Spika, Kamati ya Fedha, Biashara na Kilimo imeyakubali mapendekezo ya Makadirio ya Mapato na
Matumizi ya Wizara ya Kilimo,Maliasili, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017, na inawaomba
Waheshimiwa Wajumbe wako wote waijadili, watoe
mapendekezo yao na hatimae kuipitisha Bajeti hii muhimu. Pia Napenda kuwashukuru
Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza lako tukufu kwa kunisikiliza kwa makini na
utulivu wa hali ya juu wakati wote nilipokuwa nikiwasilisha hotuba hii.
Mheshimiwa
Spika, naomba kuwasilisha.
………………………….
Mhe.
Yussuf Hassan Iddi,
Mwenyekiti,
Kamati
ya Fedha, Biashara na Kilimo,
Baraza
la Wawakilishi,
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment