Habari za Punde

Waziri Castico Ameitaka Jamii Kutoa Masharikiano na Vijana Wanaotoka Sober House.

Na Miza Kona – Maelezo.
Waziri wa Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Vijana, Wanawake na Watoto  Moudline Castico ameitaka jamii kutoa mashirikiano kwa vijana wanatoka katika nyumba za kurekebisha tabia (Sober House) ili Vijana hao wasirudie  kutumiaji  dawa za kulevya.

Amesema sio jambo zuri  kuwabagua na kuwanyanyapaa  vijana hao kwa kuwatenga na kuwanyooshea vidole kwa kisingizio kuwa  ni wateja kwa vile wanahitaji msaada mkubwa  ili waenelee kubadilika   na  waweze kutoa mchango wao katika ujenzi wa Taifa.

Waziri Castico ameyasema hayo huko Chukwani katika Ukumbi wa Baraza la Wawakilishi wakati vijana hao walipotembelea Barazani hapo katika shamrashamra za kuadhimisha Siku ya kupambana na Dawa za Kulevya Duniani.

Amesema jamii isipokuwa tayari kuwapa ushirikiano  vijana hao wanaweza kupata madhara makubwa na kurejea tena katika kutumia dawa hizo.   
Amewapongeza vijana hao pamoja na Tume ya Taifa ya Kuratibu na Kudhibiti  Dawa za Kulevya kwa juhudi kubwa wanazochukuwa  katika  kuwasaidia kuwajenga katika maadili mema.

Nae Mwakilishi wa Jimbo la Welezo Hassan Khamis Hafidh amesema dawa za kulevya ni janga la taifa hivyo jamii inapaswa  kuwafichua wafanyabiashara wanaoingiza na kusambaza dawa hizo bila ya woga na kuhakikisha kuwa wanachukuliwa hatua za kisheria.

Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Kuratibu na Kudhibiti dawa za kulevya Bi. Kheriyangu Khamis ameomba kupatiwa  eneo la kufanyia kazi vijana hao  kwa vile hivi sasa ni wajasiriamali wenye vipaji  tofauti na wanaweza kufanya shughuli za kujikimu kimaisha.

Nao vijana hao wameiomba jamii iwakubali na kuwapa  mashirikiano  na kuacha tabia ya kuwanyanyapaa kutokana hali waliyokuwa nayo  awali kwani tayari wameshabadilika na wapo tayari kuisadia jamii kupiga vita janga hilo lisiendelee kuathiri  vijana.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.