Habari za Punde

Miswada minne kujadiliwa kikao kijacho cha BLW



TAARIFA  KWA VYOMBO VYA HABARI.       
Ndugu, Waandishi wa Habari.
Kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kutujaalia uzima, afya njema na utulivu na pia kutuwezesha kutekeleza majukumu yetu  ya kila siku.

Pili, nikushukuruni sana ndugu waandishi wa habari kwa kazi nzuri mnayoifanya ya kuwapasha habari wananchi juu ya masuala mbali mbali  katika jamii yetu ikiwemo kazi na majukumu ya Baraza la Wawakilishi.

Pia  napenda kuwashukuru sana kwa mashirikiano mazuri  mliyonayo kwetu. Baraza la Wawawakilishi linakupongezeni sana na kuwaomba muendelea kuwa karibu na Ofisi yetu ili kuwafahamisha wananchi habari mbali mbali zinazohusiana na Baraza lao tukufu.

Ndugu Waandishi wa Habari, Baraza la Wawakilishi linachukua hatua mbali mbali katika kuhakikisha kunakuwa na ushiriki mkubwa zaidi wa wananchi hasa katika mchakato wa utungaji wa Sheria za nchi yetu. Miongoni mwa hatua hizo ni kurekebishwa kwa kanuni  zetu na hatimae kuelekeza   miswada kusomwa kwa mara ya kwanza katika Mkutano mmoja na baadae kujadiliwa na kupitishwa katika Mkutano wa Baraza unaofuatia ili kutoa fursa ya kutosha kwa wananchi kushiriki katika kutoa maoni yao. Kufuatia mabadiliko hayo, Kanuni inaelekeza baada ya miswada hiyo kusomwa mara ya kwanza itangazwe kwa wananchi ili waifahamu miswada hiyo na waweze kushiriki kutoa maoni yao mbali mbali.

Ni matarajio yetu kuwa maoni yatakayotolewa na wananchi, kwa kiasi kikubwa yatazisaidia Kamati zitakazoichambua miswada hiyo ili kuifanya miswada hiyo kuwa bora zaidi na hatimaye kupata sheria zitakazozingatia kwa upana zaidi maslahi ya wananchi.

Ndugu Waandishi wa Habari, Katika Mkutano wa Tatu wa wa Baraza la Tisa la Wawakilishi unaotarajiwa  kuanzia mwishoni mwa mwezi ujao  miswada minne ambayo tayari ilisomwa kwa mara ya Kwanza katika Mkutano uliopita itajadiliwa, miswada yenyewe ni kama ifuatayo;-

1.     MSWADA WA SHERIA YA (UTAFUTAJI NA UCHIMBAJI) MAFUTA NA GESI ASILIA, 2016. Mswada huu pamoja na mambo mengine utakuwa na lengo la kuanzisha Kampuni ya Maendeleo ya Mafuta na Gesi Asilia Zanzibar (ZPDC) ambayo itashiriki katika shughuli za utafutaji na uendelezaji wa Mafuta na Gesi Asilia kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

2.    MSWADA WA SHERIA YA MAREKEBISHO YA SHERIA YA SUZA  NA MAMBO MENGINE YANAYOHUSIANA NA HAYO. Mswada huu una lengo la kuunganisha Taasisi ya Uongozi wa Fedha (ZIFA), Taasisi ya Maendeleo ya Utalii (ZIToD) na Chuo cha Sayansi ya Afya (CHS) kuwa chini ya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA).

3.    MSWADA WA SHERIA YA KUANZISHA TAASISI YA ELIMU YA ZANZIBAR NA MAMBO MENGINE YANAYOHUSIANA NA HAYO. Mswada huu unalenga kupendekeza kuanzishwa kwa Taasisi ya Elimu Zanzibar, ambayo itakuwa ni wakala wa Serikali na itakuwa na jukumu la kuandaa mitaala, vifaa vya kufundishia, kufanya tafiti za elimu zinazohusiana na maendeleo ya mitaala na kuimarisha vifaa vya kujifunzia ili kuhakikisha utoaji wa elimu kwa wananchi.

4.    MSWADA WA SHERIA YA MAREKEBISHO YA SHERIA MBALI MBALI NA MAMBO MENGINE YANAYOHUSIANA NA HAYO. Mswada huu unarekebisha baadhi ya vifungu vya Sheria; zikiwemo Sheria ya Mahusiano Kazini, Sheria ya Mahkama za Mahakimu, Sheria ya Mahkama ya Biashara, Sheria ya Madawa na Usambazaji Haramu wa Madawa ya Kulevya, Sheria ya Mashirikiano baina ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi, Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma, Sheria ya Biashara, Sheria ya Chuo Kikuu cha Kilimo Kizimbani na Sheria ya Mfuko wa Maendeleo ya Jimbo. Marekebisho hayo yanayopendekezwa katika Sheria hizo ni kwa ajili ya kufanya marekebisho ya makosa yaliyomo katika Sheria hizo na vile vile kuweka masharti bora ili kwenda sambamba  na malengo  ya kuwepo kwa Sheria husika.

Ndugu  waandishi wa Habari,  katika kuhakikisha kwamba wananchi wanapata fursa  na kushiriki  katika Shughuli hii ya utungaji wa Sheria, Afisi ya baraza la wawakilishi inawaomba  watume maoni yao kwa  kwa Katibu wa Baraza la Wawakilishi kwa njia ya maandishi kabla ya tarehe 9/9/2016.





Aidha, nakala za miswada hiyo zinapatikana katika Afisi ya Katibu wa Baraza la Wawakilishi na hivyo kila mwananchi atakayependa, anaweza kuomba kupatiwa nakala hizo.




Maoni yatumwe kupitia anauni zifuatazo:-
1.     Sanduku la Posta (S.L.P. 902, Zanzibar)
2.    Barua pepe (zahore@zanlink.co au
3.    Yaletwe Afisi ya Baraza iliyopo Chukwani
1.     Afisi ndogo ya Baraza la Wawakilishi – Wete Pemba .

Mwisho kabisa napenda kuwashukuruni tena Ndugu Waandishi wa Habari wa mashirikiano yenu mnayoendelea kutupa katika kuwapasha habari wananchi.

Ahsanteni sana kwa kuniskiliza.

……………………
Amour M Amour,
Kny: KATIBU,
BARAZA LA WAWAKILISHI,
ZANZIBAR.
Tarehe 17/8/2016




No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.