Habari za Punde

Pereira: Nitapambana na waliopandikizwa kupanga safu katika uchaguzi wa CCM

  Katibu wa NEC,  Idara ya Organazesheni CCM Taifa, Nd. Pereira Ame Silima akisalimiana na Mwenyekiti wa CCM  Mkoa wa Kusini Ungujakichama, Ramadhan  Abdallah  Ali “ Kichupa”  mara baada ya kuwasili katika Ofisi za  Mkoa huo zilizopo Dunga  Wilaya ya Kati Unguja.
 atibu wa NEC,  Idara ya Organazesheni CCM Taifa, Nd. Pereira Ame Silima akitoa nasaha kwa viongozi wa CCM Mkoa na Wilaya za Kusini na Kati Kichama katika ziara ya kiongozi huyo visiwani Zanzibar.
 Baadhi ya viongozi na Watendaji wa ngazi mbali mbali za Chama na jumuiya zake  Mkoa wa kusini na Wilaya zake kichama. ( PICHA NA AFISI KUU CCM ZANZIBAR).

NA IS-HAKA OMAR, ZANZIBAR.

CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimewataka viongozi na watendaji wa zamani wa ngazi za matawi waliowania tena nafasi za uongozi katika uchaguzi unaoendelea hivi sasa ndani ya chama hicho kutoshiriki kwenye vikao vya kuchuja na kujadili fomu za wagombea wa nafasi za uongozi.

Tahadhari hiyo imetolewa na Katibu wa NEC, Idara ya Organazesheni CCM Taifa, Nd. Pereira Ame Silima katika mwendelezo wa ziara yake huko Mkoa wa Kusini kichama Unguja, alisema mtu aliyewania nafasi ya uongozi ndani ya chama hicho hana haki ya kujadili na kuchuja fomu za wagombea wenzake kwani kufanya hivyo ni kinyume na Katiba ya Chama hicho.

Alisisitiza kwamba katika zoezi hilo ni lazima kila kiongozi asimamie taratibu za uchaguzi ili kuepuka malalamiko yasiyokuwa ya lazima.

“ Kuna baadhi ya matawi kumetokea changamoto za baadhi ya wagombea kujadili na kupitisha fomu za wagombea wenzao jambo ambalo ni kinyume na taratibu za Kikatiba hivyo hatuwezi kuvumilia vitendo hivyo ni bora uchaguzi urejewe katika maeneo yaliyoripotiwa ukiukaji wa miongozo yetu”, alisema Nd. Pereira.

Nd. Silima alisema dhamira ya chama hicho ni kuhakikisha chaguzi zote zitakazofanyika ndani ya chama na jumuiya kuhakikisha wanapatikana viongozi bora waliopatikana kwa mujibu wa matakwa ya Kikatiba na sio watu binafsi.

Katibu huyo aliweka wazi msimamo wake kwamba atapambana  vikali na baadhi ya watu waliopandikizwa katika uchaguzi huo ili wapange safu na makundi ya viongozi wanaowataka wao kwa baadhi ya ngazi za uongozi .

Aidha  aliwasihi viongozi hao kumpa ushirikiano wakati wa utekelezaji wa majukumu ya kiutendaji hasa katika jukumu la kufanikisha uchaguzi unaoendelea na kuhakikisha unakamilika kwa kiwango kilichokusudiwa.

“  Lengo la ziara yangu ni kujitambulisha kwenu kwani toka nilipoteuliwa sijawahi kuja kwenu kubadilishana mawazo  pia naomba ushirikiano katika Idara yangu ya organazesheni ambayo jukumu lake la msingi ni kusimamia  shughuli zote za chaguzi za chama na dola pamoja na masuala ya takwimu za wanachama.”, alisema Silima.

Akiwasilisha  taarifa ya maendeleo ya uchaguzi  wa chama hicho kwa ngazi za Matawi, Kaimu Katibu wa Wilaya ya Kusini Kichama Unguja, Hafidh Hassan Mkadam  alieleza kuwa changamoto iliyojitokeza katika zoezi hilo ni baadhi ya Viongozi wa ngazi husika kufanya uteuzi bila ya kuzingatia kanuni ya uchaguzi na katiba ya CCM, hali iliyopelekea baadhi ya matawi kurejea zozezi hilo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.