Habari za Punde

Ustadhi atuhumiwa kumbaka mwanafunzi wa miaka kumi nne, ampa ujazito


  Na Khadija Kombo--ZBC.Pemba

Jeshi la Polisi  Mkoa wa kusini Pemba, linamshikilia  Ustaadhi wa Madrasa ya msikiti wa Ijumaa Miembeni  Chake Chake Kisiwani Pemba, Khamis Rashid Ali (35), mkaazi  wa mvumoni   Chake Chake  kwa tuhuma za kumbaka   mwanafunzi wake mwenye umri wa miaka kumi nanne  (14) na kumsababishia ujauzito hali  ambayo imempelekea kumuathiri mtoto huyo kimwili  na  kisaikolojia.

Akizungumza na mwandishi wa habari hizi,  Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kusini Pemba (RPC) ,Mohammed Sheikhan Mohammed    alithibitisha kukamatwa  kwa mtuhumiwa huyo   kwa tuhuma za kumbaka na kumpatiaujauzito mtoto mdogo (14)   hivi sasa Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi na utakapo kamilika  watamfikisha mahakamani  kwa kujibu tuhuma hizo.

Kamanda Sheikhan, alisema mara baada ya kupata tuhuma hizo walimchukua mtoto huyo  na kumpeleka  Hospitali  kupimwa na vipimo vilionesha  kuwa mtoto anaujauzito wa miezi saba na siku tano.

Bibi wa mtoto huyo ambae ni wa mwanzo kugundua   tukio hilo ambae jina lake limehifadhiwa, alisema alipelekewa mtoto huyo na mama yake mzazi kwa lengo la kukaa nae  kwa kipindi cha wiki mmoja kutokana na mama huyo  kupata dharua na kusafiri.

"Kwa vile huyu alikuwa ni mtoto wa kike anahitaji kuwa chini ya uangalifu wa mtu wakati wote ndio akaona amlete huku kwangu lakini ahh, kumbe mtoto alishakuwa na mtihani" alisema bibi huyo.

Akielezea kwa masikitiko bibi huyo, alisema   aligundua tukio hilo baada ya mtoto wake mwengine  alieona hali ya  mabadiliko ya dada yake huyo na kumuuliza  juu ya hali  hio.

"Mama vipi mbona huyu dada tumbo lake limekuwa kubwa na hakuwa na tumbo kama hili  na mimi ndipo niliposhituka nikaanza kumchunguza kwa makini" alielezea  bibi huyo.

Bibi huyo, aliendelea kufahamisha kwamba baada ya uchunguzi aligundua mambo mengi kwani mbali ya kukua kwa tumbo lakini pia hata nguo zake kifuani zilikuwa zikimbana sana  tofauti na ilivyokuwa hapo awali.

"Baada ya kuona hayo moja kwa moja nilianza kuyatia watuni na ndipo alipopelekwa hospitali na kugundulika kuwa ana ujauzito wa miezi saba",alieleza bibi huyo.

Alipoulizwa na mwandishi wetu  kuhusu  ninani aliyempa ujauzito bibi huyo alisema  mtoto mwenyewe alipohojiwa alisema  aliyempa ujauzito huo  ni mwalimu wake wa madrasa  na akamtaja kuwa ni mwalimu Khamis Rashid.

Akizungumza kwa huzuni huku machozi yakimtoka  mtoto huyo  alisema Ustadh huyo alimbaka ndani ya Ofisi ya  madrasa  ambayo imo ndani ya Msikiti wa Ijumaa Miembeni Chake Chake.

"Ilikuwa ni mwezi wa pili mwaka huu, ustadh alituita  Ofisini tukaandike kombe  kila mmoja alikuwa anaandika na anae maliza anatoka nje mimi nikawa wa mwisho kumaliza  hivyo aliukomea mlango  kisha akaniambia ananipenda  nikamwambia mwalimu  sitaki mimi ni mtoto mdogo hakuniachia ndipo aliponibaka" alieleza mtoto huyo.

Mama mzazi wa mtoto huyo, ambae  alikuwa akizungumza huku akikata chozi alisema  kwamba yeye  hakujua kabisa  kama mtoto wake anaujauzito  tukio ambalo limemuathiri sana moyoni mwake.

"Mtoto wangu ni mdogo sana kiumri na kimaumbile  hivyo kila nikifikiri na mtihani uliompata ni mzito kwake naendelea kuteketea" alisikitika mama huyo.

Hivyo alisema  wakati wote  alikuwa akiwaangalia sana watoto wake  wa kike na wakiume kutokana na kuhofia hayo hayo ndipo alipopata  safari akaamua kumpeleka kwa  bibi yake lakini kumbe kule madrasa alikofikiria kuwa ni sehemu salama ndiko alikofikwa na janga mtoto wake .

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.