Habari za Punde

Waziri wa Afya atembelea na kukagua ujenzi wa vituo vipya vya afya vya mradi wa ORIO

 Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo akizungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Rans Nassor Salim Khamis inayojenga vituo 15 vya afya vya Mradi wa Orio alipotembelea kituo cha Kiboje wa pili (kulia) Meneja Ujenzi wa Kampuni ya Rans Ali Nassor.

 Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo akitembelea ujenzi wa kituo kipya cha afya Kiboje akiambatana na Mkuu wa Wilaya ya Kati Mashavu Sukwa (kushoto) meneja wa Ujenzi wa Kampuni ya Rans Ali Nassor.

 Meneja wa Ujenzi wa Kampuni ya Rans Ali Nassor akimpa  maelezo Waziri wa Afya juu ya ukarabati wa kituo cha afya cha Uroa alipofanya ziara ya kutembelea vituo vya Mradi wa Orio.
 Muonekano wa kituo kipya cha afya cha Kijini Matemwe kinachojengwa kwa ushirikiano wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali ya Uholanzi kupitia Mradi wa Orio.

 Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Kijini Matemwe baadaya kuangalia maendeleo ya ujenzi wa kituo kipya cha afya cha kijiji hicho.
Mafundi wa Kampuni ya Rans wakiendelea na ujenzi katika kituo kipya cha afya cha Chaani kubwa Wilaya Kaskazini A.
Picha na Makame Mshenga.


Na Ramadhani Ali – Maelezo                       
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inaendeleza  dhamira yake ya kuleta mabadiliko makubwa katika sekta ya afya kwa kuimaisha huduma za afya na kujenga vituo vyenye hadhi vijijini.
Dhamira hiyo  inaendelea kutekelezwa kwa pamoja na wafadhili wa maendeleo wanaunga mkono juhudi zinazochukuliwa na Serikali katika kufikiaq malengo hayo.
Waziri wa Afya Mahmoud Thabit Kombo ameeleza hayo alipotembelea vituo vitatu vipya vya afya vya Kiboje, Kijini Matemwe na Chaani kubwa na kituo cha Uroa kinachofanyiwa ukarabati mkubwa.
Amesema serikali ya Uholanzi kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia mradi wa Orio hivi sasa unaendelea na ujenzi wa vituo 15 vya afya nane vikiwa vinajengwa Unguja.
Waziri Mahmoud aliwaeleza wananachi wa sehemu hizo kuwa  lengo la kujengwa vituo hivyo nikuwasogezea huduma za afya  karibu na sehemu wanazoishi na kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Hospitali kuu za mijin
Amewahakikishia wananchi kuwa vituo vinavyojengwa kupitia mradi wa Urio vitakapomalizika vitakuwa na vifaa vya kisasa na vitatoa huduma zote muhimu zikiwemo wodi za kujifungulia.
Aliongeza kuwa Wizaara ya Afya inajiandaa kuhakikisha kuwa vituo vyote vinavyojengwa vinakuwa na wafanyakazi wa fani zote muhiumu ili kuwapunguzia shida.
“Wananchi wa Kijini kituo chenu  ambacho ni cha daraja la pili kitakapomalizika  kitatoa huduma zote muhimu na wagonjwa watatoka mjini kuja kutafuta matibabu hapa,”Waziri aliwahakikishia.
Amewataka wananchi wanaoishi karibu na vituo hivyo vitakapomalizika kuvitumia kikamilifu ili kuwapunguzi gharama za kufuata huduma ya matibabu Hospitali kuu ya Mnazimmoja.
Hata hivyo amewaomba akinababa wa Kijini na Chaani kushirikiana na wake zao katika kupanga uzazi kwani kiwango cha kuzaa katika maeneo hayo kimekuwa kikubwa.
“Kama hamtashirikiana baba na mama katika kupanga uzazi itafika wakati kitanda kimoja kitakuwa na wazazi wanne jambo ambalo halipendezi,” aliwatanabahisha Waziri wa Afya .
Aliwataka vijana kushirikiana na wazee katika kuvilinda na kuvitunza  vituo hivyo vya afya wakijua kuwa ni mali yao na vinahitaji kukaa muda mrefu kutoa huduma.
Mkurugenzi Kinga na Elimu ya Afya Dkt. Fadhil Mohamed aliwaeleza wananchi kuwa vituo vyote vya afya vya daraja la pili  vitakuwa na  nyumba ya daktari na vitatoa  huduma za uzazi kwa saa 24.
Dkt. Fadhil alisema huduma nyengine za kawaida zitatolewa katika muda wa kawaida wa kazi na akitokea mgonjwa wa  dharura baada ya saa za kazi atahudumiwa.
Meneja wa ujenzi wa vituo hivyo Ali Nassor Al Miskry wa Kampuni ya Rans amemuhakikishia Waziri wa Afya kuwa ujenzi wa vituo hivyo utakamilika mwezi Disemba na Januari mwakani vitaanza kutumika.
Alisema vifaa vitakavyotumika katika  vimeshapakiwa katika meli na vinatarajiwa kuwasili mwisho wa mwezi wa kumi na kazi ya kuvifunga zitafanyika mara baada ya ujenzi kukamilika.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.