Habari za Punde

Egypt Air karibuni kuanza kutua Zanzibar


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                                    19.04.2018
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameipongeza azma ya Shirika la Ndege la Misri (Egyptair) ya kuanzisha safari zake kati ya Misri na Zanzibar hatua ambayo itakuza uchumi na kuimarisha sekta ya utalii hapa nchini.

Dk. Shein aliyasema hayo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Makamo wa Rais wa Shirika la Ndege la Misri (Egyptair) Mohamed Alabbady, aliyefuatana na Balozi wa Tanzania nchini Misri Meja Jenarali Issa Suleiman Nassor pamoja na Maafisa wa Shirika hilo na kumueleza jinsi Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ilivyoipokea kwa mikono miwili azma hiyo.

Rais Dk. Shein  alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iko tayari kutoa ushirikiano wake mkubwa kwa Shirika hilo la ndege la Misri (Egyptair), kama inavyoendelea kutoa kwa mashirikia mengine makubwa ambayo tayari yanafanya safari zake na Zanzibar likiwemo Shrika la Ndege la Qatar, Ethiopia, Kenya, Afrika Kusini, Uturuki, Oman, Izrail, Ukraine na Mashirikika mengine kutoka nchi kadhaa duniani.

Aliongeza kuwa kuanzishwa kwa safari za ndege kati ya Misri na Zanzibar pia, kutaimarisha sekta ya utalii hapa Zanzibar, sekta ambayo imeleta mafanikio makubwa katika kukuza uchumi wa nchi ambapo inachangia pato la taifa kwa asilimia 20 na asilimia 80 za fedha za kigeni.

Dk. Shein alieleza kuwa mbali ya kuimarika kwa sekta ya utalii hapa Zanzibar pia, kuanza kwa safari kwa Shirika hilo kutasaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha sekta ya biashara kati ya pande mbili hizo sambamba na kuwaweka karibu wananchi wa Afrika Kaskazini na Afrika ya Mashariki.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza jinsi ya mashirika kadhaa ya ndege duniani ambayo  yameonesha dalili za kutaka kuanza safari zake hapa Zanzibar likiwemo Shirika la ndege la Abudhabi la Etihad na Shirika la ndege la Arabia (Air Arabian) la Sharjah.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alisisitiza kuwa hatua ya shirika hilo kuonesha azma yake hiyo kutaimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya Zanzibar na Misri ambapo nchi hiyo iliweza kuiunga mkono Zanzibar katika sekta za maendeleo ikiwemo sekta ya afya, kilimo, habari na elimu.

Pamoja na hayo, Rais Dk. Shein alimueleza Makamo huyo wa Rais wa Shirika la Ndege la Misri (Egyptair) juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuhakikisha huduma za uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume zinaimarika ikiwa ni pamoja na kuendeleza ujenzi wa jengo jipya la abiria katika uwanja huo wa ndege.

Mapema, Makamo wa Rais wa Shirika la Ndege la Misri (Egyptair) Mohamed Alabbady alimueleza Rais Dk. Shein azma ya Shirika hilo ya kuanza safari zake za ndege kati ya Misri na Zanzibar.

Makamo huyo wa Rais wa Shirika la Ndege la Misri alimueleza Rais Dk. Shein kuwa tayari Shirika hilo limeshatoa uwamuzi wake huo na limo katika mchakato wa mwisho katika kuhakikisha safari hizo za ndege zinaanza haraka iwezekanavyo.

Alabbady alieleza kuwa anaamini uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu uliopo kati ya Misri na Zanzibar utaimarika kwa kiasi kikubwa baada ya kuanza kwa safari za ndege za Shirika hilo sambamba na kutoa fursa zaidi kwa wananchi wa pande mbili hizo kutembeleana.

Aidha, Makamo huyo wa Rais wa Shirika la Ndege la Misri alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa kuanza kwa safari za ndege za (Egyptair) kutaimarisha sekta ya utalii hapa Zanzibar kutokana Zanzibar kuwa na vivutio vingi vinavyowavutia watalii ambavyo maeneo mengine duniani havipo.

Pia, aliongeza kuwa watalii kutoka nchini Misri nao pia, watapata fursa za kuja Zanzibar kiurahisi baada ya kurahisishwa safari za ndege na Shirika hilo ambalo lina hamu kubwa ya kushirikiana na Zanzibar katika kuhakikisha sekta ya mawasiliano zikiwemo safari za ndege kupitia Shirika hilo kati ya pande mbili hizo zinaimarika.

Sambamba na hayo, kiongozi huyo alitoa pongezi kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara yake ya Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji pamoja na Ofisi ya Ubalozi wa Tanzania nchini Misri kwa mashirikiano mazuri aliyoyapata hatua ambayo imeweza kurahisisha kwa kiasi kikubwa azma ya Shirika hilo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.