Na Jeshi la Polisi
Timu ya Migomba
kutoka Wilayani Rufiji mkoani Pwani wametawazwa kuwa mabingwa wa kombe la Mkuu
wa Jeshi la Polisi nchini IGP Simon Sirro (Sirro Cup 2018 Kibiti) baada ya
kuichapa timu ya Mjawa ya Wilayani Kibiti kwa mikwaju ya penati 12-11 katika
fainali iliyopigwa katika uwanja wa Samora Kibiti.
Mchezo huo ulikuwa
mkali kwa dakika zote tisini ambapo kila timu ilijitahidi kutafuta nafasi
lakini mpaka dakika tisini zinakamilika hakuna timu iliyoweza kuona nyavu za
timu pinzani na hivyo kuamuriwa kupigwa kwa mikwaju hiyo iliyopelekea Migomba
kuibuka mabingwa.
Kutokana na ushindi
huo Migomba walikabidhiwa kombe, pesa taslimu shilingi milioni moja na seti
moja ya jezi huku Mjawa wakipata fedha taslimu laki tano na seti moja ya jezi
wakati mshindi wa tatu timu ya Mipeko alipata fedha taslimu laki tatu na seti
moja ya jezi.
Akizungumza baada ya
kuwakabidhi zawadi mabingwa hao, Mkuu wa Mkoa wa Pwani amemuomba IGP Simon
Sirro kuendelea kuandaa kombe hilo kwa kuwa limesaidia kuinua vipaji vya vijana
wa Wilaya za Mkuranga, Kibiti na Rufiji na kuimarisha usalama kupitia michezo.
“Bila usalama
tusingekuwepo leo hii hapa, hivyo nawaasa kuendelea kutoa taarifa za uhalifu
ili zifanyiwe kazi kwa maana bila usalama hii burudani tusingeiona hapa na
namuomba IGP mwakani tena afanye hivi hivi” Alisema Ndikilo.
Kwa Upande wake Mkuu
wa Kitengo cha Michezo ndani ya Jeshi la Polisi Kamishna
Msaidizi wa Polisi (ACP)
Philip Kalangi alisema jumla ya timu 52 kutoka Wilaya za Mkuranga, Kibiti na
Rufiji zilishiriki michezo hiyo iliyobeba kauli mbiu ya Kibiti Salama, Jamii
Salama ikiwa na lengo la kuwakutanisha wakazi wa maeneo hayo kupitia michezo na
kupiga vita uhalifu.
Kalangi alisema
Programu hiyo ya michezo inafanywa pia katika mikoa mbalimbali kupitia kwa
Wakuu wa Polisi wa Mikoa na Wakuu wa Polisi wa Wilaya na ni endelevu ili
kusaidia ushirikishwaji wa jamii katika mapambano dhidi ya uhalifu.
No comments:
Post a Comment