Habari za Punde

Alhaj Dk.Shein ameshiriki Futari iliyoandaliwa na PBZ BENKI


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein ameongoza futari maalum iliyoandaliwa na Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ) na kupongeza juhudi zinazoendelea kuchukuliwa na Benki hiyo katika kufikia malengo iliyojiwekea.

Hafla hiyo ya futari ilifanyika katika ukumbi wa Hoteli ya Verde Mtoni Mjini Zanzibar ambayo ilihudhuriwa na viongozi wa dini na Serikali, wateja na wanahisa wa Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ) pamoja na wananchi mbali mbali.

Akizungumza kwa niaba ya Rais wa Zanzibar, Mkuu wa Mkoa wa Mjini Magharibi Ayoub Mohamed Mahmoud alisema kuwa kujumuika kwa pamoja katika futari ni jambo jema na kutumia fursa hiyo kutoa shukurani kwa niaba ya waalikwa waliohudhuria katika futari hiyo adhimu.

Aidha, alieleza kuwa kufutari kwa pamoja ni sehemu ya utamaduni wa Wazanzibari wa kufutari kwa pamoja katika mwezi wa Ramadhani ambapo hapo zamani kwa mjini na mashamba kulikuwa na utamaduni huo ambao ulisaidia kuiweka jamii pamoja  sambamba na kuwasaidia wale waliokosa futari na wale ambao hawakuwa na sehemu ya kufutari.

Hivyo, aliiomba Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ) na Taasisi nyengine kuendelea na utamaduni huo ambao unakumbusha mambo ambayo yalikuwa yakifanywa hapo siku za nyuma ya kufutari kwa pamoja na kuweza kujenga uhusiano mwema na udugu.

Alieleza kuwa Rais Dk. Shein amefurahi kwa futari hiyo iliyoandaliwa na Benki ya (PBZ) pamoja na waalikwa wengine wote waliohudhuria katika futari hiyo.

Mapema Mkurugenzi Mwendeshaji Juma Ameir alieleza mafanikio yaliopatikana kutoka Benki hiyo na kusisitiza haja ya kuiimarisha Benki ya Kiislamu na kutumia fursa zilizopo kwa ajili ya kuendeleza miradi mbali mbali kwa wananchi na Serikali.

Alieleza kuwa kwa kipindi hichi hasa katika kuelekea uchumi wa viwanda Benki ya Kiislamu inaweza kusaidia kwa kiasi kikubwa kufikia lengo la uchumi huo ikiwa ni pamoja na kufanya mashirikiano na kueleza kuwa Benki hiyo milango yake iko wazi.

Alieleza kuwa mtaji wa Benki umeongezeka kutoka Bilioni 57 hadi kufikia Bilioni 71 ambapo faida kabla ya kodi imeongezeka kutoka Bilioni 18.7 hadi 21.8 ambapo faida baada ya kodi imefikia Bilioni 13.1 ikilinganishwa na mwaka 2016.

Nae Mjumbe wa Bodi ya Sheria ya Benki ya Kiislamu Abdalla Twalib akitoa shukurani kwa niaba ya wafanyakazi na uongozi wa (PBZ) kwa waalikwa wote waliohudhuria katika futari hiyo akiwemo Rais wa Zanzibar Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.