Habari za Punde

Hotuba ya kuakhirisha mkutano wa 10 wa Baraza la Wawakilishi uliojadili Bajeti ya Serikali


HOTUBA YA MAKAMU WA PILI WA RAIS WA ZANZIBAR, MHE. BALOZI SEIF ALI IDDI WAKATI WA KUTOA HOJA YA KUAKHIRISHA MKUTANO WA KUMI WA BARAZA LA TISA LA WAWAKILISHI ULIOJADILI BAJETI YA SERIKALI YA MAPINDUZI YA ZANZIBAR KWA MWAKA FEDHA 2018/2019 - TAREHE 29 JUNI, 2018


Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa hatuna budi kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu, Mwenye wingi wa rehma, Muumba mbingu na ardhi na vilivyomo ndani yake kwa kutujaalia uhai na afya njema na kutuwezesha kufanikisha Mkutano huu wa Kumi wa Baraza la Tisa ulioanza tarehe 09 Mei, 2018. Ninafuraha kuona kwamba shughuli zote zilizopangwa katika ratiba ya Mkutano huu zimekamilika kwa wakati na kwa ufanisi mkubwa wa kupigiwa mfano.

Mheshimiwa Spika, Kwa mara nyengine tena tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kuiweka nchi yetu katika hali ya amani, utulivu, umoja, upendo na mshikamano mkubwa miongoni mwa wananchi wetu. Hali hii imetuwezesha sisi viongozi na wananchi kutekeleza majukumu yetu ya kiuchumi na kijamii kwa ufanisi jambo ambalo limechangia kuimarisha uchumi na ustawi wa nchi yetu. Hivyo, sote hatuna budi kuhakikisha kuwa tunaisimamia, tunailinda na kuidumisha hali hii kwa mustakbali wa nchi yetu na wananchi wake.

Mheshimiwa Spika, kwa umuhimu na uzito wa kipekee napenda kumpongeza kwa dhati Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Ali Mohammed Shein, kwa miongozo yake mbali mbali ya busara na hekima anayoitoa kwetu inayotuwezesha kusimamia vyema majukumu tunayopangiwa ya kuiendesha Serikali yetu.  Kwa hakika, Dkt. Ali Mohamed Shein ni dira yetu ya matumaini katika kujenga uchumi imara ambao unaoimarika kila mwaka na kuleta tija kwa wananchi ambao unatokana na usimamizi na utekelezaji bora wa Ilani yetu ya CCM ya mwaka 2015 - 2020. Mafanikio haya tumeyapata kutokana na nia yake thabiti kwa wananchi wake.  Nampongeza sana Rais wetu kwa juhudi zake na kuona mbali katika kuiletea nchi yetu maendeleo endelevu.

Mheshimiwa Spika, vile vile, napenda kutoa pongezi zangu kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa namna anavyosimamia utekelezaji wa majukumu yake ya kuiongoza nchi yetu. Aidha, nampongeza kwa dhati namna anavyokisimamia na kukiongoza Chama chetu cha Mapinduzi na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  Sote ni mashuhuda wa jinsi alivyoweza kurudisha nidhamu ya utendaji kazi, kuondoa ubadhirifu wa mali za umma na kuwezesha wananchi wa Tanzania kufaidika kwa pamoja na rasilimali za nchi na kupata huduma za kijamii ipasavyo.  Hongera Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. 

Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii kukushukuru na kukupongeza wewe Mheshimiwa Spika pamoja na Naibu wako, Mhe. Mgeni Hassan Juma, Wenyeviti wa Baraza, Katibu wa Baraza na Watendaji wote wa Baraza la Wawakilishi kwa kuliendesha Baraza letu kwa umahiri na ufanisi mkubwa. Mmefanya kazi kubwa katika kipindi hiki cha Baraza la Bajeti ambalo lilikuwa na mambo mengi. Naamini busara zako pamoja na viongozi wenzako zimechangia kwa kiasi kikubwa kufanikisha mkutano huu ambao leo tunafikia tamati.

Mheshimiwa Spika, pia, napenda kuwashukuru Waheshimiwa Wajumbe wenzangu wa Baraza la Wawakilishi kwa kutumia haki yao ya Kikatiba na Kidemokrasia kwa kuchangia na kuuliza maswali mbali mbali ambayo Waheshimiwa Mawaziri na Manaibu Mawaziri wamejitahidi kuyapatia ufafanuzi wa kina. Nawashukuru sana Waheshimiwa Mawaziri na Manaibu Mawaziri kwa kazi mlioifanya ya kuwaelewesha Waheshimiwa Wajumbe na wananchi wetu kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, katika Mkutano huu wa Kumi wa Baraza la Tisa tulijadili na kupitisha Bajeti ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa mwaka wa fedha 2018/2019. Waheshimiwa Wajumbe walipata nafasi ya kuzichangia kwa umahiri, uweledi na uwazi bajeti zote za Kisekta na kuzipitisha.  Kadhalika, kwa umoja wetu tuliweza kuipitisha Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2018/2019, jambo ambalo litaiwezesha Serikali yetu kutekeleza mipango yake ya kimaendeleo iliyojipangia kwa ufanisi mkubwa.
Mheshimiwa Spika, napenda kutoa ombi langu kwa Waheshimiwa Wajumbe wenzangu pale mtakapogundua kuwa mipango tuliyoipanga katika Baraza letu hili Tukufu haiendi kama tulivyokubaliana naomba msisite kuishauri Serikali hata kabla ya muda wa kikao cha Baraza hakijafikia kwani kuna vikao vyetu halali ambavyo vina uwezo wa kuufanyia kazi ushauri huo.
Mheshimiwa Spika, Mkutano huu pia umejadili Miswada Miwili (2) na kuipitisha kuwa Sheria.  Miswada yenyewe ni:-

(i)                   Mswada wa Sheria ya Matumizi (Appropriation Bill); na
(ii)                  Mswada wa Sheria ya Fedha (Finance Bill).

Hata hivyo Miswada ifuatayo imesomwa kwa mara ya kwanza:-

(i)                   Mswada wa Sheria ya Wakala wa Uchapaji;
(ii)                  Mswada wa Sheria ya Usimamizi wa Mahkama;
(iii)                 Mswada wa Sheria ya kuanzisha Ofisi ya Ukaguzi wa Elimu Zanzibar.
 
Aidha, katika Mkutano huu jumla ya maswali ya msingi 279 na maswali ya nyongeza ....... yaliulizwa na kupatiwa ufafanuzi wa kina na Waheshimiwa Mawaziri. Kuna maswali mengine yaliyoahidiwa kujibiwa kwa maandishi kutokana na sababu mbali mbali.  Napenda kuwathibitishia Waheshimiwa Wajumbe kuwa maswali yote ya nyongeza ambayo yameahidiwa kujibiwa kwa maandishi, majibu yake yatafikishwa kwenu kwa muda muafaka.

Mheshimiwa Spika, hali ya upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama Zanzibar ni ya kuridhisha.  Upatikanaji wa maji umefikia asilimia 62 ya mahitaji ya wananchi. Bado kuna asilimia 38 ya wananchi wetu ambao wanaendelea kusumbuka na huduma ya maji safi na salama, hali hii inatokana na kuongezeka kwa idadi ya watu, uchakavu wa miundombinu ya maji na kuongezeka kwa shughuli za kiuchumi na kijamii mijini na vijijini kunakopelekea kutokuwepo kwa uwiano kati ya maji yanayozalishwa na mahitaji halisi. Ili kukabiliana na tatizo hilo, Serikali kupitia Mamlaka ya Maji (ZAWA) inaendelea kutekeleza miradi 7 ya maji chini ya Programu Kuu mbili ya Uhuishaji na Upanuzi wa Shughuli za Maji Mijini na Programu ya Usambazaji Maji Vijijini.  Programu hizo zina lengo la ujenzi wa matangi, ujenzi wa majengo ya mitambo ya kutibu maji, uchimbaji na uendelezaji wa visima, ulazaji wa mabomba mapya, kudhibiti upotevu wa maji pamoja na ukarabati wa miundombinu ya maji. Juhudi hizi zinafanywa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana na wananchi pamoja na Washirika wa Maendeleo.

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa wito kwa wananchi wanaopata huduma ya maji kuchangia huduma hii ili Serikali ipate nguvu ya kuendelea kutoa huduma kwa wananchi wengine wenye upungufu wa maji katika maeneo yao.  Sambamba na juhudi hizo, Serikali inaendelea kuwapatia maji wananchi wake wenye ukosefu wa huduma hii kupitia magari maalum ili kuwaondolea usumbufu wa kutafuta huduma ya maji safi na salama masafa marefu. Ninawaomba wananchi waendelee kuwa wastahamilivu kwa wale wanaopata usumbufu wa maji kwani Serikali inaendelea na juhudi za kulipatia ufumbuzi suala hilo. Sambamba na hilo, napenda kumpongeza Mkurugenzi Mkuu wa ZAWA, Ndugu Mussa Ramadhan Haji kwa juhudi yake ya kuwapatia maji safi na salama kwa kiwango kikubwa katika muda mfupi baada ya uteuzi wake.  Ni matumaini yangu kwamba utaziendeleza juhudi zake hizo.

Mheshimiwa Spika, suala la uuzaji wa ardhi bila ya kufuata sheria limekuwa likiibuwa mizozo mingi katika nchi yetu. Kwa bahati mbaya uuzaji huu wa ardhi umekuwa ukichangiwa na baadhi ya watendaji wa Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati na baadhi ya Masheha wetu. Jambo hili halikubaliki na wale wote wanaojishughulisha na vitendo hivi watachukuliwa hatua za kisheria.  Natoa agizo kwa Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya kuwafuatilia Masheha wanaoendeleza tamaa zao za kuuza maeneo ya ardhi bila ya kufuata sheria, hatua kali zichukuliwe licha ya kuachishwa Usheha.  
Ni vyema wananchi wakaelewa kuwa mara tu baada ya Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya Januari, 1964, ardhi yote imewekwa chini ya mamlaka ya Serikali, hivyo ardhi ni mali ya Serikali na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, ndie msimamizi mkuu. Kwa hivyo kuuza mali ya Serikali bila ya idhini yake tafsiri yake ni wizi wa mali ya umma. Natoa wito kwa wananchi wote kujiepusha na tabia ya kuuza ardhi kwani jambo hili ni kosa kisheria.  Hivyo, Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati ndio yenye mamlaka ya kuuza ardhi kisheria kwa idhini ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein na sio mtu au Taasisi nyengine yoyote nchini.

Mheshimiwa Spika, katika msimu uliopita wa mvua za Masika zilizoambatana na upepo mkali, Zanzibar kama sehemu nyengine za Afrika Mashariki ilikumbwa na mvua kubwa zilizosababisha athari mbali mbali ikiwa pamoja na vifo vya watoto wanne (4), uharibifu mkubwa wa miundombinu hasa barabara na makaazi ya watu. Katika kuwafariji wananchi wake, Serikali imetoa ubani kwa wafiwa na kuwasaidia baadhi ya wananchi waliopatwa na maafa kwa kuwapa msaada wa chakula pamoja na baadhi ya vifaa vya ujenzi.  Aidha, Serikali inaendelea na juhudi za kurekebisha athari zilizotokea hasa za ukarabati wa barabara katika maeneo mbali mbali nchini. 

Mheshimiwa Spika, napenda kuchukuwa fursa hii kutoa pole kwa wananchi wote waliopatwa na maafa katika maeneo mbali mbali ya visiwa vyetu Unguja na Pemba. Hata hivyo, kwa mara nyengine tena Serikali inaendelea kutoa wito kwa wananchi kujihadhari na majanga kwa kuepuka ujenzi holela pia kutokujenga katika maeneo hatarishi yakiwemo mabonde na njia asili za maji pamoja na kuepuka kulaza mabati katika nyumba zetu ili kupunguza maafa yanayosababishwa na mvua na upepo hapa visiwani kwetu.  Nawapongeza wananchi kwa juhudi za awali walizozichukua za kuzibua mashimo na kujenga mitaro ili kuepuka mkusanyiko wa maji na kuweza kupita kirahisi.  Hongereni sana wananchi kwa juhudi mlizozichukua.

Mheshimiwa Spika, kama tunavyojua kwamba vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa wanawake na watoto unaendelea kuwa kero kubwa katika jamii yetu. Ili kukabiliana na vitendo hivyo, Serikali imeandaa Mpango kazi wa Kitaifa wa Kupambana na Vitendo vya Ukatili na Udhalilishaji wa Wanawake na Watoto.  Mpango huu maalum wa miaka 5 (2017 - 2022) ambao utaongeza juhudi za kupambana na kadhia hii. Sambamba na mpango huo, Serikali imezifanyia marekebisho baadhi ya Sheria zinazohusiana na udhalilishaji na ukatili wa wanawake na watoto ikiwemo Sheria ya Makosa ya Jinai Nam. 6 ya mwaka 2018 na Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai ya Nam. 7 ya mwaka 2018, ili kuhakikisha kuwa watendaji wa makosa hayo wanapata adhabu inayostahiki ili kupunguza na kuyaondoa kabisa matendo hayo mabaya yanayotia aibu nchi yetu, pamoja na kutoa haki kwa waathirika wa vitendo vya udhalilishaji. Sheria hizo tayari zimeshasainiwa na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi ambazo zinatoa adhabu kali pamoja na kuondoa dhamana kwa watuhumiwa wa vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa kijinsia.
Mheshimiwa Spika, Sheria hizo zimeziongezea nguvu Mahkama za Wilaya na Mikoa za kuweza kutoa adhabu kali zaidi kwa waliotiwa hatiani. Waheshimiwa Wajumbe wenzangu, Taasisi zinazohusika, wazee, walezi na wananchi wote, napenda kuchukuwa fursa hii kutoa wito kwenu tuendelee kushirikiana kwa hali na mali katika kupambana na kadhia hii.  Aidha, nawanasihi wazee wenzangu kuwa linapotokea tukio la udhalilishaji katika familia zetu tuache tabia ya kumaliza masuala haya kienyeji na kuondoa muhali ili Sheria iweze kuchukua mkondo wake, vyenginevyo ni kudhoofisha juhudi za Serikali katika kupambana na vitendo hivyo.  Imani yangu kuwa tukishirikiana kwa pamoja suala la udhalilishaji litabakia kuwa historia, wananchi watakuwa na amani na vizazi vyetu vitajengeka kitabia na kuwa na maadili mema.  Naomba tushirikiane kwani “Umoja ni Nguvu na Umoja ni Ushindi”.
Napenda kuwakukumbusha wananchi maneno aliyosema Mheshimiwa Rais Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi wakati akilihutubia Baraza la Eid El Fitri tarehe 15 Juni, 2018, alisema:
Napenda kuwaasa wazazi na walezi kwamba linapotokezea kosa la udhalilishaji ambalo limefanywa na mtu wa familia, hatupaswi kabisa kulitolea hukumu au kulimaliza kifamilia.  Tunapoamua kuyamaliza matatizo haya kifamilia au kuchelea kutoa ushahidi sahihi katika vyombo vya sheria, inakuwa ni sawa na kudhoofisha jitihada za Serikali na kuyaendeleza maovu.”  Hivyo, nawasisitiza wananchi kuwa mtu yeyote ambae atamkingia kifua mdhalilishaji na yeye atachukuliwa kuwa ni mdhalilishaji na hatua kali dhidi yake zitachukuliwa.

Mheshimiwa Spika, katika kupambana na usafirishaji, uingizaji, usambazaji na utumiaji wa dawa za kulevya Zanzibar, Serikali kupitia Tume ya Kitaifa ya Kuratibu na Kudhibiti Dawa za Kulevya inaendelea na kazi ya kusimamia na kuratibu mapambano dhidi ya dawa hizo.  Pia, Tume inaratibu utekelezaji wa Sheria ya Dawa za Kulevya Zanzibar. Katika utekelezaji wake imefanya mafunzo kwa Mahakimu wa Mikoa na Wilaya za Mahkama za Zanzibar, Jeshi la Polisi, Waendesha Mashtaka, na Mamlaka ya   Kuzuia Rushwa na Uhujumu Uchumi juu ya Sheria ya Dawa za Kulevya ili waweze kuielewa na kuitekeleza ipasavyo Sheria hiyo. Aidha, Tume inaendelea kutoa elimu ya kinga dhidi ya matumizi ya dawa za kulevya kwa lengo la kuwaokoa vijana wetu na matumizi ya dawa hizi.  Vile vile, Tume inaendelea na utekelezaji wa Mpango wa tiba na marekebisho ya tabia kwa waathirika wa matumzi ya dawa za kulevya kwa kushirikiana na taasisi mbali mbali na jamii kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, Tume kwa kushirikiana na wadau wa udhibiti wa dawa za kulevya imeandaa mkakati wa kuhakikisha kuwa kesi zote za dawa za kulevya zinawasilishwa Mahkamani haraka ili kuhakikisha kwamba kesi hizo zinapata ufumbuzi wa haraka na kuepusha kuharibiwa kwa ushahidi.  Pia, Tume imeshaanza kazi ya uangamizaji wa dawa za kulevya pamoja na kuyafanyia kazi maeneo makorofi ya dawa za kulevya kwa kuliwezesha Jeshi la Polisi kushirikiana na Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa dhidi ya mapambano na kurudisha heshima ya nchi yetu.  Hata hivyo, juhudi za pamoja bado zinahitajika. Naiomba jamii isichoke tuendelee kutoa taaluma kwa vijana wetu juu ya athari za dawa hizo ili kuwaokoa vijana wetu ambao ndio nguvu kazi ya Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu Uchumi (ZAECA) inaendelea na kazi ya kuelimisha jamii juu ya athari za rushwa na uhujumu uchumi nchini. Mamlaka imetoa elimu kwa wananchi kupitia mikutano ya hadhara pamoja na Skuli tofauti za Unguja na Pemba, vipindi vya Redio na Televisheni pamoja na machapisho mbali mbali.  Vile vile, Mamlaka imefanikiwa kufunga mitambo kwa ajili ya programu ya kupiga simu namba ya bure ambayo ni 113. Madhumuni ya huduma hii ni kurahisisha kutoa taarifa ya vitendo vya rushwa na uhujumu Uchumi. Tayari mafanikio ya utumiaji programu ya kupiga simu yameanza kuonekana kwani wananchi wengi wamepata ari na utayari wa kuripoti matukio ya rushwa na uhujumu wa uchumi. Napenda kutoa wito kwa wananchi kuendelea kuitumia namba hii kuyaripoti matukio ya vitendo vya rushwa ili hatua za haraka ziweze kuchukuliwa. 

Mheshimiwa Spika, Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu Uchumi imezindua Mkakati Jumuishi wa Kitaifa wa Kuzuia Rushwa na Uhujumu wa Uchumi.  Lengo la Mkakati huu ni kuishirikisha jamii katika mapambano dhidi ya rushwa.  Sambamba na mkakati huo, Mamlaka inaendelea kufanya kazi ya udhibiti wa vitendo vya Rushwa na uhujumu wa uchumi katika Taasisi na Idara mbalimbali za Serikali. Udhibiti huo umepelekea Mamlaka kuokoa jumla ya Shilingi 169,028,120/=. Lengo la udhibiti huo ni kuweza kuzuia upotevu wa mapato ya Serikali na kupunguza vitendo vya Rushwa katika utoaji wa huduma kwa wananchi bila ya pingamizi zozote, na bila ubaguzi wa aina yoyote.

Mheshimiwa Spika, hali ya usalama barabarani nchini ni tishio kwa jamii kutokana na uendeshaji ovyo wa vyombo vya moto. Vijana wajulikanao kama T1 bado hawajadhibitiwa ipasavyo. Kadhalika alama za usalama barabarani bado hazijafuatwa na madereva walio wengi. Mambo yote haya yanachangia kwa kiasi kikubwa kutokea kwa ajali za mara kwa mara katika barabara zetu, jambo ambalo hupelekea kuwasababishia wananchi kupata ulemavu au vifo.  Kutokana na hali hiyo, Serikali hairidhishwi hata kidogo na hali ya usalama barabarani.

Mheshimiwa Spika, naliagiza Jeshi la Polisi na Idara zinazohusika na vyombo vya moto kushughulikia ipasavyo usalama wa barabarani kwa kufanya kazi zao kwa uadilifu ili kuokoa maisha ya wananchi wetu na vyombo vyao. Hivyo, madereva wote wahakikishe kuwa wanafuata sheria za usalama barabarani na kupunguza mwendo kasi katika maeneo ya makaazi ya watu yakiwemo skuli na hospitali ili watu wetu watembee barabarani wakiwa katika hali ya amani.  Inasisitizwa pia waendesha vyombo vya moto vya magurudumu mawili wafuate sheria ya kuvaa kofia ngumu ili kuokoa maisha yao pindipo wakipata ajali.  Kutokufanya hivyo ni kuvunja sheria.

Mheshimiwa Spika, itakumbukwa kuwa kila ifikapo tarehe 05 Juni ya kila mwaka huwa tunaadhimisha Siku ya Mazingira Duniani.   Kwa mwaka huu wa 2018, Kaulimbiu ya maadhimisho hayo ni “Pambana na Uchafuzi wa Mazingira kwa kukabiliana na takataka za Plastiki” (Beat Plastic Pollution). Katika kuadhimisha siku hii, Ofisi yangu kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali zimeanzisha Kampeni Maalum ya Usafi na Utunzaji wa Mazingira katika Skuli za Msingi na Sekondari kwa Unguja na Pemba.  Lengo kuu la kuanzisha kampeni hiyo ni kujenga utamaduni wa kutunza na kuhifadhi mazingira miongoni mwa watoto wetu tangu wakiwa wadogo kwani kama wasemavyo wahenga, ‘mtoto umleavyo ndivyo akuavyo’ na ‘udongo upate ulimaji‘.

Mheshimiwa Spika, napenda kuzipongeza Taasisi zote za Serikali na za watu binafsi pamoja na wananchi wote walioshiriki katika shughuli mbali mbali za uhifadhi wa mazingira kwa kufanya usafi na upandaji wa miti ikiwemo miche ya mikarafuu, matunda na viungo ambayo jumla ya miche 3,910,401 ilipandwa kwa Unguja na Pemba.

Mheshimiwa Spika, Kwa upande wa misitu, jumla ya hekta 116 za mashamba na hifadhi za Serikali zimepandwa miti katika msimu huu. Misitu ya jamii hekta 383, mashimo ya mchanga hekta 6 na kando mwa bahari hekta 56.   Haya ni mafanikio makubwa katika kuhifadhi mazingira yetu.  Hata hivyo, natoa wito kwa wananchi tuitunze miti hii iliyopandwa ili ikuwe na kuleta manufaa kwetu na vizazi vijavyo.

Mheshimiwa Spika, hali ya uzalishaji na upatikanaji wa chakula nchini imeendelea kuimarika katika msimu wa 2017/2018. Uzalishaji wa chakula kwa ujumla umefikia tani 357,932 ukilinganisha na mahitaji ya tani 583,651 ya chakula kwa sasa.  Kutokana na uzalishaji huo, hivi sasa Zanzibar inajitosheleza kwa chakula kwa asilimia 61 ukilinganisha na asilimia 42 iliyorekodiwa kwa mwaka 2016.  Mafanikio haya yanatokana na kuwepo kwa hali nzuri ya hewa iliyopelekea uzalishaji kuwa mzuri na kuimarika kwa mazao ya mpunga, muhogo, ndizi, viazi vitamu, mahindi, mboga na matunda. Kadhalika, Serikali inajitahidi kutoa ruzuku kwa wakulima kwa kushirikiana na Taasisi zisizo za Kiserikali katika kuunga mkono juhudi za kuongeza uzalishaji kwa kutoa taaluma ya kilimo cha kisasa na matumizi bora ya teknolojia ambayo yamechangia kwa kiwango kikubwa upatikanaji wa chakula cha kutosha nchini.

Mheshimiwa Spika, wakati wa uwasilishaji wa Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Waheshimiwa Wajumbe wameonyesha kutokuridhishwa kwao na kiwango cha ujenzi wa skuli za Serikali zilizojengwa na zinazoendelea kujengwa nchini. Serikali kwa upande wake imeridhia kuundwa kwa Kamati Teule ya kuchunguza suala hili. Naomba kuisisitiza Kamati hiyo kufanya kazi zake kwa uaminifu na uadilifu mkubwa kwa maslahi ya nchi yetu.  Pia, Serikali inaahidi kuifanyia kazi taarifa itakayowasilishwa na Kamati hiyo kwa kuwachukulia hatua za kisheria watu wote watakaobainika au watakaohusika na ubadhirifu au kadhia hiyo ya ujenzi huo wa kiwango cha chini ambao umeipotezea fedha nyingi Serikali yetu na kuhujumu uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, uchumi wa Zanzibar unaendelea kuimarika na kukua siku hadi siku, hali hii inatokana na ukusanyaji mzuri wa mapato na kuzuia uvujaji wa mianya ya mapato hayo, kama yalivyokwisha elezewa kwa ufasaha na undani na Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango. 

Mafanikio haya yameiwezesha Serikali kutekeleza majukumu yake kwa uhakika kama ilivyojipangia. Naamini kwamba, Bajeti ya mwaka 2018/2019 ambayo tumeipitisha hivi punde na kwa uongozi imara na mahiri wa Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein tutaitekeleza kwa asilimia mia moja na kuleta manufaa kwa wananchi wa nchi yetu.  Nia ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuondoa utegemezi katika Bajeti yetu.  Mengi yameelezwa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango wakati akiwasilisha hotuba ya Bajeti kwa mwaka wa fedha wa 2018/2019.

Mheshimiwa Spika, kwa mara nyengine tena napenda kuwashukuru wale wote waliotuwezesha kukamilisha shughuli zilizopangwa kwenye Mkutano huu kwa ufanisi mkubwa tukiwa katika hali ya amani, utulivu, upendo na mshikamano mkubwa.  Pongezi hizo pia ziwafikie watendaji wote wa Baraza hili la Wawakilishi wakiongozwa na Katibu wa Baraza, Ndugu Raya Issa Msellem.  Vile vile, nawapongeza Wakalimani wetu wa lugha ya alama ambao wamewawezesha Waheshimiwa Wawakilishi na wananchi wenye ulemavu wa kusikia kufuatilia yote yaliyokuwa yakiendelea ndani ya Baraza lako Tukufu.  Hali kadhalika, navishukuru vyombo vyote vya habari vilivyoshiriki kikamilifu katika mkutano huu kwa kuwapatia wananchi taarifa juu ya mwenendo mzima wa majadiliano ya Wajumbe yaliyokuwa yakiendelea hapa Barazani.

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia niwatakie Waheshimiwa Wawakilishi kila la kheri na mafanikio mema katika kuwatumikia wananchi wao Majimboni mwao na utekelezaji wa ahadi zao na Ilani ya CCM ya mwaka 2015 – 2020 kwa vitendo. Pia, nachukua nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukamilisha vyema funga ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, ambapo Mtume wetu Muhammad (SAW) alisema “mwanzo wa mwezi wa Ramadhani ni Rehma, katikati yake ni Msamaha na mwisho wake ni Kuachwa Huru na moto”, imani na mafunzo hayo yalipelekea kusherehekea Sikukuu ya Eid el Fitri kwa salama, amani na utulivu mkubwa.  Pia, tuliyojifunza katika mwezi huo Mtukufu wa Ramadhan tuendelee kuyatekeleza.  Huku tukimuomba Mwenyezi Mungu atuongoze katika njia iliyonyooka, njia ya wale walioneemeshwa sio ya wale waliokasirikiwa au ya wale walioghadhibikiwa na pia kuiendeleza amani na utulivu wa nchi yetu.  Aidha, ninawatakia Waheshimiwa Wajumbe wote safari njema na mrudi salama Majimboni mwenu na hasa wale Wajumbe wenzetu wanaokwenda Pemba.

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo, naomba sasa kwa heshima na taadhima kutoa hoja kwamba, Baraza lako Tukufu liahirishwe hadi siku ya Jumatano tarehe 19 Septemba, 2018 saa 3.00 barabara za asubuhi Mwenyezi Mungu akitujaalia.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.