Habari za Punde

Rais wa Zanzibar Dk Ali Mohamed Shein Ajumuika katika Iftari na Wananchi wa Mkanyageni Mkoa wa Kusini Pamba..


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, akisalimiana na Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh. Saleh Omar Kabi alipowasili katika viwanja vya Skuli ya Mkanyageni Mkoa wa Kusini Pemba kuhudhuria hafla ya Iftar ilioandaliwa na Rais wa Zanzibar kwa Wananchi wa Mkoa huo.


WANANCHI wa Mkanyageni, Mkoa wa Kusini Pemba wameeleza kuridhika kwao na uongozi wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk.Ali Mohamed Shein kutokana na kuwajali wananchi hatua ambayo imeipelekea  Zanzibar kuendelea kupata neema.

Hafla hiyo ya futari iliandaliwa na Alhaj Dk. Shein kwa ajili ya wananchi wa Mkanyageni ilifanyika katika viwanja vya skuli ya Mkanyageni, Mkoa wa Kusini Pemba ambayo ilihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa dini, vyama vya siasa, Serikali pamoja na wananchi wa Mkanyageni na vijiji vya jirani.

Mke wa Rais wa Zanzibar Mama Mwanamwema Shein nae aliungana pamoja na akiwa mama wenzake wa Mkanyageni katika futari hiyo pamoja na viongozi wanawake wa Kitaifa na wananchi wengine.

Akitoa neno la shukurani kwa niaba ya wananchi wa Mkanyageni, Maalim Abdalla Yussuf Ali alieleza kuwa uongozi wa Rais Dk. Shein umeonesha dhahiri kuwajali wananchi wa Zanzibar hatua ambayo imejenga mustakbali mwema katika kuimarisha maendeleo endelevu hapa nchini.

Maalim Abdalla alieleza kuwa Wananchi wa Mkanyageni wanakila sababu ya kujivunia uongozi wa Rais Dk. Shein kutokana na imani kubwa anayowaonesha wananchi wa Zanzibar hatua ambayo imeipelekea Zanzibar kuendelea kupata neema za Mwenyezi Mungu.

Wananachi hao walieleza kuwa kuridhika kwao si kwa futari tu aliyowaandalia ambao ni utamaduni aliouweka muda mrefu bali wameridhika na mambo mengi ya maendeleo anayoyafanya Rais Dk. Shein katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ambayo kila mmoja anayaona.


Aidha, wananchi hao walitumia fursa hiyo kumpongeza na kumshukuru Alhaj Dk. Shein kwa kuwaalika kwenye futari hiyo na kuweza kukaa nae pamoja huku wakitumia fursa hiyo kumuombea dua kwa Mwenyezi Mungu ili aendelee kuwa na hekima na busara katika uongozi wake.

Pamoja na hayo, wananchi hao walieleza kuwa uongozi wa Rais Dk. Shein umekuwa ukisisitiza umoja na mshikamano jambo ambalo na wao kwa upande wao wamekuwa wakilipa kipaumbele kwa kutambua umuhimu wake.

Nae Mkuu wa Mkoa Kusini Pemba Hemed Suleiman Abdalla akitoa neno la shukurani kwa wananchi hao kwa niaba ya Rais Dk. Shein aliwashukuru na kuwapongeza kwa kukubali muwaliko huo na kushiriki pamoja katika futari hiyo maalum aliyowaandalia.

Alitumia fursa hiyo kueleza fadhila za kufutarisha na kusisitiza haja ya kuendelea kumcha MwenyeziMungu hasa katika kipindi hichi cha mwezi Mtukufu wa Ramadhani..

Aidha, alieleza haja ya kuendelea kushikamana na kushirikiana na kupendana kwani wananchi wote wa Zanzibar ni wamoja na kila mmoja amekuwa akimtegemea mwenzake na kusisitiza kuwa umoja huo walioonesha katika futari hiyo ni vyema wakauendeleza pia, katika shughuli nyengine za maendeleo.

Sambamba na hayo, katika neno hilo la shukurani lililotolewa kwa niaba ya Rais Dk. Shein na Mkuu wa Mkoa huo lilieleza kuwa Alhaj Dk. Shein yuko tayari wakati wote kushirikiana na wananchi kwa kutambua kuwa ushirikiano ndio njia pekee ya kuimarisha maendeleo na kuleta umoja miongoni mwa wananchi.

Pia, kiongozi huyo alilieleza haja kwa wananchi kuendelea kuliombea Taifa ili lizidi kupata neema, baraka na kuimarisha amani na utulivu uliopo.

Alhaj Dk. Shein amemaliza ziara yake Kisiwani Pemba  iliyoanza Jumanne Juni 5 mwaka huu ambapo alianza kwa kuwafutarisha wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Pemba huko katika viwanja vya Ikulu ndogo Micheweni na siku ya tarehe 6 aliwafutarisha wananchi wa Mkoa wa Kusini Pemba katika Ikulu ndogo ya Chake Chake na anatarajiwa kuanza ziara kama hiyo katika Mikoa ya kisiwani cha Unguja.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.