Habari za Punde

Serikali Kutekeleza Miradi Kwa Kushirikiana na Sekta Sekta Binafsi Yenye Thamani ya Mabilioni ya Shilingi.

Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb), akifungua semina ya siku moja iliyowahusisha Mawaziri, Naibu Mawaziri na viongozi wengine waandamizi wa Serikali na Taasisi zake, kuhusu Ubia Sekta ya Umma na Binafsi (PPP), iliyofanyika katika ukumbi wa  Kambarage, Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dodoma.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na watu wenye Walemavu, Mhe. Jenista Mhagama (Mb), akuzungumza wakati akiahirisha semina ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP) yaliyoandaliwa na Wizara ya Fedha na Mipango kwa kushirikiana na Benki ya Dunia, Jijini Dodoma.
Mshauri wa Masuala ya Kisheria katika mradi wa Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP) kutoka Benki ya Dunia, Philip Kelly akiwasilisha mada katika semina ya siku moja ya  PPP, iliyofanyika katika ukumbi wa Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dodoma.
Waziri wa mambo ya Ndani ya Nchi, Mhe. Kangi Lugola (Mb) (kulia) akiwa na Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi -CCM (2015) wakati aliposhiriki semina ya Siku moja iliyohusisha Mawaziri, Naibu Mawaziri na viongozi wengine waandamizi wa Serikali na Taasisi zake, kuhusu Ubia Sekta ya Umma na Binafsi (PPP), iliyofanyika katika ukumbi wa  Kambarage, Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dodoma. Kushoto ni Naibu Waziri wa fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Ashatu Kijaji (Mb).
Baadhi ya Washiriki wa Semina ya siku moja iliyohusisha Mawaziri, Naibu Mawaziri na viongozi wengine waandamizi wa Serikali na Taasisi zake, wakifuatilia mada kuhusu Ubia Sekta ya Umma na Binafsi (PPP), iliyofanyika katika ukumbi wa  Kambarage, Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dodoma.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na watu wenye Walemavu, Mhe. Jenista Mhagama (Mb), (kushoto) akisoma makabrasha kuhusu Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP) yaliyoandaliwa na Wizara ya Fedha na Mipango kwa kushirikiana na Benki ya Dunia, Jijini Dodoma. kushoto kwake ni Naibu Waziri Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji Mhe. Mhandisi Stella Manyaya (Mb) na anayefuatiwa ni Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii Mhe. Japhet Hasunga.
 Mshauri wa Masuala ya Kisheria katika mradi wa Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP) Bw. Philip Kelly (katikati) akifafanua jambo wakati wa semina ya siku moja ya  PPP, iliyofanyika katika ukumbi wa Wizara ya Fedha na Mipango, Jijini Dodoma. Kushoto ni Mtaalamu wa Masuala ya PPP, Bw. Craig Sugden na kulia ni Bw. Abhijit Bhaumik, wote watatu wanatoka Benki ya Dunia.
Washiriki wakiwa katika picha ya pamoja baada ya kuahirishwa kwa Semina ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP) yaliyoandaliwa na Wizara ya Fedha na Mipango kwa kushirikiana na Benki ya Dunia,  yaliyohusisha Mawaziri na Manaibu waziri, Jijini Dodoma.

(Picha na Kitengo Cha Mawasiliano Serikalini-WFM)

Na. Benny Mwaipaja, WFM, Dodoma
Serikali ya Tanzania imepiga hatua kubwa katika kuanzisha 
na kutekeleza miradi mikubwa ya maendeleo kwa ubia kati 
ya Sekta ya Umma na  Binafsi (PPP) ambapo miradi  zaidi ya 
11 iko katika hatua mbalimbali za utekelezaji lengo likiwa 
ni  kufanikisha azma ya kuwa na uchumi wa viwanda.

Hayo yamesemwa na Kamishna wa Idara ya  Ubia Sekta ya 
Umma na Binafsi (PPP),  Wizara ya Fedha na Mipango, Dkt. 
John Mboya  wakati akiwasilisha mada ya utekelezaji wa 
dhana ya ushirikishwaji wa sekta binafsi katika miradi ya 
maendeleo nchini kwenye semina iliyowashirikisha 
mawaziri, naibu mawaziri na baadhi ya watendaji wa serikali 
iliyofanyika kwenye ukumbi wa Wizara ya Fedha na Mipango 
jijini Dodoma.

Akiwasilisha mada hiyo, Dkt. John Mboya amesisitiza 
umuhimu wa kuwepo kwa  umakini mkubwa katika uandaaji 
na utekelezaji wa dhana hiyo ya ubia Sekta ya Umma na 
Binafsi kwa kuzingatia sheria, sera, miongozo, kanuni na 
taratibu mbalimbali zilizopo.

Aidha alizitaka taasisi na wadau wa utekelezaji kuwa tayari 
kujifunza kutoka katika nchi zilizoendelea kupitia dhana hii 
ya ushirikikishwaji wa sekta binafsi katika kuchochea ukuaji 
wa viwanda na uchumi wa nchi kwa ujumla.

Dkt. Mboya aliitaja baadhi ya miradi iliyoko katika hatua 
mbalimbali ya utekelezwaji kwa Ubia kati  ya Sekta ya Umma 
na Binafsi kuwa ni  mradi wa mabasi yaendayo haraka 
(DART), Ujenzi wa Viwanda vya dawa, mradi wa VETA 
utakaohusisha ujenzi wa vyuo 10 ambavyo vinatarajiwa 
kutoa ujuzi mbalimbali kwa wanafunzi wapatao 90,000 ili 
kukidhi mahitaji ya wataalamu watakao saidia kufanikisha 
uchumi wa viwanda.

"MIradi Mingine ni Ujenzi wa Bandari ya Mwambani, 
barabara ya Dar es salaam hadi Chalinze, Ujenzi wa Reli 
kwenye miradi ya Mchuchuma hadi Mbambabay mikoa ya 
Kusini ya Lindi na Mtwara, Ujenzi wa Reli kuanzia Tanga, 
Arusha hadi Musoma, na  mradi wa umeme wa Chuo Kikuu 
cha Dodoma.

Akijibu swali la Naibu Waziri Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa 
na Serikali za Mitaa,   Josesph Kakunda, aliyetaka kujua 
kuhusu kuondolewa kwa sheria ya utekelezwaji  wa miradi 
kwa Ushirikishwaji wa Pamoja kati ya serikali na sekta 
binafsi (Joint Venture) ambayo haikufanikiwa kama 
ilivyokusudiwa hapo awali, Dkt. Mboya alisema kuwa sheria 
hiyo haijaondolewa bali miradi hiyo itatekelezwa kupitia 
sheria ya Kampuni.

Akichangia katika mjadala wa semina hiyo, Naibu Waziri wa 
Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Mhandisi Stella Manyanya, 
alisema ni vema wakati wa kuchagua miradi wahusika wawe 
makini ili kuepuka kuanzisha miradi inayofanana na ambayo 
inaweza kuwa chanzo cha kufa kwa miradi iliyotangulia.

"Ninashauri kuwepo kwa fursa ya ushirikishwaji katika 
miradi midogo ambayo ina manufaa kwa wananchi ikiwemo 
ya ujenzi wa nyumba za waalimu" Alisema Mhandisi 
Manyanya

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Abdallah Ulega, alizitaka 
taasisi ambazo zinatekeleza miradi kwa ubia na sekta binafsi 
zielezee umma wa watanzania mafanikio yaliyopatikana ili 
kuhamasisha wadau wengine kufuata nyayo hizo 
huku  akitolea mfano Shirika la Maendeleo ya Petroli  nchini 
(TPDC) ambalo nalo liko katika utekelezaji wa dhana hiyo.

Mwenyekiti wa semina hiyo  Naibu Waziri wa Fedha na 
Mipango, Dkt. Ashatu Kijaji, alisema kuwa Serikali 
imepeleka Muswada Bungeni unaohusu PPP, ambao 
ukipitishwa na Bunge linalotarajiwa kuanza Septemba 4, 
2018, utekelezaji wa ubia huo utakwenda kwa kasi zaidi ili 
kuiwezesha nchi kufikia malengo yake ya kukuza uchumi na 
kuleta maendeleo ya wananchi.

Kwa upande wake, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, 
Sera, Bunge , Kazi,Vijana, Ajira na Walemavu, Jenister 
Mhagama, akiahirisha mafunzo hayo, aliwataka wadau wa 
semina hiyo kuendelea kukutana na kuelimishana hadi hapo 
marekebisho ya sheria hiyo ya Ubia Sekta ya Umma na 
Binafsi (PPP) yatakapofanyika.

"Utekelezwaji wa dhana hii ya Ubia Sekta ya Umma na 
Binafsi ndio njia rahisi itakayosaidia kukamilisha miradi 
mingi ambayo imeainishwa katika ilani ya uchaguzi ya 
Chama Cha Mapainduzi (CCM) na kwenye Mpango wa 
Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano, bila ushirikiano huu 
na sekta binafsi hatuwezi kufikia uchumi wa viwanda kwa 
kasi inayotakiwa’’ Alisema Waziri Mhagama.

Semina hiyo ya siku moja imeendeshwa na wataalamu wa 
masuala ya Ubia Sekta ya Umma na Binafsi kutoka Benki ya 
Dunia, ambapo Jumapili, kamati tatu za Bunge zitapatiwa 
elimu na kujengewa uwezo kuhusu dhana hiyo ya PPP. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.