Habari za Punde

Tanzania Yadhihirisha Utekelezaji wa Haki za Binaadamu.


                                              
Na.Judith Mhina -Maelezo Dar.
Kitendo cha Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kushtakiwa mara nyingi zaidi katika Mahakama ya Afrika ya Haki ya Binadamu ni ushahidi tosha kuwa Serikali imetoa 
uhuru wakushtakiwa kutokana na makubaliano ya Kimataifa yaliyosainiwa na Serikali yenyewe.

Maneno hayo yamethibitishwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Samia Suluhu Hassan ambaye amesema kuwa, Serikali itahakikisha Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu (AfCPHR) kuwa itatekeleza kwa ukamilifu amri na hukumu mbalimbali zinazotolewa na mahakama kama ambavyo imeainishwa katika mkataba wa kuridhia mahakama hiyo.

Kutokana na taarifa iliyoripotiwa na gazeti la Mtanzania, toleo Na. 9013 la tarehe 25 Agosti 2018 lenye kichwa cha Habari “Tanzania yaongoza kwa kushtakiwa Afrika ” ambapo Serikali ya Tanzania imedhihirika kuwa na mashtaka 117 katika Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu yenye jumla ya kesi 180.

Tanzania kama nchi ni kinara wa kulinda haki za binadamu Afrika Mashariki na kati na ndio maana Makamu wa Rais, Mhe Samia amesema “Serikali itaendelea kushirikiana na mahakama hiyo katika kulinda haki hizo.  Hivyo kitendo cha kuwa na mashauri mengi zaidi katika mahakama hiyo inatokana na uelewa mkubwa wa wananchi katika kutafuta haki zao pia urahisi wa kuifikia mahakama hiyo. 

Uhuru wa kuishtaki Serikali upo katika nchi ambayo ina uhuru wa kweli na Utawala wa Sheria na hili ni jambo muhimu sana Watanzania kulifahamu. Nchi ambazo hazijali Haki za Binadamu huwezi kuishtaki Serikali, ndio maana Tanzania imeridhia makubaliano mbalimbali ya Kimataifa na kikanda.

Baadhi ya mikataba hiyo ambayo imeandaliwa na Chama Cha Wanasheria Tanzania Bara “ Zijue Haki za  Binadamu, Sheria katika lugha  rahisi ni kama vile “Tamko la Kimataifa la Haki za Binadamu la Mwaka 1948”.  Tamko hili limekubaliwa na kupitishwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa tarehe 10 Desemba, mwaka 1948.

Hivyo, Tamko hilo ndilo chimbuko la kulindwa kwa haki za binadamu duniani kote. Tamko hili linajumuisha, kwa pamoja, aina zote za haki za binadamu, yaani haki za kiraia na kisiasa, na haki za kiuchumi, kijamii na kiutamaduni.

Tamko la Kimataifa la haki za binadamu ni “tamko” halina masharti ya kuzibana nchi kutekeleza haki za binadamu kisheria. Pamoja na kuwa halina nguvu kisheria. Tamko hili linaheshima kubwa sana kimataifa na nchi nyingi wamelitambua na kuingiza kwenye katiba zao. Tanzania imefanya hivyo katika Ibara ya 9 (f) ya Katiba ya nchi ya mwaka 1977.

Nyingine ni “Mkataba wa Kimataifa wa Haki za Kiraia na Kisiasa wa Mwaka 1966. Ambao ulipitishwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mwaka 1966 na kuanza kutumika Machi, 1976. Tanzania imeukubali na kuuridhia mkataba huo tarehe 11 Septemba 1976.

Kama nchi Tanzania ina jukumu la kuheshimu na kuwahakikishia watu wote uwepo wa haki hizi bila ubaguzi wa aina yoyote, kama vile rangi, kabila, lugha, dini, asili au utaifa wao; Kupitisha sheria na hatua nyingine za kulinda haki zilizomo kwenye mkataba pale ambapo sheria au hatua zozote hazijafanywa;

Aidha, sheria zimeweka utaratibu kuhakikisha mtu yeyote aliyeingiliwa au kukiukwa kwa haki na uhuru wake anapata ufumbuzi kama vile kulipwa fidia;  Kuhakikisha usawa kati 
ya wanaume na wanawake katika kufaidi haki za kiraia na kisiasa zilizoorodheshwa kwenye mkataba.

Vilevile, kuna Mkataba wa Kiafrika wa Haki za Binadamu na Haki za Watu wa Mwaka 1981 Mkataba huu ulipitishwa na wakuu wa nchi na serikali za Umoja wa Nchi za Afrika (OAU), Nairobi – Kenya mwaka 1981.

Hadi leo nchi zote za Afrika ni wanachama wa Mkataba huu. Nchi wanachama zina wajibu wa kutambua haki, uhuru na wajibu uliomo kwenye mkataba na kuchukua hatua za kisheria kuzipa nguvu haki. Mkataba wa Kiafrika wa Haki za Binadamu na Haki za Watu unatambua na kulinda aina zote za haki za binadamu yaani haki za kisiasa, kiraia, kiuchumi, kiutamaduni na kijamii.

Mfano wa haki za binadamu zinazotambuliwa na kulindwa kwa Haki za Binadamu ni pamoja na Haki ya kutobaguliwa, usawa, haki ya Zijue Haki za Binadamu  7 kuheshimiwa, haki na uhuru ya kuabudu na kujumuika na wengine. Ulinzi wa Haki za Binadamu Mlinzi wa kwanza wa haki hizi ni binadamu mwenyewe.

Akitembelea Mahakama hiyo Wakili Mkuu wa Serikali, Dkt.Julius Mashamba na Naibu wake Dkt Ally Possi, wametimiza wajibu wao wa kufuatilia mahakama hiyo, kujua nini kimejiri ili kuhakikisha kila Mtanzania ana haki ya kusikilizwa na kutendewa haki.

“Wengi wanaolalamika haki zao katika kesi za jinai hazijatekelezwa kwa namna kesi zilivyosikilizwa na kuchelewa kupata nakala za mwenendo wa kesi ili wakati rufaa au kunyimwa msaada wa sheria” amesema Dkt. Mashamba ameongeza kuwa, jambo kubwa lililofanya kutembelea Mahakama hiyo ni wingi wa kesi hizo na hasa zikichukuliwa kama zimekuwa zikifanana kwani wengi hudai kutopata masaa wa kisheria wakati mahakama za ndani zilizotoa uamuzi wake.

Chimbuko na Utambuzi wa Haki za Binadamu kwa kipindi kirefu haki za binadamu zimekuwepo na kuongoza maisha ya mwanadamu kulingana na asili ya kila mwanadamu. Kukua na kutambulika kwa haki za binadamu kumepitia madaraja kadhaa kulingana na hatua kadhaa za kukua kwa jamii.

Kabla ya karne ya 19 haki hizi zilikandamizwa na kupuuzwa na jamii, serikali iliyotawala katika jamii husika na wakati mwingine mataifa yaliyoingia kutawala mataifa mengine. 

Hali hii ililawalazimisha watetezi wa haki za binadamu kufanya kazi ya ushawishi ili kuanza hatua ya kuainisha na kuzitambua haki za binadamu.

Hatua ya kwanza kabisa ya utambuzi wa haki za binadamu ilitokana na kuzidi kwa vitendo vya ubaguzi, ukatili, unyanyasaji, kutumikisha watu kwa kuwaita watumwa na uonevu dhidi ya binadamu na matendo mengine ya aina hiyo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.