Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, Atuma Salamu za Rambirambi kwa Rais wa Indonesia Kufuatia Tetemeko la Ardhi na Tsunami


STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
  Zanzibar                                                       01.10.2018
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, amemtumia salamu za rambirambi Rais wa Jamhuri ya Indonesia, Joko Widodo kufuatia tetemeko la ardhi lililoambatana na tsunami lililotokea katika kisiwa cha Sulawesi Ijumaa ya Septemba 28, 2018 na kusababisha vifo na majeruhi kadhaa.

Kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na wananchi wake,Rais Dk. Shein alituma salamu hizo za rambi rambi kwa serikali, familia pamoja na ndugu, jamaa na marafiki wa Jamhuri ya Indonesia kufuatia tukio hilo kubwa la kusikitisha lililosababisha vifo vya watu wapatao 832 na majeruhi kadhaa.

Kufuatia tukio hilo la tetemeko la ardhi lililoambatana na tsunami ambapo limetokea kwenye kisiwa cha Sulawesi katika Jamhuri ya Indonesia, Rais Dk. Shein amemtumia salamu hizo za rambirambi Rais Widodo wa Indonesia na kumtaka kuwa na subira katika kipindi hichi kigumu cha msiba.

Aidha, salamu hizo za rambirambi alizozituma Rais Dk. Shein alimuomba MwenyeziMungu awape moyo wa subira ndugu, jamaa, marafiki na wanafamilia wote wa Marehemu pamoja na wananchi wa Indonesia katika tukio hilo la kuhuzunisha.

Salamu hizo zilipongeza na kuunga mkono juhudi kubwa zilizochukuliwa na Serikali ya Jamhuri ya Indonesia katika hatua zote zilizozichukua na timu za uokozi sambamba na kuiweka katika mazingira mazuri jamii iliyoathirika.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alimuomba Mwenyezi Mungu kuzilaza roho za marehemu mahala pema peponi pamoja na kumuomba MwenyeziMungu awajaalie majeruhi wote kupona kwa haraka. Amin.

“Tunamuomba Mwenyezi Mungu awajaalie wale wote waliopata majeraha kupona kwa haraka…..…na tunapongeza juhudi za uokozi jinsi zilivyochukuliwa” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo liyotolewa na Rais Dk. Shein.

 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.