Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) alipokuwa akitoa hutuba yake katika sherehe za Uzinduzi wa Mradi wa mfumo wa uimarishaji wa usalama katika Mji wa Zanzibar uliofanyika leo katika ukumbi wa Sheikh Idrissa Abdulwakil Kikwajuni Mjini Zanzibar,[Picha na Ikulu.] 3/10/2018.
Dk. Shein aliyasema hayo
leo katika hafla ya uzinduzi wa Mradi wa Ulinzi wa Mji Salama, hafla
iliyofanyika katika ukumbi wa Idrissa Abdulwakil, Kikwajuni Mjini Zanzibar ambapo
kabla ya hapo alizindua Kituo cha Mfumo wa kuimarisha usalama kilicho Maisara.
Akiwa Maisara Rais Dk.
Shein alipata maelezo juu ya uendeshaji wa kituo hicho pamoja na kupata maelezo
juu ya ufanyaji kazi wa vifaa vya mradi huo zikiwemo gari maalum za kuangalia
usalama, pikipiki pamoja na kupata maelezo ya matumizi ya ‘drone camera’.
Akitoa hotuba yake
katika uzinduzi huo hapo katika ukumbi huo, Rais Dk. Shein alisema kuwa lengo
la Serikali ni kuhakikisha kwamba sifa njema ya Zanzibar kuwa ni sehemu salama
yenye utulivu inabakia na inakuwa ya kudumu na inaendelea kuwa ni kichocheo cha
kuongeza kasi ya maendeleo ya nchi katika nyanja zote.
Alisema kuwa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania zimekuwa zikibuni mikakati mbali mbali na kuvitumia vyombo vyake vya
ulinzi na usalama ili kuhakikisha kuwa nchi na watu wake wako salama.
Kwa hivyo, Rais Dk.
Shein alieleza kuwa Serikali imeamua kuweka vifaa vya kisasa vya ulinzi kwa
lengo lan kuimarisha hali ya usalama katika mji wa Zanzibar kwani vifaa hivyo
vinauwezo mkubwa wa kuwabaini wahusika wa matukio mbali mbali kwa haraka na
ufanisi mkubwa.
Rais Dk. Shein alitumia
fursa hiyo kuwahimiza wananchi kuvitumia vyema vifaa hivyo na wavitunze ili
viweze kutumika kwa muda mrefu na wote wawe walinzi wa nchi yao huku
akisisitiza kuwa amani, umoja na usalama hivi sasa utaimarika zaidi.
Dk. Shein alisema kuwa
suala la kusimamia usalama wa wananchi popote walipo ni jukumu la msingi la
Serikali ambapo wajibu huo umebainishwa wazi katika Ibara ya 9 Kifungu cha 7
(b) cha Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 kinacholeza kwamba.
“Usalama na hali nzuri
kwa wananchi itakuwa ndiyo lengo kubwa la Serikali”, alinukuu Dk. Shein.
Aidha, Rais Dk. Shein
aliwatahadharisha wale wote wanaofanya magendo ya karafuu, sukari, mafuta na
bidhaa nyengine hasa katika maeneo ya visiwa vidogo vidogo waache mara moja
kwani mambo hivi sasa yamebadilishwa huku akisema kuwa mradi huo utaendelezwa
katika awamu ya Pili kwa Mikoa ya Kusini na Kaskazini Unguja na mikoa yote ya
Pemba.
Alisema Serikali imeweka
mazingatio ya kiulinzi katika kuhakikisha usalama wa Mji Mkongwe kutokana na
umuhimu wa hadhi ya kuwa hazina ya Zanzibar na Urithi wa Kimataifa kama
unavyotambuliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Sayansi, Elimu na Utamaduni
(UNESCO).
Dk. Shein alieleza
kuridhika kwake kuona kuwa utekelezaji wa Mradi huo unafanywa kwa pamoja baina
ya wataalamu wa kigeni na wataalamu Wazalendo huku akisisitiza kuwa utaratibu
huo unasaidia kuwaachia ujuzi wataalamu wazalendo ili waweze kuutumia katika
kuuendeleza mradi huo hata baada ya kuondoka wataalamu wa kigeni.
“Kuna usemi katika lugha
ya Kiengereza uanaosema “The ball is in your court”, yaani sasa mpira umo ndani
ya kiwanja chenu, kwa hivyo ni jukumu la wataalamu wetu wajitume na wafanye
kazi kwa bidii na maarifa, ili waweze kujenga uwezo na hatimae waweze
kujitegemea kutokana na taaluma walioipata”,alisema Dk. Shein.
Aidha, Rais Dk. Shein
alisisitiza haja ya kuuweka mji wa Zanzibar katika hali ya usafi na kueleza
kuwa kutokana na uwepo wa mradi huo hivi sasa anamatumaini makubwa kuwa suala
la usafi litaimarika kwani wale wote wanaokwenda kinyume na hali hiyo
wataonekana.
Sambamba na hayo, Rais
Dk. Shein alisisitiza haja ya kuimarisha amani na usalama na kueleza kuwa
hakuna mbadala wa amani na umoja kwani vitu hivyo vina gharama kubwa kuvipata
pale vinapokosekana.” Zanzibar salama inawezekana”,alisisitiza Rais Dk. Shein.
Nae Waziri wa Nchi Ofisi
ya Rais, Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara Maalum za SMZ Haji Omar
Khair alisema kuwa mradi huo umekuja kwa lengo la kutekeleza matakwa ya Ilani
ya Uchaguzi ya CCM pamoja na kutekeleza ahadi yake wakati alipokuwa akiinadi
Ilani hiyo pale aliposema kuwa Wapiganaji wa vikosi vya SMZ watafanya kazi kwa kutumia
teknolojia ya kisasa kwa kuwaongezea vitendea kazi pamoja na kuimarisha maslahi
yao.
Lengo la mradi huo ni
kuimarisha usalama katika Mji wa Zanzibar pamoja na kuimarisha uchumi kwani bila
ya mawasiliano na usalama hapatakuwa na uchumi mzuri “sasa mambo yatakuwa
bambam”alisisitiza Waziri.
Alisema kuwa sasa
kutapatikana taarifa zote na hakuna atakaedanganya hasa wale wakusanyaji mapato
na kueleza kuwa Zanzibar inategemea biashara na utalii na moja lililoibuliwa na
maabara ya utalii ni kuimarisha usalama.
Aliongeza kuwa sasa mji
wa Zanzibar ni salama pamoja na kueleza kuwa Dk. Shein amewawezesha kuweza
kukabiliana na matukio ya kihalifu na yale ya uokozi kwa kukabiliana nayo
kisasa kutokana na vitendea kazi vya kisasa.
Alisema kuwa watendaji 56
wenye elimu ya Digirii wamepatiwa mafunzo kwa ajili ya kuendesha mradi huo
ambao watakuwa wafanyakazi wa Idara ya Vikosi vya Ulinzi na usalama na hivi
karibuni watapelekwa vijana maalum masomoni na kusema kuwa Kampuni ya “ROM
Solution Ltd” wataukabidhi mradi huo kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
mwaka 2020 lakini tayari hivi sasa kimeshaanza kufanya kazi.
Mapema Katibu Mkuu wa
Wizara hiyo Radhia Rashid Haroub alisema kuwa Serikali iliamua kuanzisha mradi
huo wa kuimarisha mfumo wa usalama hapa Zanzibar katika mwezi April mwaka 2015
na kutilioana saini na Kampuni ya “ROM Solution Ltd”.
Kuimarisha ulinzi
kufikia katika kiwango cha Kimataifa, katika maeneo ya uwanja wa ndege,
bandarini, Mji Mkongwe na baadhi ya barabara kuu za kuingilia katika Mji wa
Zanzibar uwanja wa ndege ikiwa ni pamoja na gari tatu katika viwanja vya ndege, mbili Unguja na moja Pemba
Alisema kuwa jumla ya Kamera
56 zimefungwa katika eneo la uwanja wa ndege na bandarini kamera 42 katika eneo
yanayozunguka Bandari, boti maalum kwa ajili ya ulinzi wa baharini nazo
umeongezeka, kamera 682 zimewekwa katika Mji Mkongwe na Kamera 96 zimewekwa katika barabara ambazo
zinauwezo wa kubaini vyombo vya usafiri vinavyokeuka sheria, ambapo kwa ujumla
Kamera 877 zimefungwa katika mradi huo.
Aliongeza kuwa ndege
zisizo rubani “drones” tatu, pikipiki 20 maalum, redio seti 50, gari 15 kwa
ajili ya mradi huo zimenunuliwa pamoja na vifaa vyenginevyo.
Nae Mkuu wa Mkoa wa
Mjini Magharibi Ayoub Mohammed Mahmoud akiwa Mwenyekiti wa Kamati ya ulinzi na
usalama katika Mkoa huo alitoa shukurani kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein kwa uamuzi wake wa kuanzisha mradi huo ambao
una umuhimu mkubwa kwa usalama wa mji wa Zanzibar
Nae Mkuu wa Kampuni ya
“ROM Solution Ltd” George Alexandru alieleza mafanikio ya mradi huo na jinsi
hivi sasa Zanzibar ilivyokuwa imepiga hatua katika suala la usalama wa mji wake
huku akieleza kuwa mji wa Zanzibar unaingia katika miongoni mwa miji salama
duniani.
Viongozi mbali mbali
walihudhuria katika hafla hiyo akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar
Balozi Seif Idd, Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali Maulid, Jaji Mkuu wa
Zanzibar pamoja na viongozi wengine wa Serikali, vyama vya siasa, Mabalozi
wadogo wanaofanya kazi Zanzibar pamoja na wananchi.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment