Na.Abdi.Shamnah. Ikulu.Zanzibar.
Nidhahiri kuwa
kwa miongo kadhaa ijayo, Wazanzibari wataendelea kukumbuka majanga makubwa
yaliotikisa umma na kuibua huzuni na majonzi yasiofutika milele.
Itakumbukwa
ilikuwa ni Julai 18, 2012 pale Meli ya Mv Skagit ilipozama katika mkondo wa
bahari ya Zanzibar, ilipokuwa safarini ikitokea jijini Dar es Salaam kuelekea
Zanzibar, ikiaminika kubeba zaidi ya abiria 200.
Tukio hilo
lilijiri, ikiwa ni kipindi cha takriban miezi kumi tu, tangu pale mshtuko
mkubwa ulipowakumba Wazanzibari baada ya tukio la kuzama kwa meli ya Mv. Spice
Islander .
Wakati meli
hiyo ikipatwa na janga hilo ikitokea
Unguja kuelekea kisiwani Pemba ilikuwa imebeba abiria zaidi ya 2,400.
Maswahibu hayo
na mengine mengi yanayowakumba wananchi, hususan wale wanaotumia bahari katika
shughuli zao za kila siku, ikiwemo kuzama kwa vyombo vya uvuvi, imekuwa ni
donda ndugu lisilopona na daima yamekuwa yakiziweka rehani roho na maisha ya
Wazanzibari kila kukicha.
Kuambatana na
matukio hayo ya kuzama kwa vyombo mbali mbali baharini na kupoteza roho na mali
za watu, kumekuwepo sababu kadhaa zinazohusishwa na majanga hayo, ikiwemo dhana
za uzembe miongoni mwa watendaji, taasisi na wakati mwengine majanga ya
kimaumbile (natural disaster).
Pamoja na hatua
za haraka zinazochukuliwa na Serikali
kupitia Idara na taasisi zake katika kufanya uokozi, pale majanga hayo
yanapojiri, bado kumekuwepo malalamiko ya kuwepo kasoro kadhaa za kiutendaji.
Kuchelewa kufika
kwa wakati eneo la tukio, uwepo wa vifaa na zana duni za uokozi, mbinu za kale
katika uokozi pamoja na mapungufu kadhaa yanayojitokeza, ni miongoni mwa
chanagmoto zinazosababisha kupoteza mamaia ya
roho za wananchi.
Aidha, huduma za mwanzo nazo zimekuwa zikipatikana
katika hali ya kulegalega, huku zikiwa hazina uhakika wa kupatikana kwake kabla
au baada ya wahanga kuokolewa.
Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar, iliyo chini ya uongozi thabiti wa Rais Dk. Ali Mohamed,
mwanamapinduzi na muumini wa amani na usalama,
imetathmin kwa kina matukio yanayoendelea kuikumba jamii kwa lengo la
kuyatafutia ufumbuzi.
Hakika
imejifunza kutokana na makosa. Baada ya tathmin ya kina imeona kuna umuhimu wa
kujikinga kutokana na maafa hayo na pale
yanapotokea kwa bahati mbaya kutokana na majaaliwa ya Mungu, basi ni vyema kuhakikisha hatua muafaka zinachukuliwa
kukabiliana na majanga hayo.
Katika
hatua hiyo imeona kuwepo umuhimu wa kuwa na vifaa bora na vya kisasa vya uokozi
pamoja na wananchi wanaoendesha shughuli zao za kimaisha baharini kupatiwa
mafunzo mbali mbali.
Hivi
karibuni, Wazanzibari waliadhimisha miaka 55 ya Mapinduzi matukufu ya 1964,
ambapo miongoni mwa miradi mikubwa na muhimu iliyozinduliwa na kupamba sherehe
hizo, ilikuwa ni 'Ufunguzi wa mradi wa Vituo vya Uzamiaji na Uokozi
Zanzibar', hafla iliyofanyika Mkoani Kisiwani Pemba.
Sherehe
hii adhimu ilihitimishwa kwa mgeni rasmi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa
Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein kuzindua kituo hicho pamoja na Boti
ya Uokozi (kwa niaba ya vituo vyengine Unguja na Pemba) .
Katika
hafla hiyo, Dk. Shein alipata fursa ya kuzungumza na wananchi kuhusu hatua ya
Serikali ya kutumia gharama kubwa katika kuimarisha usalama
wa wananchi na mali zao, hususan wale wanaotumia bahari katika shughuli
zao za kila siku .
Amesema
Serikali imelazimika kubuni mradi mkubwa wa 'Zanzibar salama' kwa lengo
la kuhakikisha maeneo ya bahari, nchi kavu
pamoja na angani yanakuwa salama muda wote.
Anasema
uzinduzi wa vituo vya Uokozi na Uzamiaji, ni awamu ya pili ya utekelezaji wa
mradi huo, ikitanguliwa na ile ya uwekaji wa CCTV Camera katika maeneo mbali
mbali ya Mji Mkongwe na maeneo mengine ya mji wa Zanzibar.
Dk.Shein
amebainisha kuwa mradi huo unahusisha mambo mbali mbali, ikiwemo ujenzi wa
vituo, vifaa vya mawasiliano, utoaji wa mafunzo kwa askari pamoja na wananchi.
Anasema
hatua ya ujenzi wa vituo hivyo inakwenda sambamba na dhamira ya Mapinduzi
matukufu ya 1964, pamoja na Ilani ya CCM ya 2015-2020 iliyoweka bayana
kuhakikisha usalama wa Wazanzibari unaimarishwa maeneo yote.
Anasema,
Serikali imelazimika kubuni mradi huo baada ya kuwepo matukio kadhaa baharini
yaliosababisha maafa makubwa ya wananchi na upotevu mkubwa wa mali zao.
Anabainisha
kuwa mradi huo ni mpango mbadala katika kukabiliana na majanga hayo, hivyo
kuwahahakikishia wananchi usalama wa kutosha muda wote na mahala popote.
Dk.
Shein alipongeza juhudi za Wizara ya Nchi (OR) Tawala za Mikoa, Serikali za
Mitaa na Idara maalum za SMZ katika kusimamia ununuzi wa vifaa hivyo,
akibainisha kuwa ni bora na vya kisasa vitakavyowahakikishia usalama
wananchi na wageni wanaouzuru hapa
nchini.
Anaeleza
kuwa pamoja na badhi ya watu kufanya matukio mbali mbali kwa lengo la kuhujumu
uchumi wa Taifa, Zanzibar itaendelea kubaki salama muda wote, sambamba na
kupata sifa kubwa duniani kote.
Anasema
suala la usalama wa nchi, ni jambo lisilo na majadala kwa kuzingatia kuwa
uchumi wa Taifa utaweza kuimarika tu pale panapokuwa na amani ya kutosha na
kutoa fursa kwa wananchi kutekeleza shughuli zao za maendeleo bila vikwazo
vyovyote.
Aidha,
amesema Ustawi wa Uchumi wa Zanzibar, unaotegemea zaidi sekta ya Utalii,
utakuwa endelevu endapo tu usalama wa
nchi utashamiri.
Akigusia
utendaji kazi wa Idara maalum za SMZ, Dk. Shein anasema taasisi hizo
zinafanyakazi kwa misingi ya sheria na Katiba ya Zanzibar.
Alisema
kikosi cha KMKM kina uwezo mkubwa wa kiutendaji na ndio maana kimekuwa
kikishiriki kikamilifu katika kukabiliana na matukio mbali mbali baharini,
ikiwemo majanga, usalama wa taifa pamoja na uhalifu (magendo) .
Dk. Shein ametumia fursa hiyo kupingana na
mitazamo ya baadhi ya watu kuwa Vikosi vya SMZ, ikiwemo JKU, KVZ, Mafunzo, KMKM
pamoja na Zimamoto zimekuwa zikifanyakazi kwa kuzingatia utashi wao.
Amewataka
wananchi wenye matatizo na askari wa vikosi hivyo kufuata miongozo ya kisheria
badala ya kujikita katika hisia pekee.
"Kazi
zinafanywa kwa kuzingatia Katiba ya Zanzibar na sheria zilizoandikwa bila ya
kudhulumu au kudhuru mtu", anasema.
Dk.
Shein aliwawahakikishia Wananchi wa Zanzibar kuwa pamoja na mradi huo kugharimu
fedha nyingi, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imefanikiwa kuutekeleza kwa
ufanisi mkubwa ikiwa haina deni lolote.
Katibu
Mkuu Wizara ya Nchi, (OR) Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara maalum za
SMZ Radhia Rashid Haroub anasema Ujenzi
wa Vituo vya Uzamiaji na Uokozi , ni mradi wa miaka minne (4), ulioanza
kutekelezwa rasmi katika mwaka wa fedha 2014/2015, ukipangiwa kutumia zaidi
ya shilingi Bilioni 5.9 hadi kukamilika
kwake.
Anasema
hata hivyo gharama hizo zimeongezeka (hakueleza ongezeko) kutokana na
mabadiliko ya thamani ya vifaa vilivyokadiriwa kununuliwa.
Anasema
mradi huo ni utekelezaji kwa vitendo wa malengo halisi ya Mapinduzi matukufu ya
1964, sambamba na utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi wa CCM ya 2015/2020 katika
kuimarisha ulinzi na usalama wa maisha ya wananchi pamoja na kuvijengea uwezo
vikosi vya Idara maalum za SMZ.
Amebainisha
kuwa mradi huo una maeneo makuu manne
(4), ambayo ni Ujenzi wa vituo vya Uzamiaji na Uokozi pamoja na Ununuzi wa Boti
za uokozi na vifaa vya uzamiaji.
Maeneo
mengine ni Ununuzi wa vifaa vya mawasiliano, pamoja na kuwapatia mafunzo
Maofisa, wapinagaji wa kikosi cha KMKM pamoja na wananchi kwa ujumla.
Katibu
Mkuu huyo anasema, malengo makuu ya mradi huo ni kujenga vituo sita (6) vya
uokozi na uzamiaji nchini kote, na kubainisha kuwa tayari mradi umeshakamilisha
ujenzi wa vituo vitatu (3) ambavyo ni Kibweni na Nungwi kwa Unguja, pamoja na
Mkoani Kisiwani Pemba.
"Vituo
vitatu ambavyo ni Kizimkazi, Wete na Msuka vitajengwa sambamba na ujenzi wa
mahanga (makaazi) ya askari kuanzia mwaka wa fedha 2019/2020", anasema.
Ameongeza
kwa kusema kuwa ujenzi wa vituo vilivyokamilika umegharimu zaidi ya shilingi
Milioni 966.8.
Anaeleza
kuwa mradi huo umelenga kununua Boti mbili za Uokozi ambazo tayari
zimeshanunuliwa, ikiwemo iliyozinduliwa, wakati nyingine iliyobaki ikitarajiwa
kuwasili nchini mwishoni mwa mwezi huu.
Akielezea
uwezo wa Boti hizo; Radhia anasema, "boti hizi zina uwezo wa kukimbia 'knotical
mile 55' kwa saa ikiwa ni sawa na kilomita 99", anaeleza.
Anasema
Boti hizo zina vifaa maalum vyenye uwezo wa kuokoa maisha ya hadi watu 400 kwa
boti ndogo na watu 600 kwa boti kubwa; kwa wakati mmoja.
Anafafanua
kwa kusema kuwa boti ndogo ina uwezo wa kubeba hadi watu 20, wakati ambapo boti
kubwa ina uwezo wa kubeba hadi watu 40 na kuwakimbiza kituoni kwa ajili ya
kupata huduma.
Anaeleza
kuwa boti hizo zimegharimu jumla ya shilingi Bilioni 12.5.
Akigusia
kuhusiana na vifaa vya uzamiaji, Radhia amesema
kuna vifaa mbali mbali ambavyo tayari vimenunuliwa, ikiwemo nguo maalum
za uzamiaji, mitungi ya gesi, mashine ya kutengenezea gesi pamoja na vifaa
vyengine vinavyotumika chini ya bahari wakati wa uokozi.
Anasema
vifaa hivyo vimeigharimu Serikali jumla ya shilingi Milioni 500.
Aidha,
anasema vifaa mbali mbali vya mawasiliano vilivyogharimu shilingi Milioni 470
vimenunuliwa, ikiwemo Mtambo wa Redio (redio base), Rada ya baharini (marine
radar), kompyuta pamoja na vifaa vya GPS.
Anabainisha
kuwa kupitia mradi huo, maofisa na wapiganaji 68 wa KMKM wamepatiwa mafunzo
yaliogharimu shilingi Milioni 30, kuhusiana
na matumizi ya vifaa hivyo.
"Pia
wananchi 850 wanaofanya shughuli za uvuvi na wasafirishaji wadogo wadogo wa
abiria na mizigo katika Mikoa mitano ya Zanzibar wamejengewa uelewa wa kuwepo
mradi huu pamoja na kupatiwa mafunzo ya kutumia vifaa vya mawasiliano kwa ajili
ya kutoa taarifa pale wanapohitaji msaada wakiwa baharini", anaongeza.
Anasema
kuwa tayari miongoni mwa wananchi hao wameanza kuvitumia vituo hivyo pale
wanapohitaji msaada.
Katika
hatua nyengine, Katibu Mkuu Radhia ameweka wazi mipango ya Wizara ya kuvipatia
vituo hivyo 'Drone' moja kati ya tatu zilizonunuliwa kupitia
mradi wa Mji salama, ili kuimarisha ulinzi wa baharini kwa njia ya anga.
Aidha,
anasema Kikosi cha KMKM kimenunua kifaa maalum (decompression chamber)
kitakachotumika kusaidia wahanga watakaoathirika kutokana na mfumo wa kupumua
pale wanapopatwa na majanga.
Anasema
kuwa upatikanaji wa huduma hiyo utawasaidia sana wahanga kurejea katika hali
yao ya kawaida.
Anaeleza
kuwa kukamilika kwa mradi huo, kutaleta mapinduzi makubwa katika sekta ya
usafiri wa baharini, katika suala zima la kuimarisha usalama wa wananchi na
mali zao, hususan wale wanaotumia bahari katika shughuli zao za kila siku.
Katibu
Mkuu huyo amechukua ahadi ya kuhakikisha kuwa wapiganaji wa KMKM watavilinda,
kuvitunza na kuvitumia vizuri vifaa hivyo, ili
kuifanya sekta ya usafiri baharini kuwa katika hali ya usalama zaidi.
Haji
Omar Kheir ni Waziri wa Nchi (OR), Tawala za Mikoa, Serikali za Mitaa na Idara
Maalum za SMZ, anasema uzinduzi wa vituo hivyo unaakisi dhamira ya Serikali ya
kuhakikisha shughuli zote za uokozi zinafanyika kwa weledi wa hali ya juu nakwa
njia za kisasa zaidi ili kuleta ufanisi.
Anasema
kupitia mradi huo Kikosi cha KMKM kitakuwa na uwezo mkubwa wa kiusalama na
kuweza kukabiliana na majanga kwa wakati muafaka.
Aliipongeza
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, chini ya uongozi thabiti wa Rais Dk. Ali
Mohamed Shein kwa kukiwezesha kikosi
hicho kwa vifaa na mafunzo kwa watendaji wake.
Salim
Hamad Khamis (65) mvuvi kutoka Makombeni
Mkoani ameipongeza Serikali kwa juhudi kubwa inazoendelea kuchukuwa kuhakikisha
wananchi wake wanakuwa salama muda zote wakati wanapokuwa katika shughuli zao
za kila siku baharini.
Anasema
hatua ya Serikali kununua boti za uokozi
zenye uwezo na kasi kubwa, itawasaidia sana wananchi, ikiwemo wavuvi wadogo
wadogo wawapo baharini katika shughuli zao za kila siku.
"..........,
hakika hili ni jambo la kushukuru sana, kumshukuru Mungu, kumshukuru Rais wetu
kwa kuona umuhimu wa kuwalinda na
kuwanusuru na majanga wananchi wake, hasa sisi wavuvi wenye vidau vidogo, muda
wote tumashakani, sasa tutakuwa na amani
na kazi zetu", anasema.
Anasema
kuwepo kwa boti hizo, sambamba na mafunzo yanayoendelewa kutolewa kwa wananchi
katika kukabiliana na majanga wawapo baharini, ni hatua muafaka na dhamira
njema ya Serikali kwa wananachi wake katika kukabiliana na majanga.
Siti
Awesu Hamad (30) ni maazi wa Makoongwe aliehudhuria kwenye hafla hiyo, anasema
uzinduzi wa kituo cha uzamiaji na uokozi ni ukombozi kwa Wazanzibari, hususan
wale wanaoendesha maisha yao kwa shughuli za baharini.
Anaiomba
Serikali kuviwezesha ipasavyo vikosi vya SMZ ikiwemo KMKM ili viweze kutekeleza
vyema majukumu yake, pamoja na kusimamia usalama wa baharini.
Ni
dhahiri kuwa uzinduzi wa Kituo cha Uzamiaji na Uokozi Mkoani Pemba, kwa niaba
ya vituo vyengine, ni mapinduzi mapya katika kuzikabili changamoto mbali mbali
za baharini.
Kuna
ukweli usio shaka kuwa sekta ya uvuvi pamoja
na ile ya mawasiliano baharini inabeba kundi kubwa la nguvu kazi ya Taifa
pamoja na kuchangia uchumi wa taifa kwa kiwango kikubwa.
Kwa
mantiki hiyo ni wazi kuwa hatua ya Serikali ya kuanzisha vituo hivyo, ni
uthibitisho wa dhamira njema kwa wananchi wake katika kukabili majanga ambayo
yamekuwa yakiongezeka kila kukicha.
Hivyo,
ni jukumu la wananchi wote, hususan wale wanaofanya shughuli za baharini
kuhamasishana ili kushiriki mafunzo yanayotolewa na watendaji wa vituo hivyo
ili kufahamu namna gani wataweza kupata msaada pale wanapopatwa na majanga ya
aina mbali mbali.
No comments:
Post a Comment