Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akihutubia wakati wa hafla ya Uwekaji wa Jiwe la Msingi Kituo Cha Afya Kianga kilichojengwa kwa Mradi wa TASAF na Nguvu za Wananchi wa Shehia ya Kianga, akiwa katika ziara yake Wilaya ya Magharibi A Unguja, kutembelea Miradi ya Maendeleo ya Wilaya hiyo.
Na.Abdi Shamnah -Ikulu Zanzibar.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed
Shein amewataka wananchi wa shehiya ya Kianga, Wilaya Magharibi 'A'Unguja kukitunza
vyema pamoja na kukitumia ipasavyo kituo cha Afya, ili kiweze kuwa endelevu na
kuleta tija kwa jamii.
Dk. Shein amesema hayo leo katika hafla ya
Uwekaji wa Jiwe la msingi la Kituo cha Afya Kianga, kilichojengwa kupitia Mfuko
wa Maendeleo ya Jamii TASAF kwa mashirikiano na wananchi.
Alisema suala la upatikanaji wa huduma bora za
Afya nchini halina mbadala, hivyo kuna haja ya kukitunza kituo hicho na
kuhakikisha wananchi wa shehiya hiyo na nyengine jirani wanafika kupata huduma.
Alisema pamoja na wananchi kuendelea na tamaduni
za kupata huduma za afya kupitia njia za jadi, kuna umuhimu mkubwa wa kukitumia
ipasavyo kituo hicho, ambacho kitaendeshwa kupitia afya ya msingi chini ya
mfumo wa Ugatuzi.
"Sisemi yale ya asili msifanye, sijasema
hivyo yale fanyeni lakini pia hospitalini mje, sitaki kuondosha
imani za watu", alisema.
Aidha Dk. Shein aliiagiza Wizara Afya kwa
kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya Magharibi "A" kuhakikisha kituo
hicho kinakuwa katika mazingira bora, ikiwa pamoja na kukipatia wataalamu wa
kukihudumia.
Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwapongeza
wananachi wa Kianga kwa uamuzi wao uliolenga kupatiwa huduma za afya, ili
kuondokana na kadhia ya muda mrefu ya kufuata huduma hizo katika vituo vya afya
vilivyopo masafa marefu.
Akigusia historia ya huduma za Afya nchini, Dk.
Shein alisema Mapinduzi ya mwaka 1964 yamekuja kuwakomboa Wazanzibari wanyonge
kuondokana na kadhia ya kukosa huduma bora za afya.
Alisema kabla ya Mapinduzi, huduma za Afya (kama
ilivyo kwa elimu), zilitolewa kwa misingi ya ubaguzi kuambatana na uwezo wa
mtu, hivyo Wazanzibari walio wengi walikosa huduma hiyo muhimu.
Katika hatua nyengine Dk. Shein aliwapongeza
watendaji wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii TASAF Zanzibar, Ofisi ya Makamo wa
Pili wa Rais pamoja na wananchi wote
waliofanikisha ujenzi wa kituo hicho.
Mapema,
Waziri wa Nchi, (OR), Tawala la Mikoa na Serikali za Mitaaa na Idara Maalum za SMZ,Mhe.Haji Omar Kheir alipongeza juhudi kubwa zinazofanywa na Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein pamoja na Rais wa
Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli za kuimarisha mfuko
huo kifedha kupitia Benki ya Dunia (World Bank).
Alisema ni haki ya wana CCM kuendelea kutembea
kifua mbele, kutokana na mafanikio makubwa yaliopatikana katika utekelezaji wa Ilani ya CCM, kupitia sekta
tofauti ikiwemo Afya.
Waziri Kheri, aliahidi kushirikiana kikamilifu na
Wizara ya Afya na kuandaa mikakati
ili kupata wataalamu bora wa
kukiendeleza kituo hicho.
Nae, Naibu Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamo wa
Pili wa Rais, Mhe.Mihayo Juma Nhunga, alisema kukamilika kwa ujenzi huo kutawaondolea
usumbufu wananchi wa Kianga kufuta huduma za Afya katika vituo vya Kizimbani
na Bumbwi sudi na Mwera.
Alisema hatua hiyo itafungua milango ya maendeleo
kwa wananchi wote wa Jimbo la Mwera.
Aidha, Naibu Katibu Mkuu, (WN) Ofisi ya Makamo wa
Pili wa Rais, Ndg.Abdalla Hassan Witawi, alisema ujenzi wa kituo hicho ulioanza
Julai, 2018 umegharimu zaidi ya shilingi Milioni 104 hadi sasa, ukifikia
asilimia 85 ya ujenzi wote.
Mitawi alizipongeza Ofisi za Mkuu wa Mkoa Mjini
Magharibi Unguja na Wilaya Magharibi 'A' pamoja na Kamati ya Uongozi wa Shehiya ya Kianga
kwa mashirkiano yao yaliofanikisha vyema ujenzi wa kituo hicho.
No comments:
Post a Comment