Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akisalimiana na Balozi wa Tanzania Nchini Zambai Mhe. Hassan Simba Yahya alipofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo leo.
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Balozi wa Tanzania Nchini Zambia Mhe. Hassan Simba Yahya alipofika Ikulu Zanzibar kuonana na kufanya mazunguzo na Rais leo.
RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza haja ya
kuendeleza uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania na Zambia.
Dk. Shein aliyasema
hayo leo, Ikulu mjini Zanzibar wakati alipofanya mazungumzo na Balozi Mteule wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Zambia Hassan Simba Yahya ambapo
mazungumzo hayo yalijikita zaidi kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya
pande mbili hizo.
Katika mazungumzo
hayo, Dk. Shein alimueleza Balozi Hassan Simba kuwa historia iliopo kati ya
pande mbili hizo ni vyema ikaimarishwa
kwa kuendeleza sekta za kiuchumi na maendeleo hasa katika kutekeza Sera ya
Diplomasia ya Uchumi.
Dk. Shein alimueleza
Balozi huyo azma ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kutekeleza Sera ya
Diplomasia ya uchumi ikiwa ni pamoja na kuhamasisha uwekezaji hasa katika sekta
ya viwanda kwani ndio kiu ya uchumi wa Tanzania hivi sasa.
Alieleza kuwa Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania na Zambia zimekuwa zikishirikiana katika nyanja mbali
mbali hasa ikizingatiwa kuwa nchi mbili hizo ni wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo
ya Nchi za Kusini mwa Bara la Afrika (SADC).
Rais Dk. Shein alisema
kuwa kwa vile Tanzania hivi sasa ndiye Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, ni vyema
mkazo zaidi ukawekwa katika kuhakikisha mashirikiano ya nchi wanachama wa
Jumuiyahiyo yanaimarika zaidi kwa azma ya kufikia malengo yaliyowekwa.
Aidha, Rais Dk. Shein
alieleza kuwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Zambia zina uhusiano na
ushirikiano wa muda mrefu ambao umesababisha watu wa pande mbili hizo kuishi
kama ndugu hasa kwa kuwepo kwa mradi mkubwa wa usafiri wa Shirika la Reli ya
pamoja kati ya Zambia na Tanzania (TAZARA).
Dk. Shein alieleza
kuwa uhusiano na ushirikiano wa
kihistoria uliopo kati ya Zambia na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni njia
moja ya kuimarika zaidi kwa mahusiano ya wananchi wa pande mbili hizo hasa
ikizingatiwa kuwepo kwa usafiri wa Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL).
Aidha, Dk. Shein
alimueleza Balozi huyo kuwa kuwepo kwa usafiri wa Shirika la Ndege la Tanzania
(ATCL) kati ya Tanzania na Zambia itakuwa chachu katikia kuimarisha uhusiano na
ushirikiano kwenye sekta ya utalii.
Pamoja na hayo, Rais
Dk. Shein alimtakia kazi njema Balozi huyo na kumueleza kuwa Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kumpa mashirikiano makubwa katika kuhakikisha
anatekeleza vyema kazi zake sambamba na kuiwakilisha vyema Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania nchini Zambia.
Akieleza kuhusu
mashirikiano katika sekta ya elimu, Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kuimarisha uhusiano kati ya vyuo vikuu vya
nchi hiyo na vile vya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania vikiwemo vyuo vikuu vya Zanzibar.
Alieleza kuwa katika
kuendeleza jambo hilo tayari wapo wanafunzi wanaotoka nchini Zambia ambao
wanaosoma katika vyuo vikuu mbali mbali vya hapa Tanzania vikiwemo vyuo vikuu
vya Zanzibar hatua ambayo inafaa kuendelezwa kwa kuwahamasisha wanafunzi kutoka
pande zote mbili.
Nae Balozi mteule wa
Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nchini Zambia
Hassan Simba Yahya alimueleza Dk. Shein kuwa suala la mashirikiano lina
umuhimu mkubwa hivyo aliahidi kulifanyia kazi kwa nguvu zake zote.
Balozi Simba alitumia
fursa hiyo kumuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa suala zima la kuendeleza historia
ilioyopo katika kukuza uhusiano na ushirikiano kati ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na Zambia ataendelea kulipa kipaumbele katika kutekeleza majukumu yake
nchini humo.
Alieleza kuwa historia
iliyopo itaendelezwa sambamba na mahusiano mema ya wananchi pamoja na viongozi
wa Jamahuri ya Muungano wa Tanzania na Zambia.
Balozi Simba alieleza
kuwa utekelezaji wa Sera ya Diplomasia ya Uchumi ambayo Tanzania kwa hivi sasa
imeipa kipaumbele atahakikisha anaifanyia kazi kwa kuitangaza vyema ili
kuhakikisha malengo yaliowekwa yanafikiwa.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment