RAIS wa Zanzibar
na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameipongeza Timu ya
Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) kwa ushindi mnono ulioipata dhidi ya Timu ya
Taifa ya Uganda.
Dk. Shein alitatoa
pongezi hizo baada ya Timu ya Taifa ya Tanzania kushinda mabao matatu kwa bila
dhindi ya Timu ya Taifa ya Uganda mechi iliyochezwa katika uwanja wa Taifa
Jijini Dar-es-Salaam hapo jana.
Rais Dk. Shein
aliipongeza Timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) kwa kuweza kufuzu katika Fainali za Kombe la Mataifa ya
Afrika (AFCON) kwa mara ya pili baada ya kusubiri kwa miaka 39.
Katika salamu zake
hizo za pongezi Rais Dk. Shein aliipongeza Timu hiyo ya Tanzania kwa ushindi
wake huo na kueleza kuwa wananchi wa Zanzibar na Tanzania nzima wamefarajika na
ushindi huo ambao utaendelea kuipa hadhi kubwa Tanzania Kitaifa na Kimataifa
katika anga za michezo.
Alieleza kuwa wananchi
wa Zanzibar na Tanzania nzima wataendelea kuiunga mkono Timu yao hiyo kutokana
na jitihada kubwa inazozichukua katika kuhakikisha inailetea ushindi Tanzania.
Rais Dk. Shein
alitumia fursa hiyo kuwapongeza wananchi wote kwa kuishangiria timu yao hiyo
katika mechi yake hiyo iliyocheza hapo jana sambamba na kuiunga mkono katika
kuhakikisha inapata ushindi mnono.
Aidha, Dk. Shein amekipongeza Chama cha Mpira wa Miguu
Tanzania (TFF), Kocha wake Mkuu Mnigeria
Emmanuael Amunike pamoja na watendaji na viongozi wote waliofanikisha ushindi
huo kwa kuonesha kiwango cha hali ya juu na hatiame kupata ushindi huo mnono
uliwapa raha Watanzania wote.
Ushindi huo uliwafanya
Star kufikisha alama 8 na kujikatia tiketi ya kwenda Misri baadae mwaka huu.
Katika mchezo mwengine
wa kundi L la (Taifa Stars), Cape Verde
walitoka sare tasa na Lesotho, hivyo timu hizo kufikisha alama 5 na 6 mtawalia
ambapo kwa matokeo hayo Star imejiunga
na vinara wa kundi hilo Uganda ambao walifuzu awali baada ya kufikisha alama
13.
Star walianza mchezo
huo kwa kasi huku wakipata hamasa kutoka kwa mashabiki zaidi ya 60,000
walioujaza uwanja wa Taifa jijini Dar –es Salaam pamoja na mashabiki walioko
nje ya uwanja kutoka Tanzania Bara na
Zanzibar.
Rajab
Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment