Na. Paschal
Dotto-Maelezo.
Rais
Dkt John Pombe Magufuli amewahakikishia
wananchi wa Nanyamba, Tandahimba, na Newala Mkoani Mtwara kuwa Serikali
itaendelea kuimarisha miundombinu ya uhakika ili kuunganisha Kanda ya Kusini
Kiuchumi na wananchi wa Mkoa huo kuendelea kufanya kazi kwa juhudi ili kuweza
kujiletea maendeleo yao.
Akizungumza
katika maeneo mbalimbali ya Mkoa huo, Rais Magufuli amesema Serikali itaanza
ujenzi wa barabara ya Mtwara-Tandahimba-Nanyamba yenye urefu wa kilometa 50 itakayogharimu
kiasi cha Tsh.bilioni 86 na kumwagiza Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
Isack Kamwelwe kutangaza zabuni ya ujenzi wa kilometa zingine na kufikia
kilometa 100 na hivyo kuunganisha kwa urahisi nyanda za kiuchumi katika mikoa
ya kusini.
“Barabara
hii itakuwa ni kiunganishi cha uchumi mikoa ya kusini, hatuwezi kushindwa
kujenga kilometa 100, lengo letu kuu ni kuiunganisha Bandari yetu ya Mtwara na
mizigo inayotoa Malawi,” alisema Rais Magufuli.
Aidha
Rais Magufuli alisema kuwa katika kuwainua wakulima wa Mkoa wa Mtwara, ambapo Serikali
imetekeleza ununuzi wa korosho kutoka kwa wananchi wenye korosho zaidi ya kilo
1500, na Tsh Bilioni 50 tayari zimetengwa kwa ajili ya kuwalipa wakulima hao, na
kwa upande wa wakulima wa korosho wenye kilo chini ya 1500 wamelipwa kiasi cha Tsh
Bilioni 578.
Rais
Magufuli amewahiza wafanyabiashara walanguzi wa zao la korosho ‘Kagomba’ kuacha kuwadhulumu wakulima
wadogo kwa kuwapa bei ambayo hailidhishi huku wakijua wametumia gharama kubwa
katika kuendeleza zao hilo, na kusema serikali ya Awamu ya tano haitarudi nyuma
kuwatetea wakulima hao.
“Utakuta
mtu amelima korosho zake, amenunua madawa, ametumia gharama kuzivuna unakuja
kumpa bei ya 1500, kwa Serikali ya Awamu ya Tano hili halikubaliki”, alisema Rais
Magufuli.
Akiongelea
miradi mingine inayotekelezwa serikali ya Awamu ya Tano kuwa ni pamoja na upanuzi wa bandari ya Mtwara, ,
upanuzi wa uwanja wa Ndege na ukarabari wa mradi wa maji wa makonde ambao
utagharimu kiasi cha Tsh.bilioni 160 zikiwa ni fedha za mikopo kutoka Serikali
ya India unaowezesha ujenzi wa miradi ya maji katika miji 28 nchini..
No comments:
Post a Comment