Habari za Punde

TAKUKURU TANGA YAMTAKA MTUMISHI ALIYECHUKUA MSHAHARA HEWA MILIONI 30 MUHEZA KUREJESHA

MKUU wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Takukuru Mkoani Tanga Christopher Mariba akizungumza na waandishi wa habari ambao hawapo pichani wakati akitoa taarifa yao ya miezi mitatu ya utendaji wao ambapo katika kipindi hicho walifungua shauri moja ambalo lilifikia mwisho na kutolewa maamuzi.
Sehemu ya waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali mkoani Tanga wakimsikiliza kwa umakini Mkuu wa Takukuru mkoa wa Tanga Christopher Mariba wakati akitoa taarifa yao ya miezi mitatu ya utendaji wao

TAASISI ya kuzuia na Kupamba na Rushwa Mkoani Tanga imemtaka aliyekuwa mtumishi wa Halmashauri ya wilaya ya Muheza Idara ya Elimu Aneth Makame kurejesha kiasi cha milioni 30 alizichukua wakati akijua tayari amekwisha kustaafu na kuisababishia serikali hasara.

Hayo yalisemwa leo na Mkuu wa Takukuru Mkoani Tanga Christopher Mariba wakati akitoa taarifa yao ya miezi mitatu ya utendaji wao ambapo katika kipindi hicho walifungua shauri moja ambalo lilifikia mwisho na kutolewa maamuzi.

Alisema mtumishi huyo aliomba kustaafu kwa hiyari akiwa na miaka 55 lakini akaendelea kuchukua mshahara kwa miaka mitano iliyofuatia na hivyo kuisababishia hasara kiasi hicho.

Alisema suala hilo linahusiana na mishahara hewa kutokana na kwamba baada ya kustaafu kwa hiari mtumishi huyo aliendelea kula mshahara na kusababisha hasara ya kiasi hicho kwa serikali huku akijua kufanya hivyo ni kosa kisheria.

Aidha alisema bado mtumishi huyo hajaanza kurejesha fedha hizo huku taasisi hiyo ikimtaka kufika ofisini kwao yeye na familia yake ili waweze kuweka utaratibu wa kuzirejesha fedha hizo haraka iwezekanavyo.

“Endapo atashindwa kufanya hivyo basi itabidi tutafute utaratibu mwengine kupata fedha hiyo nah ii itakuwa ni pamoja na kuuza nyumba au mali yoyote anayomiliki…kabla ya maamuzi hayo mshtakiwa alikuwa amekwisha kukaa mahabusu takribani mwaka mmoja na nusu bila dhamana”Alisema.

Mkuu huyo wa Takukuru Mkoa alisema pia katika kipindi hicho mkoa huu umeokoa kiasi cha sh.milioni 2,190,500 kilicho kuwa kimechukuliwa kinyume cha sheria na taratibu za fedha .

“Pamoja na kiasi hicho kurejeshwa tumewaandikia barua waajiri wa wahusika kwa lengo la kuweza kuchukua hatua za kinidhamu /kiutawala dhidi ya watumishi waliohusika na matendo hayo “Alisema.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.