Habari za Punde

Uzinduzi wa Majengo ya Ofisi za Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Kisiwani Pemba leo.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akiondoa kipazia kuashiria kuweka Jiwe la Msingi la Majengo ya Ofisi za SMZ Kisiwani Pemba . Uzinduzi huo umefanyika leo.kulia Waziri wa Fedha na Mipango Zanzibar Mhe. Balozi Mohammed Ramia Abdulwawa. 
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema kuwa miongoni mwa malengo makuu ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni kuona kwamba watumishi wa umma wanafanya kazi zao wakiwa katika mazingira yaliyo bora na salama zaidi.
Dk. Shein aliayasema hayo leo katika hafla ya uzinduzi wa Jengo la Ofisi za Serikali huko Gombani Chake Chake Pemba, Mkoa wa Kusini Pemba, ambapo viongozi mbali mbali wa vyama na serikali pamoja na wananchi na wafanyakazi walihudhuria.
Rais Dk. Shein alisema kuwa uzinduzi wa jengo hilo ni miongoni mwa vielelezo muhimu vya utekelezaji wa lengo hilo kwani majengo ya ofisi ndio mahali pa kufanyia kazi ambapo hutumia muda mwingi ambayo ni theluthi moja ya siku nzima baada ya kutoka nyumbani.
Alieleza kuwa kuwa na mahala pazuri pa kufanyia kazi kunampelekea mtendaji afanye kazi kwa furaha, umakini na kujiamini Zaidi na ndio maana Serikali imeamua kujenga.
Aliongeza kuwa ujenzi wa jengo hilo ni jitihada za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia maamuzi ya Baraza la Mapinduzi ambapo hatua yote hiyo ni kuwawwzesha wafanyakazi katika mazingira mazuri.
Alieleza kuwa ujenzi huo unatokana na baadhi ya ofisi kuchakaa, nyengine hazina nafasi ya kutosha kwa ajili ya watumishi pamoja na wananchi wanaofika kwa ajili ya kupatiwa huduma.
Hata hivyo, Rais Dk. Shein alisema kuwa baadhi ya Wizara na Taasisi nyengine za Serikali zililazimika kukodi nyumba kutokana na uhaba wa majengo halisi ya kiofisi hali ambayo haipendezi hivyo Serikali itaendelea kujenga majengo ya Ofisi Unguja na Pemba.
Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali imejenga ofisi hizo ili kurahisisha utoaji wa huduma hivyo, kila mfanyakazi ahakikishe kwamba anawajibika ipasavyo kulingana na dhamana na majukumu ya kazi aliyopangiwa.
Hivyo, aliwataka wafanyakazi wahakikishe wanatumia vizuri muda wa kazi kwa kufanya mambo yanayopaswa kufanywa katika sehemu za kazi.
Alisema kuwa Serikali itaongeza mshahara kwa kima cha chini na juupale mapato yatakapoongezeka kwa wafanyakazi kuzidi kujituma na kuendelea kufanya kazi kwa ari, taratibu na nidhamu za kazi.
Alisisitiza wafanyakazi kufanya kazi kwa masaa manane ya kazi kwa siku kwani hatua hiyo itaongeza ufanisi na kuongeza mapato huku akisisitiza haja kwa wafanyakazi kutunza siri za kazi kwani nyenzo kubwa katika Utawala Bora sambamba na kujiepusha na malumbano.
Aliongeza kuwa kuna haja ya kutafuta namna itakayowezesha kudhibiti matumizi ya simu za mikononi wakati wa saa za kazi kwani kumekuwa na malalamiko mengi kwa wananchi katika sehemu mbali mbali juu ya suala matumizi mabaya ya simu.
“Wafanyakazi wanatumia muda mwingi kazini kuchati na kuperuzi katika mitandao ya kijamii vile vile natoa indhari kwa wale wanaotega kazi kwamba kuwepo kwa ofisi hizi ndani ya jengo moja kusichukuliwe kuwa ni ukaribu wa marafiki kuonana kirahisi kwa ajili ya mazungumzo”,alisisitiza Dk. Shein.
Aidha, Dk. Shein aliwahimiza viongozi na wafanyakazi wote watakaotumia jengo hilo wahakikishe kwamba wanalitumia vizuri pamoja na vifaa na miundombinu mengine ili viweze kudumu Zaidi.
Pia, alieleza kuwa ofisi hizo mpya zitaongeza ari na hamasa ya wafanyakazi ili waweze kufikia malengo yaliyowekwa ya kutoa huduma bora Zaidi kwa wananchi huku akisisitiza kuwa jengo hilo litasaidia hata zile taasisi ambazo zimechakaa huku taratibu zikiandaliwa kujenga ofisi nyengine Zaidi.
“Na zile taasisi ambazo hazina pa kukaa zitaletwa hapa hapa huku Serikali ikiendelea kujenga majengo mapya”,alisema Dk. Shein.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alisema kuwa utekelezaji wa miradi hiyo mikubwa ya maendeleo ni kielelezo cha juhudi za kuendeleza fikra, falsafa na malemgo ya Mapinduzi ya mwaka 1964 kwa kuzingatia miongozo ya viongozi na wazee waliotangulia.
Alisisitiza kwamba Waasisi wa Mapinduzi chini ya Marehemu Mzee Abeid Amani Karume walihakikisha kwamba panakuwa na uwiano wa kasi ya maendeleo baina ya Unguja na Pemba.
Alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya Awamu ya Saba na Awamu zote zilizotangulia zimekuwa zikiyaendeleza haya kwa kasi na ari ile ile ya Kimapinduzi licha ya kwamba wapo wanayoyabeza.
Alisema kuwa kuimarika kwa uchumi kumeiwezesha Awamu hii kuyafanya maslahi ya wafanyakazi yawe bora kwa mara nne pamoja na kuubadilisha mshahara wa kima cha chini kwa asilimia mia moja.
Rais Dk. Shein alisema kuwa mambo yote yanayofanywa ikiwa ni pamoja na ujenzi wa majengo hayo ni kwa mujibu wa Katiba ya Zanzibar Ibara ya 10.
Alitumia fursa hiyo kuipongeza Kampuni za ndani za Zanzibar za “Quality Building Contract” iliyojenga ofisi hizo pamoja na Kampuni ya “ZANCON”iliyokuwa Mshauri elekezi na msimamizi wa ujenzi huo.
Nae Waziri wa Fedha na Mipango Mohamed Ramia Abdiwawa alieleza kuwa juhudi hizo za ujenzi zinatokana na utekelezaji wa Ilani ya CCM sambamba na azma ya Mapinduzi Matukufu ya Januari 12, 1964 na kutoa pongezi kwa Mawaziri wawili waliomtangulia ambao ni Omar Yussuf Mzee na Dk. Khalid Salim kwaa kusimamia vyema mchakato wa ujenzi huo.
Nae Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango Khamis Mussa alisema kuwa ujenzi wa jengo hilo lenye vyumba 145 umegharimu jumla ya TZS Bilioni 13.6 ambazo ni fedha za mapato ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Alisema kuwa miongoni mwa Wizara ambazo zina ofisi katika majengo hayo ni sita kwa hivi sasa ambazo ni Wizara ya Fedha na Mipango, Wizara ya Katiba na Sheria, Wizara ya Kazi Uwezeshaji Wazee, Wanawake na Watoto, Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati na Wizara ya Vijana, Utamaduni na Michezo.
Mapema baada ya kulizindua jingo hilo Rais Dk. Shein alipata fursa ya kulitembelea jengo hilo katika Ofisi za Wizara zote ndani ya jengo hilo na kupata maelezo.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.