Mheshimiwa Spika,
Kwanza kabisa napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu, mwingi wa Rehma
kwa kutujaalia uhai na afya njema na kutuwezesha
kufanikisha Mkutano huu wa Kumi na Nne wa Baraza la Tisa ulioanza tarehe 08 Mei, 2019 hadi leo tarehe 28 Juni, 2019 tunapouahirisha.
Mkutano
ambao tumeweza kupokea na kujadili Bajeti ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
kwa mwaka wa fedha 2019/2020, na jumla ya Wizara 15 ambazo bajeti zao
zimewasilishwa, zimejadiliwa na kupitishwa makadirio yao ya mapato na matumizi
kwa mwaka wa fedha 2019/2020.
Mheshimiwa Spika,
Aidha,
Mswada wa Sheria ya Matumizi (Appropriate Bill) na Mswada wa Sheria ya Fedha
(Finance Bill) iliwasilishwa, kujadiliwa na kupitishwa katika Baraza lako
Tukufu. Kupitishwa kwa Miswada hiyo
itaiwezesha Serikali kukamilisha taratibu za kisheria katika matumizi ya fedha
pamoja na watendaji kuendelea kusimamia na kutekeleza matumizi hayo ya fedha za
Serikali. Pia, Baraza limepokea taarifa
za Serikali zifuatazo:-
- Taarifa ya Serikali kuhusu ripoti ya
kuchunguza majengo ya Skuli 19 za
Sekondari Zanzibar.
- Kauli ya Serikali juu ya Hoja ya Mjumbe kuhusu
maombi ya wananchi wa Jumuiya ya Waendesha Boda Boda Zanzibar juu ya
kupatiwa fursa ya kuendelea na kazi ya kusafirisha abiria ili kujipatia
kipato.
- Taarifa ya Serikali juu ya Hoja ya Mjumbe
kuhusu maombi ya baadhi ya wananchi wa Unguja na Pemba kuhusu suala la
usafiri wa meli baina ya Visiwa vya Unguja na Pemba. Kauli zote hizo zilijadiliwa na
kupitishwa.
- Baraza pia limepokea Ripoti ya Mdhibiti na
Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ya mwaka wa fedha 2016/2017 ambayo
itajadiliwa katika kikao kijacho.
- Mswada wa Sheria ya Kuwaenzi Viongozi wa
Kitaifa Pamoja na Mswada wa Sheria ya Utawala wa Baraza la Wawakilishi
nayo imesomwa kwa mara ya kwanza.
Shughuli zote tulizojipangia katika Mkutano huu
zimekamilika kwa wakati muafaka na kwa mafanikio makubwa.
Mheshimiwa Spika,
Kwa namna
ya pekee, natoa pongezi zangu za dhati kwa Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali Mohammed Shein na Dkt. John Pombe Magufuli,
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uongozi wao mahiri na makini katika
kusimamia na kufuatilia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka
2015 – 2020 pamoja na Serikali zetu hasa katika suala zima la kuimarisha
maadili, kuondosha rushwa, ufisadi na utekelezaji wa sheria na taratibu za nchi
yetu.
Mheshimiwa Spika, Aidha, nakupongeza wewe binafsi Mheshimiwa Zubeir
Ali Maulid, Spika wa Baraza letu Tukufu, Naibu Spika, Mheshimiwa Mgeni Hassan
Juma Wenyeviti wote wa Baraza pamoja na Katibu wa Baraza na timu yake yote kwa
usimamizi mzuri wa shughuli za Baraza letu Tukufu. Chini ya uongozi wako wa busara na weledi
tumeweza kujadiliana kwa uwazi na pale tulipotafautiana busara iliweza kutumika
kusawazisha tofauti hizo. Sina budi pia
kuwashukuru na kuwapongeza Wajumbe wote wa Baraza lao Tukufu kwa kazi nzuri
waliyoifanya ya kupitisha Bajeti ya Serikali kwa mashirikiano makubwa na kwa
kauli moja, na kukifanya kikao hiki kumalizika kwa amani, utulivu na kwa
usalama pamoja na mafanikio
makubwa. Kufanya hivyo, Waheshimiwa
Wajumbe niseme kuwa mmejijengea nyinyi wenyewe na Baraza letu Tukufu heshima
kubwa mbele ya wananchi. Ahsanteni sana.
Mheshimiwa Spika, katika Kikao hiki jumla ya maswali ya msingi 157 na maswali ya nyongeza .........
yaliulizwa na yalijibiwa kwa ufasaha na ufafanuzi wa kina na Waheshimiwa
Mawaziri husika. Maswali ambayo
hayakuweza kujibiwa kwa sababu yalihitaji taarifa za ziada kama vile takwimu,
ahadi zilitolewa maswali hayo kujibiwa kwa maandishi.
Mheshimiwa Spika,
Hivi punde tulikamilisha kazi ya Kikatiba ya kupitisha kwa vishindo
bajeti yetu kwa mwaka ujao wa fedha 2019/2020.
Ambapo katika mwelekeo wetu wa bajeti hiyo kiuchumi inakadiriwa kufikia
asilimia 7.8, mfumko wa bei unatarajiwa kudhibitiwa kwa kuendelea kuwa na
kiwango cha tarakimu moja, mapato ya ndani kuongezeka kwa asilimia 24, kutoka
TZS. 790.8 Bilioni kwa mwaka wa fedha 2018/19 hadi TZS. 859 Bilioni kwa mwaka
2019/2020. Aidha, Serikali inatarajia kufanya marekebisho ya mishahara kwa
wafanyakazi wake wenye uzoefu pamoja na makundi mengine ambayo hayajanufaika na
nyongeza za mishahara iliyopita.
Mheshimiwa Spika, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya
usimamizi wa Kiongozi wetu mahiri, Mheshimiwa Dk. Ali Mohamed Shein itasimamia
kikamilifu ahadi zake za utekelezaji wa vipaumbele vya Taifa kwa mwaka
2019/2020, ambavyo ni elimu bure hadi Sekondari, matibabu bure pamoja na dawa
za lazima, ukamilishaji wa Mradi wa ujenzi wa jengo jipya la abiria katika
Kiwanja cha Ndege cha Abeid Amani Karume kwa kutumia fedha zetu wenyewe za
ndani, kuanza kwa ujenzi wa bandari mpya ya Mpigaduri na kuanza kwa ujenzi wa
hospitali mpya ya rufaa ya Binguni.
Mheshimiwa Spika, Hayawi hayawi, huwa! Na mstahamilivu
siku zote hula mbivu, mtakumbuka kuwa tarehe 23 Oktoba, 2018 tulitiliana
saini na Kampuni ya Utafutaji wa Mafuta na Gesi Asilia ya Ras Al Khaimah (RAK
GAS) ya kufanya utafiti juu ya uwepo wa mafuta na gesi asilia katika vitalu vya
Zanzibar. Hatua hiyo ilimalizika
ikafuata hatua ya kuzichambua data na viashiria vilivyopatikana. Zoezi hili
lipo ukingoni kumalizika, na ifikapo mwezi Septemba mwaka huu matokeo ya
utafiti huo yatakabidhiwa rasmi Serikalini na baadae kama alivyotoa ahadi
Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kuwa matokeo
hayo yatatangazwa kwa wananchi hadharani.
Nitoe wito kwa wananchi wote kuendelea kuwa wastahamilivu na wazidishe
dua zao ili majibu ya utafiti huo yawe mazuri na Inshaallah kwa uwezo wa
Mwenyezi Mungu yatakuwa mazuri kama tunavyoyatarajia. Ameen.
Mheshimiwa Spika, napenda kuwaeleza wananchi kuwa Bandari ya mafuta
ya Mangapwani nayo itajengwa katika mwaka mpya wa fedha, kukamilika kwake
kutasaidia kuongeza uwezo wa kuipokea shehena kubwa ya mafuta kwa wakati mmoja
na kuweza kusambaza mafuta kwa ufanisi ndani na nje ya nchi. Hivyo, tutaweza
kuondosha kabisa tatizo la upungufu wa mafuta nchini na kuongeza ukusanyaji wa
mapato ya Serikali maradufu.
Mheshimiwa Spika, Yajayo Yanafurahisha, muda mfupi kutoka sasa meli mpya ya kisasa katika
ukanda wetu huu ya kubeba mafuta MT Ukombozi itawasili na kukabidhiwa rasmi
Serikalini. Meli hiyo imenunuliwa kwa
kutumia bajeti zetu za ndani. Kuwasili
kwa meli hiyo itasaidia kwa kiasi kikubwa kujitosheleza katika usafirishaji wa
mafuta na kupelekea kupunguza gharama za usafirishaji wa nishati hiyo.
Mheshimiwa Spika, ujenzi wa shule tatu za ghorofa zitakazokuwa na
dakhalia zake pamoja na kuzipatia vifaa vyote vinavyohitajika vikiwemo vya
maabara, maktaba na fanicha, zitajengwa mbili Unguja na Pemba moja. Kwa upande wa Unguja zinatarajiwa kujengwa
katika Mkoa wa Mjini Magharibi na Kaskazini Unguja na kwa Pemba itajengwa
katika Mkoa wa Kaskazini. Skuli hizo
zitajengwa kupitia mkopo nafuu unaotolewa na BADEA. Ujenzi huo utafanyika wakati ambapo skuli 9
zile za ghorofa zikiwa mbioni kuanza kuchukua wanafunzi mara tu baada ya
kuwekwa fanicha na vifaa vya maabara.
Pia, Vyuo vitatu vya Elimu Mbadala navyo vitaanza kufanya kazi katika
mwaka huu wa bajeti vitaanza kufanya kazi, vyuo hivyo ni vile vya Maruhubi,
Makunduchi kwa Unguja na Daya kwa Pemba.
Mheshimiwa Spika, miongoni mwa mambo yaliyozungumzwa kwa hamasa kubwa
katika mkutano huu lilikuwa ni suala zima la ajira kwa vijana wetu. Tumekusikieni Waheshimiwa, na Serikali
imekuwa ikichukua hatua mbali mbali ili kuhakikisha vijana wetu wanakuwa na
ajira, tunaujua ukubwa wa tatizo hili ambalo ni tatizo la dunia na sio kwa
Zanzibar peke yake au Tanzania. Hata
hivyo, kwa kutambua hilo kupitia mfuko wa vijana Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar imetenga Shilingi Bilioni Nne za Kitanzania kwa ajili ya kuwapatia
mikopo ili waweze kujiajiri. Nitoe wito
kwa vijana kujikusanya kutafuta mradi wa kufanya ili kuitumia vizuri fursa
hiyo.
Mbali na
mfuko huo, Serikali ya Abudhabi kupitia mfuko wa Khalifa (Khalifa Fund) utatoa
TZS. Bilioni 23 kwa Zanzibar kwa ajili ya kusaidia tatizo la ajira kwa vijana
wetu, kupatikana kwa fedha hizo inatokana na ziara aliyoifanya Mheshimiwa Rais
wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi katika Falme za Kiarabu
mwishoni mwa mwaka jana. Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar nayo itaongeza kiasi kama hicho kilichotolewa na Abudhabi
Fund ili kusaidia miradi ya vijana.
Aidha,
kupitia Mpango wa kunusuru Kaya Masikini chini ya Mfuko wa Maendeleo ya Jamii
(TASAF) kwa kipindi cha mwaka 2019/2020 utaendelea na kutekeleza Awamu ya Tatu
kwa kuyapa kipaumbele maeneo ya ukuzaji wa uchumi na kupunguza umasikini wa
kipato; kuinua ubora wa maisha na ustawi wa jamii; pamoja na utawala bora na
uwajibikaji. Utekelezaji wake utahusisha
Shehia zote za Unguja na Pemba. Awamu
hii itatoa msisitizo wa walengwa kufanya kazi zaidi ili kuweza kuongeza kipato
chao kwa kujishughulisha na kazi za kiuchumi ili kuondokana na umasikini
mapema.
Mheshimiwa Spika, Muungano wetu unaendelea kuimarika ndani ya miaka
55 ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali zetu mbili zimekuwa
zikiendelea kutatua changamoto zinazojitokeza kupitia mazungumzo baina ya pande
mbili.
Mwezi
Februari mwaka huu, Kikao cha Pamoja cha SMT na SMZ chini ya Uenyekiti wa
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania kilikutana Dodoma pamoja na mambo mengine kilipitisha utaratibu mpya
wa mawasiliano, kwa kuwepo kwa vikao vya Kisekta mara kwa mara pamoja na kuunda
Kamati ya Fedha, Uchumi na Biashara na Kamati ya Utawala, Katiba na
Sheria. Lengo la Kamati hizo ni kuhakikisha
kuwa changamoto au kero zinazojitokeza zinatatuliwa kwa haraka bila ya kusubiri
Kikao cha Kamati ya Pamoja baina ya SMT na SMZ.
Mheshimiwa Spika, Wiki mbili zilizopita niliongoza timu ya baadhi ya
Mawaziri na Watendaji wengine wa Serikali
kwenda Dodoma kukutana na Viongozi Wakuu wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania, wakiongozwa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Waziri Mkuu na Katibu Mkuu Kiongozi wa Tanzania Bara na Waziri wa Nchi, Ofisi
ya Makamu wa Rais (Muungano). Lengo la mkutano
huo lilikuwa ni kuwasilisha kwa ndugu zetu hali ya kutoridhishwa kwa Serikali
ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa baadhi ya mambo yanavyotokea. Miongoni mwa mambo hayo ni pamoja na kukwama
kwa miradi mikubwa ya SMZ kunakosababishwa na Sheria za Mikopo, Dhamana na
Misaada kama ilivyofanyiwa marekebisho yake ya mwaka 2017, pamoja na masharti
mapya ya mikopo kutoka kwa wakopeshaji kama vile EXIM Bank ya China. Mkutano uliendeshwa vizuri katika hali ya
kindugu na kufahamiana, na sote kwa pamoja tumebadilishana mawazo na
kuzitafutia ufumbuzi changamoto hizo.
Nichukue
nafasi hii kwa dhati kabisa kuwashukuru Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu
wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Kassim Majaliwa,
Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania kwa jinsi ambavyo walivyotupokea, kutusikiliza na jinsi
walivyotuelewa. Ni matumaini yangu na ya
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuwa masuala hayo yatapata ufumbuzi muda
mfupi ujao na Muungano wetu utaendelea kuwa imara zaidi.
Mheshimiwa Spika, Msimu huu wa
masika nchi yetu ilishuhudia mvua kubwa ambayo ilisababisha uharibifu mkubwa wa
miundombinu na makaazi ya wananchi.
Jumla ya nyumba 3,837 zimeathirika na mvua, kati ya hizo nyumba 3,037
kutoka Unguja na 800 kutoka Pemba.
Serikali ilichukua hatua ya kugawa vifaa vya kujengea na chakula kwa
walioathirika na mvua hizo. Kwa mara
nyengine tena, nawasihi wananchi wanaoishi katika maeneo hatarishi, mabondeni
wahame katika maeneo hayo. Aidha,
tuendelee kuwa na utamaduni wa kufuatilia taarifa za kitaalamu zinazotolewa na
Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania, Kanda ya Zanzibar kupitia vyombo vya habari
ili wananchi waweze kunusuru maisha yao na mali zao. Vile vile, tufuate maelekezo ya kitaalamu
yanayotolewa na Serikali kupitia Wizara ya Afya ya kujikinga na maradhi ya
mripuko yakiwemo matumbo ya kuharisha.
Miongoni mwa maelekezo yanayotolewa ni pamoja na kuchemsha maji kabla ya
kunywa, kusafisha mazingira, kuosha mikono kabla ya kula na mengineyo. Pia, nawakumbusha wazee na walezi wawe karibu
sana na watoto wao ili kuwaepusha kutembelea maeneo hatarishi.
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na hatua za kukamilisha ujenzi
wa misingi ya kuondosha maji yanayotuwama sehemu mbali mbali za nchi yetu. Kukamilika kwa misingi hiyo kutapunguza kwa
kiasi kikubwa kutuwama kwa maji barabarani hadi gari kushindwa kupita itakuwa
ni historia. Tayari misingi yenye urefu
wa mita 2,485 katika maeneo ya Bubujiko, Kidombo, Toronto, Jambiani Kibigija na
barabara ya Uwanja wa Ndege imekamilika na kuanza kazi.
Mheshimiwa Spika, tutambue kuwa ajali za barabarani zinaendelea
kuleta madhara makubwa kwa jamii na Taifa kwa ujumla. Kwani ajali hizo huondoa maisha ya ndugu zetu
ambao ndio tegemeo la familia zetu na ndio nguvu kazi ya Taifa letu. Pia baadhi yao hupata ulemavu ambao kwa kiasi
kikubwa hupunguza uwezo wao wa uzalishaji mali katika kujipatia kipato chao. Hivyo, nawasihi wasimamizi pamoja na wananchi
kuchukua tahadhari wanapoendesha vyombo vya moto wakiwa barabarani.
Mheshimiwa Spika, niruhusu kwa niaba yenu, niwapongeze wasimamizi wa
Mradi wa Uendelezaji Huduma Mjini (ZUSP) kwa kusimamia miradi iliyo chini ya
mpango huo ikiwemo mradi mkubwa wa kujenga misingi ya maji machafu katika
maeneo ya Kijangwani, Kwahani, Kibandamaiti, Sebleni, Mnazimmoja, Kwa mzushi,
Karakana, Mtopepo, Darajabovu, Kwamtipura, Mboriborini, Shaurimoyo, Saateni,
Mwanakwerekwe, Kwa Mtumwajeni, Nyerere, Kwa Wazee, Sogea, Mikunguni,
Kwaalamsha, Mpendae, Jang’ombe, Kilimani, Meya, Urusi na Migombani.
Vile vile,
si muda mrefu kutoka sasa miji yetu itaondokana kabisa na kiza totoro, ili
kuepukana na wahalifu ambao walikuwa wakinufaika kutokana na kuwepo kwa kiza
hicho.
Ninafuraha
kuwajulisha wananchi kuwa kazi za kuweka taa katika miji yetu imeanza na taa
hizo zitawekwa Unguja na Pemba. Kwa
upande wa Pemba taa za barabarani zitawekwa katika barabara za Mkoani, Chake
Chake na mji wa Wete. Kwa upande wa
Unguja taa za barabarani zitawekwa katika barabara za Uwanja wa Ndege,
Mnazimmoja, Mwanakwerekwe, Kiembesamaki, Mombasa, Kilimani, Kinazini, Mikunguni
na Mwembenjugu.
Mheshimiwa Spika, ujenzi wa jaa la kisasa huko Kibele unaendelea na
tayari umeshafikia asilimia zaidi ya 10, jaa hilo litahusisha eneo la kutenga
taka, ambazo baadhi yake zitatengenezwa
mbolea. Kumalizika kwa jaa hilo la
kisasa na la aina yake kwa ukanda wetu wa Afrika, litasaidia jitihada zetu za
kukusanya taka na kuzigeuza taka hizo kuwa ni bidhaa ambazo zitakuwa ni
kichocheo kingine cha ajira kwa vijana wetu.
Pia tutapunguza gharama kubwa inayotumiwa na Serikali katika kununua
mbolea kutoka nje ya nchi.
Mheshimiwa
Spika, Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984
kifungu cha 23(4), imeeleza kuwa:-
“Kila mzanzibar ana
wajibu wa kulinda, kuhifadhi, kudumisha uhuru, mamlaka, ardhi na umoja wa
Zanzibar “.
Nawaomba
Wajumbe na wananchi wote wa Zanzibar watambuwe kuwa ardhi ni rasilimali muhimu katika maendeleo ya nchi na wananchi
wake kiuchumi na kijamii. Hivyo, kwa mujibu wa Katiba na Sheria za Zanzibar,
rasilimali hii bado itaendelea kuwa mali ya Serikali. Wananchi na Taasisi
zitapewa ardhi kwa matumizi yao tu na haitoruhusiwa kuuzwa, kurithi, kugaiana
au kupeana kwa namna yoyote ile bila ya utaratibu na amri itayotolewa na
Serikali kwa mujibu wa sheria.
Mheshimiwa Spika, Zanzibar kwa sasa ina Sheria tisa
zinazohusiana na matumizi bora na endelevu ya ardhi lakini bado kumejitokeza
baadhi ya Viongozi, Watendaji wa Serikali na wananchi kutokuziheshimu Sheria
hizo na kuwa madalali wa kuuza au
kuchukuwa ardhi bila kufuata sheria na taratibu zilizopo, hali ambayo
inasababisha dhulma na migogoro mingi
katika jamii yetu, hivyo nawaomba watendaji wote waliopewa dhamana ya usimamizi
wa sheria za ardhi wawe wazalendo watumie taaluma zao ili kutatua migogoro ya
ardhi iliyopo kuanzia ngazi ya Shehia, Wilaya, Mikoa na Taifa kwa ujumla.
Serikali haitomvumilia na itamchukulia hatua kali mtu yeyote atakaekuwa
na tabia ya udalali au kuchukuwa ardhi kwa utashi wake na kwenda kinyume na
Sheria za nchi yetu.
Serikali
inatambua kuwa kuna baadhi ya wanaojiita wawekezaji wa kizalendo ambao hupewa
ardhi na badala yake huitumia ardhi hiyo
kwa kuitia sokoni na kuiuza kwa mamilioni ya dola. Jambo hili halikubaliki na
Serikali itawanyang’anya ardhi watu hao endapo watabainika.
Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuchukua hatua mbali mbali za
kupunguza au kuondosha kabisa migogoro ya ardhi ikiwemo kuimarisha Mahakama za
Ardhi nchini, kuendeleza hatua za maandalizi ya upimaji wa miji mipya Unguja na
Pemba, kutoa elimu kwa wananchi juu ya utekelezaji wa Sheria na Miongozo
inayotolewa juu ya usimamizi wa matumizi mazuri ya ardhi nchini.
Mheshimiwa Spika, naomba kuwaeleza wananchi kuwa, Serikali inaendelea kuhimiza matumizi
mazuri ya rasilimali zote nchini ikiwemo mchanga, kokoto na mawe. Katika utekelezaji wa rasilimali hizo,
Serikali imeelekeza utaratibu wa kufuatwa kwa upatikanaji wa mchanga kwa
mahitaji ya ujenzi nchini, kwa mujibu wa utaratibu huo mwananchi anaehitaji
mchanga anatakiwa kuanzia kwa Sheha ambapo atapewa maelekezo ya ujazaji wa fomu
husika hadi kufikia kulipia Benki.
Utaratibu huo wa Serikali unatoa nafasi nzuri na bei muafaka kwa manufaa
ya pande zote. Pamoja na kusisitiza
utekelezaji wa agizo hilo la Serikali, nachukua nafasi hii kuvitaka vyombo
husika kuwachukulia hatua za kisheria wale wote wanaokwenda kinyume bila ya
kuwaonea muhali.
Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kuwashukuru Waheshimiwa Wawakilishi kwa namna wanavyoshirikiana na Watendaji
na wananchi katika kuendelea kudhibiti mifuko ya plastiki nchini ikiwa ni
sehemu ya kuimarisha usafi wa mazingira. Mafanikio makubwa ya zoezi hilo
yameendelea kupatikana kiasi ambacho hata wenzetu Tanzania Bara na wao wameanza
zoezi hili rasmi tarehe 01 Juni, 2019. Tunawapongeza
sana! Nawaomba tuendelee
kushirikiana, Serikali itaendelea kuwachukulia hatua za kisheria kwa wale wote
watakaokiuka maelekezo ya udhibiti huo ili kuhakikisha mazingira yetu
yanaimarika.
Mheshimiwa Spika,
Tatizo la matumizi ya Dawa za
Kulevya limeendelea kuathiri sekta mbali mbali za uzalishaji na hivyo
kudhoofisha ukuaji wa uchumi na afya za Wazanzibari hasa vijana ambao ni nguvu
kazi ya Taifa letu. Serikali kwa kushirikiana na washirika mbali mbali wa ndani
na nje ya nchi imefanya jitihada za kukabiliana na tatizo hili ambapo mwaka 2015 jumla ya kesi 183 sawa na kilo
68.6 za dawa za kulevya ziliripotiwa,
mwaka 2018 kesi 654 sawa na kilo 722.22 za dawa za kulevya
zilikamatwa. Jitihada hizo zinalenga
kupunguza madhara na matumizi ya Dawa za Kulevya, pamoja na kudhibiti
uingizaji na usambazaji wa dawa hizo
hapa nchini.
Miongoni mwa jitihada hizo ni kuendeleza Kituo
cha Tiba na marekebisho ya tabia kilichopo Kidimni, kuhakiki vielelezo vya kesi za
dawa za kulevya, kuteketeza dawa za kulevya zilizopo katika maeneo ya uhifadhi
wa kisheria na
kufanya marekebisho ya Sheria ya Dawa za kulevya.
Mheshimiwa Spika,
Mahakama
ni mhimili tunaouamini ambao una Mamlaka ya kutekeleza utoaji wa haki pasina
kuingiliwa na mhimili mwengine wowote, tunawaomba watendaji wa muhimili huu
kuendelea kutekeleza sheria ipasavyo kwa wale wote watakaokiuka taratibu za
sheria wakiwemo wasafirishaji, wauzaji na watumiaji wa dawa za kulevya. Kwa kufanya hivyo, tutaifanya Zanzibar kuwa
huru dhidi ya uingizwaji wa dawa za kulevya na kutumia nguvu kazi yake vizuri
kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu.
Mheshimiwa
Spika, Suala la mgawanyo wa madaraka kati ya
mihimili mitatu ya dola, yaani Serikali (Mamlaka ya Utendaji), Baraza la
Wawakilishi (Mamlaka ya Kutunga Sheria) na Mahakama (Mamlaka ya kutekeleza
utoaji wa haki), imepewa umuhimu mkubwa na kuainishwa katika Katiba ya Zanzibar
ya mwaka 1984 kifungu cha 5A.
Mheshimiwa
Spika, Baraza la Wawakilishi ni chombo
kitukufu chenye hadhi na heshima ya pekee, kinachofuata Sheria, Kanuni,
Miongozo na Maadili kwa Wajumbe na Watendaji wake. Chombo hiki kipo kwa ajili
ya kuwakilisha na kuwaletea maendeleo wananchi wa Zanzibar. Hivyo, ni vyema kwa
baadhi yetu Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi kuwacha kuzungumzia maslahi yao
binafsi au kuwatetea baadhi ya watu kwa maslahi yao au utashi wao na kusahau
wajibu wao waliopaswa kutekeleza katika Majimbo yao waliyochaguliwa.
Mheshimiwa
Spika, asilimia kubwa ya Wajumbe wa Baraza
lako Tukufu ni wa Chama cha Mapinduzi
(CCM), hivyo, katika Ilani ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 - 2020 ukurasa wa 236
kifungu namba 189 kinasomeka:-
“…..ili
Chama cha Mapinduzi kiendelee kukubalika na kuaminiwa na wananchi ni muhimu
viongozi wake wawe karibu na wananchi kwa kuwatembelea, kuwasikiliza kero zao
na kuzitafutia majawabu......”
Waheshimiwa
wenzangu wa Baraza la Wawakilishi, nawaomba
sana turudi katika maeneo yetu, ili tukamalizie Utekelezaji wa Ilani yetu ya
CCM ya 2015 -2020 pamoja na ahadi nyengine kama tulivyowaahidi wananchi wetu,
tukumbuke kuwa kuna msemo wa
Kiswahili unaosema kuwa:
“Ada
ya Mja hunena Muungwana ni Kitendo”
Ni vyema Wajumbe tuwatendee wananchi
wetu matendo mema na mazuri ili na wao wakumbuke fadhila za matendo hayo katika
wakati ujao.
Mheshimiwa Spika,
Katika kuharakisha na kuimarisha maendeleo ya
Majimbo yetu ya uchaguzi, Serikali imeshatoa fedha za Mfuko wa Maendeleo ya
Jimbo kwa Majimbo yote 54 kwa Unguja na Pemba. Nawakumbusha Waheshimiwa
Wawakilishi wa Majimbo kushirikiana na Kamati zao katika matumizi ya fedha
hizo. Vile vile, tunawasisitiza kufanya marejesho kwa wakati ili taratibu za
kupata fedha za awamu nyengine ziweze kufanyika mapema iwezekanavyo.
Mheshimiwa Spika,
Kwa mara
nyengine tena, nakupongeza wewe binafsi, na wale wote waliofanikisha Mkutano
huu wakiwemo Waandishi wa Habari, Wakalimani wa lugha ya alama na wananchi wote
wa Zanzibar kwa kuendelea kudumisha amani na utulivu na kumuunga mkono
Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Ali
Mohammed Shein. Mungu alibariki Baraza letu la Wawakilishi, Mungu aibariki
Zanzibar na watu wake, Mungu aibariki Tanzania.
Mheshimiwa Spika,
Baada ya maelezo
hayo, naomba sasa kwa heshima na taadhima kutoa hoja kwamba Baraza lako Tukufu
liakhirishwe hadi siku ya Jumatano tarehe 18 Septemba, 2019 saa 3.00 barabara
za asubuhi panapo majaaliwa.
Mheshimiwa Spika, nomba kutoa hoja.
No comments:
Post a Comment