Habari za Punde

SMZ Kujenga Kiwanda Kikubwa Cha Kusarifu Mwani Zanzibar.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iko katika hatua za mwisho za makubaliano ya ujenzi wa kiwanda kikubwa cha kusarifu mwani kwenye eneo la Chamanangwe, Kisiwani Pemba.

Dk. Shein aliyasema hayo katika ufunguzi wa Maonyesho ya Nane Nane yaliyofanyika huko Langoni, Wilaya ya Magharibi “A” Mkoa wa Mjini Magharibi ambayo yalihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa vyama vya siasa na Serikali akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd pamoja na wananchi wengine.

Rais Dk. Shein alisema kuwa ujenzi wa kiwanda hicho utafanyika kwa mashirikiano kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Kampuni ya OCEAN FRESH pamoja na Kampuni ya KAPA CARAGEENAN NUSANTARA kutoka nchini Indonesia.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein alisema kuwa kukamilika kwa ujenzi wa kiwanda hicho cha mwani kutapelekea kufanyika mabadiliko makubwa ya kilimo cha mwani, uzalishaji wake, bei pamoja na maendeleo yake ya hapo baadae.

“Mwani ni zao linaloshughulikiwa na wananchi wengi humu visiwani mwetu hasa kina mama, kwa kuwaunga mkono wananchi hao katika jitihada zao za kulima na kuuza zao hilo, Serikali imekusudia kuliendeleza zao la mwani”,alisisitiza Rais Dk. Shein.

Aidha, Rais Dk. Shein alisema  kuwa azma hiyo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ni miongoni mwa ajenda zake kuu ambazo imezipangia Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi izitekeleze kwa kushirikiana na Wizara ya Biashara na Viwanda.

Dk. Shein amekuwa akichukua juhudi za makusudi katika kuliimarisha zao la mwani ambapo katika ziara yake aliyoifanya mwezi Agosti mwaka jana 2018 nchini Indonesia alipata fursa ya kutembelea na kukutana na uongozi wa Kampuni ya mwani ya ‘AGAR Swallow’ ya nchini Indonesia kwa lengo la kukuza mashirikiano katika kuliimarisha zao la mwani hapa Zanzibar.

Alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iko tayari kushirikiana na Indonesia katika kuhakikisha zao hilo linaimarika kwani Zanzibar ni miongoni mwa wazalishaji wakubwa wa zao hilo duniani hivi sasa.

Dk. Shein pia, aliueleza uongozi huo kuwa azma moja wapo ya kufanya ziara ya kukitembelea kiwanda hicho ni kujifunza sambamba na kuangalia utaalamu unaofanyika kwa lengo la kupanua wigo kutoka kwa kampuni hiyo kubwa na yenye uzoefu wa muda mrefu nchini humo.

Nao uongozi wa Kampuni ya mwani ya ‘AGAR Swallow’ ya nchini Indonesia uliahidi kushirikiana na Zanzibar katika kuliimarisha zao la mwani ambalo limekuwa ni miongoni mwa zao kuu la biashara katika visiwa vya Zanzibar wakati ulipofanya mazunguzo na Rais Dk. Shein katika ofisi za Kampuni hiyo zilizopo mjini Jakarta wakati alipokitembelea kiwanda hicho.

Katika mazungumzo hayo, Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni hiyo Hendrico Soewardjono alimueleza Rais Dk. Shein azma ya Kampuni hiyo ya  kushirikiana na Zanzibar katika kuliendeleza na kuliimarisha zao la mwani.

Alieleza kuwa Kampuni hiyo tayari imepata mafanikio makubwa ambapo aina ya bidhaa yake ya unga wa mwani ambayo hutengenezewa bidhaa mbali mbali za vyakula na dawa imekuwa na soko kubwa na bidhaa zake huzisafirisha nchi mbali mbali duniani.

Aliongeza kuwa kutokana na Zanzibar kuliendeleza zao hilo la mwani na kulimwa kwa wingi Kampuni yake iko tayari kutoa ushirikiano unaohitajika ikiwa ni pamoja na kutoa mafunzo juu ya uendelezaji wa  zao hilo pamoja na utafutaji wa masoko.

Mkurugenzi Mkuu huyo alimueleza Dk. Shein kuwa aina ya unga anaotokana na mwani wa aina ya grasilarias unaotengenezwa kiwandani hapo umekuwa ukitumika sana kwa kutengenezea bidhaa mbalimbali ambazo zimekuwa maarufu duniani.

Alieleza jinsi wanavyolisarifu zao la mwani huku akieleza kuwa miongoni mwa bidhaa zinazotengenezewa unga huo ni vyakula, vipodozi, dawa zikiwemo dawa za meno pamoja na kutengeneza bidhaa nyengine mbali mbali.

Aidha, kiongozi huyo wa Kampuni ya AGAR alieleza namna Serikali ya Indonesia kupitia Kampuni yake hiyo inavyoliendeleza na kulisimamia zao la mwani pamoja na kushirikiana na kampuni ndogo ndogo zinazofanya biashara ya zao hilo nchcini humo.

Pia, kiongozi huyo alieleza kuwa kutokana na Kampuni hiyo kupata mafanikio makubwa itakuwa ni jambo la busara kushirikiana na Zanzibar katika kuliimarisha zao hilo pamoja na kuja kuonesha uzoefu na mafanikio waliyoyapata kwa lengo la kuwasaidia wakulima wa mwani wa Zanzibar

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.