Habari za Punde

Ukuaji wa Usawa wa Kijinsia, Tanzania Inakuja Juu katika Nchi za SADC


Katibu Mtendaji wa SADC, Dkt.Stagomena Tax,(katikati), Waziri wa Nishati, Dkt.Medard Kalemani, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, Mtendaji Mkuu wa  Taasisi ya Kusini mwa Afrika kwenye Masuala ya Utafiti(Southern Africa Association Reseach SADC), Munetsi  Madakufamba na Mjumbe wa Taasisi ya Kusini mwa Afrika kwenye Masuala ya Utafiti (Southern Africa Association Reseach SADC) Madaraka Nyerere wakionesha nakala za macahapisho  ya Usawa wa Kijinsi.

Na. Paschal Dotto - Maelezo Dar es Salaam.                                                                         
Tanzania imepiga hatua kubwa katika masuala ya usawa wa kijinsia kwa yake miongoni mwa nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za kusini mwa Afrika (SADC) kwa kuwawezesha wanawake kuweza kujikita zaidi katika kujiwezesha kukuza mitaji na kuinua uchumi wao.

Akizungumza katika uzinduzi wa Machapisho ya kuimarisha usawa wa jinsia na uwezeshaji wanawake kwa Nchi za Kusini mwa Afrika, uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere, Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe.Ummy Mwalimu, alisema kuwa Tanzania imepiga hatua kubwa katika kutambua sheria za usawa wa kijinsia kwani baadhi ya masuala ya kuwawezesha wanawake  katika sekta mbalimbali yanaonekana.

Waziri Ummy aliyataja machapisho  hayo kuwa ni chapisho la Mkakati wa SADC kuhusu wanawake, Amani na Usalama, ufuatiliaji kuhusu masuala ya Jinsia na Maendeleo, Mkakati wa SADC kwa ajili ya kushughulikia ukatili wa kijinsia, Ufuatiliaji wa SADC kuhusu sekta ya nishati na Mpango-kazi wa SADC katika suala la Maendeleo yote yakilenga kuwawezesha wanawake wa Jumuiya ya Kusini mwa Afrika.

“Serikali ya Tanzania inatambua uwepo wa usawa wa kijinsia pamoja na uendelezwaji wanawake katika nchi yetu, na hili limetambuliwa katika Katiba yetu kama suala muhimu kwa haki za binadamu, na lipo kwenye dira ya maendeleo ya 2025 ambapo wanawake wamehusishwa zaidi katika kuifikisha Tanzania uchumi wa kati”, Waziri Ummy.

Waziri alisema kuwa mwaka 2000 Serikali iliweka sera kuhusu masuala ya wanawake na maendeleo ya kijinsia nchini, ambapo katika katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kifungu namba 66(1) kinachoeleza ushiriki wa wanawake katika masuala ya bunge kwa Asilimia 30.

Katika kutekeleza hilo, Serikali iliweka viti maalum kwa wabunge wanawake, na mpaka sasa ubunge kwa wanawake viti vimeongezeka kutoka asilimia 22 mwaka 2005 mpaka asilimia 37 mwaka 2019, na. kwa kuzingatia zaidi, nchi imeweza kuweka historia kwa Nchi za Kusini mwa Afrika kwa kuwa na Makamu wa Rais mwanamke (Samia Suluhu Hassan).

Waziri Ummy alisema idadi ya majaji imeongezeka kutoka asilimia 34 mwaka 2005 mpaka asilimia 41 mwaka 2019, akaongeza kuwa kwa sasa Tanzania inatekeleza mpango wa kuwainua wanawake wajasiriamali kwa kuwapa mikopo nafuu kwa shughuli zao za ujasiriamali.

Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa SADC, Dkt.Stagomena Tax alisema kuwa Serikali ya Tanzania inafanya vizuri katika kuweka usawa kwa jinsia zote, akaeleza kuwa katika tathmini, sera za kikanda na kitaifa zimehuishwa lakini  bado ukanda huo wa Afrika haujafikia malengo ya kuwa asilimia 50 kwa 50 hasa katika masuala ya siasa.

Dkt.Stagomena alisema katika ukanda huo wa Afrika nchi zinazofanya vizuri kwenye masuala ya siasa kwa kuweka 50 kwa 50 ni pamoja na Afrika Kusini na Visiwa vya Ushelisheli, lakini kwa nchi ambazo zinakuja vizuri kwa sasa ni Tanzania.

“Ukiongelea Usawa wa Kijinsia kwenye siasa ni maana ya 50 kwa 50, katika ukanda wetu wa Kusini mwa Afrika, nchi ambazo zimefikia hatua hiyo ni Afrika ya Kusini na Sheliseli, lakini Tanzania ipo kwenye nafasi nzuri kwa nchi ambazo ziko juu”, Dkt.Stagomena Tax.

Aidha, Dkt. Stagomena alieleza kuhusu masuala ya nishati na kueleza jinsi Tanzania inavyokuja kutatua masuala nishati kwa kujenga mradi mkubwa wa umeme Julius Nyerere Hydro Power Project(JN HPP), na mkakati mkubwa kwa SADC ni kuweza kuzalisha na kuleta umeme pamoja “kwenye power pool”, kwa hiyo mradi huo utasaidia ukanda huo wa Afrika.

Naye, Waziri wa Nishati, Dkt.Medard Kalemani, alieleza jinsi Tanzania inavyojikita katika kutekeleza mipango mikakati ya kufikia Megawati 10,000 ifikapo mwaka 2025, ambapo Tanzania itaweza kuchangia umeme mkubwa kwenye “Power pool” ya nchi za SADC na kuweza kuimarisha upatikanaji wa umeme ukanda huo wa Afrika.

“Mkakati mkubwa wa SADC ni kuimarisha miundombinu ambayo inachochea ukuaji wa uchumi wa viwanda, na nchi wanachama tumekubaliana mambo makubwa manne ambayo ni kuzalisha umeme wa kutosha kama nchi, kujihakikishia umeme unaotabirika, na kuchangia umeme katika mradi wa pamoja unaoitwa (SADC Power Pool)”, Alisema Dkt.Medard Kalemani.

Alisema kuwa Tanzania ina vyanzo vingi vya kuzalisha umeme ikiwemo gesi ambayo kwa sasa inazalisha kiasi cha Megawati 884, lakini Serikali inafanya jitihada za kuvumbua gesi asilia ambayo ipo takribani futi za ujazo trilioni 57.54 na kati ya hiyo trilioni 8.8 inatumika kuzalishia umeme kwa sasa.

Alisema kuwa masuala ya kuwa na umeme mwingi kwa Nchi za Kusini mwa Afrika kutasaidia wanawake wengi kutotumia nishati mbadala kama vile kuni inayotokana na ukataji miti, kwa hiyo machapisho hayo yamekuja muda muafaka wa kufanya mapinduzi ya nishati kwa Nchi za SADC.

Baadhi ya Machapisho ya Usawa wa Kijinsi kwa nchi za Jumuiya ya Nchi za Kusini mwa Afrika SADC yaliyozinduliwa leo Katika Mkutano wa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, Waziri wa Nishati, Dkt.Medard Kalemani na Katibu Mtendaji wa SADC, Dkt.Stagomena Tax, katika Kituo cha Mikutano cha Kimtaifa Julias Nyerere Jijini Dar es Salaam.


Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, akizungumza katika uzinduzi wa Machapisho ya Usawa wa Kijinsi kwa nchi  za Jumuiya ya Nchi za Kusini mwa Afrika SADC yaliyozinduliwa Agosti 14, 2019, katika Kituo cha Mikutano cha Kimtaifa Julias Nyerere Jijini Dar es Salaam.


Mjumbe wa Taasisi ya kusini mwa Afrika kwenye masuala ya Utafiti(Southern Africa Association Reseach SADC) Madaraka Nyerere, akizungumza na Waandishi wa Habari(hawapo pichani ) kuhusu ushirikiano wa Taasisi hiyo na SADC katika masuala ya utafiti wa nchi hizo.


Katibu Mtendaji wa SADC, Dkt.Stagomena Tax (katika waliokaa) akiwa kwenye picha ya pamoja na Mawaziri pamoja na watendaji wengine kutoka nchi za SADC mara baada ya uzinduzi wa Majarida mbalimbali yanayohusu masuala ya usawa wa kijinsia nchi za SADC yaliyozinduliwa leo Agosti 14, 2019, katika Kituo cha Mikutano cha Kimtaifa Julias Nyerere Jijini Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.