Katibu Mtendaji wa
SADC, Dkt.Stagomena Tax,(katikati), Waziri wa Nishati, Dkt.Medard Kalemani,
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, Mtendaji
Mkuu wa Taasisi ya Kusini mwa Afrika
kwenye Masuala ya Utafiti(Southern Africa Association Reseach SADC),
Munetsi Madakufamba na Mjumbe wa Taasisi
ya Kusini mwa Afrika kwenye Masuala ya Utafiti (Southern Africa Association
Reseach SADC) Madaraka Nyerere wakionesha nakala za macahapisho ya Usawa wa Kijinsi.
Na. Paschal Dotto - Maelezo Dar es Salaam.
Tanzania imepiga hatua kubwa katika masuala ya usawa
wa kijinsia kwa yake miongoni mwa nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za
kusini mwa Afrika (SADC) kwa kuwawezesha wanawake kuweza kujikita zaidi katika kujiwezesha
kukuza mitaji na kuinua uchumi wao.
Akizungumza katika uzinduzi wa Machapisho ya
kuimarisha usawa wa jinsia na uwezeshaji wanawake kwa Nchi za Kusini mwa
Afrika, uliofanyika katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere,
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Mhe.Ummy Mwalimu,
alisema kuwa Tanzania imepiga hatua kubwa katika kutambua sheria za usawa wa
kijinsia kwani baadhi ya masuala ya kuwawezesha wanawake katika sekta mbalimbali yanaonekana.
Waziri Ummy aliyataja machapisho hayo kuwa ni chapisho la Mkakati wa SADC
kuhusu wanawake, Amani na Usalama, ufuatiliaji kuhusu masuala ya Jinsia na
Maendeleo, Mkakati wa SADC kwa ajili ya kushughulikia ukatili wa kijinsia,
Ufuatiliaji wa SADC kuhusu sekta ya nishati na Mpango-kazi wa SADC katika suala
la Maendeleo yote yakilenga kuwawezesha wanawake wa Jumuiya ya Kusini mwa
Afrika.
“Serikali ya Tanzania inatambua uwepo wa usawa wa
kijinsia pamoja na uendelezwaji wanawake katika nchi yetu, na hili
limetambuliwa katika Katiba yetu kama suala muhimu kwa haki za binadamu, na
lipo kwenye dira ya maendeleo ya 2025 ambapo wanawake wamehusishwa zaidi katika
kuifikisha Tanzania uchumi wa kati”, Waziri Ummy.
Waziri alisema kuwa mwaka 2000 Serikali iliweka sera
kuhusu masuala ya wanawake na maendeleo ya kijinsia nchini, ambapo katika
katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kifungu namba 66(1) kinachoeleza
ushiriki wa wanawake katika masuala ya bunge kwa Asilimia 30.
Katika kutekeleza hilo, Serikali iliweka viti maalum
kwa wabunge wanawake, na mpaka sasa ubunge kwa wanawake viti vimeongezeka
kutoka asilimia 22 mwaka 2005 mpaka asilimia 37 mwaka 2019, na. kwa kuzingatia zaidi,
nchi imeweza kuweka historia kwa Nchi za Kusini mwa Afrika kwa kuwa na Makamu
wa Rais mwanamke (Samia Suluhu Hassan).
Waziri Ummy alisema idadi ya majaji imeongezeka kutoka
asilimia 34 mwaka 2005 mpaka asilimia 41 mwaka 2019, akaongeza kuwa kwa sasa
Tanzania inatekeleza mpango wa kuwainua wanawake wajasiriamali kwa kuwapa
mikopo nafuu kwa shughuli zao za ujasiriamali.
Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa SADC, Dkt.Stagomena
Tax alisema kuwa Serikali ya Tanzania inafanya vizuri katika kuweka usawa kwa
jinsia zote, akaeleza kuwa katika tathmini, sera za kikanda na kitaifa
zimehuishwa lakini bado ukanda huo wa
Afrika haujafikia malengo ya kuwa asilimia 50 kwa 50 hasa katika masuala ya
siasa.
Dkt.Stagomena alisema katika ukanda huo wa Afrika nchi
zinazofanya vizuri kwenye masuala ya siasa kwa kuweka 50 kwa 50 ni pamoja na
Afrika Kusini na Visiwa vya Ushelisheli, lakini kwa nchi ambazo zinakuja vizuri
kwa sasa ni Tanzania.
“Ukiongelea Usawa wa Kijinsia kwenye siasa ni maana ya
50 kwa 50, katika ukanda wetu wa Kusini mwa Afrika, nchi ambazo zimefikia hatua
hiyo ni Afrika ya Kusini na Sheliseli, lakini Tanzania ipo kwenye nafasi nzuri
kwa nchi ambazo ziko juu”, Dkt.Stagomena Tax.
Aidha, Dkt. Stagomena alieleza kuhusu masuala ya
nishati na kueleza jinsi Tanzania inavyokuja kutatua masuala nishati kwa kujenga
mradi mkubwa wa umeme Julius Nyerere Hydro Power Project(JN HPP), na mkakati
mkubwa kwa SADC ni kuweza kuzalisha na kuleta umeme pamoja “kwenye power pool”,
kwa hiyo mradi huo utasaidia ukanda huo wa Afrika.
Naye, Waziri wa Nishati, Dkt.Medard Kalemani, alieleza
jinsi Tanzania inavyojikita katika kutekeleza mipango mikakati ya kufikia
Megawati 10,000 ifikapo mwaka 2025, ambapo Tanzania itaweza kuchangia umeme
mkubwa kwenye “Power pool” ya nchi za SADC na kuweza kuimarisha upatikanaji wa
umeme ukanda huo wa Afrika.
“Mkakati mkubwa wa SADC ni kuimarisha miundombinu
ambayo inachochea ukuaji wa uchumi wa viwanda, na nchi wanachama tumekubaliana
mambo makubwa manne ambayo ni kuzalisha umeme wa kutosha kama nchi,
kujihakikishia umeme unaotabirika, na kuchangia umeme katika mradi wa pamoja
unaoitwa (SADC Power Pool)”, Alisema Dkt.Medard Kalemani.
Alisema kuwa Tanzania ina vyanzo vingi vya kuzalisha
umeme ikiwemo gesi ambayo kwa sasa inazalisha kiasi cha Megawati 884, lakini
Serikali inafanya jitihada za kuvumbua gesi asilia ambayo ipo takribani futi za
ujazo trilioni 57.54 na kati ya hiyo trilioni 8.8 inatumika kuzalishia umeme
kwa sasa.
Alisema kuwa masuala ya kuwa na umeme mwingi kwa Nchi
za Kusini mwa Afrika kutasaidia wanawake wengi kutotumia nishati mbadala kama
vile kuni inayotokana na ukataji miti, kwa hiyo machapisho hayo yamekuja muda
muafaka wa kufanya mapinduzi ya nishati kwa Nchi za SADC.
Baadhi ya Machapisho
ya Usawa wa Kijinsi kwa nchi za Jumuiya ya Nchi za Kusini mwa Afrika SADC
yaliyozinduliwa leo Katika Mkutano wa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii,
Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, Waziri wa Nishati, Dkt.Medard Kalemani
na Katibu Mtendaji wa SADC, Dkt.Stagomena Tax, katika Kituo cha Mikutano cha
Kimtaifa Julias Nyerere Jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Afya,
Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, akizungumza katika
uzinduzi wa Machapisho ya Usawa wa Kijinsi kwa nchi za Jumuiya ya Nchi za Kusini mwa Afrika SADC
yaliyozinduliwa Agosti 14, 2019, katika Kituo cha Mikutano cha Kimtaifa
Julias Nyerere Jijini Dar es Salaam.
Mjumbe wa Taasisi ya
kusini mwa Afrika kwenye masuala ya Utafiti(Southern Africa Association Reseach
SADC) Madaraka Nyerere, akizungumza na Waandishi wa Habari(hawapo pichani )
kuhusu ushirikiano wa Taasisi hiyo na SADC katika masuala ya utafiti wa nchi
hizo.
Katibu Mtendaji wa
SADC, Dkt.Stagomena Tax (katika waliokaa) akiwa kwenye picha ya pamoja na
Mawaziri pamoja na watendaji wengine kutoka nchi za SADC mara baada ya uzinduzi
wa Majarida mbalimbali yanayohusu masuala ya usawa wa kijinsia nchi za SADC
yaliyozinduliwa leo Agosti 14, 2019, katika Kituo cha Mikutano cha Kimtaifa
Julias Nyerere Jijini Dar es Salaam.
No comments:
Post a Comment