Habari za Punde

Sherehe za Uzinduzi wa Meli Mpya ya Mafuta ya MT.Ukombozi II.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akiwahutubia Wananchi na Wafanyakazi wa Shirika la Meli Zanzibar, wakati wa hafla ya Uzinduzi wa Meli Mpya ya Kisasa ya Mafuta MT.Ukombozi II, uliofanyika katika bandari ya Malindi.  

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amelitaka Shirika la Meli Zanzibar kuwa na mipango madhubuti ya mafunzo kwa watendaji na waongozaji wa vyombo vya baharini, ili kuweza kufanyakazi zao kwa weledi.

Dk. Shein amesema hayo katika sherehe za uzinduzi wa Meli mpya ya Mafuta ya MT. Ukombozi ll, zilizofanyika Bandarini Malindi, mjini hapa.

Alisema wafanyakazi wanaoendesha vyombo baharini wana jukumu kubwa katika utekelezaji wa kazi zao, hivyo ni vyema kwa Shirika hilo likawa na mipango madhubuti katika  upatikani wa mafunzo ya muda mrefu, kati na muda mfupi ili waweze kutekeleza kazi zao kwa ufanisi.

Aliutaka uongozi huo kutotosheka na utaalamu walionao watendaji wake, hivyo akataka ratiba maalum za mafunzo ziandaliwe, sambamba na kuwapa mishahara na stahiki zote zinazoendana na ukubwa wa kazi wanazofanya.    

 “Hawa wanafanya kazi nzito sana, sio rahisi kuranda na meli baharini kila siku, nasisistiza upatikanaji wa taaluma katika kuendesha vyombo hivi”, alisema.

Aidha, aliutaka uongozi huo kuhakikisha watendaji hao wanajuwa kanuni na sheria za nchi pamoja na zile za kimataifa, ili waweze kutekeleza vyema kazi zao.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kusisitiza umuhimu wa wafanyakazi wa meli hiyo kufanyakazi kwa misingi ya uwajibikaji,  uadilifu na nidhamu, kwa kigezo kuwa hatua hiyo itawajengea heshima.

“Lazima tuzingatie nidhamu ya kazi zetu, mfanye kazi kwa kuzingatia imani, nidhamu na uwajibikaji kikamilifu”, alisema.

Vile vile, Dk. Shein aliwataka watendaji wa meli hiyo kuendeleza ushirikiano uliopo kati yao, sambamba na kusisitiza umuhimu wa kuwepo uangalifu na umakini ili uwepo  usalama wa wafanyakazi na mali za serikali.

Aidha, alisifia ubora wa meli hiyo kwa kuwa katika viwango vya kimataifa, kama ilivyo kwa meli ya MV, Mapinduzi ll.

Dk. Shein aliwatanabahisha wananchi akiwataka kuwa wazalendo kwa kuwa na utamaduni wa  kuvipenda na kuvitukuza vilivyo vyao, badfala ya kuviponda.

“Hii ni meli yetu sote watu wa Zanzibar……imenunuliwa na Serikali yetu kwa manufaa yetu”, alisema.

Alieleza kuwa ujio wa meli hiyo unatarajiwa kuondoa kabisa tatizo la upungufu wa mafuta linalojitokea mara kwa mara nchini, akibainisha kuwa hivi sasa Serikali italazimika kuhoji pale nishati hiyo itakapoadimika.

Aidha, alisema uaptikanaji wa meli hiyo ni kichocheo katika uharakishaji wa ujenzi wa Bandari mpya ya Mpigaduri,

Katika hatua nyengine, Dk. Shein alisema uamuzi wa Serikali wa kujenga Bandari ya Mpigaduri upo pale pale, ukitarajiwa kuanza mishoni mwa mwaka huu au mapema mwakani.

Alisema serikali tayari imefanikisha maandalizi ya ujenzi wa Bandari mpya kwa ajili ya Mafuta na Gesi katika eneo la Mangapwani, kwa kuweka miundombinu, ikiwemo uwekaji wa umema, ujenzi wa barabara pamoja na nyumba kwa ajili ya wakaazi wa Dundua.

Aidha, alisema Serikali imefanikisha ununuzi wa meli za MV Mapinduzi 11, MT Ukombozi 11 ambapo kwa ujumla zimegharimu zaidi ya shilingi Bilioni 136 , pamoja na mambo mbali ya maendeleo, kutokana na kuimarika kwa uchumi wake, hatua inayotokana na ukusanyajii mzuri wa mpato.

Mapema, Waziri wa Ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji, Sira Ubwa Mamboya alisema ujenzi wa meli hiyo ni utekelezaji wa Ilani ya CCM ya 2015-2020, na kubainisha kuwa kwa kiasi kikubwa serikali imekamilisha ahadi zake.

Alisema Wizara hiyo inalenga kuaanda utaratibu maalum kwa Wazanzibari wote wenye nia ya kuiona  meli hiyo kupata fursa hiyo, sambamba na kuahidi kuitunzwa ili iweze kuleta tija kwa Taifa.

Nae, Waziri wa Fedha na Mipango, ambae pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ujenzi wa Meli hiyo, Balozi Mohamed Ramia, alisema meli hiyo ni bora na kubainisha kuwa thamani yake inaendana na hali halisi ya mahitaji, hivyo kuwa kichocheo katika uingizaji wa mapato na kukuza uchumi wa Taifa.

 Aidha, akitowa salam mjenzi wa meli hiyo kutoka Kampuni ya DAMEN ya nchini Uholanzi Ronald Maat, alisema meli hiyo imeundwa kwa kufuata viwango vya kimataifa na kuzingatia usalama baharini.

Alitowa pongezi kwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa uamuzi wake wa kujenga meli hiyo na kubainisha azma ya Kampuni kuiunga mkono Serikali kwa juhudi zake za kuifanya kuwa na vyombo vya uhakika vya usafiri  baharini,  hususan katika usafirishaji wa mafuta.

Mapema, Katibu Mkuu Wizara ya ujenzi, Mawasiliano na Usafirishaji, Mustafa Aboud Jumbe alisema ujenzi wa meli hiyo iliyotengenzwa na Kampuni ya DAMEN kutoka Uholanzi, umegharimu shilingi Bilioni 36 hadi kukamilika kwake.

Alisema ujenzi huo umegharamiwa na serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na kubainisha kuwa fedha zote zimeshalipwa katika Kampuni husika.

Alisema meli hiyo yenye urefu wa mita 86.21 ina uwezo wa kubeba tani 3,500 za mafuta ya aina nne, ikiwemo mafuta taa, Dizeli, Petroli na mafuta ndege.

Katika hafla hiyo,pamoja na mambo mengine kulifanyika tukio la makabidhiano ya meli hiyo baina ya mjenzi kutoka Kampuni ya DAMEN na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.