Habari za Punde

Ardhi Iliyotengwa Kwa Ajili ya Kilimo Zanzibar ni Vyema Ikatumika Kwa Shughuli Hiyo na si Vyenginevyo -Dk. Shein.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akimsikiliza Mkurugenzi wa Idara ya Kilimo cha Umwagiliaji Maji Ndg. Haji Hamad Salum, akitowa maelezo ya Ujenzi wa Mradi wa Miundombinu ya Kilimo cha Umwagiliaji wa Maji (kulia kwa Mkurugenzi) Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe.Balozi Seif Ali Iddi,wakiwa katika eneo la ujenzi wa Mradi huo  katika Kijiji cha Kinyasini Kisongoni Wilaya ya Kaskazini “A” Unguja, (kushoto kwa Rais) Waziri wa Kilimo Maliasili Mifugo na Uvuvi.Mhe.Mmanga Mjengo Mjawiri na Naibu Waziri wa Kilimo Maliasili Mifugo na Uvuvi Mhe.Dkt. Makame Ali Ussi. Wakiwa katika eneo la ujenzi huo


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza kuwa ardhi iliyotengwa kwa ajili ya kilimo  hapa Zanzibar ni vyema ikatumika kwa ajili ya shughuli hiyo na si vyenginevyo.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo katika hotuba yake aliyoitoa katika uwekaji wa jiwe la msingi la ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji maji huko Kinyasini Kisongoni, Wilaya ya Kaskazini B, Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Alieleza kuwa kilimo ni ardhi, hivyo endapo ardhi haitokuwepo kilimo hakitofanyika kwani hata historia ya Zanzibar inaonesha wafanyakazi na wakulima walishindwa kulima kabla ya Mapinduzi kutokana na kunyanganywa ardhi yao.

Rais Dk. Shein alisema kuwa hapa Zanzibar hivi sasa ardhi imekuwa ndogo sana kutokana na matumizi mabaya ya ardhi yanayofanywa na baadhi ya wananchi.

Akieleza historia ya ardhi, Rais Dk. Shein alisema kuwa miaka mingi kabla ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12, 1964 Wazanzibari waliteseka katika kutafuta ardhi na pale walipotaka kulima ilibidi wakapige magoti kwa wakoloni.

Alisema kuwa madhila ya kunyanyaswa katika ardhi yao yaliondoshwa na Mapinduzi yaliyomg’oa Sultani mnamo Januari 12, 1964 ambapo ni miaka 56 tokea kutokea Mapinduzi hayo.

Alisema kuwa uhuru wa Zanzibar unahisabika rasmi kuanzia Januari 12, 1964 na kupelekea sekta zote ikiwemo ardhi kuwa huru na tarehe 8 Machi 1964 hayati mzee Karume alitoa tangazo rasmi la SMZ ikiwa ni amri na sheria ya Serikali ambayo ilitengenezwa utaratibu wa sheria na katiba juu ya sekta hizo ikiwemo ardhi.

Rais Dk. Shein aliyanukuu maneno ya Hayati mzee Karume aliyoyasema kwamba “shamba lolote lililokuwa asili yake ni serikali halafu serikali ile ya kifisadi imelichukua shamba hili na imemuuzia jamaa yake kwa njia ya hadaa shamba hili litarudi serikalini, ardhi yote ya Unguja na Pemba ni mali ya serikali na kila mtu wa Unguja na Pemba ana haki ya kuitumia..”

Rais Dk. Shein alisema kuwa mashamba 745 yalihodhiwa na watu wachache kabla ya Mapinduzi ambapo kuna mmoja alikuwa na mashamba 300 pekee yake na mtu wa chini alikuwa na mashamba matatu ambapo waliuziana kwa matabaka na hakukuwa na Mwafrika aliyekuwa na shamba.

Wananchi wa Zanzibar hawakuwa na  shamba la kulima na badala yake aliyekuwa akitaka kulima alitakiwa kujiunga na chama cha Hizbu hali ambayo Chama Cha ASP kilipelekea kununua shamba la Kilombero ambalo lilinunuliwa chini ya uongozi wa Marehemu Mzee Karume.

Alieleza kuwa mnamo tarehe 11 Novemba 1964 Marehemu Mzee Karume aligawa heka tatu tatu kwa wananchi ambapo walitakiwa walime katika maisha yao yote na sio wajenge au wakate viwanja.

Alieleza azma ya Serikali ya Awamu ya Saba ya kuongeza idadi ya matrekta ili wananchi wapate kulima kwa ufanisi zaidi na kuweza kuwasaidia wakulima wa mpunga hasa akina mama ambao wamekuwa wakifanya kazi kubwa katika kilimo hicho.

Aliongeza kuwa Serikali imekuwa ikiongeza mazingira mazuri zaidi hasa katika kilimo cha mpunga ili kulima kwa faida ambapo pia, juhudi zimechukuliwa katika kuhakikisha kiwanda cha matreka kinafufuliwa.

Alisema kuwa Serikali imetayarisha Sera ya Kilimo pamoja na Mpango Mkuu wa Kilimo ambavyo ndio vitu vikubwa ambavyo vimepelekea kubuniwa miradi mbali mbali kama huo uliozinduliwa hivi leo.

Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Awamu ya Saba imekuwa ikiwafidia wakulima kwa asilimia 75 ya gharama zote na asilimia 25 zinabaki kwa wananchi kwenye pembejeo kama vile matreka, mbolea, mbegu bora na dawa za kuulia magugu.

Aidha, Rais Dk. Shein aliwashajiisha wananchi wa Zanzibar kutumia mchele wa Zanzibar ambao ni mzuri na una sifa zote.

Pia, Rais Dk. Shein alieleza kuwa kilimo ni maji hivyo, lazima maji yawepo ili kuweza kulima kilimo cha kisasa cha umwagiliaji maji ambacho ni cha uhakika na ndio maana Serikali ikaanzisha miradi hiyo.

Sambamba na hayo, alieleza hatua za Serikali zilizochukuliwa katika kuimarisha sekta ya kilimo ikiwa ni pamoja na kuanzisha Taasisi ya Utafiti ya Kilimo Zanzibar kwa lengo la kuuendeleza utafiti wa mazao mbali mbali hapa nchini.

Alieleza hatua zinazochukuliwa katika kukiimarisha Chuo cha Kilimo cha Kizimbani ikiwa ni pamoja na kukiunganisha na Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA).

Pia, alieleza hatua zitakazochukuliwa katika kuondosha matumizi ya majembe ya mikono na badala yake alieleza hatua zitakazochukuliwa katika kuhakikisha matrekta yanaongezeka.

Alisema kuwa mradi huo umechelewa kutokana na urasimu uliokuwepo ndani ya Wizara hiyo lakini hatimae imewezekana na kuanza vyema.

“Nayasema haya wananchi wajue kwamba tumejichelewesha wenyewe kutokana na urasimu......tumechelewa kuanza lakini hatimae tumeanza vizuri sana na kwa umakini mkubwa”, alisema Dk. Shein.

Aidha, Rais Dk. Shein aliitaka Wizara ya Kilimo kuongeza kasi kwenye kazi zao na kundoa mivutano miongoni mwao na wawe wamoja na pale wanapopewa maelekezo na Serikali wayafanyie kazi na wasishindane kwani ushindani hauna tija.

Alisema kuwa mambo hayo hayampi matumaini na badala yake yanamtia hofu kwani lengo lake ni kuhakikisha asilimia 80 ya chakula kinapatikana hapa nchini kutokana na mikakati ya Serikali kinyume na hivi sasa ambapo kinapatikana kwa asilimia 40.

Alieleza kuwa Mradi huo ni vyema ukaenda vizuri na baada ya miezi 24 uweze kufanya kazi na kuleta tija kwa wananchi wa Zanzibar huku akisisitiza umuhimu wa kushauriana.

Nae Waziri wa Kilimo , Maliasili, Mifugo na Uvuvi Mmanga Mjengo Mjawiri alisema kuwa azma ya Wizara hiyo ni kuhakikisha kuwa kilimo kinacholimwa hapa nchini kinakuwa na tija kubwa huku akieleza agizo la Serikali katika sekta ya kilimo.

Alisema kuwa katika kutekeleza Ilani ya uchaguzi ya CCM Wizara hiyo imepiga hatua kubwa juhudi ambazo zinatokana na ushauri mzuri wa Rais Dk. Shein.

Alisema kuwa Wizara hiyo itaendelea kuwatumia wataalamu hao katika sekta ya kilimo hasa katika kilimo cha mpunga huku akisisitiza hatua zitakazochukuliwa ili wakulima walime kwa faida na thamani.

Nae Naibu Mwakilishi Mkuu wa Benki ya Exim ya Korea Bwana Kang Sang Jin alieleza jinsi ya umuhimu wa mradi huo ambao utasaidia kwa kiasi kikubwa kukuza uchumi wa Zanzibar sambamba na kuendeleza mashirikiano kati ya nchi hiyo na Zanzibar.

Alieleza mashirikiano yaliopo kati ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Kilimo pamoja na Mkandarasi wa Mradi ambaye anafanya kazi vizuri huku akieleza kuwa mradi huo utaimarisha sekta ya kilimo na kuongeza uzalishaji chakula.

Nae Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Malisiali, Mifugo na Uvuvi katika risala yake alieleza kwamba uwekeaji wa jiwe la Msinmgi wa ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji maji unadhihirisha kuanza rasmi utekelezaji wa Mradi huo unaotekelezwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia mkopo kutoka Benki ya Exim-Korea.

Alisema kuwa mradi huo utaendelezana kujenga miundombinu katika eneo la hekta 1,524 katika mabonde 7 ya umwagiliaji maji kwa Unguja na Pemba.

Akitaja mgawanyo wa mradi huo aliyataja maeneo ya Cheju hekta 803, Kinyasini hekta 217, Kobokwa hekta 194, Kilombero hekta 100, Chaani hekta 71, Makwararani hekta 78 na Mlemele hekta 61.

Alisema kuwa mradi huo pia, utajumuisha ujenzi wa miundombinu ya misingi ya umwagiliaji, mabwawa manne makubwa ya kukinga na kuhifadhi maji ambapo moja kati ya hayo ni hilo la Kinyasini, Chaani kwa upande wa Unguja na mabonde ya Mlemele na Makwararani.

Aliongeza kuwa mradi huo utachimba visima 49 na kuweka pampu zake ambapo visima 33 vitachimbwa katika bonde la Cheju, visima 33 Cheju, visima 10 Kibokwa na visima 6 vitachimbwa katika bonde la Kilombero.

Kwa upande wa gharama za utekelezaji mradi huo, Katibu Mkuu huyo alisema kuwa jumla ya dola za Kimarekani takriban milioni 64.304  ambapo kati ya fedha hizo dola milioni 50 ni mkopo kutoka Benki ya Exim- Korea NA Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inachangia kiasi cha dola za Kimarekani milioni 14.804.

Alisema kuwa mpaka sasa tayari Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Kilimo kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha na Miango imeshaweza kulipa fidia kwa wananchi takriban 327 yenye thamani ya jumla ya TZS Bilioni 1.145.

Aidha, alisema kuwa mradi huo utaongeza uzalishaji wa mpunga katika maeneo ya umwagiliaji maji kutoka tani 5,400 kwa mwaka 2018 na kukadiriwa kufikia tani 2,384 kwa mwaka ifikapo mwaka 2021 ambapo ongezeko litafikia uzalishaji wastani wa tani 60,000 za mpunga na kugunguza kwa asilimia 70 ya uagiziaji wa mvheke ncje ya nchi.

Mapema Rais Dk. Shein alipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Idara ya Umwagiliaji Haji Hamid ambaye alimueleza kwamba mkataba wa ujenzi wa mradi huo ulitiwa saini tarehe 06.12.2018 baina ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Wizara ya Kilimo, Maliasi, Mifugo na Uvuvi na Kampuni ya ujenzi ya KOLON-HANSONL kutoka Jamhuri ya Watu wa Korea.

Pia, alieleza kuwa Kampuni ya KRC-DASAN JV ambayo inatoka Korea ndio Mshauri Mwelekezi wa Mradi huo wa umwagiliaji maji ambao ni mkubwa kabisa kuwahi kutekelezwa hapa Zanzibar huku akitumia fursa hiyo kumueleza uendelezaji wake.

Viongozi wa Jimbo la Kiwengwa kwa niaba ya wananchi wa Jimbo hilo nao kwa upande wao walitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa juhudi kubwa anazozichukua katika kuwapelekea miradi ya maendeleo ikiwa ni pamoja na kutekeleza kwa vitendo Ilani ya Uchaguzi ya CCM huku wakieleza mafanikio yatakayopatikana kutokana na mradi huo.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.