Hotuba ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein. Katika Sherehe za Mapinduzi Kuadhimisha Miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar. Uwanja wa Amaan Jijini Zanzibar 12-1-2020.
Mabibi na Mabwana, Assalam Aleikum.
Tuna wajibu wa
kumshukuru Mwenyezi Mungu, Muumba wa Mbingu na Ardhi na vyote vilivyomo ndani
yake, kwa kutujaaliya afya njema na kutuwezesha kujumuika katika Uwanja huu wa
Amaan, kwa ajili ya kuadhimisha kilele cha Sherehe za miaka 56 ya Mapinduzi
Matukufu ya Zanzibar, ya tarehe 12 Januari, 1964. Natoa shukurani zangu za
dhati kwaviongozi wote wa Kitaifa wakiongozwa na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania; Dkt. John Pombe Joseph
Magufuli,kwa kuja kuungana nasi katika kilele cha Sherehe za Miaka 56 ya
Mapinduzi yetu.Kadhalika, natoa shukurani kwa viongozi wengine wote wa Serikali
ya Jamhuriya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar mliopo
madarakani na mliostaafu, Waheshimiwa Mabalozi na Wawakilishi wa Mashirika ya
Kimataifa, wageni wetu pamoja na Viongozi wa Dini na Vyama vya Siasa kwa kuja kujumuika nasi
katika sherehe hizi adhimu na muhimu. Kwenu nyote, nasema Ahsanteni sana.
Shukurani za pekee nazitoa kwenu, ndugu
wananchi,kwa kuhudhuria kwa wingi katika Maadhimisho haya ya miaka 56 ya
Mapinduzi, mkionesha furaha kubwa
mliyonayo; ambayo ni kielelezo cha kuzithamini sherehe hizi. Sote tuna wajibu
wakutambua thamani ya maadhimisho ya Mapinduzi ya tarehe 12 Januari, 1964, kwa
sababu Mapinduzi ndio yaliyoikata minyororo ya ubaguzi na aina zote za dhulma
zilizokuwa zikiwakabili wafanyakazi na wakulima wa Zanzibar. Kwa hivyo, Mapinduzi ndio yaliyoikomboa
Zanzibar na watu wake na kuleta uhuru wa kweli kwa wananchi wote wa
Zanzibar. Ni ukweli uliowazi kwamba
Mapinduzi ndio yaliyofungua ukurasa mpya wa maendeleo ya Zanzibar na watu wake
na tutaendelea kuyasherehekea maadhimisho haya kwa furaha, vifijo na nderemo
kila mwaka.
Ndugu
Wananchi,
Kila tunaposherehekea maadhimisho ya
Siku hii muhimu, inatupasa tuwakumbuke waasisi wa Mapinduzi, walioongozwa na
Jamadari wetu, Marehemu Mzee Abeid Amani Karume, pamoja na viongozi wenzake
waliojitoa muhanga kwa ajili ya kuikomboa Zanzibar. Tunamuomba Mwenyezi Mungu
awalaze mahali pema Peponi waasisi wetu wa Mapinduzi waliokwishatangulia mbele
ya haki. Vile vile, Mola awape afya njema na umri mrefu, waasisi wetu walio
hai,ili tuendelee kunufaika na hekima na
busara zao, katika kuyadumisha malengo ya Mapinduzi yetu.
Ni dhahiri kwamba
mafanikio tuliyoyapata katika sekta zote za maendeleo katika kipindi cha miaka
56 ya Mapinduzi, yametokana na kuendelea kuwepo sababu za msingi za kufanyika
kwa Mapinduzi hayo kwa kuondoa ubaguzi na dhulma, kuendeleza umoja, mshikamano
na usawa kwa watu wote; pamoja na amani
na utulivu. Kwa hivyo, ni jukumu letu sote tufahamu kwamba hakuna mbadala wa
amani katika maendeleo ya mtu mmoja mmoja, jamii na taifa kwa jumla.
Ni wajibu wetu
sote tuisimamie amani, na tuifuate misingi ya sheria, kwa sababu matukio ya
uvunjaji wa amani huanza na vitendo vinavyopingana na sheria za nchi. Kwa hivyo,
natoa wito kwenu ndugu wananchi, kila mmoja wetu azingatie umuhimu wa amani na
usalama kuwa ni jambo la msingi na lazima.
Ndugu Wananchi,
Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar, ya Awamu yaSaba, tangu iliopoingia madarakani tarehe 3
Novemba, mwaka 2010, imepata mafanikio ya kuridhisha. Tunafarajika na mafanikio
tunayoyapata katika utekelezaji wa mipango yetu mikuu, ikiwemo MKUZA Awamu ya
I, II na III, Ilani ya Uchaguzi Mkuu ya CCM ya2010 na 2015, Dira ya Maendeleo
ya 2020 pamoja na Mipango ya Maendeleo ya Kimataifa.Mafanikio hayo yanatokana
na jitihada mbali mbali za pamoja zinazofanywa na Serikali, Mashirika na
Taasisi mbali mbali za Kitaifa na Kimataifa zinazotuunga mkono, utendaji mzuri
wa viongozi wa ngazi zote, mamlaka mbali mbali, watumishi wa umma pamoja na
ushirikiano wa kizalendo kutoka kwa wananchi. Kwenu nyote nasema, Ahsanteni
sana.
Ndugu Wananchi,
Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba, katika kipindi cha miaka tisa, imeendelea
na juhudi za kutekeleza mipango ya mageuzi ya kiuchumi, ili kuhakikisha kwamba
uchumi na ustawi wa wananchi wa Zanzibar unaimarika. Juhudi hizo ni pamoja na
kuiimarisha na kuiendeleza hali ya amani na utulivu zilizopelekea kuongezeka kwa Pato Halisi la
Taifa kwa mara 1.6 zaidi kutoka thamani ya TZS Bilioni 1,768 mwaka 2010, hadi
kufikia thamani ya TZS Bilioni 2,874 mwaka 2018. Vile vile, kasi ya ukuaji wa
uchumi imeongezeka kutoka asilimia 4.3 mwaka 2010 hadi kufikia asilimia 7.1
mwaka 2018. Kadhalika, Pato la Mwananchi nalo limeongezeka kutoka TZS 942,000,
sawa na Dola za Kimarekani 675 mwaka 2010, hadi kufikia TZS 2,323,000, sawa na Dola
za Kimarekani 1,026, mwaka 2018. Hilo ni ongezeko la asilimia 147 kwa thamani
ya fedha za Tanzania. Haya ni mafanikio
makubwa tuliyoyapata.
Kadhalika, mfumko
wa bei nao kasi yake imepungua kutoka
asilimia 14.7 mwaka 2011 hadi asilimia 3.9 mwaka 2018. Hatua hio imewawezesha
wananchi kupata bidhaa muhimu kwa bei inayoridhisha.
Vile vile,
kuimarika kwa uchumi kumepelekea ongezeko la ukusanyaji wa mapato mwaka hadi
mwaka. Kwa mwaka wa fedha 2018/2019, mapato ya ndani yalifikia TZS Bilioni
748.9, ikilinganishwa na jumla ya TZS Bilioni 181.1 zilizokusanywa mwaka
2010/2011. Hili ni ongezeko la makusanyo la mara 4.1. Utegemezi wa bajeti umepungua na umefikia
wastani wa asilimia 5.7 mwaka 2018/2019, kutoka wastani wa asilimia 30.2 mwaka
2010/2011. Natoa pongezi kwa Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) pamoja na Mamlaka ya
Mapato Tanzania (TRA) kwa kutekeleza vizuri majukumu yao kwa kipindi chote cha
miaka tisa. Hongereni sana.
Jitihada za
kuendeleza uwekezaji zimefanikiwa katika kipindi cha miaka 9 ambapo Mamlaka ya Kukuza Uwekezaji
Zanzibar (ZIPA), imeweza kuwavutia wawekezaji katika miradi ya maendeleo kwa
sekta mbali mbali. Hadi kufikia mwaka
2018, jumla ya miradi ya uwekezaji 304 yenye mtaji waDola za Kimarekani Bilioni
3.74 imetekelezwa. Miradi hio imetengeneza ajira zipatazo 16,866.
Ndugu Wananchi,
Jitihada kubwa za
kuimarisha sekta ya elimu zimefanywa na Serikali katika awamu mbali mbali,
katika kipindi cha miaka 56 iliyopita, kwa madhumuni ya kuyatekeleza malengo ya
Mapinduzi ya kutoa elimu bure bila ya ubaguzi kama ilivyotangazwa na Marehemu
Mzee Abeid Amani Karume, tarehe 23 Septemba, 1964. Katika kutekeleza uamuzi huo,
Serikali imeongeza Bajeti ya Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, mara 3.8,
kutoka TZS Bilioni 47.093 mwaka 2010/2011 hadi TZS Bilioni 178.917 mwaka
2019/2020.
Ndugu Wananchi,
Ongezeko la idadi
ya skuli, taasisi nyengine za elimu na wanafunzi katika ngazi zote, ni miongoni
mwa mafanikio yaliyofikiwa katika Sekta ya Elimu. Hadi mwaka 2019, idadi ya
Skuli za Maandalizi imefikia 382 zenye wanafunzi 85,974; ikilinganishwa na
skuli 238, zilizokuwa na jumla ya wanafunzi 29,732 katika mwaka 2010. Skuli za
msingi zimeongezeka na zimefikia skuli 381, zenye wanafunzi 290,510 mwaka 2019,
kutoka skuli 299 zilizokuwa na jumla ya wanafunzi 226,812, mwaka 2010. Hadi
kufikia mwishoni mwa mwaka 2019, zipo jumla la Skuli za Sekondari 284 zenye
wanafunzi 130,713 ikilinganishwa na skuli 105 zilizokuwa na wanafunzi 80,008, mwaka 2010.Majengo kadhaa ya ghorofa
ya skuli za Msingi na Sekondari yamejengwa, Unguja na Pemba.
Hivi sasa tunapoadhimisha
miaka 56 ya Mapinduzi ya Zanzibar, elimu ya juu inatolewa katika vyuo vikuu vitatu; Chuo Kikuu cha Taifa cha
Zanzibar (SUZA), Chuo Kikuu cha Zanzibar(ZU) na Chuo Kikuu cha Al-Sumeit. Vyuo
hivi vina idadi ya wanafunzi 7,090, wanaosoma kuanzia ngazi ya Cheti hadi
Shahada ya Uzamivu (PhD), ikilinganishwa na wanafunzi 3,572waliokuwepo katika mwaka
2010/2011. Katika kipindi cha miaka tisa (9) cha uongozi wa Awamu ya Saba,
jumla ya wanafunzi 9,648 walihitimu katika Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar
(SUZA) kwa kupata vyeti, stashahada na shahada mbali mbali.
Ndugu Wananchi,
Wanafunzi wa elimu
ya juu, masomo yao yanagharamiwa na Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu ya Zanzibar
na baadhi yao wanalipiwa na Bodi ya Mikopo ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.Bodi ya Mikopo ya Zanzibar imeshatumia jumla ya
TZS Bilioni 60.2, kwa ajili ya kuwadhamini wanafunzi 4,145 wa elimu ya juu
katika vyuo vikuu mbali mbali vya ndani na nje ya nchi. Serikali inawalipia
gharama zote wanafunzi wanaofaulu daraja
kwanza katika mitihani ya kidato cha sita, kutoka wanafunzi 10 mwaka 2016 hadi
60 mwaka 2019.
Ndugu Wananchi,
Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar inatekeleza kwa mafanikio makubwa Sera yake ya kutoa
matibabu bure kama ilivyoanzishwa mara tu baada ya Mapinduzi ya tarehe 12
Januari, 1964.
Kutokana na kuongezeka
kwa bajeti ya Wizara ya Afya kwa mara 9.6 kutoka TZS Bilioni 10.81 mwaka
2010/2011 hadi TZS Bilioni 104.24 mwaka 2019/2020, huduma za afya zimeimarika
sana na zinaendelea kutolewa bure. Ongezeko la fedha za bajeti zimesaidia sana
katika kuziimarisha huduma za tiba na kinga
katika hospitali, vituo vya afya na zahanati zote kwa Unguja na Pemba. Serikali imeziimarisha huduma za Hospitali ya
Mnazi mmoja hadi kufikia hadhi ya hospitali ya rufaa na sasa inatambuliwa rasmi
kuwa ni hospitali ya kufundisha madaktari, miongoni mwa hospitali za Jumuiya za
Nchi za Afrika ya Mashariki.
Jitihada za
Serikali za kusomesha madaktari, wakiwemo madaktari bingwa, zimewezesha
kuongeza idadi ya madaktari na watumishi wengine wa afya. Jitihada hizi zimeimarisha uwiano wa
madaktari na watu wanaohudumiwa. Hivi sasa daktari mmoja anawahudumia watu
6,276 (1:6,276) kutoka daktari mmoja kuwahudumia watu 31,838 (1:31,838), mwaka
2010. Kwa hivyo, kutokana na kuongezeka kwa
idadi ya madaktari na wataalamu wengine mbali mbali wa fani za afya,
upatikanaji wa vifaa vya kisasa vya uchunguzi wa maradhi na nyenzo mbali mbali
za kufanyia kazi, pamoja na kuimarishwa kwa maeneo ya kufanyia kazi kumepelekea
huduma zatiba na kinga zizidi kuimarika.
Jitihada za Serikali
za kupambana na Malaria zinaendelezwa na kasi ya kuenea kwake bado ipo chini ya
asilimia moja (0.4%), ingawa baadhi ya maeneo machache ya Mjini yamebainika
kuongezeka wagonjwa wa Malaria.Juhudi zinaendelezwa za utoaji elimu kwa wananchi,
ugawaji wa vyandarua vyenye dawa ya muda mrefu na upigaji wa dawa za ndani ya
nyumba na maeneo yenye mazalia ya mbu.
Ndugu Wananchi,
Kadhalika,
maambukizo ya UKIMWI yameendelea kushuka na
hivi sasa yamefikia kiwango cha asilimia 0.4 kutoka asilimia 0.6 mwaka
2010. Kuhusu vifo vinavyotokana na uzazi vimepungua na vimefikia 155 kwa kila
vizazi hai 100,000, ikilinganishwa na vifo 288 kwa kila vizazi hai 100,000
katika mwaka 2010. Jitihada za
kuwaelimisha wajawazito wajifungulie hospitali badala ya majumbani, zimesaidia
sana, ambapo mwaka 2010 wajawazito 51,912 walijifungulia majumbani
ikilinganishwa na 37,803 mwaka 2019.
Pamoja na
mafanikio niliyoyaelezeakatika hotuba yangu hii, kwa kudhibitiwa kwa baadhi ya
maradhi, lakini zipo changamoto zilizobainika katika hospitali zetu za Unguja
na Pemba; ambazo ni kuongezeka kwa maradhi yasiyoambukiza kama vile maradhi ya
sukari, matatizo mbali mbali ya maradhi ya moyo, maradhi ya figo, saratani ya
shingo ya kizazi na saratani nyengine.
Matarajio yangu ni kwamba wataalamu wa Taasisi ya Utafiti ya Afya na
wengine waliopo katika Idara mbali mbali za hospitali zetu na kwa kuendelea
kushirikiana na wataalamu wengine wa Kimataifa; watafanya kazi zao za utafiti
kwa bidii, ili Serikali iweze kuchukua hatua za kukabiliana na maradhi hayo.
Ndugu
Wananchi,
Serikali imeendelea kuziimarisha huduma
za maji safi na salama katika Mikoa yote ya Unguja na Pemba. Utekelezaji wa
mradi wa maji wa Mkoa Mjini Magharibi, kwa mkopo wa Dola za Kimarekani Milioni
21.246 kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika, niliouelezea katika hotuba yangu ya
miaka miwili iliyopitaumekamilika na umezinduliwa tarehe 6 Januari, 2020.Mradi
huu unatarajiwakuwanufaisha wananchi wanaoishi
katika Shehia 11 za Mji Mkongwe na Shehia 16 za maeneo mingine, kwa kupata
kiwango cha maji cha uhakika katika matumizi yao ya kila siku.
Kwa upande wa Mkoa wa Kaskazini Unguja,
hivi sasa vijiji vya Mkoa huo vinaendelea kupata huduma bora za maji safi na
salama,tangu mwezi wa Aprili 2018, ulipokamilika mradi uliotekelezwa na Kampuni ya “First Highway
Engineering of China”.
Kwa upande wa Pemba, huduma za maji
safi na salama zinapatikana kwa kiwango kizuri, ingawa bado zipo baadhi ya changamoto
katika baadhi ya maeneoambayo zinaendelea kufanyiwa kazi.
Mradi wa maji wa Wilaya ya Magharibi
“A” na “B” na maeneo mengine, wa mkopo wa Benki ya Exim kutoka India wa Dola za
Kimarekani Milioni 92 unatarajiwa kuanza baadae mwaka huu.
Ndugu Wananchi,
Kwa lengo la kuwawezesha wananchi kiuchumi na kukabiliana
na tatizo la ajira, Serikali ilianzisha Mfuko wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi
katikamwaka 2014, ambaounatoa mikopo isiyo na
riba na yenye masharti nafuu kwa wananchi.Hadi kufikia tarehe 30 Juni,
2019, jumla ya mikopo 2,997 yenye thamani ya TZS Bilioni 4.0, imeshatolewa kwa
wananchi wa Unguja na Pemba.
Vile vile, katika
jitihada hizo, mnamo mwezi wa Septemba, 2019, Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar, imeanzisha Mfuko wa Vijana, ili kuwawezesha kiuchumi, utakaokuwa na
jumla ya Dola za Kimarekani Milioni 20, sawa na TZS Bilioni 46 kwa kipindi cha
miaka 5 ijayo. Katika fedha hizo, Dola
za Kimarekani Milioni Kumi ni msaada kutoka kwenye Mfuko wa Khalifa Fund wa Sheikh
Khalifa Bin Zayed Al Nahyan, Rais wa UAE
na Dola Milioni Kumi zimetolewa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Hatua hio
itasaidia sana katika juhudi zinazochukuliwa na Serikali katika kukuza ajira na
ustawi wa vijana. Mipango ya matumizi ya
fedha hizo imekamilika na utekelezaji wa mpango huo utaanza, baadae mwaka huu.
Kuhusu vikundi vya
ushirika na SACCOS, Serikali imeviendeleza, ambapo kuanzia mwaka 2010/2011 hadi
Oktoba 2019, jumla ya vyama 39 vya Ushirika vya Akiba na Mikopo na vyengine
1,652 vya uzalishaji mali vimesajiliwa.Hatua hio, imeongeza idadi ya vyama vya
ushirika vilivyosajiliwa kufikia 3,676 hadi mwezi Oktoba 2019.Mwamko wa
wananchi wa kujiunga na SACCOS umepelekea kuongezeka kwa mitaji ya taasisi
hizo kutoka TZS Bilioni 3.5 mwaka
2013,hadi TZS Bilioni 14.3 mwaka 2019.
Ndugu Wananchi,
Katika kukabiliana
na changamoto zinazowakabili vijana, katika kipindi cha miaka tisa iliyopita,
Serikali imechukua hatua ya kuviwezesha vikundi 796 vya vijana kwa kuvipatia
mikopo kupitia Mfuko wa Uwezeshaji, ili wajiajiri katika shughuli za kilimo,
ufugaji na ushonaji. Kadhalika,katika mwaka 2015, Serikali ilianza kutekeleza
azma ya kuanzisha Mabaraza ya Vijana katika ngazi zote, ambayo yamekuwa ni
taasisi muhimu za ushirikishwaji wa masuala ya vijana nchini. Hadi kufikia
Disemba 2019, jumla ya vijana 16,340 wakiwemo wanawake 8,537 na wanaume 7,803
wamesajiliwa katika Mabaraza hayo.
Serikali kupitia
Programu ya Ajira kwa Vijana inakamilisha hatua za kuwaingiza vijana 660 katika
mafunzo maalumu ya amali ya miezi sita (6), na baada ya mafunzo hayo vijana
watapewa zana za kilimo, vifaa vya uvuvi na ufugaji pamoja na vifaa vya ushonaji.
Jumla ya vijana 220 wamepewa mafunzo maalumu ya kazi, kwa msaada wa Serikali na
Shirika la Kazi Duniani (ILO), ili waweze kujiajiri katika sekta ya utalii.
Ndugu Wananchi,
Mpango kazi wa
miaka mitano wa kumaliza vitendo vya ukatili na udhalilishaji wa wanawake na
watoto uliozinduliwa mwezi Agosti, 2017, umeanza kuonesha mafanikio na mwamko
wa wananchi umeongezeka katika kuyaripoti matukio hayo. Jumla ya matukio 1,091 ya udhalilishaji
yaliripotiwa katika vituo vya Polisi Unguja na Pemba kwamwaka 2017/2018
ikilinganishwa na matukio 2,449 yaliyoripotiwa mwaka 2016/2017. Matukio haya yalipungua kwa idadi ya 1358,
sawa na asilimia 124.5. Kwa mwaka 2019,
matukio ya vitendo vya ukatili na udhalilishaji vilivyoripotiwa katika vituo
vya Polisi vya Mikoa yote na yalikuwa ni 941.
Idadi hii ni upungufu wa matukio 150
ambayo ni sawa na asilimia 15.9. Jumla ya mashauri 1028 ya udhalilishaji
wa kijinsia yalifunguliwa katika mahakama za Mkoa katika kipindi cha miaka 9
iliyopita. Mashauri 630 yalitolewa
uamuzi na mashauri 398 yanaendelea.
Serikali itaendelea kuwachukulia hatua za kisheria wanaowadhalilisha
wanawake na watoto.
Ndugu wananchi,
Kwa kutambua kuwa
Wazee ni hazina kubwa ya nchi yetu na wana mchango mkubwa kwa maendeleo ya nchi yetu, Serikali imeendelea
kutoa huduma mbali mbali katika kuwatunza wazee kwenye maisha yao ya kila siku,
kwa wale wanaoishi katika nyumba za wazee Unguja na Pemba. Jumla ya wazee 28,022 waliofikia umri wa
miaka 70 na zaidi wameendelea kulipwa posho la TZS 20,000 kwa kila mwezi ikiwa
Pencheni ya Jamii.
Kutokana na Sera
ya Hifadhi ya Jamii iliyoandaliwa mwaka 2014, hivi sasa Serikali inaandaa
Mswada wa Sheria kuhusu wazee ambao tayari umepelekwa Baraza la Wawakilishi.
Kadhalika, kupitia mfuko wa TASAF, jumla ya wananchi 31,993 wamepatiwa fedha
kwa ajili ya shughuli za ujasiriamali, biashara ndogo ndogo, kilimo na ufugaji. Vile vile, jumla ya TZS Bilioni 40 zimetumika,
ili kugharamia miradi 656, yenye kuzinufaisha familia maskini kuhusiana na masuala ya
afya na elimu.
Kwa upande wa watu
wenye Ulemavu, Mfuko wa Watu wenye Ulemavu, ulioanzishwa katika mwaka 2012, ili
kuwawezesha kiuchumi, wenye jumla ya TZS Milioni 167,unatarajiwa kuanza kutoa
huduma hivi karibuni baada ya kukamilika kwa taratibu za kuuendesha mfuko huo.
Vile vile, katika kipindi hiki cha miaka tisa, watu wenye Ulemavu walisaidiwavifaa
na nyenzo 2,226 ambavyo viligawiwa Unguja na Pemba.
Ndugu Wananchi,
Katika kipindi cha
miaka tisa, shughuli za biashara nchini zimeendelea vyema. Jumla ya bidhaa zenye thamani ya TZS Bilioni 1,923.49
ziliingizwa nchini ikilinganishwa na bidhaa zenye thamani ya TZS Bilioni 710.5
zilizosafirishwa kwenda nje ya nchi.
Kadhalika, biashara
baina Tanzania Barana Zanzibar imeendelea kufanyika. Bidhaa zenye thamani ya
TZS Bilioni 71.3zilisafirishwa kwenda Tanzania Baramwaka 2011 ikilinganishwa na
bidhaa zenye thamani ya TZS Bilioni 24.2 zilizosafirishwa mwaka 2018. Vile vile bidhaa zenye thamani ya TZS Bilioni
114.4 ziliingizwa nchini kutoka Tanzania Bara mwaka 2011 ikilinganishwa na
bidhaa zenye thamani ya TZS Bilioni 269.66 zilizoingizwa nchini mwaka 2018.
Serikali zetu mbili zitaendelea kuhakikisha kwamba biashara baina ya pande zetu
mbili za Muungano inaendelea kufanyika na inaimarishwa, kwa kila upande.
Ndugu Wananchi,
Kuhusu biashara ya
karafuu, jumla ya tani 33,549.79za karafuu kavu zenye thamani ya TZS Bilioni
448.684 zimenunuliwa kutoka kwa wakulima katika kipindi cha mwaka 2010 hadi
2019, na jumla ya tani za karafuu 32,142.17 zenye thamani ya Dola
za Kimarekani 297,707,844, sawa na TZS Bilioni 553.89 zimeuzwa nje ya
nchi. Katika kipindi cha miaka tisa (9)
mfululizo Serikali ilimlipa mkulima kiwango cha asilimia 80 ya bei ya karafuu katika
soko la dunia, ambayo ni sawa na TZS 14,000; kwa kilo moja ya karafuu kavu za
daraja la kwanza. Vile vile, Serikali
imeanzisha bima maalumu kwa wakulima
wanaopata ajali na kutoa zawadi kwa wakulima bora. Hatua hizo zimewaongezea
wakulima wa karafuu ari na juhudi ya kukiendeleza kilimo hicho.
Mpango Mkakati wa
Miaka 10 wa kuliendeleza zao hilo umefanikiwa sana, ambapo jumla ya miche
ya mikarafuu 2,617,994 imeoteshwa kuanzia mwaka 2011 hadi 2017, na baadhi ya mikarafuu hio, hivi sasa
imeshaanza kuzaa. Vituo vipya na vikubwa vya kununulia karafuu vilijengwa na
utaratibu mpya wa kuishughulikia biashara ya karafuu ulitekelezwa kwa mafanikio
makubwa.
Nawashukuru
wakulima wa karafuu wa Unguja na Pemba kwa kuziuza karafuu zao katika ZSTC na
nawapongeza wananchi, ZSTC, Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi,
Vikosi vya Ulinzi na Usalama na Idara Maalum za SMZ na Vikosi Kazi vyote, kwa
kuliendeleza na kuliokoa zao la karafuu, kupambana na magendo ya karafuu na
kuyadhibiti.
Ndugu Wananchi,
Sekta ya viwanda
imeendelea kutoa mchango mkubwa katika kipindi hiki cha Awamu ya Saba. Mchango
wa sekta hio katika Pato la Taifa
umeongezeka kutoka asilimia 8.2 mwaka
2013, hadi kufikia asilimia 17.8 mwaka 2018. Utengenezaji wa bidhaa katika
baadhi ya viwanda vilivyokuwepo awali na vingine vilivyoanzishwa katika miaka ya hivi karibuni
na wawekezaji binafsi, unazidi kuimarika. Kiwanda cha Mafuta ya Makonyo na Arki za Mimeakilichopo Wawi – Pemba,
kimeimarishwa kwa kufunga mitambo mipya, mashine na vifaa vyengine vipya na vya
kisasa, vilivyogharimu jumla ya TZS Bilioni 5.4. Mipango ya Serikali ya kuanzisha kiwanda cha
kusarifu mwani kitakachoendeshwa kwa njia ya ubia na wawekezaji wa
Indonesia, sasa imekamilika. Kiwanda hicho kitajengwa huko Chamanangwe
Wete Pemba, hivi karibuni.
Wakala wa
Maendeleo ya Viwanda Vidogo Vidogo, na vya Kati (Small and Medium Industries
Development Agency - SMIDA) umeanzishwa, baada ya kutungwa kwa Sheria Namba 2 ya Wakala wa Maendeleo ya Viwanda Vidogo Vidogo, na vya Kati Zanzibar ya mwaka 2018.
Jumla ya watu 180,851 wameajiriwa au kujiajiri katika sekta ya viwanda. Natoa
pongezi maalum kwa wawekezaji katika sekta binafsi kwa kuendelea kuziunga mkono
juhudi za Serkiali za kuiimarisha sekta
hio.
Ndugu Wananchi,
Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar, ya Awamu ya Saba, imefanya juhudi za kukuza Sekta ya Utalii kwa kushajiisha
uwekezaji na ujenzi wa hoteli zinazohitajika
kwa maendeleo ya sekta hio. Tangu mwaka 2010
hadi 2019, jumla ya hoteli 153 za daraja mbali mbali zimejengwa katika
maeneo mbali mbali ya Unguja na Pemba. Hadi kufikia Novemba 2019, Zanzibar ilikuwa na jumla ya hoteli
509 zilizosajiliwa na zinazotoa
huduma, ambazo miongoni mwao, 26 ni za nyota tano na 20 za nyota nne.
Kadhalika, juhudi
kubwa zimefanywa za kuitangaza Zanzibar katika masoko mapya ya Ulaya na Asia.Idadi
ya watalii wanaowasili Zanzibar imeongezeka mara 4 kutoka 133,000 mwaka 2010 hadi kufikia watalii 538,264
mwaka 2019. Hapana shaka lengo lililowekwa katika Ilani ya CCM kwa ajili ya
Uchaguzi Mkuu wa 2015 la kuhakikisha kwamba ifikapo mwisho wa mwaka 2020
watalii wanaoingia Zanzibar wanafikia 500,000, hivi sasa lengo hili limevukwa
kwa zaidi ya watalii 38,264 kabla ya kufikia mwisho wa mwaka 2020. Serikali itaongeza jitihada za kuiimarisha
sekta hio, ili idadi ya watalii hasa wa daraja la juu, wanaotembelea nchi yetu
izidi kuongezeka.
Ndugu Wananchi,
Kwa lengo la
kukuza uchumi, kupata lishe bora na kuwa na usalama wa chakula nchini, Serikali
imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha kilimo cha mazao mbali mbali. Katika
kipindi cha miaka minane iliyopita, Serikali imeendelea kuimarisha kilimo cha
mpunga kwa kutoa ruzuku ya asilimia 75
za pembejeo mbali mbali. Teknolojia
ya kisasa ya kilimo cha mpunga cha Shadidi ilitumika kupitia Mradi wa kuongeza
uzalishaji na tija (ERPP) ambayo imechangia kuongezeka kwa mavuno ya zao la mpunga.
Jitihada hizo za Serikali, kwa jumla
zimepelekea kuongezeka kwa mavuno ya mpunga kutoka tani 21,014 mwaka 2010 hadi
tani 47,507 mwaka 2018. Ongezeko hili ni
mara 2.3 zaidi. Mazao mengine ya
chakula, matunda na mboga nayo yaliongezeka kutoka tani 289,481 mwaka 2010 na
kufikia tani 375,837 mwaka 2018, sawa na ongezeko la asilimia 30. Hali hio
imetuwezesha kujitosheleza kwa chakula kwa asilimia 60 mwaka 2018 kutoka
asilimia 51 mwaka 2011 ambapo asilimia nyengine 40 za mahitaji yetu ya chakula
yanaingizwa nchini na wafanyabiashara mbali mbali. Nawapongeza wafanyabiashara wote kwa
kuendelea kufanya kazi na Serikali yao na kuiunga mkono.
Katika
kukiimarisha na kukiendeleza kilimo cha umwagiliaji maji cha mpunga, tarehe 2
Januari, 2020 ulizinduliwa rasmi Mradi wa ujenzi wa Miundombinu ya Umwagiliaji Maji
katika mabonde saba ya mpunga; manne yapo Unguja na matatu Pemba. Mabonde hayo yana ukubwa wa hekta 1,524. Mradi wa ujenzi wa miundombinu ya umwagiliaji
maji Unguja na Pemba, umegharimu Dola za Kimarekani Milioni 50 ikiwa ni mkopo
wa Benki ya Exim ya Jamhuri ya Korea na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar
imechangia Dola za Kimarekani Milioni 14.
Vile vile, Mpango
wa Maendeleo ya Sekta ya Kilimo ya Zanzibar (Zanzibar Agricultural Development
Programme - ASDP) utakaogharimu Dola za Kimarekani Milioni 148 kwa muda wa
miaka 10, tayari umeanza kutekelezwa na baadhi ya Washirika wa Maendeleo
wameanza kusaidia.
Ndugu Wananchi,
Kwa lengo la
kuongeza kasi ya mapinduzi ya ufugaji, mwaka 2017 Serikali ilianzisha Taasisi
ya Utafiti wa Mifugo, ili kuzishughulikia changamoto za wafugaji na kuzitafutia
ufumbuzi. Vituo vinne vya huduma za
mifugo vimefanyiwa matengenezo makubwa.
Kwa lengo la kuimarisha huduma za kinga, tiba na huduma za ugani,jumla
ya vijana 224 wamepatiwa mafunzo ya kitaaluma pamoja na vifaa vya kutolea
huduma katika shehia zao. Vile vile,
jumla ya vikundi 18 vya ufugaji wa ng’ombe wa maziwa na vikundi 16 vya ufugaji wa mbuzi wa maziwa vimeanzishwa ambapo
ng’ombe wa maziwa wenye mimba 368 na mbuzi wa maziwa 720 walitolewa bure kwa
vikundi hivyo.
Ndugu Wananchi,
Katika kuendeleza
sekta ya uvuvi,Serikali ilianzisha Kampuni ya Uvuvi, ZAFICO mwaka 2017. Kampuni
hio tayariimenunua meli mpya ya uvuvi iitwayo Sehewa II, iliyotengenezwa Sri
Lanka ambayo imegharimu TZS Bilioni
1.13.Meli hio ilizinduliwarasmi tarehe 2 Disemba, 2019 na itaanza kazi ya uvuvi
kwenye Bahari Kuu hivi karibuni. Vile
vile, Kampuni ya ZAFICO katika muda mfupi ujao itaanza ujenzi wa chelezo na
mtambo wa kusarifu samaki hapo kwenye bandari ya Malindi.
Jitihada za
kuimarisha sekta ya uvuvi zimewezesha kuongezeka kwa kiwango cha samaki
kinachovuliwa kutoka tani 25,396 mwaka 2010 hadi tani 35,441 mwaka 2018. Jitihada hizi za Serikali zitapata mafanikio
makubwa baada ya kukamilika mradi wa ujenzi wa soko jipya la kisasa la samaki
pamoja na bandari ya kushushia samaki katika eneo la Malindi. Mradi ambao uliwekewa jiwe la msingi tarehe 3
Januari, 2020. Ujenzi huu wa jumla ya
Dola za Kimarekani Milioni 11.529 sawa na TZS Bilioni 26.4 ni msaada uliotolewa
na Shirika la JICA la Japan. Kwa mara nyengine natoa shukurani zangu za
dhati kwa uongozi wa JICA na Serikali ya Japan kwa msaada huu mkubwa wenye
lengo la kuimarisha sekta ya uvuvi ya Zanzibar.
Ndugu Wananchi,
Katika kipindi
hiki cha Awamu ya Saba, Serikali imepanga na kutekeleza mikakati mbali mbali,
ikiwemo kuanzishwa kwa Idara ya Mipango Miji na Vijiji, mwaka 2013, kutayarisha
na kuandaa Mpango Mkuu Mpya wa Kuendeleza miji mbali mbali ya Zanzibar pamoja
na Jiji la Zanzibar (Zanzibar City).
Hivi sasa,
tunashuhudia maendeleo makubwa ya ujenzi wa nyumba za kisasa za makaazi,
biashara na za kutoa huduma mbali mbali hapa Zanzibar. Mradi wa ujenzi wa Mji
wa Kisasa wa Fumba unatekelezwa na Kampuni ya S.S Bakhresa, Mradi wa ujenzi wa
nyumba za Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (ZSSF)huko Mbweni, ambao unakaribia
kumalizika na Mradi wa Ujenzi wa nyumba katika eneo la Nyamazi unaotekelezwa
na Kampuni ya CPS, inaendelea vizuri. Vile vile, Serikali imeanzisha mradi wa
ujenzi wa nyumba za makaazi za kisasa za ghorofa sita, majengo ya matumizi
mengine, barabara na kadhalika, katika mtaa wa Kwahani, ambapo tarehe 9
Januari, 2020 mradi huo uliwekewa jiwe la msingi.
Mradi wa ujenzi wa
maduka makubwa ya biashara hapo Michenzani niliouelezea miaka miwili iliyopita
ambao unajengwa na Mfuko wa Hifadhi ya Jamii Zanzibar (ZSSF), hivi sasa
unaendelea vizuri. Katika majengo hayo mawiili yanayojengwa, jengo la kwanza
litajulikana kwa jina la ”Michenzani Shoping Mall” na lile la pili linalojengwa
katika kiwanja cha Maskani Kaka ya Muembe Kisonge, litajulikana kwa jina la ”Sheikh
Thabit KomboMall”. Tarehe 4 Januari,
2020 Mawe ya Msingi yaliwekwa kwa ajili ya ujenzi huu. Ujenzi huu unatarajiwa kukamilika katika
kipindi cha miezi sita (6) ijayo na utagharimu jumla ya TZS Bilioni 36.94 kwa
yote mawili. Pembeni mwa maduka haya
makubwa litajengwa jengo jengine kwa ajili ya kuegesha gari (car park), za
wananchi watakaokwenda kwenye maduka hayo.
Vile vile, katika kipindi hiki majengo kadhaa ya Ofisi mbali mbali za
Serikali Unguja na Pemba, yalijengwa.
Ndugu Wananchi,
Serikali imeweza
kuufikisha umeme katika shehia zote za Unguja na Pemba. Hadi sasa, umeme
umefikishwa kwenye vijiji 518, pamoja na visiwa vidogo vidogo vitano (5), vilivyoko
Pemba. Visiwa hivyo niKisiwa Panza, Makoongwe, Shamiani (Mwambe), Fundo na
Uvinje. Hivi sasa, jitihada zinafanywa za kupeleka umeme katika kisiwa cha
Kokota na Njauhuko Pemba na kazi hiyo, inatarajiwa kuanza baadae mwaka huu.
Hivi sasa,
Serikali imeanza kutafuta njia mbadala za kupata vyanzo vya nishati ya umeme,
kutokana na ongezeko la mahitaji ya nishati hio. Kutokana na utafiti uliofanywa kwa kushirikiana na Umoja wa Ulaya
(EU), umebaini kuwepo kwa uwezekano mkubwa wa kupata umeme kutokana na nishati
ya jua. Serikali inalifanyia kazi suala
hili.
Ndugu Wananchi,
Sekta ya Mafuta na
Gesi Asilia ni eneo jengine la nishati ambalo Serikali inaendelea
kulishughulikia. Baada ya Kampuni ya RAK GAS ya Ras Al Khaimah na Kampuni ya
Mafuta na Gesi Asilia ya Zanzibar (ZPDC), kutia saini Mkataba wa Uzalishaji naMgawanyo
wa Mafuta na Gesi Asilia tarehe 23
Oktoba, 2018, kazi za utafutaji wa mafuta na gesi asilia katika kitalu cha
Pemba - Zanzibar zimeendelea vizuri.
Taarifa za utafiti uliofanywa angani, kwenye kina kikubwa cha bahari,
kina kidogo nanchi kavu kwa Unguja na Pemba. Taarifa hizo zinaendelea kufanyiwa
uchambuzi na wataalamu. Majadiliano kati
ya wataalamu wa Zanzibar na Ras Al Khaimah yanaendelea kuhusu utafiti huo
uliofanywa. Serikali itaendelea kutoa
taarifa kwa wananchi kuhusu maendeleo ya kaziya uchimbaji wa mafuta na gesi
asilia, hatua kwa hatua.
Ndugu Wananchi,
Mafanikio
yamepatikana katika kuimarisha miundombinu ya barabara ambapo, jumla ya
kilomita 129 za barabara zimejengwa kwa kiwango cha lami, Unguja na Pemba. Hivi
sasa kazi ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami Unguja, zenye urefu wa
kilomita 62.9 zinaendelea kujengwa, pamoja na kilomita 15 zilizobakia za
Ole-Kengeja. Kadhalika, ujenzi wa barabara ya Bububu-Mahonda-Mkokotoni
(kilomita 31) umekamilika na tayari barabara hio imezinduliwa tarehe 10
Januari, 2020. Vile vile, Serikali
imejenga daraja na barabara yenye urefu wa mita mia nne hapo Kibonde Mzungu, kwa
lengo la kukabiliana na changamoto zilizokuwa zikitokea katika maeneo ya
Kibondemzungu.Taa za barabarani zimewekwa kwenye daraja hilo. Mradi huo umekamilika
na umezinduliwa tarehe 9 Januari, 2020; ambapo kazi inayoendelea sasa ni
kuunganisha barabara ya eneo hilo na barabara iliyoishia kituo cha Polisi
Fuoni.
Ndugu Wananchi,
Katika kuongeza
ufanisi wa shughuli za bandari, Serikali
imefanya jitihada ya kununua zana za kisasa za kazi kwa ajili ya
kuimarisha huduma za bandari za Unguja na Pemba. Kwa upande wa bandari ya
Malindi,hatua hiyo imeongeza kasi ya
utoaji wa huduma ambapo hivi sasa, meli
kubwa zinazofika katika bandari hio, zenye uwezo wa kubeba makontena 6,000,
zinaweza kuhudumiwa kwa siku tatu tu badala ya wiki moja, kama ilivyokuwa hapo
kabla.
Uamuzi wa Serikali
wa kujenga Bandari mpya ya Mpigaduri upo pale pale. Ujenzi huo umechelewa kutokana na uamuzi wa
Serikali wa kuziangalia upya gharama za ujenzi zilizokisiwa mwanzo pamoja na
kuandaa michoro na ramani ya ujenzi huo.
Ujenzi huo unatarajiwa kuanza baadae mwaka huu.
Ujenzi wa bandari
ya Mafuta na Gesi Asilia huko Mangapwani niliouelezea mwaka jana nao unaendelea
vizuri. Miundombinu ya barabara, umeme
na maji inaendelea kutekelezwa. Wananchi wanaoishi katika maeneo hayo tayari
wamejengewa nyumba mpya kwenye eneo jengine kwa ajili ya makaazi yao. Kazi inayoendelea hivi sasa, ni kuandaa
michoro ya bandari hio, na kukamilisha majadiliano ya mkopo wa fedha wa Dola za
Kimarekani Milioni 140 kwa ajili ya ujenzi wa wa Bandari ya Mpigaduri na
Mangapwani.
Katika kipindi cha
miaka tisa iliyopita, Shirika la Bandari la Zanzibar lilitoa huduma kwa meli za
kigeni 1,509 kwa kuchukua mizigo mchanganyiko yenye uzito wa tani milioni 2.6. Kadhalika abiria 20,499,164 waliitumia
bandari ya Unguja na abiria 9,541,686 walizitumia bandari ya Pemba.
Mbali ya meli ya
MV Mapinduzi II iliyonunuliwa kwa gharama ya Dola za Kimarekani Milioni 30.4
kutoka katika Kampuni ya Daewoo ya Korea kuwa inaendelea kutoa huduma vizuri,tarehe
1 Oktoba, 2019, Serikali ilizindua meli nyengine mpya ya mafuta inayoitwaMT
Ukombozi II, iliyotengenezwa na Kampuni ya “Damen Shipyard”ya Uholanzi, kwa
gharama za EuroMilioni 14.3, sawa na wastaniwa TZS Bilioni 36. Meli hio ina
uwezo wa kuchukua tani 3,500 za mafuta kwenye visima vinne vilivyomo ndani ya meli
hio. Baada ya kununuliwa meli hii na ile
meli ya zamani ya MT Ukombozi I iliyopo, nnatarajia tatizo la kuadimika kwa mafuta
halitokuwepo.
Ndugu Wananchi,
Katika
kuziimarisha huduma za Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume, kazi
zote zilizopangwa kwa asilimia kubwa tayari zimekamilika; isipokuwa ujenzi wa
Jengo la Abiria “Terminal 3” ambao unaendelea.
Jengo hili lilichelewa baada ya kukosekana fedha za ziada za Mradi. Fedha hizo sasa zimetengwa kwenye Bajeti ya
mwaka 2019/2020. Kazi ya ujenzi imeanza
tena baada ya kusita kwa muda wa miaka mitatu na tunatarajia kwamba jengo hilo
litakabidhiwa Serikali katika mwezi wa Septemba, 2020.
Kwa upande wa
Uwanja wa ndege wa Pemba, Serikali imeuimarisha kwa kutia taa kwenye njia ya
kurukia, kutulia na maegesho ya ndege na
yamefanyika matengenezo makubwa ya jengo la abiriapamoja na kuongeza eneo la
maegesho ya ndege. Hivi sasa urefu wa njia ya kurukia na kutulia ndege
umeongezwa kutoka mita, 1,500 hadi mita 2,300. Hatua hizi zimesaidia kuuongezea
hadhi uwanja huo kutoka daraja la nne hadi la tatu.
Pamoja na jitihada
za kuimarisha Uwanja wa Pemba, zilizofanywa na Serikali, Benki ya Maendeleo ya
Afrika (AfDB), imesaidia kufanyika kwa kazi ya upembuzi yakinifu pamoja na michoro
yote “design” kwa ajili ya ujenzi wa Uwanja mpya wa kisasa wa Pemba. Ripoti yaupembuzi yakinifu tayari ishapelekwa
AfDB kwa ajili ya kuombewa fedha za ujenzi, kwa kuzingatia taratibu ziliopo.
Ndugu Wananchi,
Kwa lengo la kuimarisha sekta ya habari na
kuongeza ufanisi, katika mwaka 2011,
Serikali ilianzisha Shirika ka Utangazaji la Zanzibar (ZBC), lenye
kushughulikia kwa pamoja matangazo ya redio na
televisheni ya Zanzibar. Juhudi kubwa zimefanywa katika kuubadilisha
mfumo wa urushaji wa matangazo ya redio na televisheni kutoka kwenye analojia na
kwenda dijitali, ili kwenda sambamba na mabadiliko ya dunia katika teknolojia
ya habari.
Hivi sasa Shirika
la ZBC linawahudumia wananchi kwa
kurusha matangazo saa 24,na linaongeza programu mpya za vipindi vinavyohusu masuala muhimu ya
kiuchumi na kijamii. Hatua nyengine ya mafanikio ni kuanza kuonekana kwa ZBC TV
kupitia king’amuzi cha DSTV katika chaneli ya 291, jambo ambalo limeongeza
idadi ya watazamaji wa televisheni ya ZBC katika nchi mbali mbali za Afrika.
Kwa upande wa
Shirika la Magazeti la Zanzibar, Shirika limefanikiwa kulichapisha Gazeti la
Serikali la Zanzibar Leo, hapa hapa Zanzibar katika Wakala wa Serikali wa
Uchapaji. Gazeti hilo sasa linapatikana na kusambazwa kwa urahisi, ikiwemo
kupitia mitandaoni. Kuanzia mwezi Novemba 2019, Shirika limeanza kuchapisha
gazeti la Kiingereza liitwalo “Zanzibar Mail”,ili kuwawezesha watumiaji wa
lugha ya Kiingereza, wakiwemo watu mbali mbali pamoja na watalii, wanaokuja
Zanzibar, kufuatilia taarifa muhimu za maendeleo ya Zanzibar.
Ndugu Wananchi,
Katika kuendeleza
sekta ya utamaduni na sanaa, ilestudio
mpya ya kisasa iliyozinduliwa Rahaleo
mwaka 2016, kwa ajili ya wasanii wa filamu na muziki inatumika vizuri.Vile
vile, kuanzia mwaka 2010 hadi sasa, bado wasanii wanaendelea kulipwa mirahaba. Tangu kuanzishwa kwa mfumo huo,
jumla ya TZS Milioni 402.80 zimekusanywa
na kugawiwa kwa wasanii na wabunifu. Vile vile, Tamasha la Filamu la Kimataifa
(ZIFF), Sauti za Busara, Tamasha la Utamaduni la Mzanzibari na mengine ya asili
yamefanyika.
Kwa lengo la kuienzi na
kuiendeleza Lugha ya Kiswahili, jumla ya
makongamano matatu ya kimataifa ya Kiswahili yamefanywa katika kipindi
cha miaka mitatu mfululizo iliyopita ambayo yaliwashirikisha wataalamu kutoka
nchi mbali mbali duniani. Makongamano hayo, yameongeza hamasa na ari kwa
wataalamu chipukizi kujifunza kutoka kwa wataalamu wakongwe katika nyanja za
isimu na fasihi ya Kiswahili.
Ndugu Wananchi,
Uwanja wa michezo
wa Mao-Zedong ambao ulizinduliwa rasmi tarehe 3 Januari, 2018 baada ya
kufanyiwa matengenezo na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China,hivi sasa
unatumika kwa michezo mbali mbali.Kadhalika, mpango wa Serikali wa kujenga
viwanja vya michezo vya wilaya hivi sasa
unaendelea vizuri, katika Wilaya tano. Kadhalika, Serikali imeendeleakuwahamasisha
wananchi wafanye mazoezi ya viungo hasa
baada ya kuitangaza tarehe mosi ya Januari ya kila mwaka, kuwa siku ya mazoezi
hayo kwa Unguja na Pemba. Hivi sasa, idadi ya vikundi vya mazoezi
vinavyoshiriki Bonanza la Mazoezi hapa Zanzibar vimeongezeka kutoka vilabu 12
mwaka 2010/2011 kutoka Unguja tu na kufikia vilabu 82 kutoka Unguja, Pemba na
Tanzania bara katika mwaka 2019.
Ndugu Wananchi,
Katika kulisimamia
suala la hifadhi ya mazingira na kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi,
jitihada kadhaa zimefanyika, ikiwemo ujenzi wa kuta na matuta ya kuzuwia uingiaji wa maji ya bahari katika maeneo ya
kilimo na makaazi ya watu.Kadhalika, jumla ya hekta 337 za mikoko zimepandwa
katika maeneo mbali mbali yaliyoingia maji ya bahari, Unguja naPemba.
Katika kukabiliana
na maafa, Serikali inaendelea na mradi
wa ujenzi wa nyumba 30, kituo cha afya, soko, msikiti na skuli, huko Nungwi,
kwa ajili ya kuwahifadhi kwa kuwapatia makaazi bora wananchi walioathiriwa na
mvua za Masika mwaka 2017. Mradi kama huo utatekelezwa katika eneo la Tumbe
huko Pemba.
Ndugu Wananchi,
Mradi wa Mji
Salama, uliozinduliwa tarehe 3 Oktoba, 2018, kwa awamu ya kwanza ambao ulihusisha
ufungaji wa kamera za uangalizi (CCTV) 877, zilizofungwa katika maeneo ya Mji
Mkongwe, Uwanja wa Ndege, bandarini na maeneo mengine ya mji Unguja. Mradi huo umeendelea vizuri ambapo sehemu yake
ya pili,iliyohusisha uokozi na uzamiaji kwenye majanga ya baharini, ilizinduliwa
rasmi tarehe 2 Januari, 2019. Mradi huu
hivi sasa, unaendelezwa kwa upande wa Pemba na unatarajiwa kuanza hivi
karibuni, katika mji wa Chake Chake.
Ndugu Wananchi,
Serikali
imeendelea kuchukua hatua za kuimarisha hali ya utendaji, maslahi na mazingira yaMahakama ya Zanzibar, Ofisi ya
Mkurugenzi wa Mashtaka, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na Ofisi
ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali ikiwa ni hatua muhimu za
kuimarisha utawala bora na demokrasia. Vile vile, Tume ya Maadili ya Viongozi
wa Umma iliyoanza kazi rasmi mwaka 2016 inatimiza wajibu wake vizuri na watumishi
wa umma nao wamehimizwa watekeleze wajibu wao kwa kuwasilisha fomu zao za Tamko
la Mali na Madeni kwa wakati uliowekwa.
Serikali imeunda
Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Kuhujumu Uchumi Zanzibar (ZAECA) mwaka 2012 kwa
lengo la kudhibiti matumzi mabaya ya madaraka na mali ya umma. Tangu kuundwa
kwake,Mamlaka hii, imepokea jumla ya tuhuma 592 za makosa ya rushwa na uhujumu
uchumi yakiwemo, kuomba rushwa, matumizi mabaya ya ofisi na mali za Serikali,
utakasishaji fedha, mgongano wa maslahi, dawa za kulevya na mengineyo. Tuhuma 482 kati yake, zinaendelea na
uchunguzi; tuhuma 82 zimepelekwa Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka na tuhuma 45
zipo Mahkamani. Tuhuma nyenginezo zilihamishiwa katika Taasisi nyengine.
Kwa upande wa
Mahakama, Serikali imeyafanyia
matengenezo majengo na ofisi za mahakama pamoja na kuyapatia vitendea
kazi. Idadi ya Majaji imeongezeka kutoka wanne mwaka 2010, hadi tisa mwaka
2019. Idadi ya Mahakimu hivi sasa imefikia 65 na Makadhi ni 12.Hivi sasa,
Serikali imeendelea na ujenzi wa jengo la kisasa la Mahakama Kuu huko Tunguu, ili kukidhi
mahitaji ya Mahakama Kuu ya Zanzibar.
Vile vile, Sheria ya Utawala wa Mahakama Namba 11 ya 2018, imetungwa na
imeanza kutumika. Aidha, sheria ya kuanzishwa “Law School” imetungwa na Baraza
la Wawakilishi na mafunzo hayo yanatarajiwa kuanza hivi karibuni.
Ndugu Wananchi,
Katika kuimarisha
utumishi wa umma na maslahi ya wafanyakazi, Serikali imefanya mageuzi makubwa ya Utumishi wa Umma hapa Zanzibar,
baada ya kupitishwa kwa Sheria ya Utumishi wa Umma Namba 2 ya mwaka 2011, na
kanuni za Utumishi wa Umma za mwaka 2014. Marekebisho ya maslahi ya Wafanyakazi
ya mishahara yalifanywa mwaka 2011, 2013, 2015 na 2017 kwa lengo la kuwapa
motisha wafanyakazi kwa kuzingatia ukuaji wa mapato yetu. Nina matumaini makubwa kwamba kutokana na hali
ya uchumi wetu unavyoendelea ndugu wafanyakazi vile vile, msishangae kuwa mwaka
huu nikakuongezeni chochote.
Kutokana na juhudi
hizo za kuimarisha maslahi ya watumishi wa Serikali, matumizi yetu katika
ulipaji wa mishahara yameongezekakutoka
TZS Bilioni 83.1 mwaka 2010/2011 hadi kufikia TZS Bilioni 417.9, mwaka
2018/2019, sawa na ongezeko la mara 5.1.Hata
hivyo, licha ya ongezeko hilo, kasi ya ukuaji wa uchumi wetu imetuwezesha
kulipa mishahara kwa wakati kwa kipindi chote hicho. Kwa upande wa watumishi wa
umma wastaafu, malipo yao ya pencheni yameongezeka kutoka TZS 25,000kwa mwezi
katika mwaka 2017 na kufikia TZS 90,000 kwa mwezi hivi sasa.
Kwa upande wa ajira
katika utumishi wa umma, kuanzia mwezi Septemba 2011 hadi mwezi Juni 2019,
Serikali, kupitia Tume ya Utumishi Serikalini, imetoa fursa za ajira 11,823
katika ngazi na sekta mbali mbali Serikalini. Vile vile, katika utaratibu wa
kuratibu upatikanaji wa ajira zenye staha ndani na nje ya nchi, Serikali
imeshirikiana na sekta binafsi na kuwezesha kupatikana kwa fursa za ajira 18,826
kati ya mwaka 2011 hadi 2019.
Ndugu Wananchi,
Kwa lengo la
kupanua demokrasia na kuongeza ushiriki wa wananchi katika mipango na
utekelezaji wa shughuli za maendeleo, Serikali iliamua kuanzisha mfumo wa
ugatuzi wa madaraka kwa wananchi; ambao utekelezaji wake ulianza rasmi mwaka 2017, kwa kuanza na sekta ya
elimu, afya na kilimo. Mafanikio ya kuridhisha yanaendelea kupatikana katika
sekta hizo zilizogatuliwa na katika ukusanyaji wa mapato.
Kadhalika, natoa
shukurani zangu za dhati kwa Waheshimiwa Wajumbe wote wa Baraza la Wawakilishi
kwa kazi kubwa waliyoifanya kupitisha Bajeti za Serikali pamoja na miswada ya
sheria,kwa lengo la kuimarisha na kusimamia sheria na utawala bora. Jumla ya Sheria 92 zilizotungwa ndani ya vipindi viwili vya Serikali ya Awamu ya Saba, ni pamoja na sheria ya Utawala wa Baraza la Wawakilishi. Haya ni matunda
ya juhudi za Waheshimiwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi.Nnawapongeza kwa
dhati kwa kazi nzuri.
Ndugu Wananchi,
Serikali ya
Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana
na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kuuendeleza na kuudumisha
Muungano wetu. Mimi na Dkt. John Pombe
Joseph Magufuli tutahakikisha kuwa Muungano wetu unadumu kwa dhamira ile ile ya
Waasisi wetu wa Muungano, Marehemu Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage
Nyerere na Marehemu Mzee Abeid Amani Karume na viongozi wetu wa awamu
zilizotangulia, ili nchi yetu iendelee kupiga hatua kubwa zaidi na ibaki kuwa
ya amani na utulivu. Tutaendelea
kutekeleza wajibu wetu wa Kikatiba na Kisheria katika kuilinda amani, utulivu
na maisha ya wananchi na mali zao.
Hatutomchelea kumchukulia hatua mtu yeyote atakayejaribu kuhatarisha
amani ya nchi yetu.
Ndugu Wananchi,
Kabla sijamaliza
hotuba yangu,natoa shukurani kwa
viongozi wa Serikali ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania pamoja na Mabalozi
na Wawakilishi wa Taasisi za Kimataifa na Binafsi na wageni wengine, kwa kuja
kuungana na wananchi katika maadhimisho haya ya miaka 56 ya Mapinduzi Matukufu
ya Zanzibar. Kadhalika, nawapongeza makamanda na wapiganaji wa Vikosi vyetu vya Ulinzi na Usalama, Idara
Maalum za SMZ, kwa kuzifanikisha sherehe zetu kwa gwaride zuri la ukakamavu lililozipamba
sherehe zetu za leo. Vile vile, natoa
shukrani kwa wasanii waliotuburudisha, vijana wetu, pamoja na wafanyakazi wa
vyombo vya habari kwa kuzitangaza sherehe zetu kwa wananchi ambao kwa sababu
mbali mbali hawakuweza kuhudhuria kwenye sherehe hizi katika Uwanja huu wa
Amaan.
Natoa shukurani za
dhati kwa Viongozi na Wafanyakazi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kwa
jitihada na uzalendo wao katika kuyatekeleza majukumu ya kuwatumikia wananchi,
hatua ambayo imetuwezesha kupata mafanikio makubwa ya kiuchumi na katika huduma
za jamii. Ni vyema tuziendeleze jitihada hizo kwa kasi zaidi, ili tuzidi kupata
mafanikio makubwa zaidi. Shukrani zangu maalum nazitoa kwako, Mheshimiwa Balozi
Seif Ali Iddi, Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwa kunisaidia na kwa ushauri
wako katika kuiongoza Zanzibar.
Kadhalika, natoa
pongezi zangu za dhati kwa Halmashauri ya Maadhimisho inayoongozwa na
Mheshimiwa Makamo wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi kwa uongozi wake mahiri
ambao umezifanikisha sherehe hizi. Shukurani
na pongezi maalumu nazitoa kwenu ndugu wananchi, kwa mara nyengine, pamoja na
wanafunzi kwa kujitokeza kwa wingi kusherehekea maadhimisho ya miaka 56 ya
Mapinduzi. Hongereni Sana.
Ndugu Wananchi,
Kama mnavyofahamu
kwamba Tume ya Uchaguzi ya Taifa ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Tume ya
Uchaguzi ya Zanzibar, hivi sasa zinaendelea na matayarisho ya Uchaguzi Mkuu,
katika tarehe itakayotangazwa hapo baadae.
Kwa hivyo, nakuhimizeni mwende mkajiandikishe kwa ajili ya uchaguzi huo;
ili muweze kuitumia haki yenu ya kidemokrasia ya kupiga kura, kwa kuwachagua
viongozi mnaowataka; utakapofika wakati.
Nakutakieni nyote
kila la kheri na baraka za mwaka mpya wa 2020. Mwenyezi Mungu atuzidishie
amani, umoja na mshikamano. Nakutakieni safari njema za kurejea nyumbani.
MAPINDUZI DAIMA
MUNGU IBARIKI ZANZIBAR
MUNGU IBARIKI TANZANIA
MUNGU IBARIKI AFRIKA
Ahsanteni kwa kunisikiliza.
No comments:
Post a Comment