Hotuba ya Mheshimiwa Kassim .
Majaliwa (MB), Waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Wakati wa Kuahirisha Mkutano wa Kumi na Nane wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Tarehe 7 Febuari , 2020
UTANGULIZI
Shukrani
1.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, namshukuru Mwenyezi
Mungu mwingi wa rehema kwa kutuwezesha kuhitimisha shughuli zote zilizopangwa
katika Mkutano huu wa Kumi na Nane wa Bunge lako Tukufu tukiwa buheri wa afya.
Aidha, kwa kuwa huu ni Mkutano wa kwanza tangu mwaka huu uanze, ninakutakia
wewe Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wenyeviti wa
Bunge, Waheshimiwa Wabunge wenzangu, watumishi wa Bunge na Watanzania wote Heri ya Mwaka Mpya 2020.
Salamu za Pole
2.
Mheshimiwa
Naibu Spika, kwa
masikitiko makubwa naungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kutoa salamu za
pole kwa Wananchi wa Jimbo la Newala Vijijini, kwako, kwa Bunge lako Tukufu na
kwa familia ya Mbunge Rashid Ajali Akbar, aliyefariki tarehe 15 Januari, 2020.
3.
Mheshimiwa Naibu Spika, naungana na
Mheshimiwa Rais wetu mpendwa kutoa pole kwa ndugu, jamaa na marafiki wa familia
za watu waliopoteza maisha kutokana na madhara ya mvua kubwa zinazoendelea
kunyesha katika maeneo mbalimbali nchini na kwa familia za watu 20 waliofariki tarehe
01 Februari 2020 katika Ibada, mjini Moshi.
4.
Mheshimiwa
Naibu Spika, sambamba na matukio hayo, Watanzania wamepokea kwa
mshtuko taarifa kuhusu vifo vya wanajeshi wetu 10 wa Jeshi la Wananchi wa
Tanzania vilivyotokea tarehe 03 Februari 2020 wakati wakishiriki mazoezi ya
Kijeshi huko Msata, mkoani Pwani na Askari watatu wa Jeshi la Polisi
waliofariki kwa ajali, mkoani Njombe. Natumia fursa hii kutoa pole kwa Jenerali
Venance Mabeyo, Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Inspekta Jenerali Simon Sirro, Mkuu
wa Jeshi la Polisi na kwa familia, ndugu, jamaa na marafiki wa askari hao.
5.
Mheshimiwa
Naibu Spika, nitumie fursa hii pia kuwapa pole Watanzania
wenzangu waliopoteza ndugu, jamaa na marafiki na wengine kusababishiwa madhara
mbalimbali kutokana na ajali za barabarani na matukio mengine. Tunamuomba
Mwenyezi Mungu aziweke roho za marehemu mahala pema peponi na awape nafuu
majeruhi wapone haraka.
Pongezi
6.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunahitimisha shughuli
zilizopangwa katika mkutano huu wa Kumi na Nane wa Bunge lako tukufu, naungana
na Waheshimiwa Wabunge wenzangu walionitangulia kumpongeza Mhe. George Boniface
Simbachawene (Mbunge wa Kibakwe) kwa kuteuliwa kwake kuwa Waziri wa Mambo ya
Ndani ya Nchi na Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu (Mbunge wa Ilala) kuwa Waziri wa
Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais anayeshughulikia Muungano na Mazingira.
7.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, nawapongeza Waheshimiwa
Mabalozi wote ambao wamepangiwa vituo vya uwakilishi hivi karibuni. Natumia
nafasi hii kuwakumbusha tena kuwa pamoja na mambo mengine, tutaendelea kupima
utendaji kazi wao kwa namna wanavyovutia uwekezaji, kutangaza utalii, kutafuta
masoko ya bidhaa zetu sambamba na kujenga taswira nzuri ya Tanzania katika
maeneo yao ya uwakilishi.
Aidha, Viongozi wote mlioteuliwa, tambueni
kuwa mnalo jukumu kubwa la kuwahudumia Watanzania hususan katika kutatua kero
mbalimbali zinazowakabili.
8.
Mheshimiwa
Naibu Spika, natumia pia nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Spika, wewe
Mheshimiwa Naibu Spika na watendaji wa Bunge kwa ubunifu na uthubutu ambao umekuwa
chachu ya mageuzi makubwa ya kiutendaji katika Bunge hili. Katika hili, nitakuwa
mchoyo wa fadhila nisipopongeza Bunge hili tukufu kwa kukabidhi majoho kwa
Maspika Wastaafu ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wao kwa Bunge hili na Taifa
kwa ujumla. Hongera sana kwa Mheshimiwa
Spika!
SHUGHULI ZA BUNGE
Maswali na Majibu
9.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mkutano huu wa 18 tunaouhitimisha
leo, jumla ya maswali 118 ya msingi
na mengine 320 ya nyongeza
yaliulizwa na Waheshimiwa Wabunge na kupatiwa majibu na Serikali. Kadhalika,
maswali 14 ya msingi na swali moja la nyongeza ya papo kwa papo
yaliulizwa na kujibiwa na Waziri Mkuu.
Miswada ya Serikali
10.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika mkutano huu, Bunge lako tukufu
lilipitisha kwa hatua zake zote Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali
(Na. 8) wa mwaka 2019 na Muswada wa Sheria ya Usuluhishi wa mwaka 2020.
11.
Mheshimiwa
Naibu Spika, miswada ifuatayo nayo ilisomwa kwa mara ya kwanza
katika Bunge lako tukufu:
(i)
Muswada
wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa Mwaka 2020;
(ii)
Muswada
wa Sheria ya Afya ya Mimea wa Mwaka 2020; na
(iii)
Muswada
wa Sheria ya Kusimamia na Kuendeleza Uvuvi wa Bahari Kuu wa Mwaka 2020.
Maazimio
ya Serikali
12.
Mheshimiwa
Naibu Spika, vilevile, Serikali kupitia Wizara ya Fedha na
Mipango iliwasilisha katika Mkutano huu Azimio la kufuta Hasara itokanayo na Maduhuli
ya Madeni ya Nyumba ya Ada na Leseni za Magari, Riba na Adhabu kwa Kipindi
kinachoishia tarehe 30 Juni, 2019.
Kamati za Kudumu za Bunge
13.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa mkutano huu, Kamati za
Kudumu za Bunge 15 ziliwasilisha Bungeni taarifa za mwaka za kazi. Taarifa hizo
zilisheheni uchambuzi wa kina, maoni, ushauri na mapendekezo mbalimbali kwa
Serikali.
Nitumie fursa hii kuwapongeza
Wenyeviti, Makamu Wenyeviti na wajumbe wote wa kamati hizo kwa kazi nzuri
waliyoifanya kuanzia maandalizi ya kazi za kamati hadi kuwasilisha taarifa zao
katika Bunge lako tukufu.
14.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imepokea hoja zilizoibuliwa
wakati wa vikao vya Kamati za Kudumu za Bunge ambazo inaamini kuwa zimeibuliwa
kwa malengo mazuri ya kuhakikisha tunaboresha utendaji kazi na uwajibikaji.
Serikali inaahidi kuzifanyia kazi hoja hizo hususan wakati huu tunapoelekea
kwenye maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Mwaka 2020/2021.
UTEKELEZAJI WA MPANGO NA BAJETI YA SERIKALI YA MWAKA
2019/2020 KATIKA NUSU YA KWANZA YA MWAKA 2019/2020 (JULAI – DESEMBA 2019)
15. Mheshimiwa
Naibu Spika, kama
itakavyokumbukwa mwezi Juni, 2019 Bunge lako tukufu lilipitisha Mpango na
Bajeti ya Serikali wa shilingi trilioni 33.1.
Kati ya fedha hizo, matumizi ya kawaida yalikuwa ni shilingi trilioni
20.85 na matumizi ya maendeleo yalikuwa shilingi trilioni 12.2.
16. Mheshimiwa
Naibu Spika, vilevile,
Novemba, 2019 Serikali iliwasilisha katika Bunge lako Tukufu Muhtasari wa
mapitio ya utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo kwa mwaka 2019/2020 na mwelekeo
kwa mwaka 2020/2021.
Kwa msingi huo, nimeona ni vema kuwaeleza
Waheshimiwa Wabunge wenzangu na wananchi baadhi ya mambo makubwa na mafanikio
yaliyopatikana hadi kufikia mwishoni mwa Desemba, 2019 ambapo ni nusu ya mwaka
wa fedha wa 2019/2020.
17. Mheshimiwa
Naibu Spika, jitihada
kubwa zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Uongozi mahiri wa
Jemadari wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Rais wa Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania zimedhihirika wazi katika nyanja mbalimbali za kiuchumi na
kijamii. Viashiria vingi vya kiuchumi vinaonesha matokeo mazuri.
18. Mheshimiwa
Naibu Spika, katika
kipindi cha Julai hadi Septemba 2019, uchumi wa Tanzania ulikua kwa asilimia
6.8. Aidha, ukuaji wa uchumi kwa nchi nyingine za Jumuiya ya Afrika Mashariki
katika robo ya tatu ya mwaka 2019 ulikuwa kama ifuatavyo: Kenya (asilimia 5.1);
Uganda (asilimia 2.7); na Rwanda (asilimia 11.9).
19. Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja
na mambo mengine juhudi za Serikali katika kuimarisha uwekezaji kwenye miundombinu
ya msingi ya barabara, reli, na viwanja vya ndege; kutengemaa kwa upatikanaji
wa huduma za maji; kuimarika kwa huduma za usafirishaji; habari na mawasiliano;
kuongezeka kwa uzalishaji wa madini hususan dhahabu na makaa ya mawe; na
kuongezeka kwa uzalishaji wa mazao ya kilimo kumekuwa chachu ya mafanikio hayo.
20. Mheshimiwa
Naibu Spika, ukuaji huo
wa uchumi umechangia kuongezeka kwa uzalishaji katika sekta rasmi na isiyo
rasmi na hivyo, kuiwezesha Serikali kukusanya mapato zaidi. Kwa mfano, katika kipindi cha Julai hadi Desemba 2019, mapato ya
kodi yaliongezeka hadi kufikia wastani wa shilingi trilioni 1.52 kwa mwezi
ikilinganishwa na wastani wa shilingi trilioni 1.30 katika kipindi kama hicho
mwaka 2018.
21. Mheshimiwa
Naibu Spika, kutokana na
juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali ya Awamu ya Tano, ikiwemo kuimarisha
mifumo ya ukusanyaji wa mapato na
kurahisisha ulipaji wa kodi, mapato ya kodi kwa mwezi Desemba, 2019
yaliweza kuvunja rekodi na kufikia shilingi trilioni 1.92.
22.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa matumizi, katika
kipindi cha Julai hadi Desemba 2019, Serikali imetumia shilingi trilioni 15.32,
sawa na asilimia 91.2 ya lengo. Fedha hizo zimetumika kwa ajili ya utekelezaji
wa miradi mbalimbali ya maendeleo, ulipaji wa mishahara ya watumishi,
ugharamiaji wa deni la Serikali, ulipaji wa madai ya ndani yaliyohakikiwa
(watumishi, wazabuni na wakandarasi) na uendeshaji wa shughuli za Serikali katika
Wizara, Idara Zinazojitegemea, Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za
Mitaa.
23. Mheshimiwa
Naibu Spika, kuimarika
huko kwa mapato kumewezesha Serikali kuendelea kuwahudumia wananchi kupitia
ujenzi na uboreshaji wa miundombinu mbalimbali kwa ajili ya shughuli za
kiuchumi na kijamii. Naomba japo kwa uchache Mheshimiwa Naibu Spika,
nitaje mafanikio
yaliyopatikana katika utekelezaji wa Bajeti ya Serikali kwa kipindi cha Julai
hadi Desemba, 2019 ikiwa ni miezi sita ya mwaka wa fedha kama ifuatavyo:
(i)
Kuendelea kwa
ujenzi wa reli ya kati ya kisasa (Standard Gauge) kwa sehemu ya Dar es Salaam –
Morogoro (KM 300) ambayo hadi Desemba 2019 ilifikia asilimia 70. Aidha, kazi za
ujenzi kwa sehemu ya Morogoro – Makutupora (KM 422) zinaendelea vizuri na
Serikali imerejesha huduma ya reli ya abiria na mizigo ya Kaskazini (Dar es
Salaam – Moshi) na jitihada zinafanywa ili iweze kufika mkoani Arusha;
(ii)
Kuendelea na
ujenzi wa Mradi wa kufua Umeme wa Maji wa Julius Nyerere ambapo kazi
zilizokamilika ni pamoja na: ujenzi wa daraja la muda namba 2; utafiti wa
miamba na udongo; uchimbaji wa mtaro wa chini kwa chini wenye urefu wa mita
147.6 na mtambo wa kuchakata kokoto namba moja;
(iii)
Kuendelea na
mradi wa usambazaji umeme vijijini (REA) ambapo hadi Desemba 2019
jumla ya vijiji 8,236 kati ya vijiji 12,268 vya Tanzania Bara vimeunganishwa na
umeme, sawa na asilimia 67.1.
Aidha, kufuatia malalamiko ya ucheleweshaji wa baadhi ya miradi ya REA,
namuagiza Waziri wa Nishati ahakikishe wakandarasi wote waliosambazwa kwenye
mpango wa REA wanakamilisha majukumu yao kwa wakati;
(iv)
Kuendelea
kuboresha Shirika la Ndege Tanzania kwa kununua ndege mpya 11. Hadi Desemba
2019, ndege nane zimepokelewa na malipo ya awali ya ununuzi wa ndege nyingine
mpya tatu yamefanyika. Aidha, Serikali imeendelea kutoa mafunzo kwa marubani,
wahandisi na wahudumu pamoja na kulipa madeni;
(v)
Kuzinduliwa kwa
Jengo la Tatu la abiria katika Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Julius
Nyerere na kuanza kutumika kuhudumia abiria; kuendelea na uboreshaji wa kiwanja
cha ndege Mwanza na viwanja vya mikoa mbalimbali;
(vi)
Kuendelea na
ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami zikiwemo barabara kuu, barabara za
mikoa na za wilaya. Mtandao wa barabara kuu umefikia kilomita 8,502 na mtandao
wa barabara za mikoa kilomita 1,756. Pia, Serikali imeendelea na ujenzi wa
Ubungo inter-change ambapo hadi
Desemba 2019 ulifikia asilimia 62 na ujenzi wa barabara ya njia nane kutoka
Kimara hadi Kibaha (asilimia 63);
(vii)
Kukamilika kwa
ujenzi wa madaraja ya: Sibiti (Singida), Momba (mpakani mwa Songwe na Rukwa),
Mlalakuwa (Dar es Salaam), Lukuledi (Lindi) na kuendelea na ujenzi wa daraja la
Selander na daraja la Kigongo – Busisi lenye urefu wa mita 3,200 na upana wa
mita 28.45;
(viii)
Kuboresha elimu
ya msingi kwa kuendelea kutekeleza programu ya elimumsingi bila ada ambapo
Serikali inagharamia chakula kwa wanafunzi 189,226 wa kutwa na bweni, posho ya
madaraka kwa walimu wakuu 23,843, fidia ya ada kwa wanafunzi 1,874,331 na
ruzuku ya uendeshaji wa shule.
Katika kipindi cha Julai hadi
Desemba 2019, Serikali imetoa jumla ya shilingi bilioni 128.1 kwa ajili ya kugharamia
elimumsingi bila ada;
(ix)
Kuimarisha
elimu ya juu, ufundi na ustawi wa jamii kwa kuendelea kutoa mikopo kwa
wanafunzi wa elimu ya juu ambapo hadi Desemba 2019 jumla ya shilingi bilioni
266.4 zimetolewa kwa wanafunzi 130,072. Kati yao wanafunzi 49,493 ni wa mwaka
wa kwanza na 80,579 wanaoendelea. Aidha, Serikali imeendelea kujenga mabweni ya
wanafunzi wa kike; kukarabati majengo ya vyuo vikuu na vyuo vya ualimu;
kuboresha vyuo vya VETA kwa kujenga na kuboresha majengo ya vyuo na kununua
vifaa vya kufundishia na kujifunzia.
Vilevile, Serikali imeimarisha vyuo vya Maendeleo ya Jamii na Ustawi wa
Jamii kwa kuanzisha vituo vitano vya ubunifu sanjari na kutekeleza programu ya
uanagenzi ili kupata ujuzi wa kujiajiri unaoendana na ushindani wa soko la
ajira;
(x)
Kuboresha
utoaji wa huduma za afya kwa kugharamia ujenzi na uboreshaji wa miundombinu ya
vituo 487 vya kutolea huduma za afya ikijumuisha vituo vya afya 320, hospitali
za halmashauri za wilaya 70, hospitali za zamani tisa na zahanati 88. Aidha,
Serikali imejenga na kuboresha miundombinu ya hospitali za rufaa za Njombe,
Simiyu, Mara, Geita, Songwe, Katavi, Seko Toure, Burigi - Chato, Mwananyamala,
na hospitali za rufaa za kanda ya kusini Mtwara, kanda ya nyanda za juu kusini
Mbeya, hospitali ya Kibong’oto na ujenzi wa Isolation
centre katika hospitali ya Taifa Muhimbili.
Pia, Serikali imekamilisha ujenzi wa nyumba 320 za watumishi wa sekta ya
afya pamoja na kugharamia ununuzi wa dawa, chanjo, vifaa, vifaa tiba na
vitendanishi ambapo shilingi bilioni 334 zimetumika. Vilevile, katika kipindi
hicho, jumla ya madaktari bingwa 311 wameendelea kulipiwa gharama za masomo ya
uzamili katika vyuo vikuu vya ndani na nje ya nchi. Kadhalika, katika kipindi
cha nusu ya pili, Serikali inakusudia kuajiri zaidi ya watumishi 4,000 wa sekta
ya afya;
(xi)
Kuendelea
kuboresha huduma ya maji safi na salama vijijini na mijini ambapo utekelezaji
wa miradi 631 unaendelea ikijumuisha miradi 558 ya maji vijijini na 73 ya maji
mijini. Miongoni mwa miradi mikubwa inayoendelea kutekelezwa ni pamoja na mradi
wa maji Arusha, mradi wa maji wa
Same–Mwanga-Korogwe na mradi wa kutoa maji kutoka Ziwa Victoria kwenda katika
miji ya Isaka, Tinde, Kagongwa, Tabora, Igunga, Uyui na Nzega. Katika kipindi
cha Julai hadi Desemba 2019, jumla ya shilingi bilioni 325.9 zimetolewa kwa
ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya maji; ikiwemo uchimbaji wa visima vifupi, vya kati na virefu;
(xii)
Kuimarisha
juhudi za ujenzi wa viwanda kwa kuboresha Shirika la Viwanda Vidogo (SIDO),
ukarabati na upanuzi wa kiwanda cha ngozi na bidhaa za ngozi cha Karanga -
Moshi na kuimarisha Shirika la Nyumbu ili kuongeza uzalishaji ikiwemo kuzalisha
magari ya zimamoto. Aidha, kumekuwa na ongezeko la ajira na uzalishaji
viwandani hususan katika viwanda vya saruji, marumaru, chuma, kusindika matunda
na mazao ya chakula ikijumuisha ubanguaji wa korosho. Kwa mfano, jumla ya tani
4,254 za korosho zilibanguliwa kupitia viwanda 17 ambavyo vilizalisha ajira za
moja kwa moja 4,066;
(xiii)
Kuendelea na
ujenzi wa meli mpya yenye uwezo wa kubeba abiria 1,200 na tani 400 za mizigo
katika Ziwa Victoria ambapo utekelezaji wake umefikia asilimia 37; ujenzi wa
chelezo umefikia asilimia 46; ukarabati wa meli ya MV Victoria umefikia
asilimia 65 na MV Butiama asilimia 60. Kuendelea na ujenzi wa kivuko kipya cha
Nyamisati – Mafia; kuendelea kukarabati vivuko vya MV Sengerema (asilimia 40);
MV Kigamboni (asilimia 60), na MV Utete (asilimia 95). Hatua nyingine ni
kukamilika kwa ujenzi wa kivuko kipya cha Kigongo – Busisi;
(xiv)
Upanuzi wa
bandari ya Dar es Salaam unaendelea ambapo ujenzi wa gati Na.1, 2 na 3 na gati
la kupakia na kupakua magari (Ro-Ro) umekamilika na kuwezesha meli ya kwanza
yenye uwezo wa kubeba magari 6,000 kuhudumiwa katika gati hilo. Aidha,
uboreshaji wa bandari za Tanga, Mtwara na bandari za maziwa makuu unaendelea;
24. Mheshimiwa
Naibu Spika, lengo
la Serikali ya Awamu ya Tano ni kuwahudumia wananchi sambamba na kuratibu vyema
utekelezaji wa miradi mbalimbali ya kimkakati na kielelezo. Kama
nilivyotangulia kueleza, miradi hiyo inayohusisha sekta ya miundombinu wezeshi,
nishati, maji, afya na elimu imekuwa chachu ya kuboresha maisha ya Watanzania
kupitia ukuaji wa sekta rasmi na isiyo rasmi.
ELIMU
Matokeo
ya Mitihani ya Kitaifa
25.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Awamu ya Tano imefanya
maboresho makubwa na uwekezaji katika sekta ya elimu nchini. Uwekezaji huo ni
pamoja na kutoa Elimumsingi Bila Ada, ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya
shule sambamba na kuimarisha ushirikiano baina ya wadau wa elimu na wananchi.
26.
Mheshimiwa Naibu Spika, matokeo chanya ya maboresho hayo ni
kuongezeka kwa kiwango cha ufaulu katika upimaji wa kitaifa kwa darasa la nne,
kidato cha pili na mitihani ya kitaifa kidato cha nne kwa kipindi cha kuanzia
mwaka 2015 hadi 2019. Aidha, shule za kata nazo zimeendelea kufanya vizuri na
kuongeza matumaini kwa Watanzania walio wengi.
27.
Mheshimiwa Naibu Spika, matokeo ya upimaji wa kitaifa wa
darasa la nne mwaka 2019 yamebainisha kuwa jumla ya wanafunzi 1,531,120 walifaulu ikilinganishwa na wanafunzi 1,213,132 waliofaulu mwaka 2018. Ufaulu
huo ni sawa na ongezeko la asilimia
26.21. Kwa upande wa kidato cha
pili, wanafunzi 514,251
walifaulu upimaji wa kitaifa kwa mwaka 2019 ikilinganishwa na wanafunzi 452,273 waliofaulu upimaji huo
mwaka 2018 sawa na ongezeko la asilimia
13.7.
28.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2019 wanafunzi 340,914 kati ya wanafunzi 422,722 walifaulu mtihani wa Taifa wa kidato cha
nne. Aidha, ubora wa ufaulu wa wanafunzi nao umeongezeka kwa Mwaka 2019. Kwa
mfano, wanafunzi 135,301 sawa na asilimia
32.01 walipata ufaulu mzuri wa daraja la kwanza hadi la tatu.
Maboresho
ya miundombinu ya elimu
29.
Mheshimiwa Naibu Spika, maboresho na uwekezaji wa Serikali
katika sekta ya elimu yamekuwa chachu ya kuongezeka kwa kiwango cha ufaulu na
wakati mwingine kuleta changamoto kwenye miundombinu ya elimu. Hata hivyo,
Serikali imeendelea kukamilisha usajili wa shule mpya, kuongeza vyumba vya
madarasa 1,218 na mabweni 14 ili wanafunzi wote waliofaulu
kuingia kidato cha kwanza mwaka 2020 waweze kuanza masomo kwa wakati.
30.
Mheshimiwa Naibu Spika, nirejee tena kusisitiza kuhusu maelekezo
niliyoyatoa Desemba, 2019 kwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya kwamba wahakikishe
miundombinu ya shule inakamilika kwa wakati na wanafunzi wote waliofaulu
wanapata fursa ya kuendelea na masomo ya kidato cha kwanza.
KILIMO
Hali ya Kilimo
31.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika msimu wa 2019/2020 mvua
zimeendelea kunyesha katika mikoa mbalimbali kwa kiwango cha kuridhisha. Hata
hivyo, baadhi ya maeneo mvua zimenyesha kwa wingi na kuathiri ustawi wa mazao
na shughuli za kilimo. Serikali kupitia Mamlaka ya Hali ya Hewa imeendelea
kutoa taarifa za mwenendo wa mvua na kutumia taarifa hizo kuwashauri wakulima
kuzalisha mazao kulingana na kiasi cha mvua katika maeneo yao.
32.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande mwingine, Serikali imejiandaa kukabiliana na tishio la
Nzige wa Jangwani ambao tayari wamevamia nchi za jirani. Serikali inafuatilia kwa
karibu na kubaini endapo kuna viashiria au uwepo wa nzige hao kwa ajili ya
kuchukua hatua za kuwadhibiti kwa wakati endapo watajitokeza. Serikali imeendelea
kujipanga vizuri katika kudhibiti tishio hilo la nzige wa jangwani pamoja na visumbufu
vyote vya mazao vitakavyotokea katika msimu huu wa kilimo.
Upatikanaji
wa Pembejeo za Kilimo
33. Mheshimiwa
Naibu Spika, katika kuongeza uzalishaji na tija kwenye kilimo, Serikali
imeendelea kuboresha mifumo ya uzalishaji na upatikanaji wa pembejeo bora za
kilimo. Hadi kufikia tarehe 30 Januari, 2020 upatikanaji wa mbegu za kilimo ulikuwa
tani 71,155. Kati ya hizo, tani 58,509 zimezalishwa hapa nchini, tani 5,175 zimeingizwa
kutoka nje ya nchi na tani 7,469 ni bakaa ya msimu wa 2018/2019.
34. Mheshimiwa
Naibu Spika, kwa
upande wa mbolea, makisio ya mahitaji
kwa msimu wa 2019/2020 ni tani 586,604 ikilinganishwa na tani 514,138 mwaka
2018/2019. Upatikanaji wa mbolea hadi kufikia tarehe 30 Januari, 2020 umefikia
tani 410,499 sawa na asilimia 70. Aidha, kwa kuwa mbolea hizo hutumika kulingana
na hatua za ukuaji wa mazao, Serikali inaendelea kuhakikisha asilimia 30
iliyobaki inapatikana na kusambazwa kwa wakulima kwa wakati.
35. Mheshimiwa
Naibu Spika, vilevile,
viuatilifu vimeendelea kusambazwa kwa
ajili ya kudhibiti visumbufu vya mazao nchini. Mathalan, hadi kufikia tarehe 30
Januari 2020, zipo jumla ya tani 2,258 za salfa ya unga na lita 160,271 za
viuatilifu vya maji vya zao la korosho kwa ajili ya msimu wa 2020/2021. Katika
zao la pamba, hadi kufikia tarehe 30 Januari 2020, ekapack 802,000 zimesambazwa kwa wakulima na ununuzi wa ekapack 8,200,000 za viuatilifu na
vinyunyizi 20,000 unaendelea.
Masoko ya Mazao ya Kilimo
36.
Mheshimiwa Naibu Spika, jitihada za
Serikali za kuongeza uzalishaji wa mazao ya chakula na biashara zinakwenda
sambamba na kuhakikisha upatikanaji wa masoko ya uhakika kwa mazao ya kilimo
yanayozalishwa nchini.
Serikali imeendelea
kuimarisha mifumo ya masoko ikiwemo mfumo wa Stakabadhi ghalani ambao umeonesha
matokeo chanya na kuwapatia faida wakulima.
37.
Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Mfumo wa
Stakabadhi Ghalani bei ya mazao ya ufuta na kakao imeongezeka. Kwa mfano, bei
ya ufuta imeongezeka kutoka wastani wa shilingi 1,000 mwaka 2017/2018 hadi
kufikia shilingi 3,500 kwa kilo katika mwaka 2019. Aidha, bei ya kakao
imeongezeka kutoka shilingi 3,200 msimu wa 2018/2019 hadi shilingi 5,000 kwa
kilo katika msimu wa 2019/2020.
38. Mheshimiwa
Naibu Spika,
Serikali inaendelea kukabiliana na changamoto zilizopo katika masoko ikiwemo
miundombinu hafifu, matumizi duni ya mfumo wa TEHAMA, utunzaji hafifu wa
kumbukumbu na malipo kwa wakulima wasiokuwa na akaunti au wenye kutumia akaunti
za benki za wakulima wenzao. Hivyo, nitoe wito kwa wakulima kufungua akaunti
kwa wakati na kuacha kutumia akaunti za wakulima wenzao ili wasicheleweshewe
malipo na kuepuka udanganyifu kutoka kwa baadhi ya viongozi wa Vyama vya
Ushirika.
Utoaji wa Huduma za Ugani
39.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuchukua hatua
mbalimbali za kuboresha utoaji wa huduma za ugani nchini ili kuongeza tija
katika kilimo. Hatua hizo ni pamoja na kuwahamisha maafisa ugani wote kutoka
Makao Makuu ya Halmashauri kwenda kwenye ngazi ya Vijiji, Kata na Tarafa. Hadi
kufikia Desemba, 2019 jumla ya maafisa ugani 753 kati ya 1,120 wamehamishwa
kwenda katika ngazi hizo. Nitumie nafasi hii tena kuziagiza Halmashauri zote
nchini kuhakikisha zinakamilisha kuwahamisha maafisa ugani wote ambao bado
hawajahamishwa.
Kuimarisha Ushirika
40.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kufanyia kazi
malalamiko kutoka kwa wakulima kuhusu mwenendo usioridhisha wa baadhi ya Vyama
vya Ushirika pamoja na watendaji wake. Lengo la Serikali ni kujenga ushirika
imara na wenye kumpatia tija mkulima.
Hivyo, kupitia Tume ya Maendeleo ya
Ushirika, Serikali imeweka mikakati mbalimbali ya kuimarisha vyama vya ushirika
ili viwe na tija kwa wakulima. Mikakati hiyo, inalenga kujenga mfumo thabiti wa
usimamizi na uhamasishaji.
41.
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua nyingine zinazochukuliwa na Serikali
ni kufanya mabadiliko ya kiutendaji,
kuajiri maafisa ushirika wapya na kuhamisha maafisa kutoka Makao Makuu kwenda Ofisi
za Mikoa na Halmashauri ili kuimarisha usimamizi wa vyama vya ushirika.
MASUALA
YA MSISITIZO
42.
Mheshimiwa Naibu Spika, yapo baadhi ya masuala ambayo
ningependa kuyawekea msisitizo kupitia hotuba yangu hii. Masuala hayo ni hali ya
mvua zinazoendelea kunyesha nchini, zoezi la usajili wa laini za simu,
uboreshaji wa daftari la uandikishaji wapiga kura na utatuzi wa migogoro ya
ardhi nchini.
Mvua
zinazoendelea kunyesha nchini
43. Mheshimiwa Naibu Spika, mvua kubwa zinazoendelea kunyesha
katika maeneo mbalimbali nchini kuanzia Oktoba, 2019 hadi Februari, 2020
zimesababisha vifo kwa watu waishio maeneo ya mabondeni, uharibifu wa nyumba, miundombinu
ya usafirishaji ikiwemo barabara, reli na madaraja. Jumla ya barabara 73 na
madaraja katika Mikoa 18 ziliathirika. Aidha, reli za Tanga
hadi Arusha na Dar es Salaam hadi Mwanza na Kigoma kwa nyakati tofauti nazo
zililazimika kufungwa kwa muda.
44. Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali kwa
lengo la kuhakikisha kuwa huduma za usafiri na usafirishaji kwa njia ya barabara
na reli katika maeneo yaliyoathirika zinarejea haraka.
45.
Mheshimiwa
Naibu Spika, Serikali inafuatilia kwa karibu taarifa zinazotolewa
na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania ili kuwafahamisha wananchi mwenendo wa hali
ya hewa na kutoa tahadhari kupitia vyombo mbalimbali vya habari na mitandao ya
kijamii. Nitumie fursa
hii kuwataka wananchi wote kuchukua tahadhari kwa kuhama sehemu za mabondeni na
kuzingatia taarifa za utabiri wa hali ya hewa zinazotolewa na Mamlaka ya Hali
ya Hewa nchini. Nichukue fursa hii kuwahimiza wananchi wachukue tahadhari kwa
kuhama kutoka mabondeni na kwenda maeneo yaliyo salama.
Zoezi
la usajili wa laini za simu
46.
Mheshimiwa Naibu Spika, itakumbukwa kwamba tarehe 27 Desemba
2019, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe
Joseph Magufuli alitoa ufafanuzi kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kusajili laini
zote za simu kwa mujibu wa sheria.
Aidha, alisisitiza kuwa ameongeza
muda wa usajili hadi tarehe 20 Januari, 2020 na kwamba baada ya muda huo kwisha
TCRA na Mamlaka nyingine husika zisitishe huduma kwa laini za simu ambazo zitakuwa
hazijasajiliwa kwa mujibu wa sheria.
47.
Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia tarehe 02 Februari 2020
kulikuwa na jumla ya laini za simu milioni 43.9. Laini milioni 31.4 sawa na
asilimia 71.6 zilikuwa zimesajiliwa kwa alama za vidole. Zoezi la usajili wa
laini za simu kwa alama za vidole ni endelevu. Uzimaji wa laini za simu
unaendelea. Kwa msingi huo, nitoe wito kwa wananchi kwamba mara baada ya kupata
namba ama kitambulisho cha uraia, nenda kwa wakala wa mtandao wako ili usajili
laini yako.
48.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninawahimiza wananchi wote ambao
hawajasajili laini zao za simu kwa sababu mbalimbali na wale ambao wanaendelea
na zoezi la kupata vitambulisho vya uraia na wamekwishapata namba za Mamlaka ya
Vitambulisho vya Taifa (NIDA) wasajili laini zao za simu kwa mujibu wa sheria
ili kuepuka usumbufu wa kusitishiwa huduma za mawasiliano.
49.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninatoa wito kwa NIDA wasogeze
huduma za kutoa namba za vitambulisho karibu na wananchi kwa kadiri
inavyowezekana. Lengo ni kutoa fursa kwa wananchi wengi zaidi kupata namba za
vitambulisho kwa ajili ya kuwawezesha kusajili laini zao za simu na vilevile,
kupata Vitambulisho vya Taifa kwa matumizi mengine muhimu.
Daftari
la Uandikishaji Wapiga Kura
50.
Mheshimiwa Naibu Spika, Tume ya Taifa ya Uchaguzi imeendelea
na zoezi la Uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwa awamu ya kwanza.
Hadi kufikia tarehe 02 Februari, 2020 imekamilisha uandikishaji wa Wapiga Kura
katika Kanda ndogo kumi na
mbili kati ya kumi na nne zilizopangwa katika ratiba ya uboreshaji wa awamu ya
kwanza.
51.
Mheshimiwa
Naibu Spika, kanda
ndogo 12
zilizokamilika zinahusisha mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Manyara, Mara, Simiyu,
Mwanza, Geita, Shinyanga, Kagera, Kigoma, Katavi, Rukwa, Tabora, Singida,
Dodoma, Songwe, Mbeya, Iringa, Ruvuma, Njombe, Lindi, Mtwara, Tanga, Morogoro
(Ulanga DC na Malinyi DC) na Tanzania Zanzibar. Aidha, kanda ndogo ya kumi na tatu inayohusisha Mkoa wa Morogoro zoezi
la uboreshaji limeanza tarehe 3 Februari, 2020 na litakamilika tarehe 9
Februari, 2020.
52.
Mheshimiwa Naibu Spika, uandikishaji wa wapiga kura ni wa
siku saba kwa kila kituo cha kuandikisha wapiga kura. Aidha, zoezi la uboreshaji
linahusisha uandikishaji wa wapiga kura wapya ambao hawajahi kuandikishwa
katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura, urekebishaji wa taarifa za wapiga kura
walioandikishwa katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 na kuondoa taarifa za wapiga
kura waliopoteza sifa ikiwemo waliofariki.
53.
Mheshimiwa Naibu Spika, idadi ya wapiga kura walioandikishwa
kuanzia kanda ndogo ya kwanza
hadi kanda ndogo ya 12 walikuwa 18,058,977.
Jumla ya wapiga kura 2,012,212 wamejitokeza
kuboresha taarifa zao sawa na asilimia 11.14
ya idadi ya wapiga kura walioandikishwa mwaka 2015 katika kanda ndogo zote 12.
54.
Mheshimiwa Naibu Spika, idadi ya wapiga kura wapya
walioandikishwa katika Kanda ndogo
zote 12 ni 5,666,343 ambayo ni
sawa na asilimia 31.38 ya idadi
ya Wapiga Kura walioandikishwa mwaka 2015 katika Kanda ndogo zote 12. Hii ni sawa na ongezeko la asilimia 14.38 la makadirio ya awali (asilimia
17).
Vilevile, idadi ya wapiga kura
walioondolewa kwa kupoteza sifa ni 14,894
ambayo ni sawa na asilimia 0.08 ya
idadi ya wapiga kura walioandikishwa mwaka 2015 katika kanda ndogo zote 12.
55.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kutoa wito kwa
Tume kuongeza kasi ya uandikishaji. Kadhalika, natoa rai kwa wananchi kutumia
haki yao hiyo ya kikatiba na kujitokeza kwa wingi kwa lengo la kuboresha
taarifa zao na kujiandikisha upya kwa wale wenye umri wa miaka 18 au
watakaofikisha umri huo ifikapo Oktoba, 2020.
Migogoro
ya Ardhi
56.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha hivi karibuni tumeshuhudia ongezeko la shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii na hivyo,
kuongezeka kwa mahitaji ya ardhi kwa ajili ya kilimo, ufugaji na uwekezaji.
Hali hiyo, imesababisha migogoro, malalamiko na kero mbalimbali zinazohusiana
na matumizi ya ardhi katika baadhi ya maeneo nchini.
57.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na juhudi
mbalimbali za kuhakikisha kuwa migogoro ya ardhi nchini inatatuliwa kwa njia ya
amani. Aidha, katika kushughulikia migogoro ya matumizi ya ardhi, Mheshimiwa
Rais wetu mpendwa, Dkt. John Pombe Magufuli ametoa kibali kwa vijiji 920 kati ya 975 vilivyokuwemo ndani ya hifadhi na mapori na maeneo ya hifadhi kuhalalishwa
rasmi kwa ajili ya shughuli za kiuchumi na kijamii.
58.
Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa, Serikali imeanza utekelezaji wa agizo la Mheshimwa Dkt. John Pombe
Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania la kusogeza huduma za ardhi
karibu na wananchi kwa kuanzisha ofisi za ardhi za mikoa 26 na kuimarisha ofisi za ardhi za halmashauri zote badala ya ofisi
za ardhi za kanda.
MICHEZO
59. Mheshimiwa Naibu Spika, sanaa
imeendelea kuwa na mchango mkubwa kwenye Pato la Taifa na hata katika
kutengeneza ajira. Kwa mfano, kwa mwaka 2018/2019 sekta hiyo ilichangia asilimia 0.29 katika ukuaji wa Pato la Taifa.
Niwapongeze wasanii wetu kwa kuendelea kulitangaza vyema Taifa letu na
fursa zake na hivyo, kuchangia maendeleo ya nchi yetu kupitia utalii na
uwekezaji. Wasanii wa muziki wa bongo fleva, maigizo, uchongaji na uchoraji wamechomoza
katika kuongeza Pato la Taifa.
60. Mheshimiwa Naibu Spika, kwa
upande wa mpira wa miguu tunampongeza mchezaji wetu, Mbwana Samatta kwa kuweka
historia ya kuwa Mtanzania wa kwanza kucheza Ligi Kuu ya Uingereza katika Klabu
ya Aston Villa. Tunamtakia kila la kheri katika Ligi Kuu ya Uingereza ambayo
ni moja ya ligi ngumu, maarufu na yenye ushindani mkubwa duniani. Nitoe rai kwa
wachezaji wetu wa ndani, nao kujifunza kupitia mafanikio ya Samatta kwa kuongeza
bidii, nidhamu na kiu ya mafanikio.
61. Mheshimiwa Naibu Spika,
vilevile, nizipongeze timu zetu za wanawake za umri wa miaka chini ya 20 (U-20)
na miaka 17 (U-17) kwa kuendelea kufanya vyema kuelekea kufuzu kushiriki Kombe la
Dunia mwaka 2022. Wakati timu ya wanawake U-20 ikipata ushindi wa nyumbani na
ugenini dhidi ya Uganda, timu ya wanawake U-17 nayo iliiondosha Burundi kwenye
mashindano kwa jumla ya magoli 6-1. Naipongeza pia Kilimanjaro Queens kwa kuchukua ushindi wa pili wa CECAFA. Kwa
mafanikio hayo ya soka nchini kwa wanawake, nalipongeza Shirikisho la Soka
nchini (TFF) kwa usimamizi mzuri bila kumsahau Mlezi wa Timu za Wanawake,
Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania.
62. Mheshimiwa Naibu Spika, nawapongeza
pia vijana wetu wa kiume chini ya miaka 20 ambao walifanikiwa kuwa mabingwa wa
michuano ya mpira wa miguu kwa CECAFA nchini Uganda. Nampongeza sana kijana
wetu Kelvin John kwa kusajiliwa na timu ya GENK ya Ubelgiji kwenye Kikosi chao
cha U-20.
63. Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa
ndondi nako tumeendelea kufanya vizuri. Nitumie nafasi hii kumpongeza bondia
wetu Salim Mtango ambaye tarehe 31 Januari, 2020 alimtwanga Bondia Surriya Tatakhun
kutoka Thailand kwa Technical Knock Out
(TKO).
64. Mheshimiwa Naibu Spika, kama
unavyofahamu, Timu yetu ya Bunge ilishiriki Michezo ya Mabunge ya Afrika
Mashariki Kampala, Uganda kuanzia tarehe 8 hadi 18 Desemba, 2019. Katika
Michezo hiyo timu yetu ya Bunge ilifanikiwa kupata jumla ya medali 18. Medali
hizo zilihusisha dhahabu tano, fedha 10 na shaba tatu. Nitumie fursa hii
kuipongeza timu ya Bunge kwa mafanikio hayo pamoja na kulitangaza vema Bunge
letu huko nje.
65. Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa
hii angalau kuwatambua kwa majina Waheshimiwa Wabunge waliotuletea medali za
dhahabu kama ifuatavyo:
(i)
Mhe. Dkt. Tulia Ackson, Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania;
(ii)
Mhe. Anatropia Theonest;
(iii) Mhe. Esther
Matiko;
(iv) Mhe.
Yosepher Komba; na
(v) Mhe. Rose
Tweve.
66. Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia
kutambua juhudi za Bwana Nick Reynolds maarufu kama Bongozozo na fujo
isiyoumiza katika kutangaza nchi yetu, vivutio vyetu vya utalii pamoja
na lugha ya Kiswahili. Ameonesha uzalendo wa kuitangaza nchi yetu licha ya kuwa
yeye si Mtanzania. Hivyo, natumia fursa hii kuwapongeza wanamichezo pamoja na
wasanii ambao wamekuwa wakifanya kazi kubwa ya kuitangaza nchi yetu sambamba na
kujipatia kipato.
67. Mheshimiwa Naibu Spika, nyote
mtakubaliana nami kuwa kwa sasa michezo na sanaa ni chanzo kikubwa cha ajira na
kipato hususan kwa vijana. Aidha, nisisitize kuwa michezo ni kinga na tiba kwa
magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo kisukari, shinikizo la damu na unene
uliopitiliza. Kutokana na faida hizo, niendelee kutoa rai kwa wananchi
kushiriki kikamilifu katika michezo. Aidha, Serikali kwa upande wake itaendelea
kuweka mfumo bora wa kisera na kisheria ili kuhakikisha sekta ya michezo inakuwa
na kuchangia ipasavyo katika Pato la Taifa.
HITIMISHO
68. Mheshimiwa Naibu Spika, nihitimishe hotuba yangu kwa
kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa michango yenu mbalimbali muhimu katika kuboresha
maisha ya wananchi wetu. Nimshukuru Katibu wa Bunge na wasaidizi wake kwa
huduma nzuri na msaada mkubwa ambao wamekuwa wakitupatia kwa kipindi chote
tulichokuwa hapa Bungeni.
69. Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru pia watendaji wa
Serikali na taasisi mbalimbali kwa kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa
weledi, umahiri na ufanisi mkubwa na hivyo, kufanikisha shughuli zilizopangwa na
Bunge lako tukufu bila kuwasahau wanahabari kwa uchambuzi wa hoja na mwenendo
mzima wa Bunge na kufikisha habari hizo kwa wananchi.
70. Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, nivishukuru vyombo vya
ulinzi na usalama kwa huduma ambazo wamekuwa wakizitoa kwa washiriki wa Bunge
hili. Pia, niwashukuru madereva wote waliotuhudumia wakati wote tukiwa hapa.
Nawatakia heri katika safari ya kurejea nyumbani.
71. Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, sasa naomba
kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu liahirishwe hadi tarehe 31 Machi, 2020 siku ya Jumanne saa tatu
kamili asubuhi katika ukumbi huu jijini Dodoma.
72. Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.
No comments:
Post a Comment