Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akiweka Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Jengo la Mahakama Kuu ya Zanzibar, linalojengwa katika eneo la Tunguu Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja hafla hiyo imefanyika leo 10-2-2020
SERIKALI ya
Mapinduzi ya Zanzibar imekuwa ikishughulikia sana suala la kuwandalia
wafanyakazi wake mazingira mazuri na yaliyo salama ya kufanya kazi ili wananchi
waweze kupata huduma kwa urahisi na bila ya usumbufu.
Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein aliyasema hayo leo katika
hafla ya uwekaji wa Jiwe la Msingi la Mahkama Kuu mpya, inayojengwa huko
Tunguu, Wilaya ya Kati, Mkoa wa Kusini Unguja ambapo hafla hiyo ni miongoni mwa
shamra shamra za wiki ya Sheria hapa nchini.
Katika hotuba yake Rais Dk. Shein alisema kuwa ndio
maana majengo kadhaa ya baadhi ya Taasisi za Serikali yaliyokuwa na ufinyu wa
nafasi au uchakavu mkubwa yamefanyiwa matengenezo na mengine kujengwa upya
katika uongozi wa Awamu zilizopita na Awamu hii ya Saba.
Aliongeza kuwa uwamuzi uliochukuliwa wa kujenga
jengo jipya la Mahkama Kuu huko Tunguu umezingatia mambo mengi ikiwa ni pamoja
na kutekeleza dhamira ya Serikali ya kuimarisha mazingira bora na salama
ya kufanyia kazi kutokana na ukweli
kwamba jengo la Mahkama Kuu ya Vuga halikidhi haja.
Alisema kuwa hapo siku za nyuma lilikuwa linatosha
kwa kutoa huduma kwa wakati huo wa karne iliyopita kulingana na mahitaji,
mazingira na teknolojia iliyopo ambapo hivi sasa shughuli zimekua zikiongezeka.
Rais Dk. Shein
alisema kuwa jengo la Mahkama Kuu ya Vuga lililojengwa miaka mia moja
iliyopita lilikidhi haja ya shughuli zake zilizokusudiwa kwa siku za nyuma kwa sababu
wakati huo idadi ya watu wote wa Zanzibar ilikuwa ndogo na kwa mujibu wa Sensa
zilizofanyika katika miaka tofauti hapa Zanzibar zinaonesha kwamba idadi ya
watu imekuwa ikiongezeka.
“Kwa upande wa Sekta ya Sheria, Serikali imefanyia
matengenezo makubwa majengo yetu ya mahkama, pamoja na kuimarisha miundombinu
ya Wizara ya Katiba na Sheria na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, ili pawe na
mazingira mazuri ya kutolea huduma kwa wananchi” alisema Dk. Shein.
Rais Dk. Shein alieleza kwamba katika eneo hilo la
Tunguu, mbali ya kujenga jengo jipya la Mahkama Kuu vile vile, Serikali
itajenga Skuli ya Sheria (Law School) na
kuitaka Wizara husika kuhakikisha ujenzi huo unafanywa hatua kwa hatua katika
Bajeti ijayo ya mwaka 2020-2021.
Aidha, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kurejea
kauli yake ya kuwataka maofisa wa ununuzi na uwagizishaji katika taasisi za
Serikali kuwa wakweli, weledi, wawazi na waaminifu na wasifanye mizengwe katika
shughuli zao za kazi sambamba na kufuata
sheria za manunuzi.
Aliwataka watendaji hao kutofanya yale ambayo
yaliwahi kusikika ambayo yamepelekea kuzorotesha miradi kadhaa na kuwaeleza
kuwa Serikali haitosita kuwachukulia hatua za kisheria pale watakapogundulika
kufanya hivyo.
Hivyo, Rais Dk. Shein aliwataka watendaji hao kuwa
waadilifu kwani Serikali imewapa dhamana hivyo ni vyema wakazitumikia dhamana
walizopewa ipasavyo.
Sambamba na hayo, rais Dk. Shein alisema kuwa
Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Awamu ya Saba, imelazimika kuimarisha sekta
ya sheria na imeunda Wizara Maalum ya Katiba na Sheria kwa lengo la kuimarisha
sekta ya sheria na muhimili wa Mahkama.
Alieleza kuwa tangu mwaka 2010, Serikali
imeuimarisha utendaji wa kazi wa mahkama katika Nyanja mbali mbali kama vile
kuzipatia mahkama hizo vitendea kazi, kuongeza majaji, mahakimu, makadhi pamoja
na kufanyia mapitio sheria mbali mbali ambapo pia, sheria 92 zimetungwa hadi Januari
2020.
Rais Dk. Shein pia, alieleza juhudi zinazoendelea
kuchukuliwa katika kuhakikisha vitendo vya udhalilishaji wa Wanawake na Watoto
vinafanyiwa kazi ipasavyo.
Pamoja na hayo, rais Dk. Shein alieleza uwamuzi wa
kuufanya mji mpya wa Tunguu kuwa ni Makao Makuu ya Muhimili wa Mahkama ni hatua
muhimu katika utekelezaji wa Mipango Miji na kuuimarisha Mji huo.
Rais Dk. Shein alieleza matarajio yake juu ya
ujenzi huo na kusema kuwa Serikali itatoa fedha za ujenzi huo kwa wakati ili
jengo hilo likamilike kwa wakati kwa mujibu wa makubaliano na Mkandarasi na
kusema kuwa katika Bajeti ya mwaka huu Serikali imeweka kipaumbele katika
majengo mawili likiwemo jengo hilo na lile la jengo jipya la abiria la uwanja
wa ndege wa Abeid Amani Karume.
Nae Jaji Mkuu wa Zanzibar Omar Othman Makungu
alitoa pongezi kwa Rais Dk. Shein kwa kutekeleza ahadi yake pamoja na
kuhakikisha Serikali anayoiongoza inaimarisha sekta ya sheria sambamba na
kuzifanyia kazi changamoto kadhaa zilizokuwepo kwenye sekta hiyo.
Aliongeza kuwa Rais Dk. Shein katika uongozi wake
amewacha alama kubwa kwa Mahkama, kwa Zanzibar na Tanzania nzima kwa jumla
kutokana na mambo mengi makubwa aliyoyafanya na kuahidi kua juhudi
zitachukuliwa za ujenzi kuhakikisha Dk. Shein analifungua jengo hilo.
Alieleza juhudi zitakazochukuliwa katika
kuhakikisha ujenzi wa skuli ya sheria unatekelezwa huku akieleza kuwa hatua ya
ujenzi wa mahkama hiyo mpya inakwenda sambamba na utekelezaji wa ujenzi wa
Mahkakama mpya katika nchi za ukanda wa Afrika Mashariki.
Waziri wa Wizara ya Katiba na Sheria Khamis Juma
Maalim kwa upande wake alitoa pongezi
kwa Rais Dk. Shein kwa kuhakikisha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inatoa
asilimia mia moja ya ujenzi wa Mahkama hiyo mpya.
Waziri huyo alieleza kuwa ujenzi huo ni miongoni
mwa utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 huku akipongeza
juhudi za Rais Dk. Shein katika kuongeza idadi ya Majaji ili kuimarisha haki na
sheria kuweza kupatikana.
Mapema Mtendaji Mkuu wa Mahakama Zanzibar,Ndg.Kai Bashir Mbarouk akitoa maelezo ya kitaalamu alisema kuwa Mkataba wa
ujenzi jengo hilo ulitiwa saini rasmi tarehe 21 Oktoba, 2019 baina ya Mahkama
na Mjenzi ambaye ni Kampuni ya ‘Advent Construction Limited’ ya Dar es Salaam.
Alieleza kuwa Mshauri wa Mwelekezi anayesimamia ujenzi huo ni kampuni
ya ‘Hab Consult’ ya Dar es Salaam ambayo pia, ndiyo iliyosanifu michoro
ya jengo hilo ambapo mradi huo unaangaliwa
na Wakala wa Majengo ya Serikali pamoja na Mhandisi wa Mahakama.
Sambamba na hayo, Mradi huo unatarajiwa kugharimu
jumla ya TZS Bilioni 14.3 fedha ambazo zote zimetolewa na Serikali ya Mapinduzi
ya Zanzibar kwa asilimia mia moja pia, kuna Kamati Maalum ya Mradi yenye
wataalamu waandamizi kutoka Taasisi mbali mbali za Serikali ambapo mambo yote
hayo yanafanywa ili kuhakikisha ujenzi huo unaendana na viwango na masharti
yaliyokubaliwa katika Mkataba.
Mapema Rais Dk. Shein alijenga tofali katika jengo
hilo ikiwa ni kiashiria cha kuweka jiwe la msingi na baadae kufungua kipazia
maalum cha jiwe la msingi ambapo katika hafla hiyo viongozi mbali mbali wa
Serikali, vyama vya siasa na wananchi walihudhuria akiwemo Makamo wa Pili wa
Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Jaji Mkuu Mstaafu wa Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania Mohammed Othman Chande na viongozi wengineo.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment