Na Mwajuma Juma, Zanzibar
Kamati ya Kitaifa ya Madawati Zanzibar inatarajia kugawa madawati 4,540 kwa Shule za Msingi za Unguja na Pemba kwa awamu ya kwanza ili kupunguza uhaba wa vikalio katika kila shule Nchini.
Akikagua madawati hayo Mwenyekiti wa kamati hiyo Haroun Ali Suleiman amesema hatua hiyo ni juhudi za Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.. Ali Mohamed Shein, katika kuhakikisha tatizo la uhaba wa madawati kwa wanafunzi linamalizika Zanzibar.
Aidha Mhe.Haroun amezitaka Shule zitakazo bahatika kupata madawati hayo kuandaa kamati za kusimamia utunzaji ili yaweze kudumu kwa muda mrefu na kutumika kama yalivyokusudiwa .
Kwa upande wake Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar Simai Mohammed Said amesema kazi inayofanywa na kamati hiyo ni ya kizalendo na imefanywa kwa wakati muafaka hali ambayo inaleta kasi ya ukuaji wa sekta ya Elimu nchini.
Nae Mkurugenzi Idara ya Sera,Mipango na Utafiti Wizara ya Elimu Zanzibar Khalid Masoud Waziri amesema madawati hayo ya awamu ya kwanza yameletwa kontena tisa,ambapo awamu ya Pili yanatarajiwa kuletwa kontena 12 na yalitarajiwa kufika hivi karibuni lakini yamechelewa kufika kutokana na maradhi ya korona yaliokumba dunia.
Madawati hayo ni michango wa wadau mbalimbali wa Elimu wakiwemo viongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na wafanya biashara mbalimbali nchini.
No comments:
Post a Comment