Mkurugenzi wa Women Wake Up (WOWAP) ambaye
pia ni Mbunge wa Viti maalum, Fatma Toufiq akiongea katika kikao hicho
kilichowakutanisha wadau wa haki za
binadamu ili kuupitia mkataba wa Afrika
unaohusu demokrasia, uchaguzi , utawala bora
na haki za binadamu kwa lengo la kuweka mikakati ya kushawishi serikali
iweze kuuridhia. Mkutano huo ulifanyika Dodoma mapema leo.
Na Mwandishi wetu,
Wadau wa haki za binadamu wamekutana leo
jijini Dodoma kujadili Mkataba wa Afrika kuhusu Demokrasi, Uchaguzi na Utawala
Bora kwa lengo la kuweka namna bora ya kushawishi watunga sera waweze kuukubali na kuuridhia ili utumike katika sheria za nchi.
Akiongea katika kikao kazi cha siku moja kilichoandaliwa na Kituo cha
Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Afisa Programu na Mratibu wa Ofisi ya Dodoma
wa Kituo hicho cha sheria, William
Mtwazi alisem kuwa lengo la kikao kazi hicho ni kuwakutanisha wadau wa haki za
binadamu ili kuupitia mkataba huo wa Afrika na kuangalia yaliyomo katika
mkataba waweze kuielimisha jamii kuhusu
mkataba huo ili nao waweze kupaza sauti zao kwa watunga sera na serikali iweze
kuuridhia.
“Kati
ya nchi wanachama 55 wa Umoja wa Afrika ni nchi tisa tu ambazo hazijaridhia
mkataba huo kutumika katika sheria zao, moja ya nchi hizo ni Tanzania, hivyo
tumekutana hapa kujadiliana na kujaribu kuangalia kwa nini mpaka sasa mkataba
huu haijauridhiwa, shida iko wapi na kutafuta namna bora ya kushawishi watunga sera kuweza kuukubali”, alisema Mtwazi
Aliendelea kusema kuwa watakapokuwa
wanaupitia mkataba huo utawasaidia kujua umuhimu wake na kupima uchaguzi
uliopita ulikuwa mzuri kiasi gani na wapi inabidi paboreshwe zaidi ili uchaguzi
uwe mzuri zaidi.
“Hii ni hatua ya kwanza ambapo wadau tumekutana kuujadili mkataba kuuelewa vizuri , hatua
itakayofata ni kukutana na mamlaka husika kama Kamati ya Kudumu ya Katiba na
Sheria ya Bunge, Wizara ya Katiba na Sheria, Wizara ya Mambo ya Nje na wadau
wengine ili kuzishawishi kuukubali na kuridhia uingizwe katika sheria zetu”,
aliongeza Mtwazi
Mkataba huo wa Afrika kuhusu Demokrasia,
Uchaguzi na Utawala bora ulitungwa mwaka 2007 katika mkutano mkuu wa Umoja wa
Afrika (AU) na kuanza kutumika mwaka 2012 baada ya nchi
kumi na tano (15) kuuridhia kama mkataba huo unavyohitaji.
Mkataba huu unasisitiza nchi wanachama kuwa
na taasisi inayosimamia uchaguzi ambao ni huru, haki, usawa na kwa uwazi ili
kujenga utamaduni wa kubadilishana uongozi kwa salama na amani.
Aidha, Mkataba huo unahimiza umuhimu wa nchi
wanachama kuwa na mifumo ya kujipima kila baada ya uchaguzi ili kuangalia
mapungufu kwa lengo la kuboresha ili kuwa na uchaguzi mzuri zaidi.
Mpaka sasa kando ya Tanzania, nchi nyingine
ambazo bado hazijaridhia ni pamoja na Kameruni, Morocco, Libya, Visiwa vya
Shelisheli, Misri, Zimbabwe na Gambia.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha kupambana
na vitendo vya ukatili wa kijinsia (CAGBV), Sophia Komba alisema kuwa mkataba
huu ukiridhiwa utaweka njia ya kuongoza kupata uchaguzi huru na wa haki kwa
sababu unasisitiza masuala ya demokrasia, haki za binadamu na utawala bora.
Komba alisema kwa kuwa Tanzania inatarajia
kufanya uchaguzi mkuu hivyo anaona ni muhimu kusisitiza
umuhimu wa kuwa na uchaguzi huru na wa haki nchini ili demokrasia iweze
kuimarika.
Afisa Programu na Mratibu wa Ofisi Dodoma
wa Kituo Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), William Mtwazi akiongea katika
kikao kilichowakutanisha wadau wa haki
za binadamu ili kuupitia mkataba wa
Afrika unaohusu demokrasia, uchaguzi , utawala bora na haki za binadamu kwa lengo la kuweka
mikakati ya kushawishi serikali iweze kuuridhia. Mkutano huo ulifanyika Dodoma
mapema leo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha kupambana na
vitendo vya ukatili wa Kijinsia (CAGBV), Sophia Komba, ambaye pia ni Mjumbe wa
Bodi ya LHRC akiongea na Vyombo vya habari katika kikao hicho
kilichowakutanisha wadau wa haki za
binadamu ili kuupitia mkataba wa Afrika
unaohusu demokrasia, uchaguzi , utawala bora
na haki za binadamu kwa lengo la kuweka mikakati ya kushawishi serikali
iweze kuuridhia. Mkutano huo ulifanyika Dodoma mapema.
No comments:
Post a Comment