Mheshimiwa Spika,
Sina budi kumshukuru Allah (S.W) mwingi wa rehma na
utukufu, kwa kutujaalia uhai na Afya njema, na kutuwezesha kukutana tena katika
Baraza hili la Tisa, kwa dhamira ya kuendelea kuwatumikia wananchi wa Zanzibar
ambao ndio sababu ya sisi kusimama katika Baraza hili.
Aidha nakushukuru na kukupongeza wewe Mheshimiwa Spika, kwa jitihada zako na
namna unavyoliongoza Baraza hili tukufu kwa ustadi na upeo mkubwa. Ni imani yangu kwamba, utaendelea kutuongoza
kwa uadilifu na ustadi wa hali ya juu kwa lengo la kuimarisha Demokrasia katika
chombo hiki muhimu cha kuwatumikia wananchi katika kipindi hiki kigumu cha
janga la maradhi ya ‘COVID 19’.
Mheshimiwa
Spika,
Pia, naomba kuchukua fursa hii, kumshukuru na
kumpongeza kwa dhati Mhe.Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na Watendaji
wake wote kwa jitihada kubwa wanazozichukua katika kulipeleka mbele gurudumu la
maendeleo ya nchi yetu na Taifa kwa ujumla.
Mheshimiwa
Spika,
Lakini pia kwa namna ya pekee, nawashukuru Wajumbe
wote wa Kamati ya Ardhi na Mawasiliano kwa kazi zao nzuri wanazozifanya wakati
wote wa kazi za Kamati, jambo ambalo limepelekea wepesi kwangu kuweza kuiongoza
Kamati hii inayosimamia Wizaramuhimu kabisa.
Wajumbe wa Kamati wameonesha umahiri, weledi na umakini wa hali ya juu
na wameweza kuijadili ipasavyo Bajeti hii na kuhoji mambo mengi ya msingi, kwa
lengo la kuhakikisha fedha
wanazoidhinisha katika Baraza hili, zinatumika vizuri na kwa lengo
lakuwaletea maendeleo wananchi wa Zanzibar.
Mheshimiwa
Spika,
Napenda kutumia fursa hii pia, kuwapongeza na
kuwashukuru Wawakilishi wote waliomo katika Baraza lako Tukufu, kwa kuendelea
kuwawakilisha na kuwatumikia wananchi waliowachagua. Ni wazi kwamba wananchi
wamejenga imani kubwa kwetu, nasi hatuna budi kurejesha imani kwao, kwa
kuwatumikia kwa dhati na kwa moyo wetu wote, kwa dhamira ya kutetea maslahi yao
katika Baraza hili tukufu.
Mheshimiwa
Spika,
Vile vile, Naomba niwakumbushe wajumbe wenzangu
kuwa kipindi chetu cha miaka mitano kimefikia ukingoni, hivyo kila mmoja wetu
ajitahidi kutekeleza aliyoahidi na kwa pamoja tutakuwa tumemsaidia Mheshimiwa
Rais kutekeleza ilani ya Chama cha Mapinduzi na kukamilisha ahadi zake kwa
wananchi waliotuchagua kwa wakati.
Mheshimiwa
Spika,
Kabla ya kuendelea na hotuba hii, kwa ruhusa yako,
na kwa heshima ya kipeee naomba niwatambue Wajumbe wa Kamati ya Ardhi na
Mawasiliano kama ifuatavyo:
1.
Mheshimiwa
Hamza Hassan Juma Mwenyekiti
2.
Mheshimiwa
Suleiman Sarhan Said M/Mwenyekiti
3.
Mheshimiwa
Hidaya Ali Makame Mjumbe
4.
Mheshimiwa
Jaku Hashim Ayoub Mjumbe
5.
Mheshimiwa
Khadija Omar Ali Mjumbe
6.
Mheshimiwa
Said Omar Said Mjumbe
7.
Mheshimiwa Ussi
Yahaya Haji Mjumbe
Mheshimiwa Spika,
Aidha,
Kamati hii inafanyakazikwa kusaidiwa na Makatibu wawili ambao wamekuwa
wakitusaidia kwa kiasi kikubwa na kwa uweledi wa hali ya juu katika kutekeleza
majukumu yetu, msaada wa makatibu hao umekuwa chachu ya mafanikio makubwaya
Kamati hii. Makatibu hao ni:
1.
Ndg. Fatma
Omar Ali Katibu
2.
Ndg. Mwaka
Mwinyi Waziri Katibu
Mheshimiwa
Spika,
Moja kati ya jukumu la msingi la Kamati yetu ni
kuchambua mapendekezo ya Serikali, kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya
Wizara ya kila mwaka, hivyo katikakutekeleza jukumu hilo lililoelezwa katika
Kanuni ya 96(1)ya Kanuni za Kudumu za Baraza la Wawakilishi (Toleo la 2016),
Kamati yangu ilikaa na kuijadili na hatimaye kupitisha Makadirio ya Mapato na
Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji na Nishati, sasa kwa ruhusa yako na
kwa niaba ya Kamati, napenda kuwasilisha maoni ya Kamati kuhusiana na Bajeti hiyo
kwa mwaka wa fedha 2020/2021.
Mheshimiwa
Spika,
Baada ya utangulizi huo sasa, naomba nitekeleze
jukumu nililopewa na Kamati la kuwasilisha maoni ya Kamati, mbele ya Baraza
lako tukufu.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa mwaka huu wa fedha Wizara ya Ardhi, Nyumba, Maji
na Nishati imepangiwa kutekeleza Programu Kuu Tatu (3) ambapo utekelezaji wake
unasimamiwa na Programu Ndogo Saba (6).
PROGRAMU
KUU YA USIMAMIZI WA ARDHI NA MAKAAZI
Mheshimiwa Spika,
Programu Kuu hii ina jukumu la kuhakikisha usalama
wa matumizi ya ardhi na huduma za makaazi bora kwa wananchi. Aidha Programu Kuu
hii inatekelezwa kupitia programu ndogo mbili ambazo ni Programu ndogo ya
Utawala wa Ardhi, Nyumba na Makaazi na Programu ndogo ya Utatuzi wa Migogoro ya
Ardhi.
PROGRAMU
NDOGO YA UTAWALA WA ARDHI, NYUMBA NA MAKAAZI
Mheshimiwa
Spika,
Dhumuni la programu ndogo hii ni kuhakikisha
usalama wa umiliki wa ardhi na upatikanaji wa makaazi bora kwa wananchi wa
Zanzibar.
Mheshimiwa Spika,
Programu ndogo hii inajumuisha Kamisheni ya Ardhi,
Ofisi ya Mthamini Mkuu wa Serikali, Shirika la Nyumba, Wakala wa Majengo,
Mamlaka ya Uhifadhi na Uendelezaji wa Mji Mkongwe, Bodi ya Usajili wa
Wakandarasi, Bodi ya Usajili wa Wasanifu, Wahandisi na Wakadiriaji wa Majengo,
Bodi ya Condominium pamoja na Bodi ya Kudhibiti Kodi za Nyumba.
KAMISHENI
YA ARDHI
Mheshimiwa Spika,
Kwa upande wa Kamisheni ya Ardhi bado wanafanya
kazi katika jengo bovu ambalo haliridhishi hata kidogo kwa wafanyakazi wa
taasisi hii, Jengo ambalo linavuja kwa kiwango kikubwa hali inayopelekea
usumbufu kwa watendaji wa Ofisi hii hasa kwa kipindi kama hiki cha mvua.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati pia inaiomba Serikali kuwapatia Kamisheni ya
Ardhi jengo jipya litakaloendana na hadhi ya utendaji wa taasisi hii na umuhimu
wake.
Mheshimiwa
Spika,
Pamoja na kazi nzuri inayofanywa na Kamisheni ya
Ardhi bado kuna tatizo la ucheleweshaji wa utoaji wa hati za haki ya matumizi
ya ardhi kwa wananchi, jambo linalosababisha ongezeko la migogoro ya ardhi
katika kisiwa cha Zanzibar. Hivyo, Kamati yangu inaitaka Kamisheni ya Ardhi
kuongeza kasi ya utoaji wa hati ya matumizi ya ardhi kwa wananchi na wawekezaji
ili waweze kutimiza malengo yao kwa wakati.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati inaiomba Serikali kupitia Wizara ya Ardhi,
Nyumba, Maji na Nishati kuifanyia mapitio ya haraka Sheria ya Ardhi hususan
katika kifungu kinachohusiana na utoaji wa “lease”
za maeneo ya uwekezaji. Kuchelewa kuifanyia mapitio Sheria hiyo ni kuikosesha
Serikali mapato yatokanayo na maeneo ya uwekezaji.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yangu imegundua miaka ya nyuma kuna watu
walipatiwa “Right of Occupance”
ambayo maeneo hayo yalipaswa kupatiwa “lease”
ambapo Serikali ingeliweza kupata Mapato katika maeneo hayo ya uwekezaji, na
hili ndilo jambo linalowafanya watu kuyadhibiti maeneo ya uwekezaji bila ya
kuyaendeleza kwa sababu wanajua kuwa hawana jukumu la kulipia wakati wanakuja
wawekezaji makini na kutaka kuwekeza katika maeneo hayo ila hawayapati jambo
ambalo hukosesha mapato Serikali na ajira kwa vijana wetu.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yangu inamuomba Mhe.Waziri kubadilisha
umiliki wa watu hao kutoka “Right of
Occupance” kuzibadili ziwe “lease”
ili kuongeza thamani ya ardhi lakini pia kupata mapato makubwa ili kuweza
kusaidi kunyanyuka kwa uchumi.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yangu inaipongeza Serikali kwa kusaidia
kutatua migogoro ya Ardhi ambayo imedumu kwa muda mrefu, migogoro mingi iliyokuwepo
tangu miaka ya 1995 lakini kwa jitihada zako Mhe. Waziri umekuwa muwazi katika
kuwasaidia wanyonge hasa wananchi wa vijijini ambao wamenyang’anywa maeneo na
wajanja mbali mbali hasa kutoka mjini.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa wale wananchi wenye asili ya maeneo hayo ambao
wamerithi au ya ukoo wao wasilazimike kupewa “Lease” kwasababu wapo katika ardhi yao lakini kwa wale ambao
wamenunua ni lazima wapewe lease ili Serikali ikusanye mapato.
Mheshimiwa
Spika,
Pia, Kamati yangu inaiomba Serikali kupitia kwako
Mhe. Waziri kulipatia ufumbuzi eneo la Fungu refu Mkokotoni ambalo wananchi wa
huko pia wanahitaji ufumbuzi ili nao waweze kulitumia kwa ajili ya shughuli zao
za kimaisha na Maendeleo ili kupambana na hali ya umaskini.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yangu kwa mara nyengine inaipongeza Wizara
kwa kuwashajiisha wananchi kusajili na kuigawa mirathi yao kwani kuna familia
nyingi zinatumia mali za Mirathi ikiwemo nyumba na Mashamba wakati bado
havijarithishwa hili ni jambo baya sana linaweza kwenda kutupatia adhabu kubwa
huko tuendako, na wengine mali hizi za mirathi ambazo hazijarithishwa pia
huzitumia mapato yake kwa ajili ya kwenda kwenye ibada ya Hijja jambo ambalo ni
haramu, kwa hiyo Kamati inaungana na Wizara katika kuwaelimisha wananchi kusajili
mali zao za Mirathi pamoja na kufuata utaratibu
wa kuzirithisha ili kila mtu apatewe haki yake na aitumie kwa mipango yake ya
Maisha.
Mheshimiwa
Spika,
Vile vile, Kamati pia inapongeza Wizara kwa
kuendelea kuzitambua Eka tatu tatu na kuzipatia hati lakini ushauri wa Kamati
kwa zile Eka ambazo zimeshajengwa nyumba za makaazi sana kwa asilimia kubwa
basi ni vyema zikabadilishwa matumizi yake ili ziendane na dhamira ya wananchi
kupewa Ekari tatu kwa ajili ya Kilimo.
Mheshimiwa
Spika,
Sambamba na hilo, Kamati yangu inaitaka Idara ya
Mipango Miji na Vijiji kuharakisha Upangaji na Upimaji wa Miji na Vijiji na
kuweka miundombinu yote muhimu ikiwemo Makaazi, Maofisi, Viwanja vya Michezo,
Maeneo ya kufanyia Ibada, Maeneo ya Kilimo, Maeneo ya wazi kwa shughuli za
kijamii pamoja na maeneo ya uwekezaji.
Mheshimiwa
Spika,
Katika Idara hii bado kuna mambo Kamati yangu
inashauri kwamba ni vyema yakatofautishwa maeneo ya Makaazi pamoja na yale ya uwekezaji
hasa katika ujenzi wa Mahoteli ya Kitalii kwani kuchanganyika maeneo ya
Mahoteli ya kitalii pamoja na Makaazi ya wananchi inachangia kuharibu silka na
utamaduni wa uzanzibari, lakini pia unawakosesha utulivu Watalii wanaokuja
kutembelea nchi yetu.
Mheshimiwa
Spika,
Pia, Kamati yangu inaishauri Idara ya Mipango Miji na
Vijiji kushirikiana na Wizara ya Ujenzi na Mawasiliano katika kupanga “Road Master Plan” pamoja na
miundombinu ya Maji Machafu kwani tumeona katika miaka ya hivi karibuni
Mafuriko yamekuja makubwa na kuathiri maisha na shughuli za kiuchumi.
OFISI
YA MTHAMINI MKUU WA SERIKALI
Mheshimiwa Spika,
Hadi hivi sasa Ofisi ya Mthamini Mkuu wa Serikali
bado inakabiliwa na changamoto ya ukosefu wa Kanuni itakayomuongoza Mthamini
katika utekelezaji wa kazi zake za uthamini hususan katika masuala ya viwango
vya tathmini ya makaazi na vipando hali inayompelekea kushindwa kutekeleza
majukumu yake kama Sheria inavyomtaka.
Mheshimiwa
Spika,
Kutokana na Kadhia hiyo, Kamati yangu inaiomba
Serikali pamoja na Wizara kuharakisha ukamilishaji na upatikanaji wa Kanuni hii
ili kuweza kuwaondolewa wananchi usumbufu katika maeneo yote yaliokusudiwa
kutekelezwa miradi ya maendeleo. Pia, Kamati yangu inaitaka Afisi ya Mthamini
Mkuu wa Serikali kuweka viwango vya tozo na ada ili ziwasaidie katika kutekeleza
Majukumu yao ya kimaisha
Mheshimiwa
Spika,
Kuchelewa kwa Kanuni hii inapelekea kuwakosesha
wananchi wetu malipo yao kwa wakati hasa katika suala ucheleweshwaji wa ulipaji
wa fidia kwa wananchi na pia wakati mwengine hupelekea kucheleweshwa kwa baadhi
ya miradi.
Mheshimiwa
Spika,
Ufinyu wa Bajeti kwa Ofisi ya Mthamini Mkuu wa
Serikali bado ni changamoto inayokwamisha utekelezaji wa majukumu yao ya kila
siku. Ofisi hadi sasa haiwezi kujikimu katika suala zima la ufuatiliaji wa
masuala ya uthamini wa mali na vipando kwa taasisi za Umma na za Binafsi.
Mheshimiwa
Spika,
Mfano mzuri Ofisi ya Mthamini ilitakiwa kufanya
uthamini wa mali na vipando katika mradi wa utanuzi wa Kiwanja cha Ndege Pemba.
Kamati inasikitishwa kuona hadi leo Ofisi ya Mthamini imeshindwa kutekeleza
suala hilo na kupelekea wananchi kuilalamikia Serikali na kushindwa kujua hatma
yao na sababu kubwa ni kuchelewa kwa kupitishwa viwango vya thamani ya mazao na
vipando ambavyo vilihitaji vipate baraka ya Bodi ambayo uzinduzi wake
ulichelewa.
Mheshimiwa
Spika,
Vile vile, Kamati inaipongeza Serikali kupitia
Wizara ya Fedha na Mipango kwa kuona umuhimu wa kuwaongezea fungu la fedha kwa
Ofisi ya Mthamini Mkuu wa Serikali kutoka katika mfumo wa ‘OC’ na kwenda katika
mfumo wa Ruzuku.
Mheshimiwa
Spika,
Pamoja na pongezi hizo, Kamati inaiona fedha ya
Ruzuku uliopangiwa Ofisi hii ni ndogo sana ambapo ni Milioni 132, 000,000 tu kwa mwaka mzima wa
fedha 2020/2021 hasa ukizingatia Ofisi ya Mthamini Mkuu wa Serikali ana
majukumu mengi ambayo ni ya kiutendaji na kiufuatiliaji zaidi ukilinganisha na
Ofisi nyengine.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yangu inaiomba Serikali kuiongezea Ofisi ya
Mthamini Mkuu wa Serikali fedha za Ruzuku kwa lengo la kuisaidia Ofisi hii
kuweza kufanya kazi zake kwa ufanisi na kwa wakati uliopangwa.
Mheshimiwa
Spika,
Ofisi hii pia ina changamoto ya ukosefu wa Ofisi
Pemba hali inayopelekea uzoroteshaji wa utekelezaji wa majukumu yao kwa upande
wa Pemba ambapo wafanyakazi waliopo Ofisi ya Unguja hulazimika kufanya kazi pia
katika maeneo ya Pemba pale inapohitajika jambo linalowaletea usumbufu mkubwa
haswa ukizingatia Ofisi yenyewe ina upungufu wa wafanyakazi.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yangu inaiomba Serikali kuharakisha
ukamilishaji wa muundo wa Utumishi kwa Ofisi ya Mthamini Mkuu wa Serikaliambao
utawapa mamlaka ya kuanzisha Ofisi ya Mthamini kwa upande wa Pemba, lengo ni
kuleta ufanisi katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku.
MAMLAKA
YA HIFADHI NA UENDELEZAJI WA MJI MKONGWE
Mheshimiwa Spika,
Kamati haridhishwi na ukusanyaji wa mapato wa Mamlaka
ya Hifadhi na Uendelezaji wa Mji Mkongwe. Kamati inatambua kwamba Mamlaka hii
ina uwezo wa kutosha wa kukusanya mapato kama ilivyopangiwa na Serikali kwani
ina vyanzo vingi ambavyo vipo hai kiutendaji. Kinachotakiwa ni usimamizi na
ufuatiliaji kupitia vyanzo hivyo.
Mheshimiwa Spika,
Kamati inaona wazi kwamba Mamlaka hii haisimamii
wala haifuatilii ipasavyo vyanzo vyake vya mapato ya ndani jambo ambalo
linalowapelekea wao kushindwa kufikia malengo ya mapato wanaokadiriwa
kuyakusanya kwa mwaka wa fedha husika.
Mheshimiwa Spika,
Mfano halisi wa hilo, mnamo mwaka 2019/2020 Mamlaka
hii ilipangiwa kukusanya katika kianzio chake cha utoaji wa vibali vya ujenzi
ilipangiwa kukusanya Milioni 150,000,000 ambapo hadi kumalizika kwa mwaka huo
wa fedha imefanikiwa kukusanya Milioni 22,640,000 tu ambapo sawa na asilimia
15.1 na kwa upande wa kianzio cha mapato ya kazi za biashara ilipangiwa
kukusanya Milioni 55,000,000 ambapo hadi kumalizika kwa mwaka huo wa fedha
imefanikiwa kukusanya Milioni 3,450,000 tu sawa na asilimia 6.3kwa kweli hii
haileti picha nzuri katika ukusanyaji wa mapato Kamati inaomba Serikali kuweka
umakini mkubwa katika usimamizi na ukusanyaji wa mapato kwa Bajeti ijayo .
Mheshimiwa
Spika,
Hali hii hairidhishi hata kidogo, Kamati yangu
inaiomba Serikali kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha na Mipango kufanya
ufuatiliaji wa karibu na wa mara kwa mara kwa taasisi zetu zote kwa lengo la
kubaini changamoto zinazowakabili katika zoezi zima la ukusanyaji wa mapato
kupitia vianzio wanavyopangiwa.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yangu inaona wazi kwamba kuna uvunjaji wa
mapato ya Serikali ndani ya Taasisi zetu. Kwa jicho la karibu tunaona wazi
kwamba Mamlaka hii kuna tatizo linalopelekea kutofikia malengo ya fedha
waliopangiwa kuyakusanya.
Mheshimiwa
Spika,
Pia, Mamlaka hii ina tatizo la kuchelewesha majibu
ya maombi ya vibali vya ujenzi kwa waombaji husika katika maeneo ya Mji Mkongwe
ambayo yana azma njema ya kuwekeza katika Hifadhi ya Mji wetu wa Kihistoria.
Mheshimiwa
Spika,
Uchelewaji wa majibu hayo kwa baadhi ya wawekezaji
wanaotaka kuwekeza katika hifadhi ya Mji Mkongwe hupelekea kuikosesha Mapato
makubwa Serikali yetu kwa maslahi ya nchi hii.
Mheshimiwa
Spika,
Kutokana na changamoto hii, Kamati inaiomba Mamlaka
hii kufanya haraka kuzijibu barua zote zinazofika ofisini kwao kwa ajili ya
maombi kwani kufanya hivyo ni kuisaidia Serikali kiingiza mapato yake ya ndani
na kinyume chake ni kuikosesha Serikali mapato hali inayopelekea kuathiri
uchumi wetu.
WAKALA
WA MAJENGO
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu inampongeza Mkurugenzi wa Waakala wa Majengo pamoja na
watendaji wake kwa kazi kubwa za kizalendo wanazozifanya za kusimamia ujenzi wa
baadhi ya taasisi za Serikali kwa kutumia gharama ndogo kulingana na uzito wa
kazi wanazozifanya.
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu inaitaka Waakala kuandaa Kanuni
zitakazowaekea makisio ya ujenzi au ukarabati tofauti na hivi sasa Wakala
anategemea ruzuku tu kutoka Serikalini kwani Wakala anao uwezo wa kuendesha
taasisi kupitia vianzio vyake vya ndani.
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yangu inaipongeza Serikali kwa kusikia kilio
chetu cha siku nyingi cha kujenga Jengo lao la Ofisi linalolingana na hadhi
yao. Kutokana na hali hiyo, Kamati yangu imefarijika kuona kuwa Wakala tayari imeshapata
eneo la kujenga Ofisi zao za kudumu.
PROGRAMU
NDOGO YA UTATUZI WA MIGOGORO YA ARDHI
MAHAKAMA
YA ARDHI
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yangu inampongeza sana Mwenyekiti mpywa wa
Mahakama ya Ardhi kwanza kwa mashirikiano yake kwa Kamati lakini pia kwa
kuendeleza yale mema yote yalioanzishwa na Mwenyekiti aliyetangulia,
akishirikiana na Mahakimu wenzake kwa kuharakisha uendeshaji wa kesi lakini pia
uharaka wa kuendesha kesi hizo na wananchi wengi wanaridhika na utendaji wa
Mahakama ya Ardhi kwa utendaji wao, isipokuwa tu Kamati imegundua kuna changamoto
nyingi katika mahakama hizo kama tulivyoelezea katika kikao kilichopita kwenye
ripoti za Kamati, kwa kifupi nizielezee baadhi yao ili iwe dira katika awamu
ijayo.
1.
Kwanza uhaba
wa wafanyakazi katika Mahakama zote za Unguja na Pemba.
2.
Uhaba wa
Mahakimu katika Mahakama zote za Unguja na Pemba jambo ambalo inambidi Mwenyewe
Mwenyekiti wa Mahakama ya Ardhi aingie kazini kwendwa kuendesha Kesi wakati
alitakiwa asimamie masuala ya kiutawala zaidi.
3.
Karibu
Mahakama zetu zote hazina Majengo yao wenyewe na zinafanyakazi katika Majengo
ya kuazima jambo ambalo linaleta shida katika utendaji wa kazi zao Kamati yangu
inaitaka Kamisheni ya Ardhi kuwapatia maeneo Mahakama ya Ardhi kwa Unguja na
Pemba ili kujenga Majengo yanayolingana na kazi zao.
4.
Changamoto
nyengine ni ukosefu wa usafiri kwa Mahakimu wote wa Unguja na Pemba jambo hili
halileti afya kwenye utoaji wa haki.
5.
Uhaba wa
Bajeti ambao umesababisha malimbikizo ya madeni ambayo watendaji ilibidi wakope
“Stationaries” pamoja na “Furnitures” ili utendaji wa Mahkama uendelee vizuri
lakini madeni hayo bado yapo hadi leo. Kamati yangu inaitaka Serikali kupitia
Wizara iwaingizie fedha za kutosha na kwa wakati ili waweze kulipa madeni na
kuweza kujikimu katika harakati zao za uendeshaji wa ofisi.
6.
Ukosefu w
usafiri kwa Wazee wa Mahakama ambapo siku za mvua wanapata usumbufu wa kufika
kazini kwa wakati na hili huleta usumbufu kwa wenye Kesi.
7.
Suala la
maslahi ya Mahakimu, Kamati yangu inaitaka Wizara kuharakisha “Scheme of
Service” ya Mahakimu ili ilingane na uzito wa kazi zao.
8.
Kamati imeona kuna ukosefu wa mavazi kwa Wazee
wa Mahakama kwani kazi zao nyingi huambatana na kutembelea baadhi ya maeneo
yenye migogoro na yenye mwitu, miiba na hata Mawe kwa hiyo Kamati inaitaka
Mahakama ya Ardhi kuwapatia vifaa ikiwemo makoti ya mvua na viatu ili waweze
kufanya kazi muda wote.
PROGRAMU
KUU YA USIMAMIZI WA HUDUMA ZA MAJI NA NISHATI
Mheshimiwa Spika,
Programu Kuu hii inasimamiwa na Mamlaka ya Maji (ZAWA), Shirika
la Umeme (ZECO), Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Maji na Nishati (ZURA),
Mamlaka ya Udhibiti wa Utafutaji na Uendelezaji wa Mafuta na Gesi Asilia
(ZPRA), Kampuni ya Maendeleo ya Mafuta na Gesi Asilia(ZPDC) pamoja na Idara ya
Nishati na Madini.
IDARA
YA NISHATI NA MADINI
Mheshimiwa
Spika,
Kwa mara nyengine tena, Kamati yangu imebaini kuwa
Idara ya Nishati na Madini haina Sera ya Nishati na Madini ambayo ndio muongozo
mkuu wa utekelezaji wa kazi za idara hii.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa kuchukuwa umuhimu wa Sera hii, Kamati yangu
inaiomba Serikali kupitia bajeti hii ya 2020/2021 kutenga fedha maalum za
ukamilishaji wa Sera hiyo muhimu kwa maslahi ya Taifa kwani kukosekana kwa Sera
hii inapelekea kukwamisha utekelezaji wa baadhi ya miradi ya uwekezaji katika
Sekta hii ya Nishati na Madini.
Mheshimiwa
Spika,
Kwani nchi yetu hivi sasa imo katika kutafuta
wawekezaji kuja kuwekeza katika Sekta ya Nishati ya Umeme Mbadala kama
inavyofahamika kuwa sio rahisi kwa muwekezaji yeyote ambaye yuko tayari kuja kuwekeza
katika nchi iliyokuwa haina Sera madhubuti itakayomuongoza katika uwekezaji,
ndio maana Kamati yangu inaitaka Wizara kukamilisha Sera hiyo ili Wawekezaji
makini waje kuwekeza ndani ya Serikali yetu.
SHIRIKA
LA UMEME (ZECO)
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu haina budi kuwapongeza Mkurugenzi Mkuu
wa Shirika pamoja na watendaji wake kwa kazi kubwa ya kutupatia huduma za
nishati ya umeme kwa muda wote wa masaa ishirini na nne.
Mheshimiwa Spika,
Pongezi maalumu ziende kwa Uongozi wa Shirika kwa
kutoa na kutekeleza agizo la Mhe. Rais alilolitoa kwa ajili ya kulipa deni lote
kutoka Tanesco kutokana na malimbikizo ya muda mrefu tunashukuru deni hilo sasa
limemalizika. Pamoja na hayo, Kmati yangu inalitaka Shirika lisibweteka deni
hilo lisije kujirudia tena.
MAMLAKA
YA UDHIBITI WA HUDUMA ZA MAJI NA NISHATI (ZURA)
Mheshimiwa
Spika,
Kamati yangu inaipongeza Mamlaka hii kwa kazi kubwa
wanayoifanya ya kuhakikisha wananchi wa Zanzibar wanapata huduma ya Maji na
Mafuta iliyo katika kiwango bora lakini pia na bei iliyo sahihi, Kamati yangu
inapongeza tena jitihada inayofanywa na Mamlaka hii kwa kuweza kuvikagua Vituo
vya Mafuta mara kwa mara ili kuhakikisha mafuta yanayotumika ni yanayokidhi
kiwango bora.
Mheshimiwa
Spika,
Pongezi maalum ziwaendee Mkurugenzi Mkuu, Naibu
Mkurugenzi Mkuu na watendaji wote kwa ubunifu wao wa kujenga jengo bora la
kisasa la Makao Makuu ya Mamlaka pamoja na Wizara nzima jambo hili ni la mfano
wa kuigwa.
Mheshimiwa
Spika,
Kwa upande wa Bandari ya Mafuta, Kamati yangubado
inaendelea kutoa masikitiko kwa Serikali kwa kuuhamisha Mradi wa Ujenzi wa Bandari
ya Mafuta na Gesi kutokuwepo chini ya usimamizi wa ZURA na kushughulikiwa na
taasisi nyengine jambo ambalo wenyewe ZURA ndio wanaojua changamoto zinazowakuta
hasa wakati mafuta yanapokosekana nchini na pale meli zinapochelewa kufika za
Mafuta hapa Zanzibar ndio maana ya kubuniwa mpango huo wa Bandari ya Mafuta na
Gesi katika eneo la Mangapwani.
MAMLAKAYA
UDHIBITI WA UTAFUTAJI NA UENDELEZAJI WA MAFUTA NA GESI ASILIA (ZPRA).
Mheshimiwa Spika,
Kamati yangu inapenda kutoa mkono wa pole kwa
wafanyakazi wote wa taasisi hii kwa kuondokewa na kiongozi wao shupavu, mahiri
na mtaalamu kwa masuala ya utafutaji na uendelezaji wa taaluma ya mafuta na
gesi asilia nchini Ndg. Omar Zubeir Ismail Mwenyezi Mungu ailaze roho ya
marehemu huyu peponi Amin.
Mheshimiwa Spika,
Mamlaka hii kwa upande wake imekabiliwa na
changamoto yaushirikishwaji mdogo wa wananchi wakati wa zoezi la Uchimbaji na
Utafutaji wa Mafuta na Gesi Asilia unapoendelea.
Mheshimiwa Spika,
Kutokana hali hii, Kamati yangu inaiomba Mamlaka
hii kuwashirikisha wananchi kikamilifu katika zoezi zima la Utafutaji na
Uchimbaji wa Rasilimali ya Mafuta na Gesi Asilia kwa yale maeneo yote
yanayopitiwa na mradi huo.
Mheshimiwa
Spika,
Kufanya hivyo ni kuondoa malalamiko kwa wananchi
dhidi ya Serikali yao na pia itasaidia kuondoa changamoto ndogo ndogo
zinazoweza kujitokeza wakati zoezi la Mradi litakapokuwa linaendelea.
Mheshimiwa
Spika,
Vile vile, Kamati yangu inaikumbusha ZPRA kwamba
bado wananchi waliyoathirika na zoezi la Mitetemo bado hawajalipwa fidia jambo
ambalo wanachi wetu wamekuwa wakililalamikia suala hilo, ingawa kwa taarifa
tulizonazo kuwa fedha za kulipa wananchi fidia zipo ila ilikuwa inasubiriwa
Bodi ya Mtathmini Mkuu wa Serikali ipitishe viwango vya malipo ili fedha hizo ziweze
kulipwa kwa Wananchi husika.
Mheshimiwa
Spika,
Kutokana na
muda nitashindwa kuzijadili baadhi ya taasisi zilizomo katika Wizara hii
nitaomba wayazingatie maoni yetu tuliowasilisha wakati wa Ripoti za Kamati.
Tunaamini zitaweza kuwasaidia katika kufanikisha majukumu yao ya kila siku.
Mheshimiwa
Spika,
Baada ya maoni hayo ambayo yamejikita katika
Programu Kuu na Ndogo zilizo na umuhimu zaidi kwa Kamati yangu, ili kuhakikisha
Wizara hii inatekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa. Kamati yangu
inazipongeza taasisi zote kama vile Bodi ya Wakadiriaji wa Majengo, Bodi ya Wakandarasi,
Bodi ya Uhaulishaji Ardhi, Bodi ya Ukondoshaji (Condominium).
Mheshimiwa
Spika,
Baada ya hotuba nzuri iliyosomwa na mheshimiwa
Waziri pamoja na Maoni haya ya Kamati ya Ardhi na Mawasiliano nawaomba wajumbe
wengine wa Baraza lako Tukufu waichaingie vyema bajeti hi na hatimaye
kuipitisha kwa lengo la kupata utekelezaji bora kwa maslahi ya wananchi wetu.
Mheshimiwa
Spika,
Mimi mwenyewe binafsi na kwa niaba ya Kamati
ninayoiongoza ya Ardhi na Mawasiliano, naiunga mkono hoja hii kwa asilimia
100%.
Mheshimiwa
Spika,
Baada ya Maelezo hayo, naomba kuwasilisha.
Ahsante,
Mhe.
Hamza Hassan Juma
Mwenyekiti,Kamati
ya Ardhi na Mawasiliano,
Baraza
la Wawakilishi,
Zanzibar.
No comments:
Post a Comment