Habari za Punde

Wanawake wa UWT Watakiwa Kujitokeza Kuchukua Fomu za Kugombea Uongozi .

Na.Mwashungi Tahir  -Maelezo   22/o6/2020.
Kamati tekelezaji ya Umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Wilaya ya Amani wametakiwa  kujitokeza  kuchukuwa fomu za uongozi katika nafasi mbali mbali katika uchaguzi utakaofanyika Oktoba  mwaka huu.
Hayo ameyasema Mwenyekiti wa umoja wa Wanawake Tanzania (UWT) Fatma Hamrani huko ofisini kwake wilaya ya Amani wakati alipokuwa akizungumza na kamati tekelezaji  kuhusiana na uchukuaji wa  fomu kwa nafasi mbali mbali za uongozi .
Amesema wanawake wasijiweke nyuma wasimame kidete katika kuchukua nafasi mbali mbali ikiwemo ubunge, uwakilishi na udiwani kwani hii ni demokrasia na kila mtu anayo haki ya kuchukuwa nafasi na kugombea wakati ukifika.
“Kinamama wenzangu tujitokezeni kwa wingi kuchukua fomu za nafasi mbali mbali kwani hii ni fursa  adhimu na tusiiwachie”alisema Mwenyekiti huyo.
Pia aliwaasa akinamama kuhamasishana na kupeyana nguvu kwa kuweka mashirikiano pindi pale wanawake  wanapojitokeza kutaka kuomba nafasi  za uongozi katika ngazi mbali za chama na serekali.
 Nae Kaimu Katibu wa Umoja wa wanawake Tanzania (UWT) Wilaya ya Amani Mwanamvua Mussa Chambo  amewataka wanawake kuwa na hamasa kwa kuchukuwa fomu za uongozi katika majimbo pindi zitakapotoka  ili waweze kuingia katika vyombo vya kutunga sheria .
“ Iwapo tutapata kushika nafasi za uongozi  tutaweza kutoa maamuzi katika vyombo hivyo katika kujikwamua kwa  kupambana na mfumo dume wa kiutawala na kupata maendeleo katika jamii”,alisema kaimu huyo.
Kwa upande wanawake hao wamesema wako tayari kuchukuwa fomu za nafasi za uongozi katika uchaguzi unaotarajiwa kufanyika mwezi wa Oktoba mwaka huu kwa ngazi mbali mbali pale muda utakapofika kwani kinamama wana mchango mkubwa katika kuleta maendeleo katika nchi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.