Waziri wa Afya Zanzibar Hamad Rashid Mohamed akizungumza neno wakati akiwatembelea wachangiaji Damu kwa hiari katika Maadhimisho ya Siku ya Uchangiaji Damu Duniani ambapo hufanyika kila ifikapo tarehe 14/06 kila mwaka .Hafla iliofanyika katika kitengo cha Damu salama Sebleni kwa Wazee Zanzibar.
Na Kijakazi Abdalla Maelezo 15/06/2020
Waziri wa Afya Zanzibar Hamad Rashid Mohamed amesema kuchangia damu ni suala la kitaifa ambalo linahitaji kuungwa mkono na kila mwananchi ili kuwasaidia wanaopatwa na matatizo ya afya.
Hayo ameyasema katika Kitengo cha Damu salama, Sebleni kwa Wazee, katika maadhimisho ya siku ya uchangiaji damu duniani ambapo kwa Zanzibar iliambatana na wananchi kuchangia damu kwa hiari.
Amesema kuwa suala la uchangiaji damu linahitaji uzalendo na halina uhusiano na itikadi za kisiasa kwani kila mwanaadamu anahitaji huduma ya damu wakati inapotokea dharura ya kuumwa ama panapotokea ajali.
Amesema Zanzibar kama zilivyo nchi nyengine duniani imekuwa na mahitaji makubwa ya damu hasa kwa akinamama wakati wa kujifungua na ajali za barabarani.
Alisema mahitaji ya damu yanaongeza kila siku kutokana na ongezeko la idadi ya watu hivyo kuwepo damu ya akiba kutasaidia kuokoa maisha ya wananchi.
Waziri Hamadi amesema katika kuhakikisha wananchi wanaondokana na changamoto ya kufuata masafa ya uchangiaji damu Serikali imefungua vituo katika Hospitali za Wilaya.
Amewataka vijana kutumia vituo hivyo katika kuchangia damu ili kuhakikisha Zanzibar inaondokana na ukosefu wa huduma ya damu salama katika hospitali.
Nae Katibu wa Jumuiya ya Wachangiaji Damu Zanzibar Hamad Bakari Mgarawa amesema mahitaji ya damu ni chupa 1705 kwa mwezi hivyo suala la kuchangia damu ni jambo muhimu.
Aidha amewataka wachangiaji damu kutumia kadi zao kwa kuhudumia familia zao na sio kuwapa marafiki ambao hawako tayari kuchangia damu.
Vilevile amesema Zanzibar kuwa na uhaba wa damu ni aibu hivyo ni vyema kuweka kipa umbele suala uchangiaji damu kwa kila mwananchi.
No comments:
Post a Comment