Habari za Punde

Dk Shein: Marehemu Mkapa aliyahifadhi na kuyalinda Mapinduzi ya 1964 kwa vitendo

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza wakati wa hafla ya maziko ya Rais Mstaaf wa Awamu ya Tatu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Benjamin William Mkapa, yaliofanyika Kijijini kwao Lupaso Mkoani Mtwara.
---
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein, amesema kuwa Rais Mstaafu wa Awamu ya Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Marehemu Bejamin William Mkapa aliyahifadhi na kuyalida Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar ya mwaka 1964 kwa vitendo.
Pia, Rais Dk. Shein aliongeza kuwa Marehemu mzee Mkapa aliuhifadhi na kuulinda Muungano wa Tanganyika na Zanzibar kwa vitendo hivyo, ataendelea kuheshimiwa kwa ari yake hiyo na uzalendo wake huo aliokuwa nao.
Rais Dk. Shein aliyasema hayo wakati akitoa salamu za wananchi wa Zanzibar na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kufuatia kifo cha Marehemu Rais Bejamin William Mkapa katika maziko yaliyofanyika huko kijijini kwake Lupaso, Mkoa wa Mtwara, Wilaya ya Masasi.
Hivyo, Rais Dk. Shein alisema kuwa wananchi wataendelea kumuenzi na kumkumbuka Rais Mkapa katika maisha yao yote sambamba na kumuombea kwa Mwenyezi Mungu.
“Takribani siku hizi sita zilizopita tulikuwa na majonzi makubwa lakini hatukusikitika kwani ndio uwezo wa Mwenyezi Mungu, hivyo ni jukumu letu kumuombea Mzee wetu huyu ili MwenyeziMungu amsamehe makosa yake na amjaalie amuweke mahala pema”
“Mwenyezi Mungu atupe hatima njema ya maisha yetu hapa duniani tukitimiza wajibu wetu katika kutekeleza majukumu yetu kama vile alivyofanya kiongozi wetu huyu Rais Benjamin William Mkapa”, alisema Rais Dk. Shein.
Hivyo, Rais Dk. Shein alisema kuwa kwa majonzi makubwa wananchi wa Zanzibar wanaungana na ndugu zao wote  wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  wananchi wa Mkoa wa Mtwara na hasa Wilaya hiyo ya Masasi katika maombolezo ya msiba huo mkubwa.
Aidha, Rais Dk. Shein alimtaka Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dk. John Pombe Joseph Magufuli kupokea salamu hizo za wananchi wa Zanzibar huku akisisitza kwamba safari hiyo ya umauti ni ya mwisho ambayo ni muhimu na ya  lazima kwa kila mwanaadamu.
Nao marais wastaafu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa nyakati tofauti walitoa salamu zao za mwisho kabla ya kuzikwa kwa Rais Mkapa na walitumia fursa hiyo kumuelezea Rais Mkapa jinsi walivyomfahamu kwa miaka mingi sambamba na utekelezaji wake wa kazi.
Rais Kikwete kwa upande wake alieleza kuwa Marehemu Mkapa alikuwa ni kiongozi mtambuzi wa manufaa ya watu wake anaowaongoza ambaye amelifanyia mengi taifa hili la Tanzania katika uongozi wake.
“Nafsi yangu kama zilivyo nafsi zenu imegubikwa kwa kuondokewa na ndugu yetu, mwenzetu huyu Rais Mkapa…………sisi Waislamu tunahusia kwa kiongozi wetu Bwana Muhammad (S.A.W)  anasema kuwa mwanaadamu kwa maumbile yake ni mkosaji na ndugu yetu ni mwanaadamu…”
“..............hivyo, huenda pengine katika umri wake amewahi kuteleza akafanya kosa asilolitaka au asilolipenda Muumba wetu basi katika hali kama hii mwenzetu akiondoka duniani basi ni vyema kumuombea msamaha kwa Mwenyezi Mungu kwani hata baba yetu Adam alikosea”, alisema Rais Mstaafu Ali Hassan Mwinyi.
Sambamba na hayo, Rais Mwinyi alisema kuwa Rais Mkapa alikuwa ni mtu mzuri sana, mwema sana na mbaridi sana lakini alikuwa ni mfanya kazi kweli kweli na alikuwa hana masihara katika kazi mambo ambayo yameleta manufaa kwa Tanzania.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliwashukuru viongozi wote na wananchi pamoja na Kamati ya Kitaifa iliyoshughulikia vyema msiba huo huku akimuelezea Rais Mkapa kuwa alipenda kwao na kuwataka Watanzania kujifunza jambo hilo kwani Mzee Mkapa aliusia kuzikwa katika kijiji alichozaliwa cha Lupaso.
Nao wanafamilia wa Marehemu Mzee Mkapa walitoa shukurani kwa wananchi na viongozi wote pamoja na Serikali kwa kuujali na kuushughulikia msiba wa Rais Mkapa ambapo maziko ya kiongozi huyo yalifanyika kwa taratibu zote za Kiserikali na kidini.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.