Mabaki ya Gari ya kubebea mafuta likiwa limeungua kutokana na ajali hiyo ya moto iliotokea wakati ikipakia mafuta katika Depot ya Puma Mtoni Jijini Zanzibar, katika ajali hiyo imesababisha kifo cha dereva wa gari hiyo.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja Simon Pasua, akizungumza na Waandishi wa habari kutokana na ajali ya moto iliotokea katika Depot ya Puma Mtoni Jijini Zanzibar na kusababisha kifo cha dereva wa gari hiyo.
Na Mwandishi Wetu
MTU mmoja alietambulika kwa jina la Hija Suleiman mkaazi wa Mwera amefariki dunia katika ajali ya moto uliotokea huko katika kituo cha mafuta depot ya PUMA Mtoni Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja.
Moto huo ambao ulitokea jana majira ya saa 8:00 mchana baada ya gari iliyokuwa ikishusha mafuta kuripuka.
Akizungumza na waandishi wa habari Kaimu Kamanda, Mkoa wa Mjini Magharibi, Simon Pasua alisema chanzo cha moto huo haikijajulikana na Polisi inaendelea na upelelezi.
Hata hivyo alisema kuwa ni mapema kuelezea chanzo cha ajali hiyo na Polisi wamefanya jitihada za kufunga eneo hilo ili kudhibiti madhara kwa wengine.
"Mnamo majira ya saa 8 mchana eneo la Mtoni depot ya PUMA gari ilikuwa inaweka mafuta katika tenki kukatokea Moto na gari kuripuka na mtu mmoja kufariki", alisema.
Hata hivyo alisema kuwa mpaka sasa hali ipo shuwari lakini bado eneo hilo lipo chini ya ulinzi mpaka wahakikishe moto huo umemaliza kabisa.
No comments:
Post a Comment