Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Afungua Maonesho ya Nanenane Viwanja vya Chamanangwe Pemba.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amewataka baadhi ya watu wakiwemo vijana kutojiingiza katika vitendo vinavyoweza kuvunja amani na utulivu nchini kwa kisingizio cha demokrasia na uchaguzi.  

Dk. Shein aliyasema hayo katika ufunguzi wa Maonyesho ya Nane Nane yaliyofanyika huko Chamanangwe, Wilaya ya Wete Mkoa wa Kaskazini Pemba ambayo yalihudhuriwa na viongozi mbali mbali wa vyama vya siasa na Serikali akiwemo Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd pamoja na wananchi wengine.

Rais Dk. Shein alisema kuwa uzoefu unaonesha kwamba  baadhi ya watu na hasa vijana hushawishiwa na watu wasio na nia njema na nchi yao, wajiingize katika vitendo vinavyoweza kuvunja amani iliyopo.

Kwa kutilia mkazo jambo hilo la kuvunja amani kwa kisingizio cha demokrasia Rais Dk. Shein alisisitiza kwamba taasisi ya haki ni Mahakama Kuu pekee hivyo, mtu anapokosa  haki yake  anatakiwa  kufungua kesi kwa lengo la kudai haki yake hiyo na sio kutoa kauli za uvunjifu wa amani.

Katika hotuba yake hiyo, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuwaasa vijana kama na kuwataka kuepuka kuingia katika mtego huo kwani hali hiyo inaweza kuhatarisha amani pamoja na maisha yao.

“Nawambia vijana mti na macho, kwamza wafahamu kwamba Zanzibar ni ya watu wote”alisisitiza Rais Dk. Shein.

Aidha, alieleza kuwa vyombo vya ulinzi vipo imara katika kukabiliana na mtu yoyote mwenye lengo la kutaka kuvunja amani kabla ya uchaguzi, wakati wa uchaguzi na baada ya uchaguzi.

“Hakuna mtu anaeweza kuja kuwatisha watu wa Zanzibar, watu wa Zanzibar wako huru katika nchi yao wamekombolewa na Mapinduzi ya Januari 12, mwaka 1964, wasitikishe kibiriti, hii serikali kama zilivyo serikali nyengine………..nawataka wananchi wajue kwamba kuna maisha baada ya uchaguzi”,alisisitiza Dk. Shein.

Rais Dk. Shein alieleza kwamba siasa ya mfumo wa vyama vingi haikuja kwa lengo la  watu kugombana kwa sababu ya siasa hivyo, aliwasisitiza vijana wanaoshawishiwa sambamba na kutengenezewa mazingira ya kuvunja amani  wajue kwamba Zanzibar ni ya watu wote na wote wanailinda.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alieleza kwamba wananchi wanahitaji kuendelea na maisha yao na kuzidi kupiga hatua za maendeleo kwa kuleta ustawi wa maisha katika jamii.

Hivyo, alisisitiza kwamba msingi muhimu wa kuiendeleza dhamira hio ni kudumisha amani, utulivu, umoja, mapenzi na mshikamano uliopo hapa nchini.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa ni rahisi sana kuivunja amani lakini si rahisi kuirejesha amani huku akieleza kuwa Zanzibar na Tanzania nzima kwa jumla  ziko salama na katika kipindi chote hichi kila mmoja anafanya kazi zake, anatembea usiku na mchana na analala vizuri bila ya hofu wala woga.

Rais Dk. Shein  alisema kuwa mafanikio yanayoendelea kupatikana katika utekelezaji wa mipango ya mandeleo yakiwemo ya sekta ya kilimo, yanatokana na kuendelea kuwepo kwa hali ya amani na utulivu.

Alieleza kuwa katika hotuba zake mbali mbali amekuwa akisisitiza umuhimu wa kuitunza, kuilinda na kuiendeleza amani iliyopo pamoja na kuwataka wananchi kujiepusha na vitendo vyote vinavyoweza kusababisha kuvunjika kwa amani iliyopo.

Aliipongeza Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi kwa ubunifu wa kaulimbiu ya maonyesho ya mwaka huu isemayo “Tudumishe amani na utulivu kwa maendeleo ya sekta ya kilimo nchini” huku akiendelea kusisitiza uimarishaji amani na utulivu nchini.

Aliongeza kuwa kauli mbiu hiyo ni muhimu wakati huu ambapo nchi inaelekea katika kufanya uchaguzi mkuu katika mwezi wa Oktoba mwaka huu.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.