Habari za Punde

Serikali Imeendelea Kuweka Mikakati Enfelevu ya Kuwawezesha Vijana Kushiriki Katika Ujenzi wa Uchumi wa Taifa - Naibu Waziri Mavunde.

Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana na Ajira Mhe. Anthony Mavunde akizungumza na Waandishi wa Habari jijini Dodoma kuhusu Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani “International Youth Day” katika Ukumbi wa Mkutano uliopo jengo la PSSSF
Sehemu ya Waandishi wa Habari wakisikiliza kwa makini taarifa ya Serikali iliyokuwa ikitolewa na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu-Kazi, Vijana na Ajira Mhe. Anthony Mavunde (hayupo pichani) alipokuwa akitoa kauli ya Serikali kuhusu maadhimisho ya ya Siku ya Vijana Duniani “International Youth Day”.

Na; Mwandishi Wetu – Dodoma
Serikali imeendelea kuweka mikakati endelevu ya kuwawezesha vijana nchini kushiriki kikamilifu katika shughuli za uzalishaji mali ili kuendelea uchumi wa Taifa.

Hayo yameelezwa na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia Kazi, Vijana na Ajira Mhe. Anthony Mavunde alipokuwa akizungumza na waandishi wa Habari kuhusu maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani “International Youth Day” ambayo uadhimishwa kila Agosti 12 huku Mwaka huu 2020 kauli mbiu ya maadhimisho hayo ikiwa ni “Ushirikishwaji wa Vijana katika Mstakabali wa Dunia”.

Naibu Waziri Mavunde alieleza kuwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa Serikali ya Mapinduzi Zanzibari inayoongozwa na Rais wa Zanzibar ambaye pia ni Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt. Ali Mohamed Shein zimekuwa zikichukua hatua mbalimbali za kuwashirikisha vijana katika nyanja mbalimbali zenye lengo la kuendeleza nchi yetu.

“Serikali yetu katika kutambua mchango wa vijana katika ujenzi wa Mataifa yao inaunga mkono kauli mbiu iliyotolewa na Umoja wa Mataifa katika kuadhimisha siku hii muhimu, hivyo itaendelea kuweka mifumo imara ya kitaasisi na kisheria ambayo inawapa vijana fursa pana ya kushiriki na kushirikishwa katika michakato yote ya maendeleo iyoyomo nchini,” alieleza Mavunde

Alieleza kuwa Serikali imeandaa Sera ya Taifa ya Maendeleo ya Vijana ambayo imetamka wazi namna mifumo ya kisheria na kitaasisi iliyoweka katika kuwezesha ushiriki wa vijana katika maendeleo ya Taifa, pia elimu bora imekuwa ikitolewa kwa vijana lengo ikiwa ni kuzalisha waataam wengi zaidi watakaolivusha taifa kuelekea kwenye mapinduzi ya sayansi na teknolojia ya kisasa.

“Inatambulika kuwa vijana ndio kundi kubwa katika jamii yoyote ile duniani na ndio wenye nguvu zaidi za kufanya kazi kwa kuleta ubunifu kutoka na mawazo mapya waliyonayo na ndio chachu ya mabadiliko ambayo huleta tija ya kisayansi na kiteknolojia,” alisema Mavunde

“Dhana ya ushirikishaji wa vijana katika masuala ya kidunia inatokana na mchango mkubwa wa vijana walionyesha katika kuleta maendeleo ya mataifa yao,”

Aliongeza kuwa katika uongozi wa Awamu ya Tano, Serikali imeendelea kuweka mikakati endelevu yenye malengo ya kuwawezesha vijana ikiwemo kuwapatia mikopo yenye riba nafuu ambayo hutolewa na Mfuko wa Maendeleo ya Vijana unaosimamiwa na Ofisi ya Waziri Mkuu, vilevile mikopo ambayo hutolewa na halmashauri za wilaya zote nchini ambapo vijana hutumia fursa hiyo kuanzisha au kuendeleza miradi mbalimbali inayowaingizia kipato.

Mheshimiwa Mavunde alieleza kuwa Serikali pia ilianzisha Programu ya Kukuza Ujuzi wa nguvukazi ya Taifa ambayo ni asilimia 56 ambapo kupitia programu hiyo zaidi ya vijana 28,941 wamekwisha patiwa mafunzo ya Uanagenzi “Apprentieship” katika fani za ufundi stadi, Vijana 20,432 wameweza kurasimishiwa ujuzi wao uliopatikana nje ya mfumo rasmi “Recognition of Prio Learning”, Vijana 5,975 wahitimu wa elimu ya juu wa fani mbalimbali wamewezeshwa kupata mafunzo ya uzoefu kazi na pia kupitia programu hiyo vijana 8,980 wamepatiwa mafunzo ya kilimo cha kisasa kutumia teknolojia ya Kitalu Nyumba “Greenhouse”.

Sambamba na hayo, Naibu Waziri Mavunde alitumia fursa hiyo kuwasihi vijana kushiriki kwa wingi kwenye Uchaguzi Mkuu wa Rais, Wabunge, Wawakilishi na Madiwani ifikapo tarehe 28 Oktoba 2020 na watambue kuwa wao ni wadau muhimu katika zoezi hilo n ani haki yao ya kikatiba.

“Vijana ni wadau muhimu katika zoezi hili, hivyo kuwawezesha kwenda kupiga kura ni haki yao waliyopewa na Katiba ya Nchi kushiriki katika shughuli za uchaguzi kwa amani na utulivu na kamwe wasitumike vinginevyo,” alisema Mavunde

Aidha Mhe. Mavunde alisema kuwa Serikali pia imeendelea kuwawezesha vijana kushiriki katika ngazi mbalimbali za maamuzi akitolea mfano mwaka huu 2020 zaidi ya asilimia 60 ya vijana wameweza kujitokeza kwa lengo la kushiriki katika sehemu ya ustawi wa taifa.

“Ni Dhahiri katika uongozi wa Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Uongozi mahiri wa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ameonyesha Imani kubwa sana kwa vijana wenye sifa za uongozi kuweza kushiriki kwenye uongozi kupitia teuzi mbalimbali na imeongeza mihemuko kwa vijana kuweza kushiriki kwenye ngazi za maamuzi,” alisema Mavunde

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.