Habari za Punde

Mawasiliano Yarejeshwa Vijiji Vya Libobe na Ming’wena Katika Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara.

Muonekano wa Barabara ya Libobe - Ming’wena yenye urefu wa kilomita 4.8 ikiwa imekamilika na kuanza kutumika.
Muonekano wa Barabara ya Libobe - Ming’wena kabla ya kujengwa na TARURA iliyopo Kata ya Libobe Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara mkoani Mtwara ambayo iliharibiwa na mvua na kukata mawasiliano kati ya vijiji vya Libobe na Ming’wena.


Na. Thereza L. Chimagu

Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) umefanikiwa kufanya ukarabati wa barabara iliyoharibiwa na mvua na kupelekea kukatika kwa mawasiliano kati ya Vijiji vya Libobe na Ming’wena vilivyopo Kata ya Libobe katika Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara mkoani Mtwara.

Akizungumzia ujenzi wa barabara hiyo Meneja wa TARURA Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara Mhandisi Patrick Kanyagha alisema, baada ya kupata changamoto ya kukatika kwa barabara hiyo waliomba fedha za dharura kutoka TARURA Makao Makuu na kupatiwa kiasi cha Shilingi Milioni 185 ambazo zilitumika kutengeneza barabara iliyopo kati ya Kijiji cha Libobe hadi Ming’wena yenye urefu wa Kilomita 4.8. kwa kiwango cha Changarawe ili wananchi waendelee na shughuli zao za kiuchumi.

” Kipande hiki cha Km 4.8 ni sehemu ya barabara ya Libobe- Ming’wena- Likwidi- Mtama yenye jumla ya urefu wa Km 19, na tulichukua maamuzi ya kutengeneza baada ya mvua kuharibu miundombinu ya barabara pamoja na kuathiri makazi ya wananchi ili kurejesha mawasiliano na kuwezesha  wananchi kusafirisha bidhaa zao kama hapo awali”, alisema Mhandisi Kanyagha.

Meneja huyo alisema kuwa   baada ya kupatiwa fedha hizo kazi walizozipa kipaumbele zilikuwa ni kurejesha tuta, kujenga “box culvert” mpya ambapo zimejengwa 8, kujenga mtaro wa maji ya mvua na kurejesha tabaka la changarawe urefu wa Km 3.5. ambapo kazi zote zimekamilika na mawasiliano yamerejea katika vijiji hivyo.

Naye, Bw. Majid Rashid ambaye ni mkazi wa   Kijiji cha Ming’wena ameipongeza Serikali kwa kutengeneza barabara katika eneo hilo kwani imesaidia kupunguza kero ya usafiri na kufanya wananchi waendelee na shughuli zao kama hapo awali.

“Tunaishukuru TARURA kwa kutujali na kutufanyia ukarabati wa  haraka kwani  tulikuwa na changamoto ya usafiri kutoka hapa hadi kufika barabara kuu ya Mpapora kwani magari na hata pikipiki yalikuwa hayapiti kabisa lakini baada ya matengenezo ya barabara tumefaidika sana na imerahisisha mawasiliano”, alisema Bw. Rashid.

Naye, Somoe Kankunje Mkazi wa Kijiji cha Ming’wena alisema, upatikanaji wa huduma mbalimbali za kijamii katika eneo hilo umerahisishwa na ukarabati wa barabara hiyo kwani hawapati shida ya usafiri na wanaendelea na biashara zao kama awali bila matatizo.

Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijni (TARURA) katika Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara unaendelea na kazi mbalimbali zikiwemo za matengenezo ya barabara na vivuko katika Wilaya hiyo ili kuwawezesha wananchi kusafiri na kusafirisha mazao Pamoja na bidhaa zao kwa urahisi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.