Habari za Punde

Serikali kuunda tume maalum kuchunguza sababu ya kuporomoka kwa sehemu ya jengo la Beit el Ajaib



 

 

                                                 STATE HOUSE ZANZIBAR

                                 OFFICE OF THE PRESS SECRETARY

                                          PRESS RELEASE

 

Zanzibar                                                                         Disemba 28, 2020

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi ameahidi kuunda Tume maalum ya Uchunguzi ili kubaini sababu zilizosababisha kuporomoka  kwa sehemu ya Jengo la Beit el Ajaib mwishoni mwa wiki iliyopita.

 

Dk. Mwinyi ameeleza hayo leo katika Ukumbi wa Sheikh Idrisa Abdul-wakil Kikwajuni Jijini Zanzibar, wakati alipokutana na  wadau mbali mbali wa Mji mkongwe.

 

Alisema iko haja ya kuunda Tume ya Uchunguzi  ili kubaini chanzo cha ajali iliotokea  pamoja na kutafuta njia zitakazowezesha kuepuka majanga, sambamba na kuwepo  uhifadhi bora wa mji huo.

 

Alisema ni jukumu la taasisi zilioko Mji Mkongwe, ikiwemo Mamlaka ya Mji Mkongwe, Wakfu na mali ya Amana pamoja na Shirika la nyumba kushirikiana ikiwa ni hatua ya kuyatafutia  ufumbuzi matatizo mbali mbali yanayokabili mji huo.

 

Alisema Tume itakayoundwa itakuwa na jukumu la kuangalia sababu zilizosababisha kuporomoka kwa sehemu ya jengo hilo  na nini kinahitaji kufanyika ili kuwepo uhifadhi bora wa Mji huo, ukihusisha majengo yake.

 

Aidha, alisema Tume hiyo itaangalia changamozo zinazokabili Taasisi zilizopewa mamlaka, akibainisha baadhi ya changamoto hizo hutokana na urasimu wa kiutendaji.

 

Alisema maeneo mengine yatakayopaswa kuangaliwa na Tume hiyo ni kuhusiana na weledi wa watendaji pamoja na muundo wa Bodi, huku akibainisha Tume hiyo itafanyakazi kuambatana na hadidu rejea.

 

“Lengo ni kutunza Mji na kuepusha maafa………..mapendekezo yanapawa kuwa ya muda mrefu, kati na mrefu  ikizingatiwa gharama nyingi zinazohitajika”, alisema.

 

Dk. Mwinyi alisema taarifa ya uchunguzi inapaswa kuainisha juu ya majengo yatakayohitaji kufungwa na wakaazi wake kuondolewa mara moja

 

Alieleza kuwa Zanzibar imepoteza nembo muhimu ya Taifa na kusema wakati umefika wa kutizama ustawi wa mji mkongwe katika jicho la aina  yake.

 

Alisema uchunguzi utakaofanywa haulengi kumtuhumu au kumuonea mtu, bali utazingatia  haki na hivyo hatua  zitachukuliwa  pale itakapobainika kufanyika uzembe.

 

Rais Dk.Mwinyi, akitoa ufafanuazi wa baadhi ya mapendekezo, alisema  katika mwelekeo wa kuwa na Mji Mkongwe uliohifadhika vyema, ni lazima kuwepo mfuko maalum wa Uhifadhi wa mji huo na kusema serikali itakuwa ya kwanza katika kuchangia, sambamba na kuwashajiisha wadau  kufanya hivyo.

 

“Serikali itaweka ‘seriousness’ katika uhifadhi wa mji mkongwe kwa kuwa na bajeti na wafanyakazi wenye taaluma pamoja na mfuko maalum, lakini pia naunga mkono suala la kuwa na ‘stone town day’”, alisema.

 

Aidha, alisema ni wakati muafaka wa kuangalia kwa makini utaratibu wa vyombo vya moto kuingia na kutoka  katika eno la Mji Mkongwe.

 

Alitumia fursa hiyo kuishukuru Serikali ya Oman kwa utayari wake katika kusaidia uhifadhi wa mji Mkongwe a Zanzibar.

 

“Gharama za uhifadhi lazima zichukuliwe na Serikali kabla ya msaada, hivyo Serikali itakuwa mstari wa mbele katika kufanikisha jambo hilo, nawaomba wadau kufanya kila linalowezekana  kutunza mji mkongwe, kwa kuwa ni chanzo kikuu cha mapato pale utakapohifadhiwa vyema”, alisema.

 

Mapema, Waziri wa Utalii na Mmabo ya Kale, Lela Mohamed Mussa pamoja na mambo mengine alisema katika tukio la kuporomoka kwa sehemu ya Jengo la Beit el Ajaib, mwishoni mw awiki iliyopita mafundi wanne walijeruhiwa na wengine wawili kufariki dunia.

 

Aidha, Mkurugenzi, Mamlaka ya Mji Mkongwe Issa Sarboko Makarani, alisema miongoni mwa faida kubwa zinazotokana na Mji Mkongwe wa Zanzibar kuwepo katika Urithi wa Kimataifa ni kupata msaada Wa matengenezo pale yanapotokezea maafa, ikiwemo kuporomoka kwa majengo yake.

 

Alisema Mamlaka ya Mji Mkongwe katika nyakatri zote imekuwa ikipata msaada mdogo wa kifedha kwa ajili ya kuyashughulikia majengo yake na ndio sababu ya kuporomoka kwa sehemu ya jingo la Beit al Ajaib na mengineyo, sambamba nakusema  ukosefu mkubwa wa wafanyakazi wenye taaluma ya Uhifadhi wa Mji Mkongwe kuwa ni changamoto kubwa inayoikabili mamlaka hiyo.

 

Nao, wadau mbali mbali wa Mji Mkongwe wakichangia katika mkutano huo; waliishauri Bodi inayosimamia uhifadhi wa Mji Mkongwe  kuwa na mainjinia wa kutosha ili kufanyakazi ya kuyakagua majengo mbali mbali yaliomo katika eneo hilo.

 

Walisema taarifa za uchakavu wa majengo ni vyema zikawa zinatumwa  UNESCO kabla ili kuepuka majanga mbali mbali ikiwemo vifo.

 

“Wizara inapaswa kuwa makini wakati wa kutafuta wajumbe wa Bodi ya Mamlaka ya Mji Mkongwe, ili kuwa na watu wanaoendana na sifa na mahitaji halisi”, alisema Siti Abasi Ali.

 

 

Aidha, walisema Serikali inapaswa kusaidia katika usimamizi wa upigaji marufuku wa vyombo vya moto, (ikiwemo Bodaboda) kuingia katika eneo la Mji Mkongwe , ikiwa ni hatua ya kuimarisha usalama.

 

Vile vile waliiomba serikali kuanzisha mfuko maalum (utakaoendeshwa kwa uwazi) katika dhana ya  kuuendeleza uhifadhi pamoja na kutoza ada maalum kwa  ajili ya kuchangia uhifadhi wa mji huo.

 

Wadau hao wamevitaka vyombo vya habari, hususan Shirika la Utangazaji Zanzibar (ZBC) kuwa na vipindi maalum vya kuutangaza Mji Mkongwe wa Zanzibar, wakati ambapo wameibua hoja kuwa wananchi wengi hawaelewi thamani ya Mji huo na utajiri mkubwa ulionao.

 

Mkutano huo uliwashirikisha viongozi wa Kitaifa na wadau mbali mbali, akiwemo Mwakilishi Wa Balozi wa Oman, Mawaziri wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Mwanasheria Mkuu wa Zanzibar Dk. Mwinyi Talib haji,  Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Saleh Omar Kaab, Mstahiki meya wa Jiji la Zanzibar Saleh Kinana, Viongozi wa Vikosi maalum vya Serikali ya Zanzibar, Wawekezaji wa sekta ya Ualii  pamoja an wadau mbali mbali wa Mji Mkongwe.

 

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 

 E-mail: abdya062@gmail.com

 

 

 

 

 

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.