Na.Sabiha Khamis - Maelezo – Zanzibar.
Mwenyekiti wa Chama cha Kuwaendeleza Washairi Zanzibar wametoa salamu za pole kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali ya Zanzibar, Familia pamoja na wananchi wote kufuatia kifo cha aliekuwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt John Pombe Magufuli.
Amesema Watanzania wapo katika majonzi makubwa ya kumpoteza kiongozi Shujaa, mchapa kazi, mzalendo, na mpenda haki ambae aliwaweka Watanzania kuwa pamoja katika kuiletea nchi maendeleo.
Ameyasema hayo katika hafla ya maadhimisho ya siku ya washairi duniani iliyofanyika katika ukumbi wa Skuli ya Mbadala Rahaleo amesema siku hio imefika katika kipindi ambacho Taifa lipo katika majonzi makubwa ya kumpoteza kiongozi wao.
“Taifa limepoteza kiongozi shujaa, mchapa kazi na mzalendo kwa nchi yake sina budi kufikisha salamu zangu za pole kwa Serikali, Familia na Watanzania wote Mungu awape nguvu na ujasiri katika kipindi hichi kigumu cha maombolezo” alisema Mwenyekiti.
Kwa upande wake Katibu wa CHAKUWAZA Said Suleiman Ali amesema kufuatia kifo cha Rais Magufuli Chama kimewaomba washairi wote kutunga shairi za maombolezo kwa kueleza mambo mbali mbali ambayo Rais Magufuli ameyefanya katika nchi yetu.
Hata hivyo amewataka washairi wote kuimarisha umoja na kujitiokeza kwa wingi katika hafla ya kuuwaga mwili wa aliekuwa Rais wa Tanzania.
Aidha amesema wamedhamiria kuitangaza siku ya washairi na kutambulika kama siku nyengine duniani kwa kuandaa shughuli mbali mbali ikiwemo makongamano, ziara pamoja na matamasha ili washairi na watu wote kuifahamu siku hio.
Amesema mashairi yamekuwa na umuhimu mkubwa kwa jamii kwani yanaelimisha na baadhi kuburudisha hivyo UNESCO wameitambulisha siku ya tarehe 21 Machi ya kila mwaka kuwa ni siku ya washairi Duniani.
No comments:
Post a Comment