Habari za Punde

Risala ya Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Hussein Ali Mwinyi Katika Kuukaribisha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani Mwaka 2021, Miladia Sawa na Mwaka 1442 Hijria.

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Hussein Ali Mwinyi.


Ndugu Wananchi,

Ni wajibu wetu kumshukuru Mola wetu Mtukufu; SubhanahuWataala kwa kuturuzuku neema ya uhai tukaweza kuifikia siku hii ya leo ambapo Waislamu na Wananchi wote wa Zanzibar na Tanzania kwa ujumla tunaungana na Waislamu wenzetu duniani kote katika kuukaribisha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kwa mwaka huu wa 2021 Miladia, sawa na mwaka 1442 Hijria.

Tunamshukuru Mwenyezi Mungu(SWT) kwa  kuturuzuku hidaya ya uzima hadi tukaweza kuukaribsha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kwa mara nyengine, kwani katika kipindi kama hiki mwaka jana, tulikuwa na Waislamu wenzetu ambao Mwenyezi Mungu (SWT) amewakhitari na wameshatangulia mbele ya haki. Tunamuomba Mwenyezi Mungu (SWT) awasamehe makosa yao na awape malazi mema. Kadhalika, na sisi tulio hai atujaalie khatma njema na umri wenye faida. Amiin!

 Ndugu Wananchi,

Katika kuupokea Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, tuweke azma na nia ya kuitekeleza ibada hii ya Saumu inayotukabili kwa imani na yakini kwani ni wajibu wetu kufunga kama ilivyokuwa kwa wale waliotangulia kabla yetu kama Mwenyezi Mungu (SWT) alivyotuamrisha katika Aya ya 183 ya Surat Al – Baqarah yenye tafsiri isemayo:

“Enyi mlioamini! mmefaradhishiwa kufunga (Saumu) kama walivyofaradhishiwa  waliokuwa kabla yenu ili mpate kumcha Mungu”

Kwa hakika, ibada ya Saumu ambayo imetukabili ina mchango mkubwa katika kuimarisha uchamungu, jambo ambalo ni jema na litatupa manufaa hapa Duniani na kesho Akhera. Kwa hivyo, tuukaribishe MweziMtukufu  wa Ramadhani kwa furaha na matumaini, na tujiandae kunufaika kutokana na neema na fadhila mbalimbali zilizo katika kipindi chote cha Mwezi huu tunaoukaribisha. Tuhimizane kutekeleza ibada za Faradhi vilevilenatukithirishe  kufanya ibada za Sunna ili kupata radhi za Mola wetu Mlezi.

Ndugu Wananchi,

Miongoni mwa ibada ambayo imesisitizwa kuifanya kwa wingi ndani ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani ni kusoma Qurani, kwani mwezi huu ndio ulioteremshwa Kitabu Kitukufu cha Qurani ambacho ni mwongozo wetu. Mwenyezi Mungu ametubainishia katika Aya ya 185 ya Surat Al-Baqarah kwa tafsiri isemayo;

“Mwezi wa Ramadhani ambao imeteremshwa ndani yakehii Qurani ili iwe uongofu kwa watu,na hoja zilizo wazi za uongofu na upambanuzi (baina ya haki na batili)”. Hadi mwisho wa aya.

Kwa hivyo, ni wajibu wetu kuutumia Mwezi Mtukufu  wa Ramadhani kwa kuisoma sana Qurani kwani kufanya hivyo kuna fadhila kubwa mbele ya Mwenyezi Mungu (SWT). Tujitahidi kuendeleza darsa Misikitini, kufanya mihadhara mbalimbali ya kutoa tafsiri ya Qurani ili usomaji wetu uzidi kuleta faida kwa kuyafahamu mafundisho yake. Kwa kufanya hivyo, tutaweza kunufaika zaidi na kupata upambanuzi utakaotuwezesha kuyaelekea zaidi mambo ya haki na kujiepusha na batili ili tupate radhi za Mwenyezi Mungu (SWT).

Ndugu Wananchi,

Katika kutafuta fadhila za Mwezi Mtukufu wa Ramadhani tumehimizwa kujitahidi sana kutekeleza ibada ya sala zote za Faradhi na sala za Sunna, kuomba dua,kusoma nyiradi mbali mbali, kufanya itikafu, na kutekeleza  Sunna nyengine zinazoambatana na Mwezi wa Ramadhani.

Ndani ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani unapatikana usiku wenye heshima kubwa wa Laylatul Qadir. Tunaelezwa kuwa, ibada ya usiku huo imebarikiwa kuliko ibada za miezi elfu moja na kwa hekimaza Mola wetu,  hakutubainishia kuwa usiku huo ni wa tarehe ipi. Hivyo, tuna wajibu wa kutafuta usiku huo kwa kufanya ibada nyingi hususan katika kumi la mwisho.

Katika kuonesha uzito wa kisimamo cha usiku kwa ajili ya kufanya ibada, Mtume wetu Muhammad (SAW) katika moja ya hadithi zake amesema kwamba.

“Mwenye kusimama usiku wa Ramadhani kwa kufanya ibada hali ya kuwa na Imani na kutarajia thawabu, amesamehewa mtu huyo, yote yaliyotangulia miongoni mwa makosa yake”(Bukharina Muslim).

Kwa hivyo, tumuombe Mola wetu atuwezeshe kutekeleza ibada hiyo katika Mwezi Mtukufu wa Ramdahni ili tuweze kunufaika na fadhila za ibada za usiku  ikiwemo kusamehewa madhambi yetu yaliyopita kwani kwa hakika mwanadamu sio mkamilifu ila Mola pekee Subhanahu Wataala.

Ndugu wananchi,

Jambo jengine tunalohimizwa kulitekeleza zaidi ndani ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani ni kutoa sadaka hasa kwa watu wenye mahitaji, Mayatima, Wazee, Masikini na Mafakiri.  Tunaelezwa kuwa ibada hii ina malipo makubwa mbele ya Mwenyezi Mungu (SWT) na inaongeza baraka, mapenzi na kuhuwisha mahusiano mema ndani ya jamii.

Mashekhe wetu wanatufunza kuwa katika mwezi Mtukufu wa Ramadhani Bwana Mtume (SAW) kutoa kwake sadaka, kuliongezeka kuliko miezi mingine. Kwa vile yeye ni Kiongozi wetu, tuna wajibu wa kumfuata na kuitekeleza Sunna hii kama walivyoitekeleza masahaba zake na wote waliofuata mwendo wake mwema na kufanikiwa kutokana na  mafundisho yake. Tumuombe Mwenyezi Mungu (SWT) atupe nguvu na uwezo wa kuyatekeleza mambo haya ya kheri.

Ndugu wananchi,

Nilipokutana na wafanyabiashara wakubwa wanaoagiza chakulatarehe 04 Machi, 2021 niliwataka, washirikiane na Serikali kufanya maandalizi mazuri katika kuhakikisha kwamba, bidhaa zote hasa za chakula muhimu kwa wananchi wa Zanzibar ziwe zinapatikana kwa kipindi cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani na baada ya hapo, kwa wingi na ubora stahiki, ili bei za bidhaa hizo zisiongezeke kama inavyotokea katika nyakati hizo. Tulikubaliana mambo kadhaa ambayo sasa tunaendelea kuyatekeleza, ikiwemo kutoa kipaumbele katika utoaji ruhusa wa kushusha mizigo kwa  meli zinazoleta bidhaa za chakula.

Inafurahisha kuona kwamba licha ya kuwepo kwa  changamoto za usafirishaji  na upatiakanaji wa bidhaa mbalimbali,  shughuli za biashara  na upatikanaji wa chakula hapa nchini zinaendelea vizuri, tunapoukaribisha  Mwezi wa Ramadhani   ikiwa  bidhaa zote muhimu zinapatikana.

Kadhalika, taarifa ya Wizara ya Kilimo, Umwagiliaji, Maliasili na Mifugo inatoa matumaini ya kuwepo kwa chakula cha kutosha miongoni mwa mazao ya chakula hasa muhogo na ndizi, mazao ambayo hutumiwa na wananchi wengi kwa futari katika Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.

Mtakumbuka kwamba tarehe 02 Aprili, 2021niliposalimiana na wananchi baada ya Sala ya Ijumaa katika Msikiti wa Amani,niliwasihi wafanyabiashara waendelee  kutoa huduma kwa wananchi kwa misingi ya uadilifu na huruma pamoja na kuzingatia sheria. Kwa pamoja, tuwafikirie wenzetu wenye kipato cha chini hasa katika kipindi hiki ambacho mahitaji ya familia yanaongezeka.Kwa msingi huo huo, wafanyabishara wa bidhaa za nguo wazingatie uwezo wa wananchi, kwani kuwakatia nguo watoto wetu katika kipindi hiki kwa ajili ya Sikukuu ni sehemu ya utamaduni wa wananchi wote wa Zanzibar.

Serikali  tayari imeshatoa bei elekezi za bidhaa muhimu za chakula. Kwa hivyo, itachukua hatua kali kwa mfanyabishara yoyote atakaebainika kupandisha bei za bidhaa au huduma  kwa utashi au  tamaa tu na  bila ya kuwepo na sababu ya msingi ya kufanya hivyo.

Ndugu wananchi,

Tunaupokea Mwezi Mtukufu wa Ramadhani wakati nchi yetu inaingia katika msimu wa mvua za Masika.Natumia fursa hii kukuhimizeni wananchi pamoja na viongozi na watumishi wa Manispaa zote juu ya umuhimu wa kuzingatia usafi katika miji yetu na hasa katika masoko na maeneo yanayohusika na uuzaji wa vyakula ili kujiepusha na maradhi ya mripuko. Tuendelee kusafisha misingi ya maji  na  njia za maji ili kujikinga na mafuriko. Ni vyema sote tuzingatie maelekezo ya wataalamu wa afya juu ya namna ya kuimarisha usafi ili kujikinga na mirupuko ya  maradhi mbalimbali.

 

Ndugu wananchi,

Mwezi Mtukufu wa Ramadhani ni chuo cha kujifunza tabia njema, tustahamiliane na tuvumiliane, tusaidiane na tuendeleze umoja na upendo miongonimwetu.  Aidha, natumia fursa hii kuwakumbusha  wananchi wenye dharura maalum na walewasiokuwa Waislamu waendeleze utamaduni wa kujizuia kula hadharani, kutokuvaa nguo zisizoendana na maadili yetu, na tuepuke matendo yatakayo wakwaza Waislamu wenye kutekeleza ibada ya funga.

 

 

 

 

 

Ndugu wananchi,

Nakamilisha risala yangu ya kuukaribisha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kwa kuwahimiza viongozi wa Mamlaka ya Usafiri na Usalama Barabarani pamoja  na Jeshi la Polisi kuhakikisha wanasimamia ipasavyo sheria za usalama barabarani wakati wote, na kuongeza nguvu zaidi  katika kipindi hiki ambacho harakati na mahitaji ya usafiri huongezeka. Wawachukulie hatua kali za kisheria  madereva watakaojaribu kuvunja  sheria  za usalama barabarani kwa kwenda mwendo wa kasi  na wale wenye tabia ya kuwasumbua wananchi kwa kuwashusha bila ya kuwafikisha  mwisho wa vituo vilivyopangwa na Serikali.

 

Kadhalika, nawahimiza viongozi wa Mamlaka ya Maji Zanzibar (ZAWA) kuhakikisha huduma ya maji zinawafikia wananchi  hasa katika maeneo ambayo huduma hio haipatikani kwa ukamilifu. Masheha wa shehia ambazo zina matatizo ya maji wawasiliane na ZAWA ili kuhakikisha hatua zinachukuliwa zikiwemo kuwapelekea wananchi magari ya maji kwa lengo la kuondokana na usumbufu wa kupatikana huduma hio muhimu.

 

Nakutakieni nyote kila la kheri na namuomba Mwenyezi Mungu (SWT) atuwezeshe kuufunga mwezi wa Ramadhani kwa salama. Tumuombe Mola wetu azikubali ibada zetu zote tutakazozifanya katika mwezi huo na katika maisha yetu yote.Aameen!

 

Wassalaamu Aleykum Wa RahmatuLlahi wa Barakaatuh.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.